Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana—Je, Mko Tayari Kubatizwa?

Vijana—Je, Mko Tayari Kubatizwa?

“Ni nani kati yenu anayetaka kujenga mnara ambaye haketi kwanza na kuhesabu gharama, ili aone kama ana kiasi cha kutosha kuukamilisha?”—LUKA 14:28.

NYIMBO: 120, 64

Makala hii na inayofuata zimetayarishwa kwa ajili ya vijana wanaofikiria kubatizwa

1, 2. (a) Ni nini huwapa watu wa Mungu shangwe leo? (b) Wazazi Wakristo na wazee wa kutaniko wanaweza kuwasaidiaje vijana waelewe maana ya kubatizwa?

MZEE mmoja Mkristo alimwambia hivi Christopher, aliyekuwa na umri wa miaka 12: “Nimekujua tangu ulipozaliwa, na ninafurahi kusikia kwamba unataka kubatizwa. Ningependa kukuuliza, ‘Kwa nini unataka kuchukua hatua hiyo?’” Mzee huyo alikuwa na sababu nzuri ya kuuliza swali hilo. Bila shaka, sisi sote tunapata shangwe kubwa tunapoona kila mwaka maelfu ya vijana duniani kote wakibatizwa. (Mhu. 12:1) Wakati huohuo, wazazi Wakristo na wazee wa kutaniko wanahitaji kuhakikisha kwamba vijana wanajifanyia uamuzi huo kwa hiari na wanaelewa maana ya kubatizwa.

2 Neno la Mungu linaonyesha kwamba kujiweka wakfu na kubatizwa ni mwanzo wa maisha ya Mkristo. Maisha hayo huleta baraka za Yehova lakini pia upinzani kutoka kwa Shetani. (Met. 10:22; 1 Pet. 5:8) Hivyo, wazazi Wakristo wanajitahidi kuwafundisha watoto wao mambo yanayohusika ili kuwa mwanafunzi wa Kristo. Inapohusu vijana ambao wazazi wao si Mashahidi, wazee wa kutaniko watachochewa na upendo kuwasaidia wahesabu gharama za kuwa mwanafunzi wa Kristo. (Soma Luka 14:27-30.) Kama vile ambavyo inahitaji mipango mizuri ili kukamilisha mradi fulani wa ujenzi, ndivyo inavyohitaji matayarisho mazuri ili kumtumikia Yehova kwa uaminifu “mpaka mwisho.” (Mt. 24:13) Lakini vijana wanaweza kufanya nini ili wao wenyewe waazimie kumtumikia Yehova katika maisha yao yote? Acheni tuone.

3. (a) Maneno ya Yesu na Petro yanatufundisha nini kuhusu umuhimu wa kubatizwa? (Mt. 28:19, 20; 1 Pet. 3:21) (b) Tutachunguza maswali gani, na kwa nini?

3 Je, wewe ni kijana unayefikiria kubatizwa? Ikiwa ndivyo, unastahili kupongezwa! Ni heshima kubwa sana kubatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova. Isitoshe, ubatizo ni takwa kwa Wakristo, na ni hatua muhimu inayoongoza kwenye wokovu. (Mt. 28:19, 20; 1 Pet. 3:21) Kwa kuwa unatamani kutoka moyoni kutimiza ahadi utakayomwahidi Yehova, unahitaji kujitayarisha kuchukua hatua hiyo muhimu. Kwa hiyo, ni vizuri ufikirie maswali matatu ambayo yanaweza kukusaidia uone kama uko tayari kubatizwa. Maswali hayo ni: (1) Je, nimekomaa vya kutosha kufanya uamuzi huu? (2) Je, ninatamani kutoka moyoni kufanya hivyo? (3) Je, ninaelewa maana ya kujiweka wakfu kwa Yehova? Acheni tuchunguze maswali hayo.

NI WAKATI GANI UNAKUWA UMEKOMAA VYA KUTOSHA?

4, 5. (a) Kwa nini si watu wenye umri mkubwa tu ndio wanaopaswa kubatizwa? (b) Eleza maana ya kuwa Mkristo mkomavu.

4 Biblia haisemi kwamba ubatizo ni hatua inayopaswa kuchukuliwa tu na watu wenye umri mkubwa au wale ambao wanatambulika kisheria kuwa watu wazima. Tunasoma hivi kwenye Methali 20:11: “Kwa matendo yake, mvulana hujitambulisha kama utendaji wake ni safi na mnyoofu.” Hata kijana mchanga anaweza kutambua umuhimu wa kufanya yaliyo sawa na maana ya kujiweka wakfu kwa Muumba wake. Hivyo, ubatizo ni hatua muhimu na inayofaa kwa kijana ambaye amekomaa vya kutosha na amejiweka wakfu kwa Yehova.—Met. 20:7.

