Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

Pindi Zenye Shangwe na Mambo Niliyojifunza Katika Utumishi wa Yehova

Pindi Zenye Shangwe na Mambo Niliyojifunza Katika Utumishi wa Yehova

NILIPOKUWA mvulana, kila mara nilipoona ndege ikipaa angani, nilitamani kusafiri kwenda kwenye nchi nyingine. Nilihisi kwamba jambo hilo haliwezekani kamwe.

Wazazi wangu waliondoka nchini Estonia wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu na kuhamia Ujerumani, ambako nilizaliwa. Wakati huo walikuwa wanajitayarisha kuhamia nchini Kanada. Nyumba yetu ya kwanza ilikuwa karibu na jiji la Ottawa, Kanada, ilikuwa ndogo, pia ilikuwa banda la kuku. Tulikuwa maskini sana, lakini angalau tulikula mayai kila asubuhi.

Siku moja, Mashahidi wa Yehova walimsomea mama yangu andiko la Ufunuo 21:3, 4. Aliguswa sana moyo na mambo aliyojifunza hivi kwamba akaanza kulia. Mbegu ya kweli ilianza kukua, na baba na mama yangu walifanya maendeleo haraka kisha wakabatizwa.

Wazazi wangu hawakuzungumza Kiingereza vizuri, lakini walimtumikia Yehova kwa bidii. Karibu kila Jumamosi, hata baada ya kufanya kazi usiku kucha katika kiwanda cha kuyeyusha madini ya nikeli huko Sudbury, Ontario, baba yangu alienda utumishi pamoja nami na dada yangu mdogo, Sylvia. Na kila juma tulijifunza Mnara wa Mlinzi tukiwa familia. Mama na baba walinifundisha kumpenda Mungu. Basi nilijiweka wakfu kwa Yehova mwaka wa 1956 nikiwa na umri wa miaka kumi. Upendo wao wenye nguvu kwa Yehova umeniimarisha katika maisha yangu yote.

Baada ya kuhitimu shule ya sekondari, nilipunguza bidii. Nilifikiri kwamba ikiwa ningekuwa painia, singefaulu kupata pesa za kutosha ili kutimiza ndoto yangu ya kusafiri kwa ndege kwenda nchi nyingine. Nilipata kazi ya kucheza muziki katika kituo cha redio, kazi ambayo niliipenda sana. Lakini nilifanya kazi wakati wa jioni; hivyo, mara nyingi nilikosa kuhudhuria mikutano na nilishirikiana na watu ambao hawakumpenda Mungu. Mwishowe, dhamiri yangu iliyozoezwa na Biblia ilinichochea kufanya mabadiliko.

Nilihamia huko Oshawa, Ontario. Nikiwa huko nilikutana na Ray Norman, na dada yake Lesli, na mapainia wengine. Wote walipendezwa nami. Kuona jinsi walivyokuwa na furaha kulinichochea nichunguze upya malengo yangu. Walinitia moyo niwe painia, nami nikaanza kupainia Septemba 1966. Nilifurahia, na maisha yalikuwa mazuri. Hata hivyo, mambo yasiyotarajiwa yangebadili maisha yangu.

YEHOVA ANAPOKUOMBA UFANYE JAMBO, JITAHIDI KULIFANYA

Nilipokuwa katika shule ya sekondari, nilijaza fomu ya kutumikia Betheli huko Toronto, Kanada. Baadaye, nilipokuwa painia, nilialikwa kutumikia Betheli kwa miaka minne. Lakini nilimpenda sana Lesli, na niliogopa kwamba ikiwa ningekubali mwaliko huo nisingemwona tena. Mwishowe, baada ya kusali sana kwa muda mrefu, niliagana na Lesli kwa huzuni na kukubali mwaliko wa kwenda Betheli.

Nilifanya kazi katika dobi ya Betheli na baadaye kazi ya ukarani. Wakati huohuo, Lesli akawa painia wa pekee huko Gatineau, Quebec. Mara nyingi nilijiuliza jambo alilokuwa akifanya na kama nilikuwa nimefanya uamuzi sahihi. Kisha nikapata moja kati ya pindi zenye shangwe zaidi maishani mwangu. Ray, ndugu yake Lesli, alialikwa Betheli. Tulipangiwa kuishi katika chumba kimoja! Hilo lilinifanya nianzishe tena urafiki pamoja na Lesli. Tulifunga ndoa siku ya mwisho ya mgawo wangu wa miaka minne—Februari 27, 1971.

