Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nguvu za Salamu

Nguvu za Salamu

“HABARI! Unaendeleaje?”

Hapana shaka kwamba umewahi kuwasalimu wengine hivyo. Huenda hata ulimkumbatia au kumpa mkono yule uliyemsalimu. Desturi na maneno yanayotumiwa katika salamu huenda yakatofautiana kutoka eneo moja hadi lingine, lakini mambo ya msingi kuhusu salamu ni yaleyale. Kwa kweli, kutowasalimu wengine au kutoitikia salamu huenda kukawafanya wahisi kwamba hatuwapendi au hatuna adabu.

Lakini si watu wote walio na mazoea ya kuwasalimu wengine. Baadhi ya watu husita kuwasalimu wengine kwa sababu wanaona haya au wanajiona kuwa duni. Wengine huona ni vigumu kuwasalimu watu wa jamii, tamaduni, au hali tofauti na yao. Ingawa hivyo, hata kuwasalimu wengine kifupi tu kunaweza kuwa na matokeo mazuri sana.

Jiulize hivi: ‘Kuwasalimu wengine kunaweza kutimiza nini? Na Neno la Mungu linaweza kunifundisha nini kuhusu salamu?’

WASALIMU “WATU WA NAMNA ZOTE”

Mtume Petro alipomkaribisha Kornelio, mtu wa kwanza wa Mataifa, katika kutaniko la Kikristo, alisema hivi: “Mungu hana ubaguzi.” (Mdo. 10:34) Baadaye, Petro aliandika kwamba Mungu “hutaka wote wafikie toba.” (2 Pet. 3:9) Huenda mwanzoni tukahisi kwamba maneno hayo yanamhusu mtu anayejifunza kweli. Lakini Petro aliwahimiza hivi Wakristo pia: “Waheshimuni watu wa namna zote, upendeni ushirika mzima wa akina ndugu.” (1 Pet. 2:17) Je, lisingekuwa jambo bora kwetu kuwasalimu wengine bila kujali rangi yao, utamaduni wao, au malezi yao? Kufanya hivyo ni mojawapo ya njia ya kuwaonyesha heshima na upendo.

Mtume Paulo aliwasihi hivi wale walio kutanikoni: “Mkaribishane, kama vile Kristo pia alivyowakaribisha.” (Rom. 15:7) Paulo alitaja kihususa majina ya akina ndugu ambao walithibitika kuwa ‘msaada wa kumtia nguvu.’ Leo, kuliko wakati mwingine wowote, ndugu na dada wanahitaji kutiwa nguvu hata zaidi kwa kuwa tunakabili shambulizi kali la Shetani dhidi ya watu wa Mungu.—Kol 4:11, maelezo ya chini; Ufu. 12:12, 17.

Mifano iliyo katika Biblia inaonyesha kwamba kuwasalimu wengine hutimiza mengi zaidi ya kuwafanya watu wajihisi wakiwa wamestarehe.

MANUFAA YA KUWASALIMU WENGINE

Wakati ulipofika wa uhai wa Mwana wa Mungu kuhamishiwa katika tumbo la uzazi la Maria, Yehova alimtuma malaika azungumze na Maria. Malaika alimwambia hivi: “Salamu, wewe uliyebarikiwa sana, Yehova yuko pamoja nawe.” Maria ‘alihangaishwa sana,’ kwa kuwa hakuelewa kwa nini malaika alizungumza naye. Malaika alipoona hilo, alimwambia Maria hivi: “Usiogope, Maria, kwa maana umepata kibali cha Mungu.” Alimweleza kwamba Mungu alikusudia amzae Masihi. Badala ya kuendelea kuhangaishwa na maneno hayo, Maria alionyesha utii kwa kusema hivi: “Tazama! Kijakazi wa Yehova! Na itendeke kwangu kulingana na tangazo lako.”​—Luka 1:26-38.

Lilikuwa pendeleo kubwa kwa malaika huyo kuwa mjumbe wa Yehova; hata hivyo hakujiona kuwa bora sana asiweze kuzungumza na mwanadamu asiye mkamilifu. Alianza kwa salamu. Je, tunaweza kujifunza jambo lolote? Tunapaswa kuwa tayari kuwasalimu wengine na kuwatia moyo. Kwa maneno machache tu, tunaweza kuwasaidia wengine na kuwapa uhakika kwamba kwa kweli wao pia ni watu wa Yehova.

