Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ukaribishaji Wageni​—Sifa Inayovutia na Inayohitajika Sana!

Ukaribishaji Wageni​—Sifa Inayovutia na Inayohitajika Sana!

“Mkaribishane bila kunung’unika.”—1 PET. 4:9.

NYIMBO: 100, 87

1. Wakristo wa karne ya kwanza walikabili hali zipi?

KATI ya mwaka 62 na 64 W.K., mtume Petro aliwaandikia barua “wakaaji wa muda waliotawanyika katika Ponto, Galatia, Kapadokia, Asia, na Bithinia.” (1 Pet. 1:1) Washiriki wa makutaniko hayo ya Asia Ndogo waliokuwa wametoka katika malezi tofauti-tofauti walihitaji kitia-moyo na mwongozo. Walikuwa wakikabili upinzani na walitukanwa. Pia walikabili “majaribu makali.” Nao waliishi katika kipindi kigumu sana. Petro aliwaandikia hivi: “Mwisho wa mambo yote umekaribia.” Naam, katika muda usiozidi miaka kumi, mfumo wa mambo wa Kiyahudi ungekomeshwa kikatili. Ni nini ambacho kingewasaidia Wakristo hao kuvumilia kipindi hicho chenye mikazo mingi?—1 Pet. 4:4, 7, 12.

2, 3. Kwa nini Petro aliwahimiza ndugu zake waonyeshe ukaribishaji wageni? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

2 Kati ya mambo mengi ambayo Petro aliwaandikia ndugu zake, aliwahimiza hivi pia: “Mkaribishane.” (1 Pet. 4:9) Katika Kigiriki neno “ukaribishaji wageni” kihalisi linamaanisha “kuwapenda sana, au kuwatendea kwa fadhili watu tusiowajua.” Hata hivyo, ona kwamba Petro aliwahimiza ndugu na dada zake Wakristo ‘wakaribishane,’ yaani, wawakaribishe watu ambao tayari waliwajua na kushirikiana nao. Ndugu na dada hao wangenufaikaje kwa kuonyesha sifa hiyo ya ukaribishaji wageni?

3 Sifa hiyo ingewasaidia kuwa na uhusiano wa karibu. Fikiria kisa chako mwenyewe. Je, umewahi kukaribishwa na mtu fulani nyumbani kwake? Je, si kweli kwamba unafurahi unapokumbuka pindi hiyo? Ulipowakaribisha baadhi ya washiriki wa kutaniko lenu, je, si kweli kwamba urafiki wenu ulizidi kuimarika? Tunapowakaribisha ndugu na dada zetu, tunapata fursa ya kuwafahamu vizuri zaidi kuliko ambavyo tungewafahamu katika pindi nyinginezo. Kadiri hali zilivyozidi kuwa mbaya, Wakristo katika siku za Petro walihitaji kuwa na uhusiano wa karibu hata zaidi. Ndivyo ilivyo pia kwa Wakristo katika ‘siku hizi za mwisho.’—2 Tim. 3:1.

4. Tutachunguza maswali gani katika makala hii?

4 Tuna fursa zipi za kuonyeshana ukaribishaji wageni? Tunaweza kufanya nini ili kushinda mambo yanayoweza kutuzuia kuwa wakaribishaji wageni? Ni nini kinachoweza kutusaidia kuwa wageni wenye adabu?

FURSA ZA KUWA WAKARIBISHAJI WAGENI

5. Tunaweza kuonyeshaje sifa ya ukaribishaji wageni katika mikutano yetu ya Kikristo?

5 Mikutanoni: Sisi huwakaribisha wote wanaohudhuria mikutano yetu kwa kuwa wao ni wageni wenzetu kwenye mlo wa kiroho. Yehova na tengenezo lake ndio waliotukaribisha. (Rom. 15:7) Wapya wanapohudhuria mikutano yetu tunashirikiana na Yehova na tengenezo lake kuwakaribisha. Kwa nini usichukue hatua ya kwanza kuwakaribisha wapya hao, bila kujali jinsi walivyovalia au kujipamba? (Yak. 2:1-4) Ukimwona mgeni ameketi peke yake, je, unaweza kumwomba aje aketi pamoja nawe? Huenda akathamini jitihada zako za kumsaidia kufuatana na programu au hata kupata maandiko yanayosomwa. Hiyo ni njia nzuri sana ya kuonyesha ‘ukaribishaji wageni.’—Rom. 12:13.

