Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Anawaongoza Watu Wake Katika Njia ya Uzima

Yehova Anawaongoza Watu Wake Katika Njia ya Uzima

“Hii ndiyo njia. Tembeeni ndani yake.”—ISA. 30:21.

NYIMBO: 65, 48

1, 2. (a) Ni onyo gani ambalo limeokoa uhai wa watu wengi? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.) (b) Ni mwongozo gani unaoweza kuokoa uhai wa watu wa Mungu?

“SIMAMA, TAZAMA, SIKILIZA.” Maneno hayo yameokoa uhai wa mamilioni ya watu. Zaidi ya miaka 100 iliyopita, alama kubwa zenye maneno hayo ziliwekwa kwenye vivuko vya reli huko Amerika Kaskazini. Kwa nini? Ili magari yasivuke wakati treni linapita. Naam, kuzingatia onyo hilo kumeokoa uhai.

2 Yehova anafanya jambo bora zaidi kuliko kuweka alama za usalama. Kwa njia ya mfano, anasimama mbele ya watu wake akiwaelekeza waepuke hatari na kuwaongoza kwenye uzima wa milele. Zaidi ya hilo, yeye ni kama mchungaji mwenye upendo, anayewaongoza na kuwaonya kondoo wake ili waepuke njia hatari.—Soma Isaya 30:20, 21.

SIKU ZOTE YEHOVA AMEWAONGOZA WATU WAKE

3. Familia ya wanadamu iliingiaje katika njia inayoongoza kwenye kifo?

3 Katika historia yote, Yehova amekuwa akitoa miongozo na maagizo hususa. Kwa mfano, katika bustani ya Edeni, Yehova alitoa maagizo yaliyo wazi ambayo yangewaongoza wanadamu ili wawe na furaha na waishi milele. (Mwa. 2:15-17) Ikiwa Adamu na Hawa wangetii, wangeepuka madhara makubwa, yaani maisha yaliyojaa maumivu ambayo mwisho wake ni kifo kisicho na tumaini. Lakini badala ya kutii, Hawa alisikiliza ushauri ulioonekana kana kwamba unatoka kwa kiumbe wa hali ya chini. Naye Adamu aliisikiliza sauti ya mke wake, sauti ya mwanadamu anayeweza kufa. Hivyo, wote walimpa kisogo Baba yao mwenye upendo kwa kukataa mwongozo wake. Kwa sababu hiyo, familia ya wanadamu kwa ujumla ikaingia kwenye njia hatari.

4. (a) Kwa nini miongozo mipya ilihitajika baada ya Gharika? (b) Hali mpya ilifunuaje maoni ya Mungu?

4 Katika siku za Noa, Mungu alitoa mwongozo uliookoa uhai. Baada ya Gharika, Yehova alitoa katazo hususa kuhusu damu. Kwa nini alifanya hivyo? Kwa sababu kulikuwa na hali mpya. Yehova alitaka kuwaruhusu wanadamu wale nyama. Hivyo, miongozo mipya ilihitajika. Yehova aliwaambia hivi: “Isipokuwa tu nyama pamoja na nafsi yake—damu yake—msile.” (Mwa. 9:1-4) Hali hiyo mpya ilifunua maoni ya Mungu kuhusu uhai, ambao ni mali yake. Akiwa Muumba na Chanzo cha Uhai, ana haki ya kuweka sheria kuhusu uhai. Kwa mfano, aliamuru kwamba mwanadamu hapaswi kumuua mwanadamu mwenzake. Uhai na damu ni vitu vitakatifu machoni pa Mungu, naye atamtoza hesabu yeyote anayetumia vitu hivyo kwa njia isiyofaa.—Mwa. 9:5, 6.

5. Tutachunguza nini, na kwa nini?

5 Acheni tuchunguze mifano michache ya jinsi Mungu alivyoendelea kutoa miongozo kwa karne zilizofuata. Kuchunguza mambo hayo kutaimarisha azimio letu la kufuata mwongozo wa Yehova tunapoelekea katika ulimwengu mpya.

