Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Angeweza Kuwa na Kibali cha Mungu

Angeweza Kuwa na Kibali cha Mungu

TUNAMTUMIKIA Yehova na tungependa kupata kibali chake, sivyo? Lakini Mungu humpa nani kibali na baraka zake? Baadhi ya watu katika nyakati za Biblia walifurahia kuwa na kibali cha Mungu ingawa mwanzoni walikuwa wamefanya dhambi nzito. Wengine waliokuwa na sifa nzuri hawakupata kibali cha Mungu. Hivyo huenda tukajiuliza, “Yehova anatazamia nini hasa kutoka kwa kila mmoja wetu?” Simulizi la Rehoboamu, mfalme wa Yuda, linaweza kutusaidia kupata jibu.

MWANZO WENYE MSUKOSUKO

Sulemani alikuwa baba ya Rehoboamu, naye alitawala Israeli kwa miaka 40. (1 Fal. 11:42) Sulemani alikufa mwaka wa 997 K.W.K. Kisha Rehoboamu akasafiri kutoka Yerusalemu na kwenda Shekemu, upande wa kaskazini ili awekwe kuwa mfalme. (2 Nya. 10:1) Je, unamwona Rehoboamu akiwa na shaka ikiwa angefaulu kufuata hatua za Sulemani baba yake, aliyejulikana kwa hekima yake ya pekee? Punde si punde, Rehoboamu angehitaji kuthibitisha kwamba alikuwa na hekima ya kutosha ya kushughulikia matatizo magumu.

Hapana shaka kwamba Rehoboamu alitambua kuwa mambo hayakuwa rahisi katika nchi ya Israeli. Muda si muda, wawakilishi wa watu walimfikia na kuwasilisha mahangaiko yao mbele yake. Walimwambia: “Baba yako aliifanya nira yetu kuwa nzito. Lakini ukiufanya utumishi mzito wa baba yako kuwa mwepesi zaidi na kupunguza nira nzito aliyotutwika, tutakutumikia.”​—2 Nya. 10:3, 4.

Rehoboamu alihitaji kufanya uamuzi mzito! Ikiwa angefanya mambo ambayo watu walimwomba afanye, basi yeye, familia yake, na watu wengine katika makao ya mfalme, wangelazimika kupunguza mambo fulani ya starehe na wangelazimika kudai machache kutoka kwa watu. Kwa upande mwingine, ikiwa angekataa kutimiza maombi hayo, huenda watu wangeasi. Basi, angefanya nini? Mfalme huyo mpya aliamua kwanza kuwaomba ushauri wanaume wazee ambao walikuwa washauri wa Sulemani. Lakini Rehoboamu akaamua pia kuwaomba ushauri vijana wa rika lake. Alifuata ushauri wao na kuamua kuwatesa watu. Aliwaambia hivi: “Nitafanya nira yenu iwe nzito zaidi, nami nitazidisha uzito wake. Baba yangu aliwaadhibu kwa mijeledi, lakini mimi nitawaadhibu kwa mijeledi yenye miiba.”​—2 Nya. 10:6-14.

Je, tunajifunza somo lolote? Ni wazi kwamba ni jambo la hekima kuwasikiliza ndugu na dada wenye umri mkubwa ambao wamekomaa kiroho. Kwa kuwa wana uzoefu mwingi, wanaweza kutambua matokeo ya uamuzi fulani na kutupatia ushauri mzuri.​—Ayu. 12:12.

“WAKALITII NENO LA YEHOVA”

Ili kupambana na uasi uliokuwa umetokea, Rehoboamu alikusanya jeshi lake. Lakini Yehova akaingilia kati kupitia nabii Shemaya na kusema: “Msipande kwenda kupigana na ndugu zenu Waisraeli. Kila mmoja wenu anapaswa kurudi nyumbani kwake, kwa maana nimesababisha mambo haya yatukie.”​—1 Fal. 12:21-24. *

Rehoboamu aliagizwa asithubutu kuwashambulia! Unaweza kuwazia jinsi jambo hilo lilivyomtaabisha! Watu wangemwonaje mfalme huyo aliyekuwa amewaambia kwamba angewaadhibu “kwa mijeledi yenye miiba” lakini ambaye sasa hangefanya lolote kuhusiana na uasi mkubwa uliokuwa umetokea? (Linganisha 2 Mambo ya Nyakati 13:7.) Bila kujali watu wangemwonaje, mfalme na majeshi yake “wakalitii neno la Yehova na kurudi nyumbani, kama Yehova alivyowaambia.”

Tunajifunza nini? Ni jambo la hekima kumtii Mungu hata ikiwa kufanya hivyo kunaweza kusababisha tudhihakiwe. Sikuzote tunapomtii Mungu tutapata kibali na baraka zake.​—Kum. 28:2.

Mwishowe hali ilikuwaje kwa Rehoboamu? Alionyesha utii kwa kuachilia mbali mpango wake wa kulishambulia taifa jipya lililokuwa limeanzishwa, na kuelekeza fikira zake katika mradi wa kujenga majiji katika maeneo ya makabila ya Yuda na Benjamini yaliyokuwa chini ya utawala wake. Akaimarisha majiji kadhaa “kwa kiwango kikubwa sana.” (2 Nya. 11:5-12) Jambo muhimu hata zaidi ni kwamba kwa kipindi fulani alishikamana na sheria za Yehova. Ufalme wa Israeli wa makabila kumi uliokuwa chini ya utawala wa Yeroboamu ulipoanza kujihusisha na ibada ya sanamu, watu wengi wa ufalme huo ‘walimuunga mkono Rehoboamu’ kwa kusafiri hadi Yerusalemu ili kuunga mkono ibada safi. (2 Nya. 11:16, 17) Hivyo, utii wa Rehoboamu uliimarisha ufalme wake.

