Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuitikia Mwito wa Tarumbeta Leo

Kuitikia Mwito wa Tarumbeta Leo

SOTE tunaamini kwamba Yehova anawaongoza na kuwategemeza watu wake kiroho katika ‘siku hizi za mwisho.’ (2 Tim. 3:1) Lakini ni wajibu wa kila mmoja wetu kumtii Yehova. Tunaweza kulinganisha hali yetu na hali ya Waisraeli walipokuwa nyikani. Walipaswa kuitikia mwito wa tarumbeta.

Yehova alimwagiza Musa atengeneze tarumbeta mbili za fedha kwa kutumia nyundo ili azitumie “kuwakusanya watu na kuvunja kambi.” (Hes. 10:2) Makuhani walipaswa kupiga tarumbeta kwa njia mbalimbali ili kuwafahamisha watu jambo walilopaswa kufanya. (Hes. 10:3-8) Leo, watu wa Mungu hupata mwongozo kwa njia mbalimbali. Fikiria njia tatu kati ya hizo zinazotukumbusha kuhusu miito ya tarumbeta katika nyakati za Waisraeli. Leo, watu wa Mungu hupata mwaliko wa kuhudhuria makusanyiko makubwa, waangalizi waliowekwa rasmi hupata mazoezi, na miongozo ya kitheokrasi kwa ajili ya makutaniko yote hurekebishwa au kubadilishwa.

MWITO WA KUHUDHURIA MAKUSANYIKO MAKUBWA

Yehova alipowataka “Waisraeli wote” wakusanyike kwenye mlango wa hema la ibada upande wa mashariki, makuhani walipiga tarumbeta zote mbili. (Hes. 10:3) Makabila yote ambayo yalikuwa yamepiga kambi kuzunguka hema hilo katika makundi manne, yalisikia mwito huo wa pekee. Wale waliokuwa wamepiga kambi karibu na mlango wangeweza kufika baada ya dakika chache. Wengine walikuwa mbali zaidi na huenda walihitaji wakati na jitihada nyingi zaidi ili wafike. Vyovyote vile, Yehova aliwataka wote wakusanyike na kunufaika.

Leo, hatukusanyiki kwenye hema la ibada, lakini tunaalikwa kwenye makusanyiko ya watu wa Mungu. Makusanyiko hayo yanatia ndani makusanyiko ya eneo na matukio mengine ya pekee, ambapo tunapokea habari na miongozo muhimu. Kotekote ulimwenguni katika nchi mbalimbali, watu wa Yehova hufurahia programu ileile. Hivyo, wale wanaokubali mwaliko wa kuhudhuria hufurahia kushirikiana pamoja na kikundi kikubwa cha watu wenye furaha. Wengine wanahitaji kusafiri mbali zaidi ili kuhudhuria. Ingawa hivyo, wale wanaoitikia mwaliko huo wanakubali kwamba jitihada zao za kufanya hivyo si za bure.

Vipi kuhusu wale walio katika vikundi vilivyo mbali na mahali ambapo makusanyiko makubwa hufanywa? Kwa msaada wa teknolojia ya kisasa, idadi kubwa ya watu hao wanaweza kunufaika na programu hiyo na hata kuhisi kwamba wao pia ni sehemu ya wahudhuriaji wa makusanyiko hayo. Kwa mfano, wakati wa ziara ya mwakilishi kutoka makao makuu, ofisi ya tawi ya Benin ilirusha programu fulani mpaka Arlit, Niger, mji wa wachimba migodi ulio kwenye Jangwa la Sahara. Wahudhuriaji 21 waliotia ndani ndugu na dada, pamoja na watu wanaopendezwa walifurahia programu hiyo. Ingawa walikuwa katika eneo la mbali, walihisi wakiwa wameungana pamoja na kusanyiko kubwa lililokuwa na watu 44,131. Ndugu mmoja aliandika hivi: “Tunawashukuru sana kutoka moyoni kwa sababu ya kuturushia programu hii. Jambo hilo lilituonyesha kwa mara nyingine tena jinsi mnavyotupenda kutoka moyoni.”

MWITO KWA AJILI YA WAANGALIZI WALIOWEKWA RASMI

Makuhani Waisraeli walipopiga tarumbeta moja tu, ‘ni wakuu peke yao, yaani, viongozi wa maelfu’ waliopaswa kufika kwenye hema la mkutano. (Hes. 10:4) Wakiwa hapo wangeweza kupata mwongozo na mazoezi kutoka kwa Musa. Mambo hayo yangewasaidia kushughulikia majukumu yao katika makabila yao. Ikiwa ungekuwa mmoja wa wakuu hao, je, usingejitahidi kufanya yote uwezayo ili uhudhurie na kunufaika?