Tulipoanza kazi ya kuzunguka mwaka wa 1975

Mimi na Lesli tulipewa mgawo wa kutumikia katika kutaniko la Kifaransa huko Quebec. Baada ya miaka mitatu, nilishangaa nilipopewa mgawo wa kutumikia kama mwangalizi wa mzunguko nikiwa na umri wa miaka 28. Nilijihisi kwamba nina umri mdogo na sina uzoefu, lakini maneno ya Yeremia 1:7, 8 yalinitia moyo. Hata hivyo, Lesli alikuwa amepatwa na aksidenti kadhaa za gari na ilikuwa vigumu kwake kupata usingizi. Basi, tulifikiri kwamba kazi ya kuzunguka ingekuwa ngumu. Ingawa hivyo, Lesli alisema hivi: “Yehova anapotuomba tufanye jambo, tunapaswa kujitahidi kulifanya, sivyo?” Tulikubali mgawo huo na kufurahia kazi ya kusafiri kwa miaka 17.

Nilipokuwa mwangalizi wa mzunguko, nilikuwa na shughuli nyingi na mara nyingi sikuwa na muda wa kutosha kwa ajili ya Lesli. Nilihitaji kujifunza somo lingine. Jumatatu moja asubuhi na mapema, kengele ya mlango wetu ililia. Hakukuwa na mtu mlangoni, lakini kulikuwa na kikapu, kitambaa, matunda, jibini, mikate, chupa ya divai, glasi, na karatasi yenye maandishi haya: “Mpeleke mke wako kwenye tafrija.” Ilikuwa siku maridadi, yenye jua. Hata hivyo, nilimweleza Lesli kwamba nilihitaji kutayarisha hotuba kadhaa na singeweza kwenda. Alielewa, lakini alihuzunika. Nilipoketi kwenye dawati langu, dhamiri yangu ilianza kunisumbua. Nilifikiria kuhusu andiko la Waefeso 5:25, 28. Nilijiambia kwamba maneno hayo kutoka kwa Yehova yalikuwa yakinitia moyo kushughulikia mahitaji ya kihisia ya mke wangu. Baada ya kusali, nilimwambia Lesli, “Twende,” naye akafurahi sana. Tuliendesha gari mpaka kwenye sehemu nzuri kando ya mto, tukatandika kile kitambaa, na kuwa na mojawapo ya siku zenye shangwe zaidi pamoja. Na bado nilifaulu kutayarisha zile hotuba.

Migawo yetu ya kuzunguka ilikuwa mingi na yenye shangwe, kuanzia huko British Colombia hadi Newfoundland. Tamaa yangu ya kusafiri ilianza kutimia. Nilikuwa nimefikiria kuhusu Shule ya Gileadi lakini sikutamani kuwa mmishonari katika nchi nyingine. Nilihisi kwamba wamishonari ni watu wa pekee, na sikufikiri ningestahili kuwa mmishonari. Isitoshe, niliogopa kwamba tungetumwa katika nchi fulani barani Afrika yenye magonjwa na vita. Nilifurahia kuwa nchini Kanada.

MGAWO USIOTARAJIWA WA KUTUMIKIA ESTONIA NA NCHI ZA BALTIKI

Kusafiri katika nchi za Baltiki

Mwaka wa 1992, Mashahidi wa Yehova walipoanza kuhubiri tena hadharani katika nchi zilizokuwa katika Muungano wa Sovieti, tuliulizwa kama tungekuwa tayari kuhamia Estonia na kuwa wamishonari. Tulishangazwa na jambo hilo, lakini tulisali kulihusu. Tukajiuliza hivi tena, ‘Yehova anapotuomba tufanye jambo, tunapaswa kujitahidi kulifanya, sivyo?’ Tulikubali, na nikajiambia, ‘Angalau hatuendi barani Afrika.’

Mara moja tulianza kujifunza Kiestonia. Baada ya kukaa miezi kadhaa katika nchi hiyo, tulipewa mgawo wa kuzungukia makutaniko. Tulipaswa kutembelea makutaniko na vikundi 46 hivi katika nchi tatu za Baltiki kutia ndani Kaliningrad, Urusi. Hilo lilimaanisha tulipaswa kujifunza kwa kiasi fulani Kilatvia, Kilithuania, na Kirusi. Halikuwa jambo rahisi. Akina ndugu na dada walifurahia jitihada zetu nao wakatusaidia. Mwaka wa 1999, ofisi ya tawi ilifunguliwa nchini Estonia, nami nikapewa mgawo wa kuwa mshiriki wa Halmashauri ya Tawi pamoja na Toomas Edur, Lembit Reile, na Tommi Kauko.

