Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Kwa nini michoro ya Mashahidi wa Yehova humwonyesha mtume Paulo akiwa na upara au na nywele chache?

Kusema kweli, hakuna mtu leo anayeweza kujua kwa uhakika mwonekano au sura ya mtume Paulo. Michoro ya mtume Paulo iliyo katika machapisho yetu ni kazi ya sanaa, na si michoro inayotegemea mambo yaliyothibitishwa kwa kuchunguza vitu vya kale.

Hata hivyo, kuna mambo fulani yanayotusaidia kuwazia jinsi mwonekano wa mtume Paulo ulivyokuwa. Kwa mfano, gazeti la Zion’s Watch Tower la Machi 1, 1902, lilitaja jambo moja. Lilisema hivi: “Kuhusu mwonekano wa Paulo: . . . Simulizi la ‘Acts of Paul and Thecla,’ . . . lililoandikwa mwaka wa 150 A. D., linatoa ufafanuzi kuhusu mwonekano wa mtume Paulo, ambao huenda ndio ufafanuzi bora zaidi na unaopatana kabisa na mapokeo. Katika simulizi hilo, Paulo anafafanuliwa kuwa mwenye ‘umbo dogo, upara, matege, mwenye misuli, nyusi zilizokaribiana; na pua ndefu.’”

Kamusi ya The Oxford Dictionary of the Christian Church (toleo la 1997) inasema hivi kuhusu simulizi hilo la kale: “Kuna uwezekano kwamba simulizi hilo lina habari fulani za kihistoria ambazo ni za kweli.” Simulizi la The Acts of Paul and Thecla lilitegemeka sana katika karne za mapema, na hilo linathibitishwa na kupatikana kwa hati 80 za Kigiriki za simulizi hilo, na vilevile tafsiri ya hati hiyo katika lugha nyingine. Hivyo, michoro yetu ya mtume Paulo inapatana na baadhi ya mambo yaliyotajwa katika masimulizi ya kale kuhusu mwonekano wa mtume huyo.

Hata hivyo, kumbuka kwamba kuna mambo mengine yaliyo ya muhimu zaidi kuliko mwonekano wa Paulo. Isitoshe, hata wakati Paulo alipokuwa akiendelea na huduma yake, watu fulani walimkosoa wakisema “akiwapo yeye mwenyewe, ni dhaifu na maneno yake ni yenye kudharaulika.” (2 Kor. 10:10) Lakini hatupaswi kusahau kwamba Paulo alikuja kuwa Mkristo wakati Yesu alipomtokea kwa njia ya kimuujiza. Pia, zingatia mambo ambayo Paulo alitimiza akiwa ‘chombo kilichochaguliwa na Kristo ili kupeleka jina la Yesu kwa mataifa.’ (Mdo. 9:3-5, 15; 22:6-8) Na fikiria manufaa tunayopata kwa kusoma vitabu vya Biblia ambavyo Yehova alimwongoza mtume Paulo kuandika.

Paulo hakujisifia mambo aliyotimiza kabla ya kuwa Mkristo, wala hakufafanua mwonekano wake. (Mdo. 26:4, 5; Flp. 3:4-6) Alikiri hivi: “Mimi ni mdogo zaidi kati ya mitume.” (1 Kor. 15:9) Baadaye, aliandika hivi: “Mimi, niliye mdogo kuliko aliye mdogo zaidi kati ya watakatifu wote, nilipewa fadhili hizi zisizostahiliwa, ili niwatangazie mataifa habari njema kuhusu utajiri usiopimika wa Kristo.” (Efe. 3:8) Ujumbe huo ndio jambo muhimu zaidi tunalopaswa kukazia na si jinsi Paulo alivyoonekana.