6. Tunapaswa kuwafikiria nani kwanza tunapopanga kuwakaribisha wageni nyumbani kwetu?

6 Kwa ajili ya viburudisho au chakula: Katika nyakati za Biblia, mara nyingi ukaribishaji wageni ulihusisha kuwakaribisha watu nyumbani kwa ajili ya mlo. (Mwa. 18:1-8; Amu. 13:15; Luka 24:28-30) Mtu alipomkaribisha mgeni kwa ajili ya chakula ilikuwa ishara ya urafiki na amani. Tunapaswa kuwafikiria nani kwanza tunapopanga kuwakaribisha wageni? Ni wale tunaoshirikiana nao kwa ukawaida, yaani, ndugu na dada zetu kutanikoni. Hali ngumu zitakapotupata, je, si ni ndugu na dada haohao watakaotusaidia? Tunapaswa kuwa marafiki washikamanifu na kuwa na amani pamoja nao wote. Inafurahisha kujua kwamba katika mwaka wa 2011, Baraza Linaloongoza lilibadili wakati wa Funzo la Mnara wa Mlinzi la familia ya Betheli ya Marekani kutoka saa 12:45 jioni hadi 12:15 jioni. Kwa nini? Tangazo hilo lilisema kwamba inaelekea Wanabetheli wengi watakuwa tayari zaidi kuwakaribisha Wanabetheli wenzao au hata kukubali mwaliko kutoka kwa Wanabetheli wengine iwapo mkutano huo ungeisha mapema. Ofisi nyingine za tawi zilifanya vivyo hivyo pia. Mpango huo umefanya Wanabetheli wawe na uhusiano wa karibu zaidi.

7, 8. Tunaweza kuwaonyeshaje ukaribishaji wageni wawakilishi wa tengenezo la Yehova?

7 Ziara za wasemaji kutoka makutaniko mengine, waangalizi wa mzunguko, na nyakati nyingine wawakilishi kutoka ofisi ya tawi hutupatia fursa za kuonyesha ukaribishaji wageni. (Soma 3 Yohana 5-8.) Mojawapo ya njia nzuri sana ya kuonyesha sifa hiyo ni kuandaa viburudisho au chakula. Je, unaweza kuwakaribisha?

8 Dada mmoja kutoka Marekani anaeleza hivi: “Kwa miaka mingi, mimi na mume wangu tumepata fursa za kuwakaribisha nyumbani kwetu wasemaji wengi pamoja na wake zao. Tulifurahia kila moja ya pindi hizo—zilikuwa zenye kuburudisha, na zaidi ya yote tulijengwa kiroho. Hatujawahi kamwe kujuta kwa kufanya hivyo.”

9, 10. (a) Ni nani ambao huenda wakahitaji kulala nyumbani kwetu kwa muda mrefu? (b) Je, watu ambao nyumba zao ni ndogo wanaweza kuwakaribisha wengine walale kwao? Toa mfano.

9 Wageni wa muda mrefu: Katika nyakati za kale, mara nyingi ukaribishaji wageni ulihusisha kuwaandalia mahali pa kulala wageni walioonekana kuwa wanyoofu. (Ayu. 31:32; Flm. 22) Leo pia, uhitaji kama huo hutokea. Mara nyingi waangalizi wa mzunguko huhitaji mahali pa kulala wanapotembelea makutaniko. Huenda wanafunzi wanaohudhuria shule za kitheokrasi na vilevile wajenzi wakahitaji mahali pa kulala. Huenda familia fulani zikapoteza makazi yao baada ya majanga ya asili, na kwa sababu hiyo wakahitaji mahali pa kuishi hadi watakapopokea msaada wa kujengewa nyumba zao. Hatupaswi kufikia mkataa kwamba wale tu walio na nyumba nzuri na kubwa ndio wanaopaswa kuwakaribisha wengine; huenda tayari wamefanya hivyo mara nyingi sana. Je, unaweza kujitolea kuwakaribisha wengine kulala nyumbani kwako, hata ikiwa nyumba yako ni ndogo?

10 Ndugu mmoja kutoka Korea Kusini anakumbuka jinsi alivyofurahia kuwakaribisha wanafunzi waliokuja kuhudhuria shule za kitheokrasi. Aliandika hivi: “Mwanzoni nilisita kwa sababu tulikuwa tumetoka tu kufunga ndoa na nyumba yetu ilikuwa ndogo. Lakini ilikuwa pindi yenye shangwe kwelikweli kuwaalika wanafunzi ili walale nyumbani kwetu. Tukiwa wenzi wapya wa ndoa, tulipata fursa ya kujionea furaha ambayo wenzi wa ndoa wanaweza kupata wanapomtumikia Yehova na kufuatia miradi ya kiroho wakiwa pamoja.”

