Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 26

“Nirudieni”

“Nirudieni”

“Nirudieni, nami nitawarudia.”—MAL. 3:7.

WIMBO 102 “Mwasaidie Walio Dhaifu”

MUHTASARI *

1. Yehova huhisije wakati mmoja wa kondoo wake anapomrudia?

KAMA tulivyoona katika makala iliyopita, Yehova anajilinganisha na mchungaji mzuri anayemtunza kwa wororo kila mmoja wa kondoo wake. Naye humtafuta kondoo yeyote aliyepotea. Yehova aliwaambia hivi Waisraeli waliokuwa wamemwacha: “Nirudieni, nami nitawarudia.” Tunajua kwamba bado Yehova anahisi vivyo hivyo kwa sababu anasema: “Sibadiliki.” (Mal. 3:6, 7) Yesu alisema kwamba Yehova pamoja na malaika hushangilia sana wakati hata mtumishi mmoja tu wa Yehova aliyekuwa amepotea anapomrudia.—Luka 15:10, 32.

2. Tutazungumzia nini katika makala hii?

2 Acheni tuchunguze mifano mitatu ya Yesu inayokazia jinsi ya kuwasaidia wale ambao wamemwacha Yehova. Tutazungumzia baadhi ya sifa hususa tunazohitaji ili kuwasaidia kondoo waliopotea wamrudie Yehova. Na tutaona kwa nini jitihada zetu za kuwasaidia walio dhaifu si za bure.

TAFUTA SARAFU ILIYOPOTEA

3-4. Kwa nini mwanamke anayetajwa kwenye Luka 15:8-10, aliitafuta kwa makini sana drakma yake iliyopotea?

3 Tunahitaji kutia bidii ili kuwatafuta wale wanaotamani kumrudia Yehova. Katika mfano wake unaopatikana kwenye Injili ya Luka, Yesu anaeleza jinsi mwanamke fulani anavyotafuta kitu chenye thamani kilichopotea, yaani, sarafu ya drakma. Mfano huo unakazia bidii anayotia ili kutafuta sarafu hiyo.—Soma Luka 15:8-10.

4 Yesu anafafanua hisia za mwanamke anayepata sarafu anayothamini ya drakma iliyokuwa imepotea. Katika siku za Yesu, inaonekana kwamba baadhi ya akina mama Wayahudi waliwapa binti zao sarafu kumi za drakma katika siku ya harusi yao. Huenda sarafu hiyo iliyopotea ilikuwa kati ya sarafu hizo kumi. Mwanamke huyo anahisi kwamba sarafu hiyo imeanguka sakafuni. Basi, anawasha taa na kutazama huku na kule, lakini haioni. Taa yake ya mafuta haitoi mwangaza wa kutosha ili kuiona sarafu hiyo ndogo ya fedha. Hatimaye, anaifagia kwa makini nyumba yote. Na hapo kwenye mavumbi aliyokusanya, anaiona ile drakma anayoithamini iking’aa kwa sababu ya mwangaza wa taa. Anapata kitulizo kwelikweli! Anawaita rafiki zake na jirani zake na kushiriki pamoja nao habari hiyo njema.

5. Kwa nini huenda ikawa vigumu kuwapata wale walioacha kushirikiana na kutaniko?

5 Kama mfano wa Yesu unavyoonyesha, jitihada inahitajika ili kupata kitu kilichopotea. Vivyo hivyo, huenda tukahitaji kutia bidii ili kuwapata wale walioacha kushirikiana na kutaniko. Huenda miaka mingi imepita tangu walipoacha kushirikiana nasi. Huenda hata wamehamia katika eneo ambalo hakuna ndugu au dada anayewajua. Lakini hapana shaka kwamba hata dakika hii, kuna baadhi ya wahubiri wasiotenda ambao wanatamani sana kumrudia Yehova. Wanataka kumtumikia Yehova pamoja na familia ya waabudu wake, lakini wanahitaji msaada wetu.

6. Wote kutanikoni wanaweza kushiriki jinsi gani katika kazi ya kuwatafuta wale wasiotenda?

6 Ni nani wanaoweza kushiriki katika kazi ya kuwatafuta wale wasiotenda? Sisi sote—wazee wa kutaniko, mapainia, watu wa familia yao, na wahubiri wa kutaniko—tunaweza kusaidia kuwatafuta. Je, una rafiki au mtu wa ukoo ambaye ameacha kutenda? Je, umekutana na mtu asiyetenda ulipokuwa ukihubiri nyumba kwa nyumba au hadharani? Mweleze mtu huyo kwamba ikiwa angependa kutembelewa, utafurahi kuwapatia wazee anwani au namba yake ya simu.

