Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

Nimefarijiwa Katika Mahangaiko Yangu Yote

Nimefarijiwa Katika Mahangaiko Yangu Yote

Kwenye ukingo wa magharibi wa Mto Indus, ambao leo upo katika nchi ya Pakistan, ndipo ulipo mji wa kale wa Sukkur. Hapo ndipo nilipozaliwa Novemba 9, 1929. Karibu na kipindi hicho, mmishonari fulani kutoka Uingereza aliwapa wazazi wangu seti ya vitabu vilivyokuwa na rangi inayong’aa. Vitabu hivyo vinavyotegemea Biblia vilinisaidia sana kubadili maisha yangu na kuwa Shahidi wa Yehova.

VITABU hivyo kumi viliitwa seti ya upinde wa mvua. Nilipovichunguza, nilitambua kwamba vilikuwa na michoro mizuri iliyonisaidia kupiga picha akilini. Hivyo, tangu nilipokuwa na umri mdogo, nilisitawisha hamu ya kupata ujuzi mwingi kuhusu Biblia, ujuzi ambao ulipatikana kwenye mabuku hayo ya pekee.

Vita vya Pili vya Ulimwengu vilipokuwa karibu kufika nchini India, maisha yangu yalianza kuwa magumu. Wazazi wangu walitengana na baadaye wakatalikiana. Sikuelewa kwa nini watu wawili niliowapenda wangeachana. Nilivunjika moyo sana na kujihisi mpweke. Nilikuwa mtoto pekee katika familia yangu, hivyo nilihisi kwamba nilikosa faraja na msaada ambao nilihitaji kwelikweli.

Wakati huo mimi na Mama tuliishi Karachi, mji mkuu wa jimbo letu. Siku moja, Fred Hardaker, daktari mwenye umri mkubwa na ambaye alikuwa Shahidi wa Yehova, alitutembelea nyumbani. Alikuwa na imani sawa na ya mmishonari aliyetuletea vile vitabu kumi. Alimpendekezea Mama aanze kujifunza Biblia. Mama alikataa lakini akasema huenda mimi ningependa kujifunza Biblia. Na bila kukawia, juma lililofuata nikaanza kujifunza Biblia pamoja na Ndugu Hardaker.

Majuma machache baadaye, nikaanza kuhudhuria mikutano ya Kikristo iliyofanyiwa kwenye kliniki ya Ndugu Hardaker. Mashahidi 12 hivi wenye umri mkubwa walikutanika hapo kwa ajili ya ibada. Walinifariji na kunitunza kama mwana wao. Ningali ninakumbuka jinsi walivyoketi pamoja nami, walivyochuchumaa ili kunitazama usoni, na kuzungumza nami kama rafiki yao wa kweli, mambo ambayo niliyahitaji sana wakati huo.

Muda mfupi baadaye, Ndugu Hardaker alinialika niandamane naye kwenye huduma ya shambani. Alinifundisha jinsi ya kutumia gramafoni kucheza hotuba fupi za Biblia zilizorekodiwa. Hotuba fulani zilikuwa na ujumbe mkali, na baadhi ya wenye nyumba hawakupendezwa na ujumbe huo. Hata hivyo, nilisisimuka sana kuwahubiria watu. Nilikuwa mwenye bidii sana kwa ajili ya kweli ya Biblia na nilipenda kuwaeleza wengine kuihusu.

Majeshi ya Japani yalipozidi kukaribia India, serikali ya Uingereza iliendelea kufanya hali iwe ngumu zaidi kwa Mashahidi wa Yehova. Mwishowe, katika mwezi wa Julai 1943, mimi binafsi niliathiriwa na hali hiyo. Mwalimu mkuu wa shule niliyosomea ambaye alikuwa pia kasisi wa kanisa la Anglikana alinifukuza shuleni eti kwa sababu “tabia yangu haikuridhisha.” Alimwambia Mama kwamba kwa kuwa ninashirikiana na Mashahidi wa Yehova ninawawekea wanafunzi wengine mfano mbaya. Mama alishtuka sana na akanizuia kushirikiana na Mashahidi. Baadaye, alinisafirisha kwenda mji wa Peshawar ambako Baba aliishi, mji uliokuwa kilomita 1,370 upande wa kusini. Kwa kuwa sikupata chakula cha kiroho na ushirika wa kiroho, nikawa asiyetenda.

