Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana​—Mnaweza Kujitayarishaje kwa Ajili ya Ubatizo?

Vijana​—Mnaweza Kujitayarishaje kwa Ajili ya Ubatizo?

“Ee Mungu wangu, nimependezwa na kufanya mapenzi yako.”​—ZAB. 40:8.

NYIMBO: 51, 58

1, 2. (a) Kwa nini kubatizwa ni jambo zito? (b) Mtu anapaswa kuwa na uhakika gani kabla ya kubatizwa, na kwa nini?

JE, WEWE ni kijana unayefikiria kubatizwa? Ikiwa ndivyo, basi kubatizwa ni heshima kubwa sana ambayo mwanadamu anaweza kupata. Hata hivyo, kama makala iliyotangulia ilivyoeleza, kubatizwa ni jambo zito. Ni hatua inayoonyesha kwamba umejiweka wakfu, yaani umetoa ahadi nzito kwa Yehova kwamba utamtumikia milele kwa kutanguliza mapenzi yake zaidi ya kitu kingine chochote maishani mwako. Ni wazi kwamba unapaswa kubatizwa ikiwa tu umekomaa vya kutosha kufanya uamuzi huo, unatamani kutoka moyoni kufanya hivyo, na unaelewa maana ya kujiweka wakfu.

2 Vipi ikiwa huna uhakika kama uko tayari kubatizwa? Au namna gani ikiwa unataka kubatizwa lakini wazazi wako wanahisi kwamba unahitaji kusubiri, labda hadi utakapopata uzoefu zaidi katika maisha ya Kikristo? Vyovyote vile, usife moyo! Badala yake, tumia nafasi hiyo kufanya maendeleo ili baada ya muda, ustahili kubatizwa. Ukiwa na kusudi hilo akilini, fikiria malengo unayoweza kujiwekea kuhusu (1) imani yako, (2) matendo yako, na (3) kuonyesha shukrani.

IMANI YAKO

3, 4. Vijana wanaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Timotheo?

3 Fikiria jinsi ambavyo ungejibu maswali haya: Kwa nini ninaamini kwamba kuna Mungu? Ni nini kinachonithibitishia kwamba Biblia ni Neno la Mungu lililoongozwa na roho takatifu? Kwa nini ninaamini kwamba kuishi kupatana na viwango vya Mungu vya maadili ni bora kuliko kuiga mtindo wa maisha wa ulimwengu? Maswali hayo hayajakusudiwa kuzusha shaka akilini mwako. Badala yake, yanaweza kukusaidia ufuate himizo hili la mtume Paulo: “Mjihakikishie wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” (Rom. 12:2) Lakini kwa nini Wakristo wa Roma walihitaji kujihakikishia wenyewe mambo ambayo tayari walikuwa wameyakubali?

4 Fikiria mfano huu unaopatikana kwenye Biblia. Timotheo aliyaelewa vizuri Maandiko. Mama na nyanya yake walimfundisha ‘tangu alipokuwa mtoto mchanga.’ Hata hivyo, Paulo alimhimiza hivi Timotheo: “Endelea katika mambo uliyojifunza na uliyoshawishiwa kuamini.” (2 Tim. 3:14, 15) Kulingana na kitabu kimoja cha marejeo, neno la awali linalotafsiriwa “uliyoshawishiwa” linatoa wazo la “kusadikishwa na kuwa na uhakika kuhusiana na ukweli wa jambo fulani.” Timotheo aliifanya kweli iwe mali yake. Naye aliikubali, si kwa sababu mama na nyanya yake walimwambia afanye hivyo, bali kwa sababu alitafakari na alijithibitishia mwenyewe mambo aliyojifunza.—Soma Waroma 12:1.

5, 6. Kwa nini ni muhimu ujifunze kutumia ‘nguvu zako za kufikiri’ ukiwa kijana?

5 Namna gani wewe? Huenda umeijua kweli kwa muda mrefu. Ikiwa ndivyo, kwa nini usijiwekee lengo la kuchunguza kwa makini msingi wa imani yako? Kufanya hivyo kutaimarisha imani yako na kutakusaidia uepuke kufanya maamuzi mabaya unaposhinikizwa na vijana wenzako, propaganda za ulimwengu, au hata hisia zako mwenyewe.

