Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Nidhamu​—Uthibitisho wa Upendo wa Mungu

Nidhamu​—Uthibitisho wa Upendo wa Mungu

“Yehova huwatia nidhamu wale anaowapenda.”—EBR. 12:6.

NYIMBO: 123, 86

1. Mara nyingi nidhamu hufafanuliwaje katika Biblia?

UNAPOSIKIA neno “nidhamu,” ni jambo gani linalokuja akilini? Mara moja huenda ukafikiria kuhusu adhabu, lakini mengi zaidi yanahusika. Katika Biblia, mara nyingi nidhamu huonyeshwa kuwa jambo zuri, na nyakati nyingine inahusianishwa na ujuzi, hekima, upendo, na uzima. (Met. 1:2-7; 4:11-13) Hiyo ni kwa sababu nidhamu inayotoka kwa Mungu huonyesha kwamba anatupenda na anatamani tupate uzima. (Ebr. 12:6) Ingawa nyakati nyingine nidhamu inayotoka kwa Mungu inaweza kuhusisha adhabu, nidhamu hiyo kamwe si yenye kukandamiza au ya kikatili. Ukweli ni kwamba maana halisi ya neno “nidhamu” inahusiana na kutoa elimu—kama elimu ambayo mzazi humpa mtoto wake mpendwa.

2, 3. Ni katika njia gani nidhamu inaweza kuhusisha kufundisha na pia kutoa adhabu? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

2 Fikiria kuhusu mfano huu: Mvulana mdogo anayeitwa Johnny anacheza mpira ndani ya nyumba. Mama yake anamwambia: “Johnny, unajua vizuri kwamba hupaswi kucheza mpira ndani ya nyumba! Unaweza kuvunja vitu.” Johnny anapuuza maagizo ya mama yake na kuendelea kucheza mpira, na bila kukusudia anavunja chungu cha maua. Mama yake atampa nidhamu ya aina gani? Nidhamu atakayotoa inaweza kutia ndani kumfundisha na pia kumpa adhabu fulani. Anapomfundisha atamweleza Johnny kwa nini jambo alilofanya ni kosa. Atamsaidia atambue hekima ya kuwatii wazazi na kumweleza kwamba sheria wanazoweka ni muhimu na zinafaa. Kisha ili kuonyesha uzito wa maneno yake, mama yake atampa adhabu inayomfaa. Kwa mfano, huenda akachukua mpira wa Johnny ili asicheze nao kwa muda fulani. Hilo litamsaidia kutambua kwamba kutotii huleta matokeo mabaya.

3 Tukiwa washiriki wa kutaniko la Kikristo, sisi ni sehemu ya nyumba ya Mungu. (1 Tim. 3:15) Hivyo, tunaheshimu haki ya Yehova ya kutuwekea viwango na vilevile ya kututia nidhamu kwa upendo tunapovunja viwango hivyo. Zaidi ya hilo, ikiwa matendo yetu yanafanya tupatwe na matokeo mabaya, nidhamu kutoka kwa Mungu itatukumbusha jinsi ilivyo muhimu kumsikiliza Baba yetu wa mbinguni. (Gal. 6:7) Mungu anatujali sana na anataka kutuepusha na mambo yanayoweza kutuletea majonzi.—1 Pet. 5:6, 7.

4. (a) Yehova hubariki mazoezi ya aina gani? (b) Tutazungumzia nini katika makala hii?

4 Tunapotoa nidhamu inayotegemea Biblia, tunaweza kumsaidia mtoto wetu au mwanafunzi wa Biblia kufikia lengo la kuwa mfuasi wa Kristo. Neno la Mungu—kifaa cha msingi tunachotumia kuwazoeza wengine—hutusaidia “kutia nidhamu katika uadilifu.” Hivyo, Biblia inaweza kumsaidia mtoto au mwanafunzi wetu wa Biblia ‘kushika mambo yote ambayo Yesu alituamuru.’ (2 Tim. 3:16; Mt. 28:19, 20) Yehova hubariki mazoezi ya aina hiyo, ambayo huwasaidia wanafunzi wa Biblia kuwazoeza wengine ili nao pia wawe wanafunzi wa Kristo. (Soma Tito 2:11-14.) Sasa acheni tufikirie majibu ya maswali haya matatu muhimu: (1) Nidhamu inayotoka kwa Mungu inaonyeshaje kwamba Mungu anatupenda? (2) Tunaweza kujifunza nini kutoka kwa watu ambao Mungu aliwatia nidhamu zamani? (3) Tunapotoa nidhamu, tunaweza kumwigaje Yehova na Mwana wake?