TAIFA JIPYA, MIONGOZO MIPYA

6. Kwa nini watu wa Mungu walipaswa kutii sheria walizopewa kupitia Musa, nao walihitaji kuwa na mtazamo gani?

6 Katika siku za Musa, miongozo iliyo wazi kuhusu mwenendo unaofaa na jinsi ya kuabudu ilihitajika. Kwa nini? Kwa mara nyingine tena, ni kwa sababu ya mabadiliko ya hali. Kwa zaidi ya karne mbili, wazao wa Yakobo waliishi chini ya utawala wa Misri, nchi iliyojaa ibada ya wafu, ibada ya sanamu, na itikadi na desturi nyingine zisizompendeza Mungu. Watu wa Mungu walipoondoka chini ya uonevu wa Wamisri, walihitaji miongozo mipya. Hiyo ni kwa sababu hawangekuwa watumwa tena, bali wangekuwa taifa huru linaloongozwa na Sheria ya Yehova pekee. Vitabu fulani vya marejeo vinasema kwamba neno la Kiebrania linalotafsiriwa “sheria” linahusiana na neno linalotoa wazo la “kuelekeza, kuongoza, na kuagiza.” Sheria ya Musa ilikuwa kama ukuta uliowalinda dhidi ya ukosefu wa maadili na ibada za mataifa mengine. Waisraeli walipomsikiliza Mungu, walibarikiwa, lakini walipopuuza mwongozo wake, walipata matokeo mabaya.—Soma Kumbukumbu la Torati 28:1, 2, 15.

7. (a) Eleza ni kwa nini Yehova aliwapa watu wake miongozo. (b) Ni kwa njia gani Sheria ilikuwa mtunzaji kwa Waisraeli?

7 Kulikuwa na sababu nyingine iliyofanya kuwe na maagizo mapya. Sheria ya Musa ilitimiza jambo muhimu sana kuhusu kusudi la Yehova. Kusudi hilo lilihusu kuja kwa Masihi, yaani Yesu Kristo. Sheria ilionyesha wazi zaidi kwamba Waisraeli hawakuwa wakamilifu. Iliwasaidia pia kuelewa kwamba wanahitaji fidia, yaani dhabihu kamilifu ambayo ingefunika kabisa dhambi. (Gal. 3:19; Ebr. 10:1-10) Isitoshe, Sheria ilisaidia kulinda ukoo ambao Masihi angetokea na kuwawezesha watu wamtambue. Naam, Sheria ilikuwa kama kiongozi wa muda, au “mtunzaji,” aliyewaongoza watu kwa Kristo.—Gal. 3:23, 24.

8. Kwa nini tunapaswa kuongozwa na kanuni zilizo katika Sheria ya Musa?

8 Tukiwa Wakristo, tunaweza pia kunufaika na miongozo iliyo katika Sheria ambayo taifa la Israeli lilipewa. Jinsi gani? Kwa kutafakari kanuni ambazo ni msingi wa Sheria hiyo. Ingawa hatuko chini ya sheria hizo, tunaweza kuziona kuwa mwongozo bora katika maisha yetu ya kila siku na katika ibada yetu kwa Mungu wetu mtakatifu, Yehova. Alihakikisha kwamba sheria hizo zimeandikwa katika Biblia ili tujifunze, tuongozwe na kanuni zake, na tuthamini viwango vya juu vya maadili vya Kikristo. Fikiria kile ambacho Yesu alisema: “Ninyi mlisikia kwamba ilisemwa, ‘Usifanye uzinzi.’ Lakini mimi ninawaambia ninyi kwamba kila mtu ambaye anaendelea kumtazama mwanamke na kumtamani tayari amefanya uzinzi pamoja naye moyoni mwake.” Kwa hiyo hatupaswi kuepuka tu uzinzi, bali pia tamaa isiyofaa ya ngono.—Mt. 5:27, 28.

9. Ni hali gani mpya zilizotokeza uhitaji wa miongozo mipya kutoka kwa Mungu?

9 Kuja kwa Yesu akiwa Masihi, kulitokeza uhitaji wa mwongozo mpya wa Mungu na kufunuliwa zaidi kwa kusudi la Yehova. Kwa nini? Kwa sababu, hali nyingine mpya zilitokea. Katika mwaka wa 33 W.K., Yehova alilikataa kutaniko la Waisraeli wa asili na akaanza kushughulika na kutaniko la Kikristo.

