Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Acheni Nuru Yenu Iangaze” ili Yehova Atukuzwe

“Acheni Nuru Yenu Iangaze” ili Yehova Atukuzwe

‘Acheni nuru yenu iangaze mbele ya watu, ili wamtukuze Baba yenu.’​—MT. 5:16.

NYIMBO: 77, 59

1. Tuna sababu gani ya pekee ya kuwa na shangwe?

INASISIMUA sana kusikia kuhusu ongezeko ambalo watu wa Yehova wanashuhudia! Mwaka jana tuliongoza zaidi ya mafunzo ya Biblia 10,000,000. Bila shaka hilo linaonyesha kwamba watumishi wa Mungu wanaacha nuru yao iangaze! Fikiria pia kuhusu mamilioni ya watu wanaopendezwa ambao walihudhuria Ukumbusho. Watu hao walijifunza kuhusu upendo ambao Mungu alionyesha alipoandaa fidia.—1 Yoh. 4:9.

2, 3. (a) Ni jambo gani ambalo halituzuii ‘kuangaza kama mianga’? (b) Kwa msingi wa maneno ya Yesu yaliyo katika andiko la Mathayo 5:14-16, tutachunguza nini?

2 Ulimwenguni pote, watu wa Yehova huzungumza lugha nyingi tofauti-tofauti. Hata hivyo, hilo halituzuii kumsifu kwa umoja Baba yetu, Yehova. (Ufu. 7:9) Hata iwe tunazungumza lugha gani au tunaishi wapi, sote tunaweza “[kuangaza] kama mianga katika ulimwengu.”​—Flp. 2:15.

3 Ongezeko tunaloshuhudia, umoja tunaofurahia, mtazamo wa kuendelea kukesha tunaojitahidi kudumisha ni baadhi ya mambo yanayomletea Yehova utukufu. Katika makala hii, tutachunguza jinsi mambo hayo yanavyoweza kutusaidia kuacha nuru yetu iendelee kuangaza.​—Soma Mathayo 5:14-16.

WASAIDIE WENGINE WAMWABUDU YEHOVA

4, 5. (a)  Zaidi ya kuhubiri, tunaweza kufanya mambo gani mengine ili kuacha nuru yetu iangaze? (b) Tunaweza kupata manufaa gani kwa kuwa wenye urafiki? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

4 “Hakuna mtu anayeweza kuwa mwaminifu na mnyoofu kwa Bwana katika siku hizi zilizosalia . . . isipokuwa atumie fursa aliyo nayo ya kuacha nuru yake iangaze.” Hayo yalikuwa maneno kwenye makala yenye kichwa “Nuru Katika Giza,” iliyochapishwa kwenye gazeti la Mnara wa Mlinzi la Juni 1, 1925 la Kiingereza. Makala hiyo iliendelea kueleza hivi: “Lazima mtu huyo afanye hivyo kwa kuwatangazia habari njema watu duniani, na kwa kuishi kulingana na njia za nuru.” Hivyo, ni wazi kwamba njia moja ya kuacha nuru yetu iangaze ni kwa kuhubiri habari njema na kufanya wanafunzi. (Mt. 28:19, 20) Pia, tunaweza kumtukuza Yehova kupitia mwenendo wetu wa Kikristo. Wenye nyumba na wapita-njia hutazama jinsi tunavyojiendesha. Tunapotabasamu kwa urafiki na kuwasalimu watu kwa uchangamfu, tunawasaidia wajue sisi ni watu wa aina gani na ni Mungu wa aina gani tunayemwabudu.

5 Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Mnapoingia katika nyumba, wasalimuni watu wa nyumba hiyo.” (Mt. 10:12) Katika eneo ambalo Yesu na mitume wake walizoea kuhubiri, lilikuwa jambo la kawaida kwa watu kuwakaribisha wageni nyumbani mwao. Leo, watu katika maeneo mengi hawana desturi hiyo. Ingawa hivyo, mtazamo wako mzuri na wenye urafiki unapowaeleza kusudi la ziara yako unaweza kumwondolea wasiwasi mwenye nyumba na kumfanya atulie. Mara nyingi, tabasamu ya kirafiki huweka msingi mzuri wa mazungumzo. Na ndugu na dada wamejionea wazi jambo hilo wanaposhiriki katika mahubiri ya hadharani kwa kutumia kigari cha machapisho. Unaposhiriki katika aina hiyo ya utumishi, huenda ukatambua kwamba watu huitikia vizuri unapotabasamu na kuwasalimu kwa uchangamfu. Mambo hayo yanaweza kuwachochea wakaribie na kuchukua machapisho yetu na pia yanaweza kukusaidia uanzishe mazungumzo.