6 Unapojifunza kutumia ‘nguvu zako za kufikiri’ ukiwa kijana, unajitayarisha kutoa majibu yanayofaa ikiwa vijana wenzako watazusha maswali kama vile: ‘Una uhakika gani kwamba kuna Mungu? Kwa nini Mungu mwenye upendo anaruhusu uovu? Inawezekanaje kwamba Mungu amekuwapo siku zote?’ Ikiwa umejitayarisha, maswali hayo hayatadhoofisha imani yako bali yatakuchochea ujifunze zaidi kibinafsi.

7-9. Eleza jinsi miongozo ya kujifunza inavyoweza kukusaidia uimarishe imani yako?

7 Kujifunza kibinafsi kwa kina kunaweza kukusaidia ujibu maswali, uondoe shaka yoyote, na uimarishe imani yako. (Mdo. 17:11) Tuna vifaa vingi vinavyoweza kukusaidia ufanye hivyo. Wengi wamefaidika kwa kuchunguza broshua Maswali Matano Muhimu Kuhusu Chanzo cha Uhai na kitabu Je, Kuna Muumba Anayekujali? Isitoshe, vijana wengi wamefurahia na wamenufaishwa na sehemu yenye kichwa “Biblia Inafundisha Nini Hasa?” inayopatikana kwenye mtandao. Mfululizo huo wa miongozo ya kujifunza unapatikana kwenye tovuti ya jw.org/sw. Tafuta kwenye MAFUNDISHO YA BIBLIA>MATINEJA. Kila mwongozo wa kujifunza katika mfululizo huo umekusudiwa kukusaidia uimarishe imani yako kuhusu habari fulani ya Biblia.

8 Tayari unajua mafundisho mengi ya Biblia, hivyo huenda ukajibu kwa urahisi baadhi ya maswali yaliyo katika sehemu hiyo ya “Biblia Inafundisha Nini Hasa?” Lakini kwa nini unaamini kwamba majibu yako ni sahihi? Miongozo hiyo ya kujifunza itakusaidia utafakari maandiko kadhaa na kisha uandike maoni yako kuhusu mambo unayosoma. Inaweza kukusaidia kupanga jinsi ya kuwafafanulia wengine imani yako inayotegemea Biblia. Sehemu hiyo inawasaidia vijana wengi kuimarisha imani yao. Ikiwa una uwezo wa kuingia kwenye mtandao, kwa nini usitumie mfululizo huo katika funzo lako la kibinafsi?

9 Kuimarisha imani yako ni jambo muhimu sana litakalokusaidia kuchukua hatua ya kubatizwa. Dada mmoja kijana alisema hivi: “Kabla ya kuamua kubatizwa, nilijifunza Biblia na nikatambua kwamba hii ndiyo dini ya kweli. Na kila siku maishani mwangu, uhakika huo unazidi kuimarika.”

MATENDO YAKO

10. Kwa nini tunatarajia kwamba Mkristo aliyebatizwa ataonyesha matendo yanayopatana na imani yake?

10 Biblia inasema hivi: “Imani, ikiwa haina matendo, imekufa yenyewe.” (Yak. 2:17) Ikiwa una imani yenye nguvu, basi tunatarajia kwamba utaonyesha jambo hilo kupitia matendo yako. Matendo gani? Biblia inayaita “matendo matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu.”—Soma 2 Petro 3:11.

11. “Matendo matakatifu ya mwenendo” ni nini?

11 Ili uonyeshe “matendo matakatifu ya mwenendo,” ni lazima uwe safi kiadili. Mwenendo wako unaonyesha nini? Kwa mfano, fikiria matendo yako katika miezi sita iliyopita. Umeonyeshaje kwamba ‘nguvu zako za ufahamu’ zimezoezwa kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa? (Ebr. 5:14) Je, unakumbuka wakati hususa ambapo ulipinga kishawishi au ulikataa kushinikizwa na vijana wenzako? Ukiwa shuleni, je, matendo yako yanapatana na imani yako? Je, unaitetea imani yako au unatenda kama wanafunzi wenzako ili uepuke kudhihakiwa? (1 Pet. 4:3, 4) Ni kweli kwamba hakuna aliye mkamilifu. Hata wale ambao wamemtumikia Yehova kwa miaka mingi, nyakati nyingine huenda wakakosa ujasiri wa kutetea imani yao hadharani. Hata hivyo, mtu ambaye amejiweka wakfu kwa Yehova anajivunia kuitwa kwa jina la Mungu, naye huonyesha hivyo kupitia mwenendo wake.