Kushoto: Nilipokuwa nikitoa hotuba kwenye kusanyiko katika nchi ya Lithuania

Kulia: Halmashauri ya Tawi nchini Estonia, iliundwa mwaka wa 1999

Tuliwafahamu Mashahidi wengi ambao hapo awali walikuwa wamehamishiwa huko Siberia. Licha ya kutendewa kwa ukatili gerezani na kutenganishwa na familia zao, hawakuwa na kinyongo. Waliendelea kuwa na shangwe na bidii katika huduma. Mfano wao ulitufundisha kwamba tunaweza kuvumilia na kuwa wenye shangwe katika hali ngumu.

Tulifanya kazi kwa bidii kwa miaka mingi, na hatukupumzika vya kutosha, basi Lesli akaanza kuhisi uchovu mwingi. Hatukutambua mara moja kwamba uchovu wake ni ule unaohusianishwa na ugonjwa wa misuli (fibromyalgia). Tulifikiria kwa uzito kurudi nchini Kanada. Tulipoalikwa kuhudhuria Shule ya Washiriki wa Halmashauri ya Tawi huko Patterson, New York, Marekani, nilidhani kwamba hatungeweza kuhudhuria. Hata hivyo, baada ya kusali sana, tulikubali kuhudhuria. Yehova alibariki uamuzi huo. Tulipokuwa kwenye shule hiyo, mwishowe Lesli alipata matibabu aliyohitaji. Hivyo, tulifaulu kurudia utendaji wa kawaida.

BADILIKO LENYE KUSISIMUA—KUHAMIA BARA LINGINE

Jioni moja mwaka 2008, tulipokuwa nchini Estonia, nilipokea simu kutoka makao makuu ya ulimwenguni pote, nikaulizwa kama ningekubali mgawo nchini Kongo. Nilishtuka, hasa kwa sababu nilihitaji kuwapatia jibu siku inayofuata. Mwanzoni, sikumtajia Lesli jambo hilo kwa sababu nilijua hatapata usingizi usiku huo. Badala yake, mimi ndiye niliyekosa usingizi, kwa sababu nilikuwa nikisali na kutaja mambo yaliyonihangaisha kuhusu bara la Afrika.

Siku iliyofuata nilimwambia Lesli jambo hilo, tukasema hivi: “Yehova anatuomba twende barani Afrika. Tunajuaje kwamba tutashindwa na hatutafurahia ikiwa hatutajaribu kwanza?” Basi, baada ya kukaa nchini Estonia kwa miaka 16, tulisafiri kwa ndege kwenda Kinshasa, Kongo. Ofisi ya tawi ilikuwa na bustani maridadi yenye utulivu. Kitu cha kwanza ambacho Lesli aliweka kwenye chumba chetu ni kadi ambayo alikuwa ameitunza tangu tulipotoka Kanada. Ilikuwa imeandikwa maneno haya: “Nawiri mahali unapopandwa.” Baada ya kukutana na akina ndugu, kuongoza mafunzo ya Biblia, na kupata furaha ya kuwa wamishonari, shangwe yetu iliongezeka. Baada ya muda, tulipata pendeleo la kutembelea ofisi nyingine 13 za tawi barani Afrika. Hilo lilituwezesha kukutana na watu wenye furaha kutoka tamaduni mbalimbali. Wasiwasi niliokuwa nao mwanzoni ulikwisha, na tulimshukuru Yehova kwa kutupatia mgawo wa kutumikia barani Afrika.

Nchini Kongo tulikaribishwa kula aina mpya ya vyakula, kama vile wadudu, na nilifikiri tungeshindwa kula. Lakini tulipoona jinsi ndugu zetu walivyofurahia chakula hicho, sisi pia tulikijaribu na tulifurahia sana.

Tulifaulu kupeleka msaada wa kiroho na wa kimwili mashariki mwa nchi hiyo ambako vikundi vya wapiganaji vilikuwa vikishambulia vijiji na kuwadhuru wanawake na watoto. Ndugu wengi walikuwa na vitu vichache sana vya kimwili. Ingawa hivyo, tulitiwa moyo sana na tumaini lao lenye nguvu katika ufufuo, upendo wao kwa Yehova, na ushikamanifu wao kwa tengenezo lake. Mfano wao ulituchochea kuchunguza upya nia yetu ya kumtumikia Yehova na kuimarisha imani yetu kwake. Baadhi ya akina ndugu walikuwa wamepoteza nyumba na mimea yao. Hilo lilinikumbusha kwamba tunaweza kupoteza upesi vitu vya kimwili na kwamba uhusiano wetu pamoja na Yehova ndilo jambo muhimu zaidi. Licha ya kukabili hali ngumu sana, ndugu hao hawakulalamika. Mtazamo wao ulitutia moyo kukabiliana na changamoto zetu na matatizo ya afya kwa ujasiri.