11. Kwa nini ndugu na dada waliohamia hivi karibuni katika kutaniko lenu wanahitaji kuonyeshwa ukaribishaji wageni?

11 Ndugu na dada waliohamia hivi karibuni katika kutaniko lenu: Huenda ndugu na dada mmoja-mmoja au familia nzima-nzima zikahamia katika eneo lenu. Baadhi yao huenda wakaja ili watumikie katika eneo lenye uhitaji mkubwa. Mapainia wanaweza kutumwa ili wasaidie katika kutaniko lenu. Kila mmoja wao ameacha mambo aliyokuwa amezoea na sasa amehamia katika eneo jipya, kutaniko jipya, na huenda akalazimika kujifunza lugha mpya au utamaduni mpya. Kuwaalika kwa ajili ya viburudisho, chakula, au kwenye matembezi kutawasaidia wapate marafiki wapya na kuwafanya wazoee mazingira yao mapya.

12. Ni jambo gani lililoonwa linaloonyesha kwamba si lazima ukaribishaji wageni uhusishe mambo mengi?

12 Hatuhitaji kufanya mambo mengi ili kuonyesha sifa ya ukaribishaji wageni. (Soma Luka 10:41, 42.) Ndugu mmoja anasema hivi anaposimulia kuhusu wakati alipoanza utumishi wa umishonari: “Tulikuwa vijana wasio na uzoefu na tuliyakosa sana mazingira ya nyumbani. Jioni moja mke wangu alilemewa sana na hisia za kukosa nyumbani, na jitihada zangu za kumtuliza ziligonga mwamba. Kisha saa 1:30 hivi jioni, tulisikia mlango ukibishwa. Tukafungua mlango na kumwona mwanafunzi wa Biblia akiwa na machungwa matatu kwa ajili yetu. Alikuwa amekuja kutukaribisha kwa kuwa tulikuwa wamishonari wapya. Tulimkaribisha ndani mwanamke huyo na kumpa maji ya kunywa. Kisha tukatayarisha chai na kinywaji cha kakao. Bado hatukuwa tumejua Kiswahili, naye hakujua Kiingereza. Lakini tukio hilo likawa mwanzo wa urafiki wetu pamoja na ndugu wenyeji, jambo tulilofurahia sana.”

KUSHINDA VIZUIZI VYA KUONYESHA UKARIBISHAJI WAGENI

13. Tunanufaikaje kwa kuwa wakaribishaji wageni?

13 Je, umeruhusu fursa za kuonyesha ukaribishaji wageni zikupite? Ikiwa ndivyo, huenda umepoteza fursa za kuwa na ushirika mchangamfu na nafasi ya kupata marafiki wa kudumu. Kuonyesha ukaribishaji wageni ni mojawapo ya dawa bora sana ya kushinda upweke. Lakini huenda ukajiuliza, ‘Kwa nini mtu asite kuonyesha ukaribishaji wageni?’ Kuna sababu kadhaa.

14. Huenda tukahitaji kufanya nini ikiwa tunahisi kwamba hatuna wakati na nguvu za kuonyesha ukaribishaji wageni?

14 Wakati na nguvu: Watumishi wa Yehova wana shughuli nyingi sana na majukumu mengi. Baadhi yao huenda wakahisi kwamba hawana wakati na nguvu za kuonyesha ukaribishaji wageni. Ikiwa hali yako iko hivyo, labda unahitaji kuchunguza shughuli zilizo katika ratiba yako. Je, unaweza kufanya marekebisho fulani ili uweze kuwakaribisha wengine au kukubali mwaliko wao? Maandiko yanawahimiza Wakristo wawe na sifa ya ukaribishaji wageni. (Ebr. 13:2) Si kosa kutenga wakati ili kuonyesha ukaribishaji wageni; kwa kweli hivyo ndivyo tunavyopaswa kufanya. Bila shaka, huenda ukahitaji kuwa tayari kupunguza muda unaotumia katika mambo yasiyo ya lazima.