Leo, wazee wa kutaniko si “wakuu”; na pia hawapigi ubwana juu ya kundi la Mungu lililo chini ya utunzaji wao. (1 Pet. 5:1-3) Lakini bila shaka wanafanya yote wanayoweza ili kulichunga kundi. Hivyo, wao huwa tayari kukubali mwaliko wa kupata mazoezi zaidi, kwa mfano kupitia Shule ya Huduma ya Ufalme. Wanapokuwa katika mazoezi hayo, wazee hujifunza kuhusu jinsi wanavyoweza kushughulikia mambo ya kutaniko kwa njia nzuri zaidi. Matokeo ni kwamba hali ya kiroho ya wazee pamoja na wote kutanikoni huzidi kuongezeka. Hata ikiwa hujahudhuria mojawapo ya shule hizo, inaelekea kwamba unanufaika kupitia wale waliohudhuria.

MWITO WA KUFANYA MABADILIKO

Nyakati nyingine, makuhani Waisraeli walipiga tarumbeta kwa mlio uliobadilika-badilika. Mlio huo uliashiria kwamba Yehova alitaka kambi yote ianze safari. (Hes. 10:5, 6) Watu walipovunja kambi walifanya hivyo kwa utaratibu wa hali juu, na ilikuwa kazi kubwa sana kwa wote waliohusika. Nyakati nyingine huenda baadhi ya Waisraeli waliona kuwa vigumu kuitikia mwito huo. Kwa nini?

Huenda baadhi yao walihisi kwamba mwito wa kuhama ulitolewa mara nyingi mno na ghafla sana. “Nyakati fulani wingu hilo lilikaa juu ya hema la ibada kuanzia jioni mpaka asubuhi tu.” Nyakati nyingine liliinuka baada ya “siku mbili, mwezi mmoja, au muda mrefu zaidi” tangu walipopiga kambi mara ya mwisho. (Hes. 9:21, 22) Na kihalisi Waisraeli walivunja kambi mara ngapi? Kitabu cha Hesabu sura ya 33 kinataja maeneo 40 hivi ambapo Waisraeli walipiga kambi.

Nyakati nyingine, baadhi ya Waisraeli walipata eneo ambalo lilikuwa na kivuli. Hapana shaka kwamba Waisraeli hao walifurahia sana kivuli hicho katikati ya ‘nyika kubwa na yenye kutisha.’ (Kum. 1:19) Hivyo, huenda wangeshawishika kufikiri kwamba ikiwa wangehama hawangepata eneo zuri huko wanakokwenda.

Makabila yalipoanza kuhama, huenda baadhi ya Waisraeli waliona kuwa vigumu kusubiri zamu yao ifike. Wote walisikia mlio uliobadilika-badilika wa tarumbeta, lakini si wote wangeweza kuondoka wakati huohuo. Mlio huo uliobadilika-badilika wa tarumbeta uliashiria kwamba makabila yaliyopiga kambi upande wa mashariki, yaani, kabila la Yuda, Isakari, na Zabuloni, yalipaswa kuondoka. (Hes. 2:3-7; 10:5, 6) Baada ya makabila hayo kuondoka, makuhani walipiga kwa mara ya pili mlio uliobadilika-badilika wa tarumbeta kuashiria kwamba kundi la makabila matatu lililopiga kambi upande wa kusini lilipaswa kuondoka. Makuhani waliendelea kufanya hivyo mpaka kambi yote ilipokuwa imehama.

Huenda ilikuwa vigumu kwako kuunga mkono baadhi ya mabadiliko ya tengenezo. Kwa nini? Huenda ulihisi umelemewa na wingi wa mabadiliko yaliyokuja bila kutarajia. Au huenda ulifurahia jinsi mambo fulani yalivyokuwa yakifanywa na ulitamani mambo hayo yasibadilike. Au kwa sababu nyingine yoyote, huenda ulihisi subira yako ikijaribiwa, na ilichukua muda ili kuzoea hali hiyo mpya. Licha ya hayo, tukiazimia kutii kama tunavyopaswa kufanya, inaelekea tutatambua kwamba mabadiliko hayo yanatufaa na kwamba Yehova anatubariki.

Katika siku za Musa, Yehova aliongoza mamilioni ya wanaume, wanawake, na watoto waliposafiri kupitia nyikani. Wasingeweza kuokoka safari hiyo ikiwa Yehova hangewatunza na kuwaongoza. Leo, sisi huendelea kuwa hai kiroho kwa sababu ya mwongozo wa Yehova. Na si hivyo tu, tunanawiri kiroho! Hivyo, acheni sisi sote tuazimie kutii kama walivyofanya Waisraeli waaminifu, waliposikia mwito hususa wa tarumbeta!