5 Kukomaa kunamaanisha nini? Ukomavu unahusisha mengi zaidi ya ukuzi wa kimwili. Biblia inasema kwamba watu waliokomaa ni wale ambao “nguvu zao za ufahamu zimezoezwa kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.” (Ebr. 5:14) Hivyo, watu waliokomaa wanajua mambo yaliyo sawa machoni pa Yehova na wameazimia moyoni mwao kushikamana na mambo hayo. Matokeo yake ni kwamba hawashawishiki kwa urahisi kufanya mambo mabaya; wala hawahitaji kukumbushwa kila mara kufanya yaliyo sawa. Kwa kweli, tunatarajia kwamba kijana anayebatizwa atashikamana na viwango vya Mungu hata wakati ambapo wazazi au watu wengine wenye umri mkubwa hawapo.—Linganisha na Wafilipi 2:12.

6, 7. (a) Eleza changamoto ambazo Danieli alikabili alipokuwa Babiloni. (b) Danieli alionyeshaje kwamba alikuwa amekomaa?

6 Je, kweli vijana wanaweza kukomaa kwa njia hiyo? Ili kujibu swali hilo, fikiria mfano wa Danieli anayetajwa katika Biblia. Huenda ilikuwa mwanzoni mwa miaka yake ya ujana alipopelekwa uhamishoni huko Babiloni, mbali na wazazi wake. Akiwa huko, Danieli aliishi katikati ya watu waliokuwa na mtazamo tofauti kabisa kuhusu mambo yaliyo sawa na yaliyo makosa. Kwa kuongezea, Danieli alikabili changamoto nyingine: Alitendewa kwa njia ya pekee sana huko Babiloni. Kwa kweli, Danieli alikuwa miongoni mwa vijana waliochaguliwa kwa uangalifu ili wakasimame mbele ya mfalme! (Dan. 1:3-5, 13) Inaonekana Danieli alikuwa na fursa ya kupata mafanikio huko Babiloni ambayo huenda hangepata kamwe nchini Israeli.

7 Kijana Danieli alitendaje? Je, alishawishiwa na maisha ya kifahari ya Babiloni? Je, aliruhusu mazingira yake mapya yabadili utambulisho wake au yadhoofishe imani yake? La hasha! Biblia inasema kwamba alipokuwa Babiloni, Danieli “aliazimia moyoni mwake kwamba hatajitia unajisi” kwa kitu chochote ambacho kilihusiana na ibada ya uwongo. (Dan. 1:8) Danieli alionyesha ukomavu wa pekee sana!

Kijana aliyekomaa hatendi kama rafiki ya Mungu akiwa Jumba la Ufalme lakini kama rafiki ya ulimwengu akiwa shuleni (Tazama fungu la 8)

8. Unajifunza nini kutokana na mfano wa Danieli?

8 Unaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa Danieli? Jambo moja ni kwamba kijana aliyekomaa yuko imara katika imani yake. Hawi kama kinyonga, ambaye hubadili rangi yake ili afanane na mazingira aliyopo. Hatendi kama rafiki ya Mungu akiwa Jumba la Ufalme lakini kama rafiki ya ulimwengu akiwa shuleni. Badala ya kurushwa huku na huku, anabaki imara hata anapokabili majaribu ya imani.—Soma Waefeso 4:14, 15.

9, 10. (a) Kijana anaweza kunufaikaje kwa kutafakari jinsi alivyotenda hivi karibuni alipokabili majaribu ya imani? (b) Ubatizo unamaanisha nini?

9 Bila shaka, hakuna aliye mkamilifu; iwe sisi ni vijana au watu wazima, mara kwa mara tunafanya makosa. (Mhu. 7:20) Hata hivyo, ikiwa unataka kubatizwa, ni jambo la hekima ujichunguze ili uone ni kwa kadiri gani umeazimia moyoni mwako kushikamana na viwango vya Yehova. Unawezaje kujua ikiwa umeazimia kabisa kufanya hivyo? Jiulize hivi: ‘Maisha yangu yanaonyesha nini inapohusu kufuata viwango vya Yehova?’ Fikiria jinsi ulivyotenda hivi karibuni ulipokabili majaribu ya imani. Je, umeonyesha kwamba una utambuzi wa kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa? Vipi ikiwa mtu fulani katika ulimwengu wa Shetani anakutendea kwa njia ya pekee, kama ilivyokuwa kwa Danieli? Je, una uwezo wa kuendelea “kufahamu yale yaliyo mapenzi ya Yehova” hata kama yanapingana na kile unachoshawishiwa kufanya?—Efe. 5:17.

