Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 25

“Mimi Mwenyewe Nitawatafuta Kondoo Wangu”

“Mimi Mwenyewe Nitawatafuta Kondoo Wangu”

“Mimi mwenyewe nitawatafuta kondoo wangu na kuwatunza.”—EZE. 34:11.

WIMBO 105 “Mungu Ni Upendo”

MUHTASARI *

1. Ni katika njia gani Yehova ni kama mama anayenyonyesha?

“JE, MWANAMKE anaweza kumsahau mtoto wake anayenyonya?” Yehova aliuliza swali hilo katika siku za nabii Isaya. Mungu aliwaambia hivi watu wake: “Hata wanawake hawa wakisahau, mimi siwezi kamwe kukusahau.” (Isa. 49:15) Mara nyingi Yehova hajilinganishi na mama. Lakini alifanya hivyo pindi hiyo. Yehova alitumia uhusiano uliopo kati ya mama na mtoto wake kufunua jinsi anavyowapenda sana watumishi wake. Akina mama wengi wanakubaliana na maneno ya dada anayeitwa Jasmin, aliyesema, “Unapomnyonyesha mtoto wako, unasitawisha uhusiano wa pekee sana utakaodumu maisha yako yote.”

2. Yehova anahisije mmoja wa watoto wake anapoacha kumtumikia?

2 Yehova anajua wakati ambapo mmoja wa watoto wake anaacha kushirikiana na kutaniko la Kikristo na anaacha kufanya kazi ya kuhubiri. Hivyo, fikiria jinsi anavyoumia sana kila mwaka kuona maelfu ya watumishi wake wakiwa wahubiri wasiotenda. *

3. Yehova anataka nini?

3 Idadi kubwa ya ndugu na dada hao wapendwa ambao wameacha kutenda hurudi kutanikoni, na tunawakaribisha kwa uchangamfu! Yehova anataka warudi, na sisi pia tunataka warudi. (1 Pet. 2:25) Tunaweza kuwasaidiaje? Kabla ya kujibu swali hilo, ingefaa kwanza tujue sababu zinazowafanya baadhi ya ndugu na dada zetu waache kuhudhuria mikutano na kushiriki katika huduma.

KWA NINI BAADHI YA WATU HUACHA KUMTUMIKIA YEHOVA?

4. Kazi ya kimwili inaweza kuwaathirije baadhi ya watu?

4 Baadhi ya ndugu na dada wamezama katika kazi zao za kimwili. Hung, * ndugu anayeishi kusini-mashariki mwa bara la Asia anakiri hivi: “Niliruhusu kazi yangu ya kimwili ichukue wakati na nguvu zangu nyingi sana. Nilijidanganya kwamba ikiwa ningekuwa na hali nzuri ya kiuchumi, ningeweza kumtumikia Yehova kwa njia nzuri zaidi. Hivyo, nilifanya kazi kwa saa nyingi zaidi. Nikaanza kukosa mikutano mara nyingi zaidi, na hatimaye nikaacha kushirikiana na kutaniko. Inaonekana kwamba ulimwengu umekusudiwa kuwafanya watu waache kuwa karibu na Mungu hatua kwa hatua.”

5. Dada mmoja aliathiriwaje na mfululizo wa matatizo aliyopitia?

5 Baadhi ya ndugu na dada wamelemewa na matatizo. Anne, dada kutoka Uingereza ni mama mwenye watoto watano. Anaeleza hivi: “Mtoto wangu mmoja alizaliwa akiwa na ulemavu mkubwa. Baada ya muda, mmoja kati ya binti zangu alitengwa na ushirika na mwana wangu mwingine akapatwa na ugonjwa wa akili. Nilishuka moyo sana hivi kwamba nikaacha kuhudhuria mikutano na kuhubiri. Mwishowe nikawa mhubiri asiyetenda.” Tunahuzunika pamoja na Anne na familia yake na pia wengine ambao wanakabili changamoto kama hizo!

6. Kwa nini mtu anaweza kuacha kushirikiana na watu wa Yehova asipofuata ushauri wa Wakolosai 3:13?

6 Soma Wakolosai 3:13. Baadhi ya watumishi wa Yehova wameumizwa kihisia na waamini wenzao. Mtume Paulo alitambua kwamba nyakati fulani huenda tukawa na ‘sababu halali ya kulalamika juu ya’ ndugu au dada. Huenda hata tumetendewa isivyo haki. Tusipokuwa waangalifu, tunaweza kuwa na kinyongo. Hatimaye, hisia za uchungu zinaweza kumfanya mtu aache kushirikiana na watu wa Yehova. Fikiria kisa cha Pablo, ndugu kutoka Amerika Kusini. Alishtakiwa kwa uwongo kwamba amefanya kosa fulani, na kwa sababu hiyo akapoteza pendeleo la utumishi kutanikoni. Alitendaje? Pablo anasema hivi: “Nilikasirika, na hatua kwa hatua nikaacha kushirikiana na kutaniko.”