MUNGU HUTUTIA NIDHAMU KWA UPENDO

5. Nidhamu inayotoka kwa Yehova inaonyeshaje kwamba anatupenda?

5 Yehova huchochewa na upendo kuturekebisha, kutuelimisha, na kutuzoeza ili tudumu katika upendo wake na katika njia ya uzima. (1 Yoh. 4:16) Hatushushii heshima kamwe au kututukana, jambo linaloweza kufanya tuhisi hatuna thamani. (Met. 12:18) Badala yake, Yehova hutuheshimu kwa kukazia sifa nzuri tulizo nazo moyoni, naye huheshimu uhuru wetu wa kuchagua. Je, hivyo ndivyo unavyoiona nidhamu inayotoka kwa Mungu, iwe ni kupitia Neno lake, machapisho yanayotegemea Biblia, wazazi Wakristo, au wazee wa kutaniko? Kwa hakika, wazee wanaojaribu kuturekebisha kwa roho ya upole na upendo tunapochukua “hatua isiyofaa” labda bila kujua, huonyesha upendo ambao Yehova anao kutuelekea.—Gal. 6:1.

6. Kwa nini kumtia mtu nidhamu kwa kumwondolea mapendeleo fulani kutanikoni kunaonyesha kwamba Mungu anampenda?

6 Hata hivyo, nyakati nyingine nidhamu inaweza kuhusisha mengi zaidi ya kumshauri au kumrekebisha mtu. Ikiwa mtu ametenda dhambi nzito, nidhamu inaweza kutia ndani kupoteza mapendeleo kutanikoni. Hata ikiwa mtu anapoteza mapendeleo kutanikoni, nidhamu ya aina hiyo inaonyesha kwamba Mungu anampenda. Kwa mfano, kupoteza mapendeleo kunaweza kumsaidia mtu atambue jinsi ilivyo muhimu kukazia uangalifu zaidi funzo lake la kibinafsi, kutafakari, na kusali. Kwa kufanya hivyo anaweza kuimarishwa kiroho. (Zab. 19:7) Baada ya muda, anaweza kurudishiwa mapendeleo yake. Hata mpango wa kutenga na ushirika watenda dhambi wasiotubu unaonyesha kwamba Yehova anatupenda, kwa sababu kupitia mpango huo kutaniko hulindwa lisiathiriwe na mambo yanayodhuru kiroho. (1 Kor. 5:6, 7, 11) Na kwa kuwa Mungu hutia nidhamu kwa kiwango kinachofaa, mpango wa kutenga na ushirika unaweza kumsaidia mkosaji atambue uzito wa kosa lake na kumchochea atubu.—Mdo. 3:19.

ALINUFAIKA NA NIDHAMU KUTOKA KWA YEHOVA

7. Shebna alikuwa nani, na alianza kusitawisha sifa gani mbaya?

7 Ili kukazia jinsi nidhamu ilivyo yenye thamani, acheni tuchunguze mifano ya wanaume wawili ambao walitiwa nidhamu na Yehova: Shebna, ambaye aliishi katika siku za Mfalme Hezekia, na Graham, ndugu wa nyakati zetu. Shebna alikuwa msimamizi-nyumba ambaye huenda ‘alisimamia nyumba’ ya Hezekia, na kwa hiyo alikuwa na cheo kikubwa. (Isa. 22:15) Hata hivyo, kwa kusikitisha alianza kuwa na kiburi na kujitafutia utukufu wake mwenyewe. Hata alijitengenezea kaburi la kifahari, na alibebwa na “magari . . . yenye utukufu”!—Isa. 22:16-18.

Tunapochochewa na unyenyekevu kurekebisha mtazamo wetu tutapata baraka za Mungu (Tazama fungu la 8 hadi la 10)

8. Shebna alipata nidhamu gani kutoka kwa Yehova, na matokeo yalikuwa nini?

8 Kwa kuwa Shebna alijitafutia utukufu wake mwenyewe, Mungu ‘alimfukuza kutoka katika cheo chake’ na mahali pake akamweka Eliakimu. (Isa. 22:19-21) Badiliko hilo lilitokea wakati Mfalme Senakeribu wa Ashuru alipokuwa akipanga kushambulia jiji la Yerusalemu. Baada ya muda fulani, mfalme huyo aliwatuma Yerusalemu maofisa kadhaa wenye vyeo vikubwa pamoja na jeshi kubwa ili kuwavunja moyo Wayahudi na kumtisha Hezekia ili ajisalimishe. (2 Fal. 18:17-25) Eliakimu alitumwa akazungumze na maofisa hao, lakini hakuwa peke yake. Alikuwa pamoja na watu wengine wawili, na mmoja wao alikuwa Shebna ambaye sasa alikuwa akitumikia akiwa mwandishi. Je, hilo halidokezi kwamba Shebna alikataa kuruhusu uchungu na kinyongo vimlemee na badala yake alikubali kwa unyenyekevu majukumu machache aliyopewa? Ikiwa ndivyo, tunajifunza mambo gani kutokana na simulizi hilo? Acheni tuchunguze mambo matatu.

9-11. (a) Tunajifunza mambo gani muhimu kutokana na kisa cha Shebna? (b) Kuchunguza jinsi Yehova alivyoshughulika na Shebna kumekutiaje moyo?

