Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Je, sifa za “tunda la roho” ni zile tu zinazotajwa kwenye Wagalatia 5:22, 23?

Mistari hiyo inaorodhesha sifa tisa za Kikristo: “Tunda la roho ni upendo, shangwe, amani, subira, fadhili, wema, imani, upole, kujizuia.” Hata hivyo, hizo si sifa nzuri pekee ambazo roho ya Mungu inaweza kutusaidia kusitawisha.

Ona kile ambacho mtume Paulo aliandika katika mistari iliyotangulia: “Matendo ya mwili . . . ni uasherati, uchafu, mwenendo mpotovu, ibada ya sanamu, kuwasiliana na roho, chuki, mizozo, wivu, milipuko ya hasira, migogoro, migawanyiko, madhehebu, husuda, ulevi, karamu zenye vurugu, na mambo kama hayo.” (Gal. 5:19-21) Hivyo, Paulo angeweza kuendelea kutaja mambo mengine ambayo pia ni “matendo ya mwili,” kama vile mambo yanayotajwa kwenye Wakolosai 3:5. Vivyo hivyo, baada ya kutaja sifa tisa nzuri, alisema hivi: “Hakuna sheria dhidi ya mambo [kama] hayo.” Kwa hiyo, Paulo hakuwa akiorodhesha sifa zote nzuri tunazoweza kusitawisha kwa msaada wa roho takatifu.

Jambo hilo linaonekana wazi tunapolinganisha orodha hiyo na mambo ambayo Paulo aliandikia kutaniko la Efeso: “Tunda la nuru lina kila namna ya wema na uadilifu na kweli.” (Efe. 5:8, 9) Ndiyo, “wema” ni sifa ya “tunda la nuru,” pamoja na uadilifu na kweli, lakini pia ni sifa ya “tunda la roho.”

Pia, Paulo alimhimiza Timotheo ‘afuatilie uadilifu, ujitoaji-kimungu, imani, upendo, uvumilivu, na upole’—sifa sita nzuri. (1 Tim. 6:11) Ni sifa tatu tu kati ya hizo, yaani, imani, upendo, na upole, zinazotajwa kuwa sifa za “tunda la roho.” Hata hivyo, Timotheo angehitaji pia msaada wa roho ili asitawishe sifa zile nyingine, yaani, uadilifu, ujitoaji-kimungu, na uvumilivu.​—Linganisha Wakolosai 3:12; 2 Petro 1:5-7.

Hivyo, andiko la Wagalatia 5:22, 23 haliorodheshi sifa zote ambazo Wakristo wanapaswa kusitawisha. Roho ya Mungu inaweza kutusaidia tusitawishe zile sifa tisa za “tunda la roho.” Lakini kuna sifa nyingine zaidi tunazohitaji kusitawisha ili tuwe Wakristo wakomavu na “kuvaa utu mpya ulioumbwa kupatana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na ushikamanifu.”​—Efe. 4:24.