12. Taja baadhi ya “vitendo vya ujitoaji-kimungu,” na unapaswa kuvionaje?

12 Namna gani “vitendo vya ujitoaji-kimungu”? Vitendo hivyo vinahusisha mambo unayofanya kutanikoni, kama vile kuhudhuria mikutano na kuhubiri. Pia vinahusisha mambo mengine ya kiroho ambayo wengine hawaoni, kama vile sala na funzo lako la kibinafsi. Mtu ambaye ameweka maisha yake wakfu kwa Yehova hataona vitendo hivyo kuwa kazi ngumu. Badala yake, atakuwa na mtazamo kama wa Mfalme Daudi, ambaye alisema hivi: “Ee Mungu wangu, nimependezwa na kufanya mapenzi yako, na sheria yako imo ndani yangu.”—Zab. 40:8.

13, 14. Ni mambo gani yanayoweza kukusaidia uwe na “vitendo vya ujitoaji-kimungu,” na baadhi ya vijana wamenufaikaje?

13 Ili kukusaidia ujiwekee malengo, kuna kurasa za mazoezi katika kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2, ukurasa wa 308 na 309. Katika kurasa hizo, kuna nafasi ya kuandika majibu yako kwa maswali kama vile, “Wewe hutaja mambo hususa katika sala zako? Sala zako zinafunua nini kuhusu upendo wako kwa Yehova?” “Funzo lako la kibinafsi linatia ndani nini?” “Wewe huenda kuhubiri hata ikiwa wazazi wako hawaendi?” Isitoshe, kurasa hizo zina nafasi zilizo wazi unazoweza kuandika malengo yoyote ambayo ungependa kujiwekea kuhusu sala, funzo la kibinafsi, na huduma yako.

14 Vijana wengi wanaofikiria kubatizwa wamenufaika sana kwa kutumia kurasa hizo za mazoezi. Dada mmoja kijana aitwaye Tilda, alisema hivi: “Nilitumia kurasa hizo kujiwekea malengo. Nilifikia malengo hayo moja baada ya lingine, na mwaka mmoja hivi baadaye nilikuwa tayari kubatizwa.” Ndugu kijana, aitwaye Patrick, alinufaika kwa njia hiyohiyo. Alisema hivi: “Tayari nilijua malengo yangu, lakini kuyaandika kulinisaidia nijitahidi sana kuyafikia.”

Je, utaendelea kumtumikia Yehova hata wazazi wako wakiacha kumtumikia? (Tazama fungu la 15)

15. Kwa nini uamuzi wa kujiweka wakfu unapaswa kuwa wa kibinafsi?

15 Swali moja muhimu unalohitaji kufikiria kwa uzito katika kurasa hizo za mazoezi ni hili: “Utaendelea kumtumikia Yehova hata wazazi na rafiki zako wakiacha kumtumikia?” Kumbuka, ukiwa Mkristo aliyejiweka wakfu na kubatizwa, wewe binafsi utawajibika mbele za Yehova. Utumishi wako kwa Mungu haupaswi kuwategemea wengine, hata ikiwa ni wazazi wako. Matendo yako matakatifu ya mwenendo na vitendo vya ujitoaji-kimungu vinathibitisha kwamba umefanya kweli iwe mali yako na unasonga mbele ili ustahili kubatizwa.

ONYESHA SHUKRANI

16, 17. (a) Ni nini kinachopaswa kumchochea mtu awe Mkristo? (b) Toa mfano unaoweza kutusaidia tuithamini fidia.