6. Wenzi fulani wa ndoa wenye umri mkubwa walipanuaje utumishi wao?

6 Wenzi fulani wa ndoa wenye umri mkubwa kutoka Uingereza wana matatizo ya afya ambayo huwazuia kushiriki kikamili katika huduma ya nyumba kwa nyumba. Licha ya hilo, waliamua kuacha nuru yao iangaze kwa kuhubiri nje ya nyumba yao. Walitoa nje meza na kuweka baadhi ya machapisho yanayotegemea Biblia wakati ambapo wazazi huja kuwachukua watoto wao kwenye shule iliyo jirani. Wengi wao wamechukua nakala za kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1 na la 2, na vilevile broshua. Dada painia katika kutaniko lao alijiunga nao kwenye mpango huo wa mahubiri. Utu wake wenye urafiki na bidii ya kutoka moyoni ya wenzi hao ilimchochea mmoja wa wazazi hao aanze kujifunza Biblia.

7. Unaweza kuwasaidiaje wageni walio katika eneo lenu?

7 Katika miaka ya karibuni, nchi nyingi zimekuwa na idadi kubwa ya wakimbizi. Unaweza kufanya nini ili kuwasaidia wamjue Yehova na kusudi lake? Kwanza, kwa nini usijifunze salamu katika lugha ambazo huzungumzwa na wageni walio katika eneo lenu? Programu ya JW Lugha inaweza kukusaidia kufanya hivyo. Pia, kwa nini usijifunze maneno machache yatakayonasa fikira zao ili wakusikilize? Kwa kufanya hivyo huenda ukafaulu kuwaelekeza kwenye Tovuti ya jw.org na kuwaonyesha video na machapisho mbalimbali yanayopatikana katika lugha yao.​—Kum. 10:19.

8, 9. (a) Tunapokea msaada gani mzuri katika mikutano yetu ya katikati ya juma? (b) Wazazi wanaweza kuwasaidiaje watoto wao kushiriki katika mikutano?

8 Kwa upendo Yehova ameandaa Mkutano wa Maisha na Huduma ili tupate matokeo mazuri zaidi katika huduma ya shambani. Mapendekezo mazuri tunayopokea katika mikutano hiyo hutufanya tusiwe na wasiwasi tunapofanya ziara za kurudia na kuongoza mafunzo ya Biblia.

9 Wapya wengi wameona kwamba watoto wetu hutoa maelezo kwenye mikutano. Wazazi, wasaidieni watoto wenu waache nuru yao iangaze kwa kuwafundisha kutoa maelezo kwa maneno yao wenyewe. Nyakati nyingine maelezo yao rahisi na yanayotoka moyoni yamewachochea wapya kutambua hii ndiyo kweli.​—1 Kor. 14:25.

ENDELEZA UMOJA

10. Ibada ya familia huchangiaje umoja katika familia?

10 Njia nyingine ya kuacha nuru yako iangaze ni kwa kuendeleza umoja katika familia yako na kutaniko lako. Wazazi wanaweza kufanya hivyo kwa kupanga kuwa na Ibada ya Familia kwa ukawaida. Wengi wao hupanga kutazama programu ya JW Broadcasting kila mwezi. Baada ya kutazama programu hiyo, kwa nini msitumie wakati kuzungumzia jinsi mtakavyotumia maishani mambo yaliyozungumziwa? Wanapoongoza ibada ya familia, wazazi wanapaswa kukumbuka kwamba mwongozo ambao mtoto mdogo anahitaji hutofautiana na ule ambao tineja anahitaji. Zungumzieni jinsi habari mlizojifunza zinavyomhusu kila mmoja katika familia ili wote wanufaike.​—Zab. 148:12, 13.

Tunajengwa tunapotumia wakati wetu pamoja na ndugu na dada wenye umri mkubwa (Tazama fungu la 11)

11-13. Wote kutanikoni wanaweza kuendelezaje umoja na kuwasaidia wengine waangaze nuru yao?