KURUDIA HALI NZURI YA KIROHO

Katika mwaka wa 1947, nilirudi Karachi ili kutafuta kazi. Nikiwa huko, nilimtembelea Dkt. Hardaker kwenye kliniki yake. Alinikaribisha kwa shangwe na furaha.

“Una tatizo gani?” akaniuliza, akifikiri kwamba nilikuja kupata ushauri wa kimatibabu.

“Daktari, mimi si mgonjwa kimwili,” nikamjibu. “Mimi ni mgonjwa kiroho. Ninahitaji kufundishwa Biblia.”

“Ungependa kuanza lini?” akauliza.

“Sasa hivi ikiwezekana,” nikajibu.

Tulifurahia sana kujifunza Biblia jioni hiyo. Nilihisi kana kwamba nimerudi nyumbani kwa sababu nilikuwa na watu wa Yehova tena. Mama alijitahidi sana kunizuia nisishirikiane na Mashahidi, lakini pindi hii nilikuwa nimeazimia kuifanya kweli iwe mali yangu. Katika mwezi wa Agosti 31, 1947, nilionyesha wakfu wangu kwa Yehova kwa kubatizwa. Punde baadaye, nikiwa na umri wa miaka 17, nikaanza kutumikia nikiwa painia wa kawaida.

NAFURAHIA UTUMISHI WA UPAINIA

Mgawo wangu wa kwanza ulikuwa kwenye jiji la Quetta, jiji ambalo hapo awali lilikuwa kituo cha majeshi ya Uingereza. Katika mwaka wa 1947, nchi ya Pakistan iligawanywa katika sehemu mbili—India na Pakistan. * Tukio hilo lilisababisha ukatili mkubwa wa kidini katika maeneo mbalimbali na mwishowe idadi kubwa sana ya watu walilazimika kuhama kuliko wakati mwingine wowote katika historia. Watu milioni 14 hivi walikimbia makwao. Waislamu walioishi India walihamia Pakistan, na Wahindu na Makalasinga walioishi Pakistan wakahamia India. Wakati wa vurugu hizo, nilipanda gari-moshi lililokuwa limejaa sana kutoka mji wa Karachi kwenda jiji la Quetta, hivyo kwa saa nyingi nililazimika kushikilia kwa shida chuma kilichokuwa upande wa nje wa gari-moshi.

Nilihudhuria kusanyiko la mzunguko huko India mwaka wa 1948

Katika jiji la Quetta, nilikutana na George Singh, painia wa pekee mwenye umri wa miaka 25 hivi. George alinipa baiskeli fulani iliyozeeka ambayo ningeendesha (au kusukuma) kwenye eneo hilo lenye milima-milima. Mara nyingi nilihubiri peke yangu. Baada ya miezi sita, nilikuwa nikiongoza mafunzo 17 ya Biblia, na baadhi ya wanafunzi hao walibatizwa. Sadiq Masih, mmoja wa wanafunzi hao aliyekuwa mwanajeshi, alinisaidia mimi na George kutafsiri baadhi ya machapisho yanayotegemea Biblia katika Kiurdu, lugha ya taifa ya Pakistan. Baada ya muda, Sadiq akawa mhubiri mwenye bidii wa habari njema.