7. Maelezo ya mzee wa kutaniko anayeitwa Thomas yanakufundisha nini?

7 Ni hatua gani zinazofaa ambazo wazee kihususa wanaweza kuchukua ili kuwapata wale wanaotamani kumrudia Yehova? Ona maelezo ya Thomas, * mzee wa kutaniko anayeishi nchini Hispania. Thomas amewasaidia zaidi ya Mashahidi 40 warudi katika kutaniko. Anaeleza hivi: “Kwanza, mimi huwauliza ndugu na dada kadhaa ikiwa wanajua mahali ambapo mhubiri fulani asiyetenda anaishi kwa sasa. Au ninawauliza wahubiri ikiwa wanamkumbuka mtu yeyote ambaye kwa sasa hahudhurii mikutano. Wengi kutanikoni hufurahia kusaidia kwa sababu wanahisi kwamba wamehusishwa katika mpango huo wa kuwatafuta. Baadaye, ninapowatembelea ndugu na dada wasiotenda, mimi huwauliza kuhusu watoto na watu wao wengine wa ukoo. Baadhi ya wahubiri wasiotenda walikuwa wakihudhuria mikutano pamoja na watoto wao ambao huenda walikuwa wahubiri wakati huo. Wao pia wanaweza kupewa msaada wa kumrudia Yehova.”

WARUDISHE KUTANIKONI WANA NA MABINTI WA YEHOVA WALIOPOTEA

8. Katika mfano wa mwana mpotevu kwenye Luka 15:17-24, Baba alimtendeaje mwana wake aliyetubu?

8 Tunapaswa kuwa na sifa gani ikiwa tunataka kuwasaidia wale wanaotamani kumrudia Yehova? Fikiria baadhi ya mambo tunayoweza kujifunza kutokana na mfano wa Yesu wa mwana mpotevu aliyeondoka nyumbani. (Soma Luka 15:17-24.) Yesu anaeleza jinsi ambavyo hatimaye mwana huyo alirudiwa na fahamu na kuamua kurudi nyumbani. Baba alikimbia ili akutane na mwana wake na kumkumbatia kwa uchangamfu, akimhakikishia kwamba alimpenda. Mwana huyo alijihisi akiwa na hatia na aliona kwamba hastahili kuitwa mwana. Baba alimwonyesha mwanaye hisia-mwenzi na mwana huyo alimmiminia hisia zake. Kisha, Baba alichukua hatua hususa za kumhakikishia mwana wake kwamba alikaribishwa nyumbani si kama mfanyakazi, bali kama mwana mpendwa katika familia. Ili kuthibitisha jambo hilo, baba huyo aliandaa karamu na kumpa mwana wake aliyetubu mavazi bora.

9. Ni lazima tuwe na sifa gani ili kuwasaidia wahubiri wasiotenda wamrudie Yehova? (Tazama sanduku “ Jinsi ya Kuwasaidia Wale Wanaotaka Kumrudia Yehova.”)

9 Yehova ni kama baba katika mfano huo. Anawapenda ndugu na dada zetu wasiotenda na anataka wamrudie. Tukimwiga Yehova, tunaweza kuwasaidia wamrudie. Ili kufanya hivyo, tunahitaji kuwa na subira, hisia-mwenzi, na upendo. Kwa nini tunapaswa kuonyesha sifa hizo, na tunaweza kuzionyeshaje?

10. Kwa nini tunahitaji kuwa na subira ili kumsaidia mtu amkaribie Yehova tena?

10 Tunahitaji kuwa na subira kwa sababu inachukua muda ili mtu apone kiroho. Wahubiri wengi waliokuwa wameacha kutenda wanakiri kwamba walianza tena kumtumikia Yehova baada ya kutembelewa mara kwa mara na wazee na wengine kutanikoni. Nancy, dada kutoka kusini-mashariki mwa bara la Asia, anaandika hivi: “Rafiki yangu wa karibu kutanikoni alinisaidia sana. Alinipenda kama dada yake mkubwa. Alinikumbusha kuhusu mambo mazuri tuliyofurahia pamoja wakati uliopita. Angenisikiliza kwa subira nilipokuwa nikimweleza hisia zangu, na hakusita kunipatia ushauri. Alithibitika kuwa rafiki wa kweli aliye tayari kunisaidia wakati wowote.”