15. Huenda baadhi ya watu wakawa na wasiwasi gani kuhusu kuwakaribisha wengine?

15 Maoni yako kujihusu: Je, umewahi kutamani kuwakaribisha wageni lakini ukahisi huwezi kufanya hivyo? Wengine wana haya na wanahisi kwamba mazungumzo hayatakuwa yenye kuchangamsha au huenda wageni hawataburudika. Wengine wana kipato kidogo na wanaamini kwamba hawawezi kuwaandalia wageni mambo mazuri kama washiriki wengine wa kutaniko. Kumbuka kwamba jambo muhimu zaidi, si nyumba ya kifahari, bali nyumba yenye mpangilio mzuri, safi, na mwenye nyumba mwenye urafiki.

16, 17. Ni nini kinachoweza kutusaidia kupunguza wasiwasi tunapofikiria kuwakaribisha wageni?

16 Ikiwa unapatwa na wasiwasi unapofikiria kuwakaribisha wageni, si wewe tu unayepitia hali hiyo. Mzee mmoja wa kutaniko kutoka Uingereza anakiri hivi: “Unaweza kupatwa na wasiwasi fulani unapojiandaa kuwakaribisha wageni. Lakini kama tu ilivyo na mambo mengine yanayohusu utumishi wetu kwa Yehova, manufaa na hisia za kuridhika tunazopata huzidi sana wasiwasi wowote ambao huenda tukawa nao. Nimefurahia pindi ambazo nimeketi pamoja na wageni wangu tukinywa kahawa huku tukifurahia mazungumzo.” Kumbuka kwamba sikuzote inafaa kuwaonyesha wageni wako upendezi wa kibinafsi. (Flp. 2:4) Karibu kila mtu hufurahia kusimulia mambo aliyojionea maishani. Pindi za kufurahia ushirika mchangamfu pamoja zinaweza kuwa ndizo pindi pekee ambazo huenda wengine wakatuomba tusimulie mambo tuliyojionea maishani. Mzee mwingine wa kutaniko anaeleza hivi: “Kuwaalika ndugu na dada nyumbani kwangu hunisaidia kuwaelewa vizuri, nami hupata wakati wa kuwajua, hasa jinsi walivyojifunza kweli.” Upendo unapotuchochea kupendezwa kibinafsi na wengine, tutafurahia ushirika mchangamfu pindi zote tunapokuwa pamoja na ndugu na dada zetu.

17 Dada mmoja painia aliyewakaribisha wanafunzi waliokuwa wakihudhuria shule mbalimbali za kitheokrasi, anakiri hivi: “Mwanzoni nilikuwa na wasiwasi kwamba nyumba yangu ilikuwa ya hali ya chini na ilikuwa na fanicha zilizotumika. Mke wa mwalimu fulani wa shule hizo aliniondolea wasiwasi. Aliniambia kwamba wanapozungukia makutaniko, majuma wanayofurahia zaidi ni majuma wanayoishi na mtu wa kiroho ambaye huenda hana vitu vingi vya kimwili lakini ambaye lengo lake kuu ni kama lao—kumtumikia Yehova na kuishi maisha rahisi. Hilo lilinikumbusha jambo ambalo mama yangu alizoea kusema tulipokuwa watoto: ‘Ni afadhali kula mboga za majani mahali penye upendo.’” (Met. 15:17) Acha upendo ukuchochee kuonyesha sifa ya ukaribishaji wageni, nawe hutakuwa na wasiwasi.

18, 19. Sifa ya ukaribishaji wageni inaweza kutusaidiaje kushinda hisia zisizofaa kuelekea wengine?

18 Jinsi unavyohisi kuelekea wengine: Je, kuna mtu kutanikoni anayefanya mambo yanayokuudhi? Huenda mwanzoni ukawa na maoni mabaya kumwelekea na maoni hayo yanaweza kudumu ikiwa hutachukua hatua yoyote kuyarekebisha. Tofauti za utu zinaweza kudhoofisha nia nzuri uliyo nayo ya kuonyesha ukaribishaji wageni. Au huenda zamani mtu fulani alikukosea, nawe umeshindwa kumsamehe.