Paulo alifahamiana na ndugu na dada wengi katika makutaniko yaliyokuwa Asia Ndogo na Ulaya. Barua zake zimejaa salamu nyingi kwa watu hususa. Tunajionea hilo tunaposoma Waroma sura ya 16. Wakristo wengi walipokea salamu kutoka kwa Paulo. Alimtaja Fibi, “dada yetu,” na kuwahimiza akina ndugu “[wamkaribishe] katika Bwana kwa njia inayowastahili watakatifu, na kumpa msaada wowote ambao huenda akahitaji.” Paulo aliwasalimu Priska na Akila akisema, “si mimi tu ninayewashukuru bali pia makutaniko yote ya mataifa.” Aliwasalimu wengine ambao leo hatujui sana habari zao—“Epaineto mpendwa wangu” na vilevile “Trifaina na Trifosa, wanawake wanaofanya kazi kwa bidii katika Bwana.” Naam, Paulo alikuwa tayari sikuzote kuwasalimu ndugu na dada zake.​—Rom. 16:1-16.

Wazia shangwe waliyopata kujua kwamba Paulo aliwakumbuka kwa upendo. Hapana shaka upendo wao kwa Paulo na miongoni mwao wenyewe uliongezeka! Ni wazi kwamba salamu hizo za upendo ziliwatia moyo Wakristo wengine na kuwasaidia waendelee kuwa imara katika imani. Naam, salamu zinazoonyesha kwamba tunapendezwa na wengine kikweli na zilizoambatanishwa na pongezi huimarisha urafiki na kuwaunganisha watumishi washikamanifu wa Mungu.

Paulo alipowasili katika bandari ya Puteoli akiwa njiani kuelekea Roma, Wakristo wa Roma walikuja kukutana naye. Paulo alipowaona kutoka mbali, “akamshukuru Mungu na kujipa moyo.” (Mdo. 28:13-15) Nyakati nyingine, huenda jambo tunaloweza kufanya ni kutabasamu tu au kuwapungia wengine mkono. Lakini hata salamu ya aina hiyo inaweza kumfariji mtu aliyeshuka moyo au aliye na huzuni.

MWANZO MZURI

Mwanafunzi Yakobo alihitaji kutoa shauri kali. Baadhi ya Wakristo walianza kufanya uzinzi wa kiroho kwa kuwa marafiki wa ulimwengu. (Yak. 4:4) Lakini ona jinsi Yakobo alivyoanza barua yake:

“Yakobo, mtumwa wa Mungu na wa Bwana Yesu Kristo, kwa yale makabila 12 yaliyotawanyika sehemu mbalimbali: Salamu!” (Yak. 1:1) Hapana shaka kwamba ilikuwa rahisi zaidi kwa wasomaji wake kusikiliza ushauri wake walipoona kupitia salamu yake kwamba Yakobo alijiona kuwa sawa nao mbele za Mungu. Naam, kuwasalimu wengine kwa unyenyekevu kunaweza kufanya iwe rahisi kuzungumzia hata mambo mazito.

Salamu nzuri yenye kugusa moyo, haidhuru ni fupi kadiri gani, inapaswa kutoka moyoni na kuonyesha tunawapenda wengine kikweli. Tunapaswa kuwasalimu watu kwa njia hiyo hata ikiwa inaonekana kana kwamba hawatazichukua kwa uzito. (Mt. 22:39) Pindi moja, dada mmoja huko Ireland aliwasili kwenye Jumba la Ufalme muda mfupi tu kabla ya mkutano kuanza. Alipokuwa akiharakisha kuingia ndani, ndugu mmoja aligeuka, akatabasamu na kusema: “Habari. Ninafurahi sana kukuona.” Hata hivyo, dada huyo aliingia tu na kuketi.

Majuma kadhaa baadaye, alimwendea ndugu huyo na kutaja kwamba kwa muda fulani amekuwa akikabiliana na hali fulani ngumu nyumbani. Alimwambia hivi: “Sikuwa na furaha hata kidogo jioni hiyo, na nilikuwa karibu sana kukosa kuja kwenye Jumba la Ufalme. Sikumbuki mambo mengi yaliyosemwa mikutanoni, ila tu salamu yako. Ulinifanya nihisi kuwa nimekaribishwa. Asante.”

Ndugu huyo hakujua salamu yake fupi ilikuwa na nguvu kadiri gani. Anasema hivi: “Dada huyo aliponiambia jinsi maneno hayo machache yalivyomgusa moyo, nilifurahi sana kwamba nilichukua hatua ya kumsalimu. Na hilo lilifanya mimi pia nihisi vizuri.”

Sulemani aliandika hivi: “Tupa mkate wako juu ya maji, kwa maana baada ya siku nyingi utaupata tena.” (Mhu. 11:1) Tunapotambua thamani ya kuwasalimu wengine, hasa Wakristo wenzetu, tutawafanya wajihisi vizuri na sisi pia tutajihisi vizuri. Hivyo, tusipuuze kamwe nguvu za salamu.