11. Kwa nini tunahitaji kuwa na hisia-mwenzi ili kumsaidia mtu anayepambana na hisia za uchungu?

11 Sifa ya hisia-mwenzi ni kama dawa yenye nguvu; inaweza kutumiwa kuponya hisia zilizoumia. Baadhi ya wahubiri wasiotenda wamekuwa wakipambana na hisia za uchungu kwa miaka mingi kwa sababu ya jambo walilofanyiwa na ndugu au dada fulani kutanikoni. Hisia hizo zimewazuia wasiwe na hamu ya kumrudia Yehova. Huenda wengine wanahisi kwamba walitendewa isivyo haki. Huenda wakahitaji mtu fulani awasikilize na kuelewa hisia zao. (Yak. 1:19) María, dada ambaye wakati fulani alikuwa mhubiri asiyetenda, anasema hivi: “Nilihitaji mtu wa kunisikiliza, mtu ambaye angenifariji nilipolia, na mtu ambaye angenipa mwongozo.”

12. Toa mfano unaoonyesha jinsi upendo wa Yehova unavyowavuta wahubiri wasiotenda warudi kutanikoni.

12 Biblia inasema kwamba upendo wa Yehova kwa watu wake ni kama kamba. Upendo wa Mungu ni kama kamba jinsi gani? Fikiria mfano huu: Wazia kwamba unazama katika bahari iliyochafuka na mtu fulani anakutupia boya ili usizame. Kwa hakika, ungethamini sana msaada wake kwa sababu litakusaidia uendelee kuelea. Lakini boya hilo pekee halitoshi kukufanya uendelee kuwa hai. Maji ni baridi, na ili uendelee kuwa hai ni lazima uingie kwenye mashua ya uokoaji. Unahitaji mtu atakayekutupia kamba na kukuvuta hadi kwenye mashua hiyo. Yehova alisema hivi kuwahusu Waisraeli waliomwacha: “Niliendelea kuwavuta kwa  . . . kamba za upendo.” (Hos. 11:4) Mungu anahisi vivyo hivyo leo kuwahusu wale ambao wameacha kumtumikia na wanaozama kwenye bahari ya matatizo na mahangaiko. Anataka wajue kwamba anawapenda, na anataka kuwavuta ili waje kwake. Yehova anaweza kukutumia ili uwaonyeshe upendo alio nao kwao.

13. Simulia kisa kinachoonyesha jinsi upendo wa kindugu ulivyo na nguvu.

13 Ni muhimu kuwahakikishia wahubiri wasiotenda kwamba Yehova anawapenda na tunawapenda pia. Pablo, ndugu aliyetajwa kwenye makala iliyotangulia, alikuwa mhubiri asiyetenda kwa zaidi ya miaka 30. Anaeleza hivi: “Nilipokuwa nikiondoka nyumbani asubuhi moja, nilikutana na dada mmoja mwenye fadhili aliye na umri mkubwa ambaye alizungumza nami kwa njia yenye upendo. Nilianza kutokwa na machozi kama mtoto. Nilimwambia kwamba inaonekana Yehova alikuwa amemtuma ili kuzungumza nami. Wakati huo hasa ndipo nilipofanya uamuzi wa kumrudia Yehova.”

WASAIDIE KWA UPENDO WALE WALIO DHAIFU

14. Kulingana na mfano ulio kwenye Luka 15:4, 5, mchungaji alifanya nini alipompata kondoo aliyepotea?

14 Tunahitaji kuendelea kuwasaidia na kuwatia moyo ndugu na dada wasiotenda. Kama yule mwana mpotevu katika mfano wa Yesu, huenda wao pia wana majeraha makubwa ya kihisia. Na huenda wamedhoofika kiroho kwa sababu ya mambo waliyopitia katika ulimwengu wa Shetani. Tunahitaji kuwasaidia waimarishe imani yao kwa Yehova. Katika mfano wa kondoo aliyepotea, Yesu anafafanua jinsi mchungaji anavyombeba kondoo mabegani mwake na kumrudisha kundini. Tayari mchungaji huyo ametumia wakati na nguvu nyingi kumtafuta kondoo huyo aliyepotea. Lakini anatambua kwamba atahitaji kumbeba na kumrudisha kwenye zizi kwa sababu kondoo hatakuwa na nguvu za kurudi peke yake.—Soma Luka 15:4, 5.