7. Dhamiri yenye hatia inaweza kumwathirije mtu?

7 Au dhamiri yenye hatia inaweza kumhangaisha sana mtu ambaye alivunja sheria ya Mungu wakati uliopita, na kumfanya ajihisi kwamba hastahili upendo wa Mungu. Hata kama alitubu na kuonyeshwa rehema, huenda akahisi kwamba sasa hafai tena kuwa miongoni mwa watu wa Mungu. Ndugu anayeitwa Francisco alihisi hivyo. Anasema hivi: “Nilikaripiwa kwa sababu ya kufanya uasherati. Ingawa mwanzoni niliendelea kuhudhuria mikutano, nilishuka moyo na kuhisi sistahili kuwa miongoni mwa watu wa Yehova. Dhamiri yangu ilinisumbua na nilisadiki kwamba Yehova hakuwa amenisamehe. Baada ya muda, niliacha kushirikiana na kutaniko.” Unahisije kuhusu ndugu na dada wanaokabili hali ambazo tumetoka tu kuzungumzia? Je, una hisia-mwenzi kuwaelekea? Na jambo muhimu zaidi ni, Yehova anahisije kuwahusu?

YEHOVA ANAWAPENDA KONDOO WAKE

Mchungaji Mwisraeli alimjali sana kondoo aliyepotea (Tazama fungu la 8 na 9) *

8. Je, Yehova huwasahau wale ambao wakati fulani walimtumikia? Eleza.

8 Yehova hawasahau wale ambao hapo awali walimtumikia, lakini kwa muda fulani wameacha kushirikiana na watu wake; pia, hasahau kazi ambayo wametimiza katika utumishi wake. (Ebr. 6:10) Nabii Isaya aliandika mfano mzuri unaoonyesha jinsi Yehova anavyowajali watu wake. Isaya aliandika hivi: “Atalitunza kundi lake kama mchungaji. Atawakusanya pamoja wanakondoo kwa mkono wake, naye atawabeba kwenye kifua chake.” (Isa. 40:11) Yehova, Mchungaji Mkuu, anahisije wakati mmoja wa kondoo wake anapoliacha kundi? Yesu alifunua hisia za Yehova alipowauliza hivi wanafunzi wake: “Mnaonaje? Mtu akiwa na kondoo 100 na mmoja apotee, je, hatawaacha wale 99 mlimani na kwenda kumtafuta yule aliyepotea? Naye akimpata, hakika ninawaambia, yeye humshangilia huyo kuliko wale 99 ambao hawakupotea.”—Mt. 18:12, 13.

9. Wachungaji wazuri katika nyakati za Biblia waliwatendeaje kondoo wao? (Tazama picha kwenye jalada.)

9 Kwa nini inafaa kumlinganisha Yehova na mchungaji? Kwa sababu mchungaji mzuri katika nyakati za Biblia aliwajali sana kondoo wake. Kwa mfano, Daudi alipambana na simba na dubu ili kuwalinda kondoo wake. (1 Sam. 17:34, 35) Bila shaka, mchungaji mzuri atatambua hata ikiwa kondoo mmoja anakosekana. (Yoh. 10:3, 14) Mchungaji wa namna hiyo atawaacha wale kondoo 99 mahali salama kwenye zizi au chini ya utunzaji wa wachungaji wenzake, na kwenda kumtafuta kondoo aliyepotea. Yesu alitumia mfano huo kutufundisha kweli hii muhimu: “Baba yangu aliye mbinguni hapendi hata mmoja wa hawa wadogo aangamie.”—Mt. 18:14.