MWONGOZO KWA AJILI YA TAIFA JIPYA LA KIROHO

10. Kwa nini kutaniko la Kikristo lilipewa sheria mpya, nazo zilitofautianaje na sheria walizopewa Waisraeli?

10 Katika karne ya kwanza, watu wa Mungu waliojiunga na kutaniko la Kikristo walipokea maagizo mapya au maelezo zaidi kuhusu ibada na mwenendo. Watumishi hao waaminifu wa Mungu walikuwa chini ya agano jipya. Waisraeli wa asili pekee ndio waliopewa Sheria ya Musa. Tofauti na hilo, Israeli la kiroho lingejumuisha watu wa mataifa mengi wenye malezi tofauti tofauti. Kwa kweli, “Mungu hana ubaguzi, bali katika kila taifa mtu ambaye anamwogopa na kutenda uadilifu anakubalika kwake.” (Mdo. 10:34, 35) Sheria ya Musa iliwaongoza Waisraeli wa asili walipokuwa katika Nchi ya Ahadi, kupitia sheria zilizochongwa kwenye mawe. Lakini Waisraeli wa kiroho wanaongozwa na “sheria ya Kristo” ambayo msingi wake ni kanuni zilizoandikwa moyoni. Hivyo, Wakristo wangeweza kutumia na kunufaika na “sheria ya Kristo” popote walipo.—Gal. 6:2.

11. “Sheria ya Kristo” inahusisha mambo gani mawili ambayo Wakristo wanahitaji kuzingatia?

11 Israeli la kiroho lingenufaika sana kwa kufuata mwongozo wa Mungu kupitia Mwana wake. Yesu alitoa amri mbili muhimu muda mfupi tu kabla ya kuanzisha agano jipya. Moja ilihusu kazi ya kuhubiri. Nyingine ilikazia mwenendo wa wafuasi wa Yesu na jinsi walivyopaswa kuwatendea waabudu wenzao. Miongozo hiyo ilitolewa kwa ajili ya Wakristo wote; hivyo inawahusu waabudu wote wa kweli leo, iwe wana tumaini la kwenda mbinguni au kuishi duniani.

12. Kazi ya kuhubiri ilihusisha jambo gani jipya?

12 Fikiria kazi ya kuhubiri habari njema ambayo wafuasi wa Yesu walipaswa kufanya. Kazi hiyo ilihusisha mambo mengi zaidi na ilihitaji mbinu mpya. Zamani, watu wa mataifa walikaribishwa walipokuja Israeli kumtumikia Yehova. (1 Fal. 8:41-43) Hali ilikuwa hivyo kabla Yesu hajatoa amri iliyo kwenye Mathayo 28:19, 20. (Soma.) Yesu aliwaambia wanafunzi wake “nendeni” kwa watu wote. Katika Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., Yehova alionyesha wazi kwamba anataka habari njema ihubiriwe katika dunia yote. Roho yake takatifu iliwawezesha Wakristo 120 kuzungumza kimuujiza lugha tofauti tofauti kwa Wayahudi na wageuzwa imani. (Mdo. 2:4-11) Baadaye, walihubiri pia katika eneo la Wasamaria. Kisha, mwaka wa 36 W.K., eneo la kuhubiri liliongezeka zaidi na kuhusisha watu wa Mataifa wasiotahiriwa. Hivyo tunaweza kusema kwamba habari njema ilianza kuhubiriwa kwa Wayahudi na hatimaye kwa watu duniani kote.

13, 14. (a) “Amri mpya” ya Yesu inahusisha nini? (b) Mfano wa Yesu unatufundisha nini?

13 Acheni sasa tuzungumzie jinsi ya kuwatendea waabudu wenzetu. Yesu alianzisha “amri mpya.” (Soma Yohana 13:34, 35.) Amri hiyo inamaanisha kwamba tunapaswa kupendana katika shughuli zetu za kila siku na vilevile kuwa tayari hata kufa kwa niaba ya ndugu zetu. Hilo ni jambo ambalo Sheria ya Musa haikutaja kihususa.—Mt. 22:39; 1 Yoh. 3:16.

14 Yesu aliweka mfano mzuri sana kwa kuwa aliwapenda wanafunzi wake bila ubinafsi. Alikuwa tayari kufa kwa ajili yao. Naye alitazamia wanafunzi wake, tukiwemo sisi, wawe tayari kufanya vivyohivyo. Kwa hiyo, tunapaswa kuwa tayari kuvumilia hali ngumu na labda hata kufa kwa niaba ya Wakristo wenzetu.—1 The. 2:8.

MIONGOZO YA MUNGU SASA NA MILELE

15, 16. Tunakabili hali gani mpya sasa, na Mungu anatuongozaje?