Nikiwa kwenye meli ya Queen Elizabeth safarini kwenda Shule ya Gileadi

Baadaye, nilirudi Karachi na kutumikia pamoja na Henry Finch na Harry Forrest, waliokuwa wamishonari wapya kutoka Shule ya Gileadi. Walinipa mazoezi mazuri sana kuhusiana na mambo ya kitheokrasi! Pindi moja niliandamana na Ndugu Finch alipoenda kuhubiri katika eneo la kaskazini mwa Pakistan. Katika eneo tambarare chini ya safu ya milima ya eneo hilo, tulikuta wanakijiji wengi wanyenyekevu waliozungumza Kiurdu na waliokuwa na kiu ya kweli ya Biblia. Miaka miwili baadaye, mimi pia nilihudhuria Shule ya Gileadi, na kisha nikarudi Pakistan na kutumikia nikiwa mwangalizi wa mzunguko wa badala. Niliishi pamoja na ndugu wengine watatu wamishonari katika makao ya wamishonari katika jiji la Lahore.

NAJIFUNZA SOMO MUHIMU

Inasikitisha kwamba katika mwaka wa 1954, wamishonari hao walishindwa kuishi pamoja kwa amani, na hivyo ofisi ya tawi ikawapa migawo mipya. Kwa sababu ya kukosa hekima, nilipendelea upande mmoja katika ugomvi huo, nami nikashauriwa vikali. Nilivunjika moyo sana na kukata kauli kwamba sikustahili tena mgawo wangu wa kiroho. Nilirudi tena katika jiji la Karachi kisha nikahamia London, Uingereza, nikitumaini kuanza upya utumishi wangu katika eneo jipya.

Jijini London, kutaniko langu lilikuwa na washiriki wengi wa familia ya Betheli ya London. Pryce Hughes, mtumishi wa ofisi ya tawi mwenye fadhili alianza kunizoeza kwa upendo. Siku moja, alinisimulia kuhusu wakati ambapo alipokea shauri kali kutoka kwa Joseph F. Rutherford, ambaye wakati huo alikuwa akisimamia kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote. Ndugu Hughes alipojaribu kujitetea, Ndugu Rutherford alimkemea kwa ukali. Nilishangaa kuona Ndugu Hughes akitabasamu alipokumbuka jambo hilo. Alisema kwamba mwanzoni alikasirika. Lakini baadaye alitambua kwamba alihitaji shauri hilo thabiti na lilionyesha kuwa Yehova anampenda. (Ebr. 12:6) Maneno yake yalinigusa moyo na kunisaidia kupata tena usawaziko wa kiroho.

Karibu na kipindi hicho, Mama alihamia London na akakubali kujifunza Biblia na John E. Barr, ambaye baadaye alitumikia kwenye Baraza Linaloongoza. Alifanya maendeleo ya kiroho hatua kwa hatua na akabatizwa mwaka wa 1957. Baadaye, nilikuja kujua kwamba kabla ya kufa, Baba pia alijifunza na Mashahidi wa Yehova.

Katika mwaka wa 1958, nilimwoa Lene, dada kutoka Denmark aliyekuwa akiishi London. Mwaka uliofuata, tulibarikiwa kupata binti, Jane, mtoto wa kwanza kati ya watoto wetu watano. Pia, nilipata mapendeleo ya utumishi katika Kutaniko la Fulham. Hata hivyo, baada ya muda, kwa sababu ya afya mbaya ya Lene, tulihitaji kuhamia eneo lenye joto zaidi. Hivyo, katika mwaka wa 1967, tulihamia Adelaide, Australia.

MSIBA WENYE KUVUNJA MOYO

Kulikuwa na Wakristo watiwa-mafuta 12 wenye umri mkubwa katika kutaniko letu katika jiji la Adelaide. Walikuwa wenye bidii sana katika kazi ya kuhubiri. Bila kukawia, tukawa na ratiba nzuri ya mambo ya kiroho.