10 Kwa nini tunauliza maswali hayo ya moja kwa moja? Kwa sababu yamekusudiwa kukusaidia uwe na mtazamo unaofaa kuhusu ubatizo. Kama ilivyotajwa awali, ubatizo ni ishara ya kwamba umetoa ahadi nzito kwa Yehova mwenyewe. Umeahidi kwamba utampenda na utamtumikia milele kwa moyo wako wote. (Marko 12:30) Kila mtu anayebatizwa anapaswa kuazimia kutimiza ahadi yake.—Soma Mhubiri 5:4, 5.

JE, UNATAMANI KUTOKA MOYONI?

11, 12. (a) Mtu anayefikiria kubatizwa anahitaji kuwa na uhakika gani? (b) Ni nini kitakachokusaidia uwe na maoni yanayofaa kuhusu mpango wa Yehova wa ubatizo?

11 Biblia inasema kwamba watu wa Yehova, wakiwemo vijana, “watajitoa kwa hiari” kwa ajili ya utumishi wake. (Zab. 110:3) Kwa hiyo, mtu anayefikiria kubatizwa anahitaji kuwa na uhakika kwamba yeye binafsi anatamani kufanya hivyo. Hilo linamaanisha kwamba unahitaji kujichunguza kwa makini. Kwa nini? Kwa sababu huenda una hali za pekee ukiwa kijana. Kwa mfano, labda umelelewa na wazazi Mashahidi.

12 Huenda umeshuhudia kwa miaka mingi vijana wengi wakibatizwa, wakiwemo baadhi ya rafiki zako na labda hata wadogo zako. Ikiwa hali yako iko hivyo, basi unahitaji kuwa mwangalifu! Usione ubatizo kama hatua ya kidesturi tu, ambayo vijana wote huchukua wanapofikisha umri fulani. Unaweza kuhakikishaje kwamba utaendelea kuwa na maoni yanayofaa kuhusu mpango wa Yehova wa ubatizo? Tumia wakati mara kwa mara kutafakari kwa nini kubatizwa ni jambo muhimu sana. Kwa kweli, unaweza kupata sababu kadhaa katika makala hii na inayofuata.

13. Unaweza kutambuaje ikiwa uamuzi wako wa kutaka kubatizwa unatoka moyoni?

13 Kuna njia zinazoweza kukusaidia utambue ikiwa uamuzi wako wa kutaka kubatizwa unatoka moyoni. Kwa mfano, sala zako zitafunua wazi ikiwa unatamani kutoka moyoni kumtumikia Yehova. Je, unasali kwa ukawaida? Na ni kwa kadiri gani unataja mambo hususa katika sala zako? Majibu ya maswali hayo yataonyesha wazi uhusiano wako na Yehova ni wa karibu kadiri gani. (Zab. 25:4) Njia muhimu ambayo Yehova hutumia kujibu sala zetu ni kupitia Neno lake. Hivyo, kujifunza Biblia kwa bidii ni njia nyingine ya kuonyesha kwamba tunatamani sana kumkaribia Yehova na kumtumikia kutoka moyoni. (Yos. 1:8) Kwa hiyo, jiulize hivi: ‘Je, huwa ninataja mambo hususa ninaposali? Je, ninajifunza Biblia kibinafsi kwa ukawaida?’ Na ikiwa familia yenu ya Kikristo huwa na Ibada ya Familia, jiulize hivi: ‘Je, ninashiriki kwa hiari katika mpango huo?’ Majibu yako kwa maswali hayo yatakusaidia utambue ikiwa uamuzi wako wa kutaka kubatizwa unatoka moyoni.

MAANA YA KUJIWEKA WAKFU

14. Eleza tofauti iliyopo kati ya kujiweka wakfu na kubatizwa.

14 Huenda wengine hawaelewi tofauti iliyopo kati ya kujiweka wakfu na kubatizwa. Kwa mfano, vijana fulani wanasema kwamba wamejiweka wakfu kwa Yehova lakini hawako tayari kubatizwa. Je, kweli hilo linawezekana? Kujiweka wakfu kunamaanisha kwamba umemwahidi Yehova kuwa utamtumikia milele. Mtu anapobatizwa, anawaonyesha wengine kwamba amejiweka wakfu. Hivyo, ubatizo ni tangazo la hadharani linaloonyesha kwamba tayari umejiweka wakfu kwa Yehova kupitia sala. Kwa hiyo, kabla ya kubatizwa unahitaji kuhakikisha kwamba unaelewa maana ya kujiweka wakfu.