Mchungaji Mwisraeli alimjali sana kondoo aliyepotea (Tazama fungu la 9)

YEHOVA HUWATAFUTA KONDOO WAKE

10. Kulingana na Ezekieli 34:11-16, Yehova aliahidi kuwafanyia nini kondoo wake waliopotea?

10 Yehova anampenda kila mmoja wetu, kutia ndani kondoo “wadogo” ambao wameliacha kundi lake. Kupitia nabii Ezekieli, Mungu aliahidi kwamba angewatafuta kondoo wake waliopotea na kuwasaidia wapate tena afya nzuri ya kiroho. Na alitaja hatua hususa ambazo angechukua ili kuwaokoa, hatua ambazo mchungaji Mwisraeli angechukua ikiwa kondoo wake alipotea. (Soma Ezekieli 34:11-16.) Kwanza, mchungaji angemtafuta kondoo, jambo ambalo lilihitaji wakati na jitihada nyingi. Kisha, baada ya kumpata kondoo aliyepotea, mchungaji angemrudisha kundini. Isitoshe, ikiwa kondoo alikuwa amejeruhiwa au alikuwa na njaa, mchungaji angemsaidia kwa upendo mnyama huyo dhaifu, angeyafunga majeraha yake, angembeba, na kumlisha. Wazee wa kutaniko, yaani, wachungaji wa “kundi la Mungu,” wanahitaji kufanya mambo hayohayo ili kumsaidia yeyote ambaye ameacha kushirikiana na kutaniko. (1 Pet. 5:2, 3) Wazee huwatafuta kondoo, huwasaidia warudi kundini, na kuwaonyesha upendo kwa kuwapa utegemezo wa kiroho wanaohitaji. *

11. Mchungaji mzuri alielewa nini?

11 Mchungaji mzuri alielewa kwamba kondoo wangeweza kupotea. Na ikiwa kondoo alienda mbali na kundi, mchungaji hakumtendea kwa ukali. Fikiria mfano ambao Yehova aliweka alipowasaidia baadhi ya watumishi wake ambao walimwacha kwa muda fulani.

12. Yehova alimtendeaje Yona?

12 Nabii Yona alikimbia mgawo wake. Ingawa hivyo, Yehova hakukatishwa tamaa haraka na Yona. Kama mchungaji mzuri, Yehova alimwokoa na akamsaidia apate tena nguvu alizohitaji ili kutimiza mgawo wake. (Yona 2:7; 3:1, 2) Baadaye, Mungu alitumia mmung’unye ili kumsaidia Yona aelewe kwamba uhai wa kila mwanadamu ni wenye thamani. (Yona 4:10, 11) Tunajifunza nini? Wazee wa kutaniko hawapaswi kukata tamaa haraka inapohusu kuwasaidia wahubiri wasiotenda. Badala yake, wazee hujitahidi kuelewa jambo lililosababisha kondoo aende mbali na kundi. Na kondoo huyo anaporudi kwa Yehova, wazee huendelea kumhangaikia na kumwonyesha upendo.

13. Tunajifunza nini kutokana na jinsi Yehova alivyomtendea mwandikaji wa Zaburi 73?

13 Mwandikaji wa Zaburi 73 alivunjika moyo alipoona ni kana kwamba waovu wanafanikiwa. Alitilia shaka ikiwa kweli kulikuwa na faida ya kufanya mapenzi ya Mungu. (Zab. 73:12, 13, 16) Yehova alitendaje? Hakumshutumu mwanamume huyo. Isitoshe, Mungu aliruhusu maneno yake yaandikwe katika Biblia. Hatimaye, mtunga zaburi huyo alikuja kutambua kwamba uhusiano mzuri pamoja na Yehova una thamani zaidi kuliko jambo lolote lingine, na unafanya maisha yetu yawe na thamani. (Zab. 73:23, 24, 26, 28) Tunajifunza nini? Wazee hawapaswi kuwa wepesi wa kuwahukumu wale wanaoanza kutilia shaka ikiwa kweli kuna faida ya kumtumikia Yehova. Badala ya kuwashutumu, wazee wanapaswa kujitahidi kuelewa kwa nini wanazungumza na kutenda kwa njia hiyo. Ni kwa kufanya hivyo tu, ndipo watakapoweza kutumia Maandiko hususa ili kuwapatia kitia-moyo wanachohitaji.