DHAMBI NA TOBA YA REHOBOAMU

Ufalme wa Rehoboamu ulipokuwa umeimarika kabisa, alifanya jambo fulani ambalo halikutazamiwa. Aliacha sheria ya Yehova na kuanza kuabudu miungu ya kipagani! Kwa nini? Je, alifanya hivyo kwa sababu ya kuathiriwa na mama yake aliyekuwa Mwamoni? (1 Fal. 14:21) Haidhuru alikuwa na sababu gani, taifa lote lilimfuata. Hivyo, Yehova akamruhusu Mfalme Shishaki wa Misri ayateke majiji mengi ya Yuda, licha ya kwamba Rehoboamu alikuwa ameyaimarisha!​—1 Fal. 14:22-24; 2 Nya. 12:1-4.

Mambo yalizidi kuwa mabaya Shishaki alipofika Yerusalemu ambako Rehoboamu alikuwa akitawala. Wakati huo, nabii Shemaya alimpa Rehoboamu na wakuu wake ujumbe huu kutoka kwa Mungu: “Mmeniacha mimi, nami pia nimewaacha ninyi mikononi mwa Shishaki.” Rehoboamu aliitikiaje ujumbe huo wa nidhamu? Aliitikia vizuri sana! Biblia inasema hivi: “Wakuu wa Israeli na mfalme wakajinyenyekeza na kusema: ‘Yehova ni mwadilifu.’” Kwa sababu hiyo, Yehova alimwokoa Rehoboamu na jiji la Yerusalemu dhidi ya maangamizi.—​2 Nya. 12:5-7, 12.

Baada ya hayo, Rehoboamu aliendelea kutawala ufalme wa kusini. Kabla ya kifo chake, alionyesha ukarimu kwa kuwapa wanawe zawadi nyingi, labda ili kuzuia uasi dhidi ya utawala wa Abiya ndugu yao, ambaye angechukua mahali pake. (2 Nya. 11:21-23) Kwa kufanya hivyo, Rehoboamu alionyesha ufahamu ambao hakuwa ameuonyesha hapo awali.

JE, ALIKUWA MWEMA AU MWOVU?

Ingawa Rehoboamu alifanya mambo fulani mazuri, alishindwa kupata kibali cha Mungu. Biblia inasema hivi kuhusu utawala wake kwa ujumla: “Alitenda maovu.” Kwa nini? Kwa sababu “hakuwa ameazimia moyoni mwake kumtafuta Yehova.”​—2 Nya. 12:14.

Tofauti na Mfalme Daudi, Rehoboamu hakusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova

Fikiria kinachomaanishwa na jambo hilo: Pindi fulani-fulani, Rehoboamu alimtii Mungu. Na alifanya mambo fulani mazuri kwa ajili ya taifa la Yehova. Lakini hakusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova wala hakusitawisha tamaa yenye nguvu ya kumpendeza. Hivyo, akatenda dhambi na kujihusisha na ibada ya uwongo. Huenda sasa unajiuliza: ‘Rehoboamu alipokubali kurekebishwa na Mungu, je, alifanya hivyo kwa sababu ya kushinikizwa na wengine au kwa sababu alitubu kutoka moyoni na alichochewa na tamaa ya kumpendeza Mungu?’ (2 Nya. 11:3, 4; 12:6) Baadaye maishani mwake, alianza tena kutenda maovu. Alikuwa tofauti kabisa na Mfalme Daudi, babu yake! Naam, ni kweli kwamba Daudi alifanya makosa, lakini maisha yake yalionyesha kwamba alimpenda Yehova, alijitoa kwa ajili ya ibada ya kweli, na alitubu kikweli alipotenda dhambi.​—1 Fal. 14:8; Zab. 51:1, 17; 63:1.

Tunajifunza somo kutoka kwa Rehoboamu. Ni jambo linalostahili pongezi mtu anapoiandalia familia yake mahitaji na kujitahidi kutimiza mambo fulani mazuri. Lakini ili tuwe na kibali cha Mungu, kwanza kabisa ni lazima tutegemeze ibada ya kweli na kushikamana nayo.

Tutafanikiwa kufanya hivyo ikiwa tutasitawisha upendo wenye kina kumwelekea Yehova. Kama tu ambavyo sisi huchochea moto ili uendelee kuwaka, tunahitaji kuendelea kuchochea upendo wetu kwa Mungu kwa kujifunza Neno lake kwa ukawaida, kutafakari mambo tunayosoma, na kudumu katika sala. (Zab. 1:2; Rom. 12:12) Kisha upendo wetu kwa Yehova utatuchochea kuwa na tamaa ya kumpendeza katika kila jambo tunalofanya. Pia, utatuchochea kutubu kikweli tunapohitaji kufanya hivyo. Tofauti na Rehoboamu, tutaendelea kushikamana na ibada ya kweli.​—Yuda 20, 21.

^ fu. 9 Kwa sababu Sulemani alikosa kuwa mwaminifu, Mungu alikuwa ameonyesha kwamba ufalme wake ungegawanyika.​—1 Fal. 11:31.