Kushoto: Nikiwatolea hotuba wakimbizi

Kulia: Kupeleka bidhaa za msaada na madawa huko Dungu, Kongo

MGAWO MPYA BARANI ASIA

Kisha tukapata mgawo mwingine usiotarajiwa. Tuliombwa tuhamie kwenye ofisi ya tawi ya Hong Kong. Hatukuwazia kamwe kwamba siku moja tungeishi barani Asia! Lakini baada ya kujionea jinsi Yehova alivyotusaidia kwa upendo katika migawo mingine yote, tulikubali mwaliko huo. Mwaka wa 2013, huku tukitokwa na machozi, tuliwaaga rafiki zetu wapendwa katika bara maridadi la Afrika, bila kujua mambo ambayo yangetokea baadaye.

Lilikuwa badiliko kubwa kuishi Hong Kong, jiji kubwa lenye watu kutoka nchi mbalimbali ulimwenguni. Ilikuwa vigumu kujifunza lugha ya Kichina. Ingawa hivyo, akina ndugu walitukaribisha kwa uchangamfu, na tulifurahia sana chakula cha nchi hiyo. Kazi ilikuwa ikipanuka upesi, lakini bei ya nyumba na viwanja ilikuwa juu sana. Basi kwa busara Baraza Linaloongoza liliamua kuuza majengo ya ofisi ya tawi. Muda mfupi baadaye, mwaka wa 2015 tulihamishiwa nchini Korea Kusini, ambako tuliendelea kutumikia. Huku, tumekabiliana tena na changamoto ya kujifunza lugha mpya, lakini tunatiwa moyo kwa sababu ingawa bado hatuzungumzi vizuri Kikorea, akina ndugu wanaona tunafanya maendeleo katika kuzungumza lugha hiyo.

Kushoto: Kuanza maisha mapya huko Hong Kong

Kulia: Ofisi ya tawi ya Korea

MASOMO AMBAYO TUMEJIFUNZA

Si rahisi sikuzote kupata marafiki wapya, lakini tulitambua kwamba tukichukua hatua ya kwanza ya kuwakaribisha wengine, inakuwa rahisi zaidi kuwafahamu watu. Tumejionea kwamba ndugu zetu wana mambo mengi yanayowaunganisha na kwamba Yehova alituumba kwa njia ya ajabu hivi kwamba tunaweza kufungua mioyo yetu na kuwapenda marafiki wengi sana.​—2 Kor. 6:11.

Tumejifunza umuhimu wa kuwaona watu kama Yehova anavyowaona na kutambua njia ambazo Yehova anatuonyesha upendo na kutuongoza maishani. Kila mara tulipovunjika moyo au kujiuliza ikiwa ndugu na dada wanatupenda, tulisoma tena kadi na barua zenye kutia moyo kutoka kwa marafiki wetu. Kwa kweli, tumejionea jinsi ambavyo Yehova alijibu sala zetu na kutupatia uhakikisho na nguvu.

Kadiri ambavyo muda umepita, mimi na Lesli tumejifunza umuhimu wa kutenga muda ili kuwa pamoja, hata iwe tuna shughuli nyingi kadiri gani. Pia, tumejifunza umuhimu wa kucheka tunapokosea, hasa tunapojitahidi kujifunza lugha mpya. Na kila jioni, tunajitahidi kukumbuka jambo lolote tulilofurahia ili tumshukuru Yehova.

Ukweli ni kwamba sikuwazia kamwe nitakuwa mmishonari na kuishi katika nchi nyingine. Ingawa hivyo, nimepata shangwe ya kujionea jinsi mambo yote yanavyowezekana kwa msaada wa Yehova. Ninakumbuka maneno haya ya nabii Yeremia: “Umenipumbaza, Ee Yehova.” (Yer. 20:7) Naam, ametupatia mambo mengi mazuri ambayo hatukutarajia na baraka ambazo hatungewazia, hata amenitimizia tamaa yangu ya kusafiri kwa ndege. Tumesafiri kwa ndege kwenda maeneo mengi kuliko nilivyowazia nilipokuwa mvulana, tumetembelea ofisi za tawi kwenye mabara matano. Katika migawo yetu yote, nimethamini sana msaada wa Lesli na roho yake ya utayari.

Sikuzote tunakumbuka kwamba tunafanya mambo haya yote kwa sababu tunampenda Yehova. Baraka tunazofurahia leo ni kionjo tu cha jinsi maisha yatakavyokuwa tutakapoishi milele wakati Yehova ‘ataufumbua mkono wake na kutosheleza tamaa ya kila kitu kilicho hai.’​—Zab. 145:16.