11 Vijana wanaweza kuendelezaje umoja katika kutaniko na hivyo kuwatia moyo wengine waangaze nuru yao? Ikiwa wewe ni kijana Mkristo, kwa nini usijiwekee lengo la kuwafahamu vizuri zaidi ndugu na dada wenye umri mkubwa? Kwa heshima, unaweza kuwaomba wakusimulie jambo fulani walilojionea katika utumishi wao kwa Yehova. Utatiwa moyo sana, na nyote mtachochewa hata zaidi kuacha nuru ya kweli iangaze. Na sote tunaweza kujiwekea lengo la kuwakaribisha kwa uchangamfu wale wanaohudhuria mikutano kwenye Jumba la Ufalme. Ukifanya hivyo, utaendeleza umoja na huenda hata ukawachochea wageni watamani kuanza kuangaza nuru. Unaweza kuwakaribisha wageni kwa kuwasalimu huku ukitabasamu kwa uchangamfu, au hata kuwasaidia wapate mahali pa kuketi. Jaribu kuwatambulisha kwa wengine ili wajihisi wakiwa wamekaribishwa.

12 Ikiwa umepewa mgawo wa kuongoza mkutano wa utumishi wa shambani, kuna mambo mengi unayoweza kufanya ili kuwasaidia ndugu na dada wenye umri mkubwa kushiriki katika utumishi. Je, wana eneo la kuhubiri linalowafaa? Katika visa vingine, unaweza kupanga waambatane pamoja na mhubiri mwingine mwenye umri mdogo kuliko wao ili aweze kuwasaidia. Pia, jitahidi kuonyesha kwamba unawajali wale ambao afya na hali zao haziwaruhusu kutimiza mengi. Naam, unapokuwa mwenye ufikirio na utambuzi unaweza kuwasaidia vijana kwa wazee, walio na uzoefu na wasio na uzoefu, kuhubiri habari njema kwa bidii.​—Law. 19:32.

13 Mtunga zaburi alichochewa kusema hivi: “Jinsi ilivyo vema na jinsi inavyopendeza ndugu kukaa pamoja kwa umoja!” (Soma Zaburi 133:1, 2.) Waisraeli walipokusanyika pamoja, walinufaika sana kwa kushirikiana na wengine waliomwabudu Yehova. Mtunga zaburi alilinganisha umoja huo na mafuta yaliyotumiwa kutia mafuta ambayo yalikuwa na harufu nzuri na yaliburudisha ngozi. Kwa nini usijiwekee lengo la kuwaburudisha wengine kwa kuendeleza umoja miongoni mwa ndugu na dada zako? Ikiwa tayari unafanya hivyo, unastahili pongezi. Je, unaweza ‘kupanuka,’ yaani, kuwafahamu vizuri zaidi ndugu na dada wengi zaidi?​—2 Kor. 6:11-13, maelezo ya chini.

14. Unaweza kufanya nini ili uache nuru yako iangaze mahali unapoishi?

14 Vipi kuhusu kuongeza jitihada zako za kuiacha nuru yako iangaze mahali unapoishi? Maneno na matendo yako ya fadhili yanaweza kuwavuta majirani wako kwenye kweli. Jiulize hivi: ‘Majirani wangu wana maoni gani kunihusu? Je, nyumba na mazingira ya nyumbani kwangu ni safi, na hivyo kulifanya eneo ninaloishi lionekane kuwa lenye kupendeza hata zaidi? Je, ninachukua hatua ya kwanza kuwasaidia wengine?’ Unapozungumza na Mashahidi wenzako, kwa nini usiwaulize jinsi matendo na mwenendo wao mzuri ulivyowafanya watu wa ukoo, majirani, wafanyakazi, au wanafunzi wenzao wabadili maoni yao? Kuna uwezekano mkubwa kwamba watakusimulia mambo mazuri waliyojionea.​—Efe. 5:9.

ENDELEENI KUKESHA

15. Kwa nini ni muhimu kuendelea kukesha?

15 Tunapojitahidi kuacha nuru yetu iangaze ni vizuri kukumbuka kwamba mtazamo wetu pia unahusika. Yesu aliwahimiza wanafunzi wake hivi tena na tena: “Endeleeni kukesha.” (Mt. 24:42; 25:13; 26:41) Ni wazi kwamba ikiwa tunaamini kwamba “dhiki kuu” iko mbali sana, yaani, haitakuja katika kipindi hiki tunachoishi, tutakosa hisi ya uharaka kuhusiana na kazi ya kuhubiri. (Mt. 24:21) Badala ya nuru yetu kung’aa kwa uangavu katika eneo tunaloishi, itafifia na huenda hata ikazimika.