15 Yesu amekuwa akiwaandalia watu wake chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa, hasa tangu alipomweka rasmi “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mt. 24:45-47) Chakula hicho kinahusisha miongozo mipya inayoenda sambamba na hali mpya zinazotokea.

16 Tunaishi wakati ambao Biblia inauita “siku za mwisho,” na mbele yetu kuna dhiki ambayo haijawahi kutokea katika historia. (2 Tim. 3:1; Marko 13:19) Zaidi ya hilo, Shetani na malaika zake wametupwa duniani na wamezuiwa katika ujirani wa dunia; na hilo limesababisha ole kwa wakaaji wa dunia. (Ufu. 12:9, 12) Isitoshe, tumepewa utume wa kufanya kampeni kubwa na isiyo na kifani ya kuwahubiria watu wa mataifa na lugha nyingi kuliko wakati mwingine wowote katika historia!

17, 18. Tunapaswa kupokeaje miongozo tunayopata?

17 Tunapohubiri, tunahitaji kutumia vifaa vinavyoandaliwa na tengenezo la Mungu. Je, unatamani kufanya hivyo? Je, uko tayari kufuata miongozo tunayopokea katika mikutano yetu kuhusu jinsi ya kutumia vifaa hivyo kwa njia bora zaidi? Je, unaona maagizo hayo kuwa mwongozo kutoka kwa Mungu?

18 Kwa kweli, ili tupokee baraka za Yehova, tunahitaji kusikiliza kwa makini miongozo yote inayotolewa kupitia kutaniko la Kikristo. Kuwa watiifu sasa kutatusaidia kufuata miongozo wakati wa “dhiki kuu,” ambayo itaondoa mfumo wote mwovu wa Shetani. (Mt. 24:21) Baada ya hapo, tutahitaji miongozo mipya ya jinsi tutakavyoishi kwenye ulimwengu mpya katika dunia isiyo na ushawishi wa Shetani.

Katika dunia Paradiso, vitabu vya kukunjwa vitafunguliwa ili kutupatia mwongozo wa jinsi tutakavyoishi katika ulimwengu mpya (Tazama fungu la 19 na 20)

19, 20. Ni vitabu gani vya kukunjwa vitakavyofunguliwa, na kutakuwa na matokeo gani?

19 Taifa la Israeli lilihitaji miongozo mipya lilipokuwa chini ya Musa. Baadaye, kutaniko la Kikristo, linaloongozwa na “sheria ya Kristo,” lilihitaji pia miongozo mipya. Vivyo hivyo, Biblia inaeleza kwamba vitabu vya kukunjwa vitafunguliwa ili kutupatia miongozo ya jinsi tutakavyoishi katika ulimwengu mpya. (Soma Ufunuo 20:12.) Inaelekea vitabu hivyo vitaeleza matakwa ya Yehova ambayo wanadamu watahitaji kufuata wakati huo. Watu wote, wakiwemo wale watakaofufuliwa, watajua mapenzi ya Mungu kwa kujifunza vitabu hivyo. Bila shaka, vitabu hivyo vitatusaidia tumjue vizuri zaidi Yehova. Kwa kutegemea ujuzi unaozidi kuongezeka wa Neno la Mungu ambalo limeongozwa na roho, pamoja na mambo yatakayofunuliwa katika vitabu vipya vya kukunjwa, bila shaka wakaaji wa dunia Paradiso watatendeana kwa upendo, heshima, na staha. (Isa. 26:9) Wazia elimu itakayotolewa chini ya uongozi wa Mfalme, Yesu Kristo!

20 Wale wanaofuata ‘mambo yaliyoandikwa katika vitabu vya kukunjwa’ watapata uzima wa milele. Majina ya wale watakaoendelea kuwa waaminifu kwa Mungu na kushinda jaribu la mwisho yatabaki milele kwenye “kitabu cha uzima.” Sisi pia tunaweza kuwa miongoni mwao! Kwa hiyo, tunahitaji KUSIMAMA ili kuchunguza Neno la Mungu, KUTAZAMA ili tuelewe maana yake, na KUSIKILIZA kwa kutii mwongozo wa Mungu sasa. Tukifanya hivyo, tunaweza kutazamia kuokoka dhiki kuu na kuendelea kufurahia daima kujifunza kumhusu Mungu wetu mwenye upendo na hekima yote, Yehova.—Mhu. 3:11; Rom. 11:33.