Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unakumbuka?

Je, Unakumbuka?

Je, umesoma kwa makini matoleo ya hivi karibuni ya Mnara wa Mlinzi? Ona ikiwa unaweza kujibu maswali yafuatayo:

Ni mambo gani manne tunayoweza kufanya ili kuboresha uimbaji wetu?

Tunaweza kusimama vizuri kwa kuinua juu kitabu chetu cha nyimbo. Tunapaswa kupumua vizuri. Tunapofungua mdomo wetu wazi na kuimba kwa sauti kubwa, tutafanikiwa kuimba vizuri.​—w17.11, uku. 5.

Ni nini kinachotuvutia kuhusu mahali ambapo majiji ya makimbilio katika taifa la Israeli yalipatikana na barabara zilizoelekea kwenye majiji hayo?

Kulikuwa na majiji sita ya makimbilio yaliyotawanyika kotekote katika nchi ya Israeli, na kulikuwa na barabara nzuri zilizoelekea kwenye majiji hayo. Hivyo, ilikuwa rahisi kwa mkimbizi kukimbilia huko haraka na kupata usalama.​—w17.11, uku. 14.

Kwa nini zawadi ya Mungu ya fidia kupitia Yesu ndiyo zawadi bora zaidi tunayoweza kupokea?

Inatosheleza tamaa yetu ya kuendelea kuishi, na inatimiza uhitaji wetu wa kukombolewa kutoka katika dhambi na kifo. Mungu aliwapenda sana wazao wa Adamu hivi kwamba akamtoa Yesu kwa ajili yetu tulipokuwa tungali watenda dhambi.​—wp17.6, uku. 6-7.

Zaburi 118:22 ilitabiri jinsi gani kuhusu kufufuliwa kwa Yesu?

Watu walimkataa Yesu kuwa Masihi na kisha wakamuua. Ili awe “jiwe kuu la pembeni,” lazima angefufuliwa.​—w17.12, uku. 9-10.

Je, wazaliwa wa kwanza tu ndio waliokuwa na haki ya kufanyiza ukoo uliomtokeza Masihi?

Baadhi ya watu walio katika ukoo uliomtokeza Yesu walikuwa wazaliwa wa kwanza, lakini si wote. Daudi hakuwa mwana wa kwanza wa Yese; ingawa hivyo, ukoo wa Masihi ulikuja kupitia Daudi.​—w17.12, uku. 14-15.

Biblia inataja baadhi ya kanuni zipi kuhusu tiba?

Chini ya Sheria, watu waliokuwa na magonjwa fulani walipaswa kutengwa mbali na wengine. Watu walipaswa kuoga baada ya kugusa maiti. Sheria iliagiza kwamba kinyesi kilipaswa kufunikwa mbali na makazi ya watu. Mtoto wa kiume alipaswa kutahiriwa siku ya nane baada ya kuzaliwa, kwani uwezo wa damu kuganda hufikia kiwango kinachofaa baada ya juma moja.​—wp18.1, uku. 7.

Kwa nini si vibaya kwa Mkristo kujipenda kwa kiwango kinachofaa?

Tunapaswa kuwapenda jirani zetu kama tunavyojipenda wenyewe. (Marko 12:31) Waume wanapaswa “kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe.” (Efe. 5:28) Ukweli ni kwamba kujipenda mwenyewe kunaweza kufikia hatua isiyofaa.​—w18.01, uku. 23.

Ni baadhi ya hatua zipi tunazoweza kuchukua ili kufanya maendeleo ya kiroho?

Tunahitaji kujifunza Neno la Mungu, kulitafakari, na kutumia mambo tunayojifunza. Pia, tunapaswa kuruhusu akili na moyo wetu uongozwe na roho takatifu na kukubali kwa shukrani msaada kutoka kwa wengine.​—w18.02, uku. 26.

Kwa nini unajimu na ubashiri si njia sahihi ya kujua kuhusu wakati ujao?

Kuna sababu kadhaa, lakini sababu kuu ni kwamba Biblia inashutumu mazoea hayo.​—wp18.2, uku. 4-5.

Tunapoalikwa kwenye mlo, tunapaswa kuuchukuliaje mwaliko huo?

Ikiwa tumekubali mwaliko fulani, tunapaswa kujitahidi kutimiza ahadi yetu. (Zab. 15:4) Hatupaswi kuvunja ahadi yetu bila sababu nzuri. Huenda aliyetukaribisha amejitahidi sana ili kuandaa mlo.​—w18.03, uku. 18.

Wanaume waliowekwa rasmi wanaweza kujifunza nini kutoka kwa Timotheo?

Timotheo aliwajali watu kikweli na alitanguliza mambo ya kiroho maishani. Alikuwa mwenye bidii katika mambo ya kiroho na alitumia maishani mambo aliyojifunza. Aliendelea kujizoeza na kutegemea roho takatifu ya Yehova. Wazee wa kutaniko na wengine pia wanaweza kuiga mfano wake.​—w18.04, uku. 13-14.