14. Kwa nini Eliya alihitaji msaada, na Yehova alimpatiaje msaada huo?

14 Nabii Eliya alimkimbia Malkia Yezebeli. (1 Fal. 19:1-3) Alifikiri kwamba hakuna mtu mwingine yeyote aliyekuwa akitumikia kama nabii wa Yehova, na alihisi kwamba kazi yake ilikuwa ya bure. Eliya alishuka moyo sana hivi kwamba akatamani kufa. (1 Fal. 19:4, 10) Badala ya kumshutumu Eliya, Yehova alimhakikishia kwamba hakuwa peke yake, kwamba angeweza kutumaini nguvu za Mungu, na kwamba bado kulikuwa na kazi nyingi kwa ajili yake. Yehova alimsikiliza Eliya kwa fadhili alipokuwa akieleza mahangaiko yake, na akampa migawo mipya. (1 Fal. 19:11-16, 18) Tunajifunza nini? Sisi sote, na hasa wazee, tunapaswa kuwatendea kondoo wa Yehova kwa fadhili. Iwe mtu anaeleza hisia zake za uchungu au anahisi kwamba hastahili rehema za Yehova, wazee watamsikiliza anapoumimina moyo wake. Kisha watajitahidi kumhakikishia kondoo huyo aliyepotea kwamba Yehova anamthamini.

TUNAPASWA KUHISIJE KUHUSU KONDOO WA MUNGU WALIOPOTEA?

15. Kulingana na Yohana 6:39, Yesu alihisije kuhusu kondoo wa Baba yake?

15 Yehova anataka tuhisije kuhusu kondoo wake waliopotea? Yesu ametuwekea kielelezo. Alijua kwamba kondoo wote wa Yehova ni wenye thamani machoni pa Mungu, hivyo alifanya yote aliyoweza ili kuwasaidia “kondoo waliopotea wa nyumba ya Israeli” wamrudie Yehova. (Mt. 15:24; Luka 19:9, 10) Akiwa mchungaji mwema, Yesu pia alifanya yote aliyoweza ili asimpoteze kondoo yeyote wa Yehova.—Soma Yohana 6:39.

16-17. Wazee wanapaswa kuwa na maoni gani kuhusu kuwasaidia wale ambao wameacha kumtumikia Yehova? (Tazama sanduku “ Jinsi Kondoo Aliyepotea Anavyohisi.”)

16 Mtume Paulo aliwahimiza wazee wa kutaniko la Efeso waige mfano wa Yesu. Aliwaambia hivi: “Ni lazima mwasaidie walio dhaifu, na kuyakumbuka maneno ya Bwana Yesu, aliposema: ‘Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea.’” (Mdo. 20:17, 35) Ni wazi kwamba wazee leo wana jukumu la pekee kuhusiana na jambo hilo. Salvador, mzee wa kutaniko kutoka nchini Hispania anasema hivi: “Ninapofikiria kuhusu jinsi Yehova anavyowajali sana kondoo wake waliopotea, ninachochewa kufanya yote ninayoweza ili kuwasaidia. Nikiwa mchungaji wa kiroho, ninasadiki kwamba Yehova anataka niwatunze.”

17 Wote waliotajwa katika makala hii ambao walikuwa wameacha kumtumikia Yehova, walipata msaada na kurudi kwake tena. Hata hivi sasa, kuna wengi zaidi ambao wameacha kumtumikia Yehova na wanataka kurudi kwake. Makala inayofuata itazungumzia kwa kina mambo tunayoweza kufanya ili kuwasaidia wamrudie Yehova.

WIMBO 139 Wazia Wakati Vitu Vyote Vitakuwa Vipya

^ fu. 5 Kwa nini baadhi ya ndugu na dada ambao wamemtumikia Yehova kwa uaminifu kwa miaka mingi wameacha kushirikiana na kutaniko? Mungu anahisije kuwahusu? Makala hii inazungumzia majibu ya maswali hayo. Pia, inazungumzia mambo tunayoweza kujifunza kutokana na jinsi Yehova alivyowasaidia baadhi ya watu katika nyakati za Biblia, ambao kwa muda fulani waliacha kumtumikia.

^ fu. 2 UFAFANUZI WA MANENO: Mhubiri asiyetenda ni yule ambaye hajaripoti utendaji wowote katika kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi kwa miezi sita au zaidi. Ingawa hivyo, wahubiri hao wasiotenda bado ni ndugu na dada zetu, na tunawapenda.

^ fu. 4 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

^ fu. 10 Makala inayofuata itazungumzia njia hususa ambazo wazee wanaweza kufuata hatua hizo.

^ fu. 60 MAELEZO YA PICHA: Kwa kuwa alimjali kondoo aliyepotea, mchungaji Mwisraeli alimtafuta na kumsaidia arudi kundini. Leo, wachungaji wa kiroho hufanya vivyo hivyo.

^ fu. 64 MAELEZO YA PICHA: Dada asiyetenda anaposubiri basi liondoke, anawaona Mashahidi wawili wakifurahia kufanya mahubiri ya hadharani.