15. Kujiweka wakfu kunamaanisha nini?

15 Kwa ufupi ni kwamba unapoweka maisha yako wakfu kwa Yehova, unajikana mwenyewe. Unamwahidi Yehova kwamba utatanguliza mapenzi yake kuliko kitu kingine chochote maishani mwako. (Soma Mathayo 16:24.) Unahitaji kuchukua kwa uzito ahadi yoyote unayotoa, lakini unapaswa kuchukua kwa uzito hata zaidi ahadi unayotoa kwa Yehova Mungu. (Mt. 5:33) Hata hivyo, unaweza kuonyeshaje kwamba umejikana mwenyewe na sasa wewe ni wa Yehova?—Rom. 14:8.

16, 17. (a) Toa mfano unaoonyesha maana ya kujikana mwenyewe. (b) Mtu anayejiweka wakfu kwa Yehova anatoa ahadi gani?

16 Kwa mfano, wazia kwamba rafiki yako anakupa zawadi ya gari. Anakukabidhi hati rasmi za gari na kukuambia, “Hili ni gari lako.” Lakini tuseme rafiki yako anaongeza hivi: “Nitabaki na funguo. Na mimi ndiye nitakayekuwa nikiendesha gari hili, si wewe.” Ungehisije kuhusu “zawadi” hiyo? Nawe ungemwonaje rafiki huyo?

17 Sasa fikiria kile ambacho Yehova ana haki ya kutarajia kutoka kwa mtu anayejiweka wakfu kwake; mtu ambaye anamwambia hivi: “Ninakupa maisha yangu. Mimi ni wako.” Vipi ikiwa mtu huyo anaanza kuishi maisha ya kinafiki, labda kwa kuanzisha kisiri urafiki wa kimapenzi na mtu ambaye si mwabudu wa Yehova? Au vipi ikiwa anakubali kazi ambayo itamzuia kushiriki kwa nafsi yote katika huduma au mikutano ya Kikristo? Je, hilo halingekuwa sawa na kubaki na funguo za gari? Mtu anapojiweka wakfu kwa Yehova, ni kana kwamba anasema hivi: “Maisha yangu ni mali yako, na si mali yangu. Ikiwa mambo unayotaka nifanye yatapingana na yale ninayotamani kufanya, basi mara zote nitafanya mambo unayotaka nifanye.” Huo ndio uliokuwa mtazamo wa Yesu alipokuwa duniani. Alisema hivi: “Nimeshuka kutoka mbinguni kufanya, si mapenzi yangu, bali mapenzi yake aliyenituma.”—Yoh. 6:38.

18, 19. (a) Maelezo ya Rose na Christopher yanaonyeshaje kwamba kubatizwa huleta baraka? (b) Unahisije kuhusu hatua muhimu sana uliyochukua ya kubatizwa?

18 Ni wazi kwamba kubatizwa ni jambo zito ambalo hatupaswi kulichukulia kijuu juu tu. Wakati huohuo, ni heshima kubwa sana kujiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa. Vijana wanaompenda Yehova na ambao wanaelewa maana ya kujiweka wakfu hawasiti kubatizwa; nao hawajutii kamwe uamuzi wao. Kijana aliyebatizwa aitwaye Rose, anasema hivi: “Ninampenda Yehova, na hakuna jambo linaloweza kunipa furaha zaidi kuliko kumtumikia. Kubatizwa ndio uamuzi bora zaidi niliowahi kufanya maishani.”

19 Namna gani Christopher, aliyetajwa mwanzoni mwa makala hii? Je, uamuzi wake wa kubatizwa alipokuwa na umri wa miaka 12 ulikuwa na msingi mzuri? Christopher anafurahi sana anapofikiria uamuzi wake wa kujiweka wakfu na kubatizwa. Alianza upainia wa kawaida akiwa na umri wa miaka 17 na aliwekwa rasmi kuwa mtumishi wa huduma alipokuwa na miaka 18. Leo anatumikia Betheli. Anasema hivi: “Kubatizwa kulikuwa uamuzi unaofaa. Ninafurahia sana kufanya kazi kwa ajili ya Yehova na tengenezo lake.” Ikiwa unafikiria kubatizwa, unaweza kujitayarishaje? Makala inayofuata itajibu swali hilo.