16 Mwanaume mmoja aliyeijua vizuri Sheria ya Musa alimuuliza hivi Yesu: “Amri iliyo kuu katika ile Sheria ni gani?” Yesu alimjibu: “Lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote.” (Mt. 22:35-37) Yesu alionyesha wazi kwamba kumpenda Yehova kwa moyo wote ndiko kunakopaswa kumchochea mtu awe na matendo ya Kikristo, ikiwemo kubatizwa. Moja ya njia bora za kukuza upendo wako kwa Yehova ni kutafakari zawadi kubwa zaidi ya Yehova, yaani dhabihu ya fidia ya Mwana wake. (Soma 2 Wakorintho 5:14, 15; 1 Yohana 4:9, 19.) Ukitafakari kuhusu fidia na kuelewa jinsi inavyokunufaisha utachochewa zaidi kuonyesha shukrani kwa sababu ya zawadi hiyo.

17 Mfano ufuatao utakusaidia kuelewa thamani ya fidia: Wazia kwamba mtu fulani amekuokoa usife maji. Je, ungeondoka tu kwenda nyumbani na kusahau jambo alilokufanyia? Bila shaka usingefanya hivyo! Ni wazi kwamba ungehisi una deni kubwa kwa mtu aliyekuokoa. Ukweli ni kwamba usingekuwa hai ikiwa asingekuokoa! Hata hivyo, tuna deni kubwa hata zaidi kwa Yehova Mungu na Yesu Kristo. Bila fidia, kila mmoja wetu angekuwa amezama, kwa njia ya mfano, katika dhambi na kifo. Lakini kwa sababu ya tendo hilo kubwa zaidi la upendo, tuna tumaini zuri ajabu la kuishi milele katika paradiso duniani!

18, 19. (a) Kwa nini hupaswi kuogopa kujiweka wakfu kwa Yehova? (b) Kumtumikia Yehova kunaboreshaje maisha yako?

18 Je, unathamini yale ambayo Yehova amekufanyia? Ikiwa ndivyo, basi ni jambo linalofaa kuweka maisha yako wakfu kwa Yehova na kubatizwa. Kumbuka, kujiweka wakfu kunamaanisha kutoa ahadi nzito kwa Yehova kwamba utafanya mapenzi yake milele, chini ya hali yoyote ile. Je, unapaswa kuogopa kutoa ahadi hiyo? Hapana. Kumbuka kwamba Yehova anakutakia mema, naye ni “mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Ebr. 11:6) Kujiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa hakutaharibu maisha yako. Badala yake, kumtumikia Yehova kutaboresha maisha yako. Ndugu mmoja mwenye umri wa miaka 24, ambaye alibatizwa kabla ya kufikia umri wa ujana, anasema hivi: “Huenda ningekuwa na uelewaji wa kina ikiwa ningekuwa na umri mkubwa, lakini uamuzi wa kujiweka wakfu kwa Yehova ulinilinda nisifuatilie mambo ya ulimwengu.”

19 Yehova yuko tofauti kabisa na Shetani, ambaye hakujali wala hakutakii mema! Shetani hawapi thawabu yoyote ya kudumu wale wanaomuunga mkono. Na kwa kweli, hana uwezo wa kufanya hivyo! Shetani mwenyewe hana habari njema zozote za kutafakari, wala hana tumaini lolote la wakati ujao. Basi anawezaje kukupatia kitu ambacho yeye mwenyewe hana? Shetani anaweza tu kukuharibia wakati wako ujao, kwa kuwa yeye mwenyewe ataangamizwa!—Ufu. 20:10.

20. Kijana anaweza kufanya nini ili afanye maendeleo na hatimaye kujiweka wakfu na kubatizwa? (Tazama pia sanduku lenye kichwa “ Mambo ya Kukusaidia Ukue Kiroho.”)

20 Ni wazi kwamba kujiweka wakfu kwa Yehova ndilo jambo linalofaa. Je, uko tayari kuchukua hatua hiyo? Ikiwa ndivyo, usisite kufanya hivyo. Kwa upande mwingine, ikiwa unahitaji muda zaidi, tumia mapendekezo yaliyotajwa katika makala hii ili ufanye maendeleo zaidi. Paulo aliwaandikia hivi Wafilipi: “Kwa kadiri ambavyo tumefanya maendeleo, na tuendelee kutembea kwa utaratibu katika kawaida hiyohiyo.” (Flp. 3:16) Ukifuata ushauri huo, baada ya muda mfupi utatamani kuweka maisha yako wakfu kwa Yehova na kubatizwa.