Katika mwaka wa 1979, mimi na Lene tulifurahi sana, Daniel, mtoto wetu wa tano alipozaliwa. Alikuwa ameathiriwa sana na ugonjwa wa Down syndrome * na hakutarajiwa kuishi kwa muda mrefu. Hata sasa ni vigumu sana kwangu kueleza maumivu makali ya kihisia tuliyopata. Tulijitoa kabisa ili kumtunza, na wakati uleule kuwatunza wale watoto wengine wanne. Nyakati nyingine, Daniel angebadilika rangi na kuwa bluu kwa sababu ya kukosa oksijeni, tatizo lililosababishwa na matundu mawili aliyokuwa nayo kwenye moyo, na hivyo tulihitaji kumkimbiza hospitali. Lakini licha ya hali yake mbaya ya afya, alikuwa na akili nyingi na aliwapenda sana watu. Pia, alipenda sana mambo ya kiroho. Familia yetu ilipokuwa ikisali kabla ya milo, angeifumbatisha mikono yake midogo, kutikisa kichwa na kusema “Amina!” kutoka moyoni. Na baada ya hapo ndipo tu angekula chakula chake.

Daniel alipokuwa na umri wa miaka minne, alipata ugonjwa wa lukemia. Mimi na Lene tulikuwa tumechoka sana kimwili na kihisia, nami nilihisi kuwa nilikuwa karibu sana kupatwa na matatizo ya akili. Lakini tulipokuwa tumeshuka moyo kabisa, Neville Bromwich, mwangalizi wetu wa mzunguko alikuja kututembelea. Usiku huo, alitukumbatia huku akitokwa na machozi. Sote tulilia. Maneno yake ya upendo na huruma yalitufariji sana. Aliondoka saa saba hivi usiku. Muda mfupi baadaye, Daniel alikufa. Kumpoteza Daniel ndio uliokuwa msiba uliotuhuzunisha zaidi maishani mwetu. Hata hivyo, tulivumilia huzuni yetu, tukiwa na uhakika kwamba hakuna chochote, hata kifo, ambacho kingeweza kumtenganisha Daniel na upendo wa Yehova. (Rom. 8:38, 39) Tunatamani sana kuwa pamoja naye atakapofufuliwa kwenye ulimwengu mpya wa Mungu!—Yoh. 5:28, 29.

KUPATA SHANGWE KWA KUWASAIDIA WENGINE

Leo, hata baada ya kupatwa na kiharusi mara mbili, bado ninatumikia nikiwa mzee wa kutaniko. Mambo niliyojionea maishani yamenifunza kuwaonyesha wengine hisia-mwenzi na huruma, hasa wale wanaopitia matatizo. Ninajitahidi kuepuka kuwahukumu. Badala yake, mimi hujiuliza hivi: ‘Mambo waliyopitia maishani yameathirije hisia zao na njia yao ya kufikiri? Ninaweza kuwaonyeshaje kwamba ninawajali? Ninaweza kuwatiaje moyo wafuate njia za Yehova?’ Ninapenda sana kufanya ziara za uchungaji kutanikoni! Kwa kweli, ninapowafariji na kuwaburudisha wengine kiroho, ninahisi kwamba ninajifariji na kujiburudisha mwenyewe.

Ninaendelea kufurahia kufanya ziara za uchungaji

Ninahisi kama mtunga zaburi aliyetangaza hivi: “Mahangaiko yaliponilemea, [Yehova alinifariji] na kunibembeleza.” (Zab. 94:19) Amenitegemeza chini ya hali ngumu za kifamilia, upinzani wa kidini, kukata tamaa kwa sababu ya makosa yangu mwenyewe, na kushuka moyo. Kwa kweli, Yehova amekuwa Baba halisi kwangu!

^ fu. 19 Mwanzoni, Pakistan Magharibi (ambayo sasa ni Pakistan) na Pakistan Mashariki (ambayo sasa ni Bangladesh) zilikuwa nchi moja, yaani, Pakistan.

^ fu. 29 Tazama makala yenye kichwa “Kulea Mtoto Aliye na Down Syndrome—Kazi Ngumu Inayothawabisha” kwenye gazeti la Amkeni! la Juni 2011.