15. Tunaweza kuwasaidiaje ndugu na dada walio dhaifu wanaotaka kumrudia Yehova? (Tazama sanduku “ Kifaa Chenye Thamani.”)

15 Huenda tukahitaji kutumia wakati na nguvu nyingi kuwasaidia baadhi ya ndugu na dada wasiotenda ili washinde udhaifu wao. Lakini kwa msaada wa roho ya Yehova, Neno lake, na machapisho tunayopokea kupitia kutaniko, tunaweza kuwasaidia wapate tena nguvu za kiroho. (Rom. 15:1) Tunaweza kufanyaje hivyo? Mzee mmoja wa kutaniko mwenye uzoefu anasema hivi: “Ndugu na dada wengi wasiotenda wanahitaji funzo la Biblia wanapoamua kwamba kwa kweli wanataka kumrudia Yehova.” * Hivyo, ikiwa utaombwa ujifunze Biblia na ndugu au dada asiyetenda, kubali pendeleo hilo kwa furaha. Mzee huyo wa kutaniko anasema hivi pia: “Mhubiri anayeongoza funzo hilo anahitaji kuwa rafiki mzuri ambaye mhubiri asiyetenda anaweza kumtumaini na kumfunulia hisia zake.”

SHANGWE MBINGUNI NA SHANGWE DUNIANI

16. Tunajuaje kwamba malaika watatusaidia?

16 Masimulizi mengi yanaonyesha kwamba malaika wanafanya kazi bega kwa bega pamoja nasi ili kutusaidia kuwatafuta wale walioacha kutenda wanaotamani kumrudia Yehova. (Ufu. 14:6) Kwa mfano Silvio, ndugu kutoka nchini Ekuado, alisali kwa bidii ili apate msaada wa kurudi kutanikoni. Alipokuwa akiendelea kusali, alisikia kengele ikilia. Wazee wawili walikuwa mlangoni. Katika ziara hiyo, walifurahi walipoanza kumpa msaada aliohitaji.

17. Tunathawabishwaje tunapowasaidia wale walio dhaifu kiroho?

17 Tutapata shangwe nyingi ikiwa tutawasaidia wale walio dhaifu kiroho kumrudia Yehova. Salvador, painia ambaye huwapa uangalifu wa pekee ndugu na dada wasiotenda anasema hivi: “Nyakati nyingine mimi hushindwa kuzuia machozi yangu ya furaha. Mimi hufurahi sana ninapofikiria jinsi Yehova alivyomwokoa mmoja wa kondoo wake wapendwa kutoka kwenye ulimwengu wa Shetani, na kwamba nimepata pendeleo la kushirikiana Naye katika kazi hiyo.”—Mdo. 20:35.

18. Ikiwa umeacha kutenda, unaweza kuwa na uhakika gani?

18 Ikiwa umeacha kushirikiana na watu wa Yehova, uwe na hakika kwamba Yehova bado anakupenda. Anataka umrudie. Utahitaji kuchukua hatua kadhaa ili umrudie. Lakini kama yule baba katika mfano wa Yesu, Yehova anakusubiri urudi kwake, naye atafurahi sana kukukaribisha nyumbani.

WIMBO 103 Wachungaji​—Zawadi Katika Wanadamu

^ fu. 5 Yehova anataka wale ambao wameacha kushirikiana na kutaniko wamrudie. Tunaweza kufanya mengi ili kuwatia moyo wale walio tayari kukubali mwaliko huu wa Yehova: “Nirudieni.” Katika makala hii, tutazungumzia jinsi tunavyoweza kuwasaidia wamrudie Yehova

^ fu. 7 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

^ fu. 15 Baadhi ya ndugu na dada wasiotenda wanaweza kusaidiwa kwa kujifunza sura fulani za kitabu Jinsi ya Kudumu Katika Upendo wa Mungu, ilhali wengine wamenufaika kwa kujifunza tena sura fulani za kitabu Mkaribie Yehova. Halmashauri ya Utumishi ya Kutaniko itaamua ni nani anayefaa zaidi kuongoza funzo hilo.

^ fu. 68 MAELEZO YA PICHA: Akina ndugu watatu tofauti wakimsaidia ndugu anayetamani kumrudia Yehova. Wanafanya hivyo kwa kuwasiliana naye, kumhakikishia kwamba anapendwa, na kwa kumsikiliza kwa hisia-mwenzi.