19 Ili kuboresha uhusiano uliopo kati ya akina ndugu na hata pia maadui wetu, Biblia inapendekeza tuonyeshe sifa ya ukaribishaji wageni. (Soma Methali 25:21, 22.) Kuwaonyesha wengine ukaribishaji wageni kunaweza kupunguza mikwaruzano na kuondoa hisia za chuki. Kufanya hivyo kunaweza kutusaidia kuona sifa nzuri za utu wa mgeni wetu, sifa ambazo Yehova aliona alipomvuta katika kweli. (Yoh. 6:44) Tunapochochewa na upendo kuwakaribisha wengine, mwaliko huo usiotazamiwa unaweza kuwa mwanzo wa uhusiano mzuri sana. Unawezaje kuhakikisha kwamba upendo ndio unaokuchochea kuwakaribisha wengine? Njia moja ya kufanya hivyo ni kufuata kitia moyo kilicho katika andiko la Wafilipi 2:3: “Kwa unyenyekevu mwaone wengine kuwa bora kuliko ninyi.” Kutambua ni kwa njia gani ndugu na dada zetu ni bora kuliko sisi—iwe ni kwa imani yao, uvumilivu wao, ujasiri wao, au sifa nyingine ya Kikristo waliyo nayo—kutafanya tuwe na upendo wenye kina zaidi kuwaelekea na kufungua njia ya kuwaonyesha ukaribishaji wageni kutoka moyoni utakaoboresha uhusiano wetu.

KUWA WAGENI WENYE ADABU

Kwa kawaida wale wanaowakaribisha wageni hujitayarisha vizuri kwa ajili ya wageni wao (Tazama fungu la 20)

20. Kwa nini tunapaswa kutimiza ahadi yetu tunapokubali mwaliko, na tunaonyeshaje kwamba tunauthamini?

20 Mtunga zaburi Daudi aliuliza hivi: “Ee Yehova, ni nani anayeweza kuwa mgeni katika hema lako?” (Zab. 15:1) Baada ya kuuliza swali hilo alizungumzia sifa za kiroho ambazo Mungu anataka wageni wake wawe nazo. Sifa moja ni kutimiza ahadi zetu kwa uaminifu: “Havunji ahadi yake, hata ikimletea hasara.” (Zab. 15:4) Tunapokubali mwaliko, hatupaswi kuvunja ahadi yetu bila sababu nzuri. Huenda aliyetukaribisha amejiandaa sana, na jitihada zake zinaweza kuwa za bure ikiwa tutavunja ahadi yetu. (Mt. 5:37) Baadhi ya ndugu na dada wamevunja ahadi ya mwaliko waliokuwa wamekubali mwanzoni, eti kwa sababu wamepata mwaliko unaoonekana kuwa bora zaidi. Je, tendo hilo linaonyesha upendo na adabu? Badala ya kuvunja ahadi yetu, tunapaswa kukubali mwaliko na kuthamini kutoka moyoni chochote ambacho aliyetukaribisha ametuandalia. (Luka 10:7) Na ikiwa kwa kweli tunalazimika kuvunja ahadi yetu kwa sababu zisizoepukika, ni tendo la upendo na ufikirio kumjulisha aliyetukaribisha haraka iwezekanavyo.

21. Kuheshimu tamaduni zinazotuzunguka kunaweza kutusaidiaje kuwa wageni wenye adabu?

21 Ni muhimu pia kuheshimu tamaduni zinazotuzunguka. Katika tamaduni fulani, watu huwa tayari kuwapokea wageni wasiotarajiwa; katika tamaduni nyingine, wageni wanapaswa kutoa taarifa mapema. Katika maeneo fulani, wale waliowakaribisha wageni huwaheshimu kwa kuwapa vitu bora zaidi walivyo navyo na kuwatanguliza badala ya familia zao; katika maeneo mengine wote hushiriki vitu vilevile pamoja. Katika maeneo fulani, kwa kawaida wageni huleta kitu fulani wanapoalikwa; katika maeneo mengine wale waliowakaribisha wageni hawatarajii mgeni alete chochote. Katika tamaduni fulani, mgeni anatarajiwa akatae mwaliko kwa upole angalau mara moja au mbili; katika tamaduni nyingine kukataa mwaliko kunaonyesha kwamba mtu hathamini mwaliko. Acheni tufanye yote tuwezayo ili waliotukaribisha wafurahi kwamba walitualika.

22. Kwa nini ni muhimu sana ‘tukaribishane’?

22 Sasa, kuliko wakati mwingine wowote, “mwisho wa mambo yote umekaribia.” (1 Pet. 4:7) Tunatarajia dhiki kuu ambayo haijawahi kamwe kuonekana duniani. Kadiri mikazo inavyozidi kuongezeka, ndivyo tutakavyohitaji kuwa na upendo wenye kina zaidi kuelekea ndugu na dada zetu. Leo hasa, shauri la Petro kwa Wakristo linafaa sana: “Mkaribishane.” Ukaribishaji wageni ni sifa inayovutia na inayohitajika sana.—1 Pet. 4:9.