16, 17. Tunaweza kufanya nini ili tuendelee kudumisha mtazamo wa kuendelea kukesha?

16 Kadiri siku hizi za mwisho zinavyozidi kuwa mbaya, sisi sote tunahitaji kuendelea kukesha. Yehova atakapochukua hatua, atafanya hivyo kwa wakati barabara. Hatuna shaka kuhusu hilo. (Mt. 24:42-44) Kwa sasa, uwe na subira na uendelee kukesha. Soma Neno la Mungu kila siku na uendelee kuwa macho kwa kusali bila kuacha. (1 Pet. 4:7) Iga mifano bora ya ndugu na dada ambao wanaonyesha kupitia maisha yao shangwe wanayopata kwa kuendelea kukesha na kuacha nuru yao iangaze. Mfano mmoja mzuri umesimuliwa katika makala yenye kichwa “Miaka Sabini ya Kushikilia Upindo wa Nguo ya Mtu Aliye Myahudi,” iliyochapishwa katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Aprili 15, 2012, ukurasa wa 18-21.

17 Tumia muda mwingi kufanya mambo yenye kujenga na kushirikiana pamoja na ndugu na dada zako. Kufanya hivyo kutakuletea shangwe nyingi, na wakati utaonekana kuwa unapita haraka. (Efe. 5:16) Katika kipindi cha miaka 100 iliyopita, ndugu zetu wamekuwa na shughuli nyingi na wametimiza mengi. Lakini tunatimiza mambo mengi zaidi leo kwa mkono wa Yehova unaotuongoza. Tunaacha nuru yetu iangaze kwa kiwango ambacho hatungewahi kamwe kuwazia.

Ziara za uchungaji hutupatia fursa za kunufaika na hekima ya Neno la Mungu (Tazama fungu la 18 na 19)

18, 19. Wazee wa kutaniko wanaweza kutusaidiaje tuendelee kuwa macho na wenye bidii? Toa mfano.

18 Imani yetu inaimarishwa sana kujua kwamba ingawa sisi si wakamilifu bado tunaweza kumtumikia Yehova kwa njia inayokubalika. Hivyo basi, onyesha kwamba unathamini mpango wa Yehova wa kuwa na wazee wa kutaniko ambao ni “wanaume [wakiwa] zawadi.” (Soma Waefeso 4:8, 11, 12.) Mzee wa kutaniko atakapokutembelea, tumia fursa hiyo kunufaika na hekima na ushauri wake.

19 Wazee wawili wa kutaniko nchini Uingereza walikubali kuwatembelea wenzi fulani wa ndoa walioomba msaada kwa sababu walikuwa na matatizo katika ndoa yao. Mke alihisi kwamba mume wake alipuuza jukumu lake la kuiongoza familia yake katika mambo ya kiroho. Mume wake alikiri kwamba hakuwa mwalimu stadi na hakupanga ratiba ya kuwa na ibada ya familia kwa ukawaida. Wazee hao waliwasaidia wenzi hao kutafakari kuhusu mfano wa Yesu. Yesu aliwatunza wanafunzi wake na alizingatia mahitaji yao. Wazee walimhimiza mume huyo aige mfano wa Yesu na kumtia moyo mke wake awe na subira. Pia waliwapa wenzi hao mapendekezo ambayo yangewasaidia kushirikiana ili wawe na ibada ya familia pamoja na watoto wao wawili. (Efe. 5:21-29) Baadaye, wazee hao wa kutaniko walimpongeza mume huyo kwa jitihada zake. Walimtia moyo asikate tamaa na aendelee kutegemea roho takatifu imsaidie kuwa mume anayeiongoza vizuri familia yake katika mambo ya kiroho. Upendo na msaada wa wazee hao ulisaidia familia hiyo iendelee kuacha nuru yao iangaze.

20. Unaweza kutarajia nini unapoendelea kuacha nuru yako iangaze?

20 Mtunga zaburi aliimba hivi: “Mwenye furaha ni kila mtu anayemwogopa Yehova, anayetembea katika njia Zake.” (Zab. 128:1) Unapoacha nuru yako iangaze kwa kuwasaidia wengine kumwabudu Mungu, kwa kujiendesha kwa njia inayoendeleza umoja, na kwa kudumisha mtazamo wa kuendelea kukesha, shangwe yako itaongezeka. Wengine wataona matendo yako mazuri, na wengi watachochewa kumtukuza Baba yetu.—Mt. 5:16.