9 Kwanza, Shebna alipoteza cheo chake. Kisa chake kinatukumbusha onyo hili: “Kiburi hutangulia kuanguka kwa kishindo, na roho ya majivuno hutangulia kujikwaa.” (Met. 16:18) Ikiwa una mapendeleo kutanikoni, ambayo huenda yanakupa kiasi fulani cha umaarufu, je, utaendelea kuwa mnyenyekevu? Je, utampa Yehova utukufu kwa vipawa vyovyote ulivyo navyo au kwa mambo uliyotimiza? (1 Kor. 4:7) Mtume Paulo aliandika hivi: “Ninamwambia kila mtu kati yenu asijifikirie mwenyewe kuliko ilivyo lazima kufikiri, bali afikiri ili awe na akili timamu.”—Rom. 12:3.

10 Pili, Yehova alipompa Shebna karipio kali, inaelekea alikuwa akionyesha kwamba aliamini Shebna angeweza kufanya mabadiliko. (Met. 3:11, 12) Hilo ni somo zuri sana kwa wale ambao huenda wakapoteza mapendeleo katika kutaniko la Mungu leo! Badala ya kukasirika na kuweka kinyongo, wanatiwa moyo kuendelea kumtumikia Mungu kwa uwezo wao wote katika hali waliyo nayo sasa, na kuiona nidhamu kuwa uthibitisho wa upendo kutoka kwa Yehova. Kumbuka, Baba yetu hatatuona kuwa watu wasioweza kubadilika maadamu tunajinyenyekeza mbele zake. (Soma 1 Petro 5:6, 7.) Nidhamu yenye upendo inaweza kuwa njia ya Mungu ya kutufinyanga, hivyo acheni tuendelee kuwa kama udongo laini mikononi mwake.

11 Tatu, wale ambao wamepewa jukumu la kuwapa wengine nidhamu, kama vile wazazi na waangalizi Wakristo, wanajifunza somo muhimu kutokana na jinsi Yehova alivyoshughulika na Shebna. Somo gani? Ingawa nidhamu inayotoka kwa Yehova inaweza kuonyesha jinsi anavyochukizwa na dhambi, inaweza pia kuonyesha kwamba anamjali mtu huyo aliyefanya dhambi. Ikiwa wewe ni mzazi au mwangalizi na unalazimika kutoa nidhamu, je, utamwiga Yehova kwa kuchukia kosa lililofanywa na wakati uleule kuzingatia sifa nzuri ambazo mtoto au mwabudu mwenzako anazo?—Yuda 22, 23.

12-14. (a) Baadhi ya watu huitikiaje wanapopata nidhamu inayotoka kwa Mungu? (b) Neno la Mungu lilimsaidiaje ndugu mmoja kubadili mtazamo wake, na kulikuwa na matokeo gani?

12 Inasikitisha kwamba baada ya kupewa nidhamu, baadhi ya ndugu na dada hulemewa kupita kiasi na hisia za uchungu na hata hujiondoa kutoka kwa Mungu na watu wake. (Ebr. 3:12, 13) Lakini je, hilo linamaanisha kwamba ndugu na dada hao hawawezi kusaidiwa? Mfikirie Graham, ambaye alitengwa na ushirika, na baada ya muda akarudishwa, kisha akawa mhubiri asiyetenda. Miaka kadhaa baadaye alimwomba mzee fulani wa kutaniko aliyekuwa amesitawisha urafiki pamoja naye amfundishe Biblia.

13 Mzee huyo anaeleza hivi: “Graham alikuwa na tatizo la kiburi. Aliwachambua wazee walioshughulikia kisa kilichofanya atengwe na ushirika. Hivyo, katika vipindi kadhaa vilivyofuata vya funzo tulizungumzia Maandiko yanayohusu kiburi na matokeo yake. Baada ya kujitazama vizuri katika kioo cha Neno la Mungu, Graham hakufurahishwa na kile alichoona! Alifanya mabadiliko makubwa sana! Baada ya kutambua kwamba alikuwa amepofushwa na kiburi kilichokuwa kama ‘boriti’ kwenye jicho lake na kwamba yeye ndiye aliyekuwa na tatizo—tatizo la kuwachambua wazee—alianza kufanya mabadiliko mara moja. Alianza kuhudhuria mikutano kwa ukawaida, kujifunza Neno la Mungu kwa bidii, na akasitawisha zoea la kusali kila siku. Pia, alianza kutimiza majukumu yake ya kiroho akiwa kichwa cha familia, jambo lililomfurahisha sana mke na watoto wake.”—Luka 6:41, 42; Yak. 1:23-25.

14 Mzee huyo anaendelea kueleza hivi: “Siku moja Graham aliniambia jambo lililonigusa moyo sana. Alisema, ‘Nimekuwa katika kweli kwa miaka mingi, na hata nimetumikia nikiwa painia. Lakini sasa ndipo ninapoweza kusema kwa unyoofu kwamba ninampenda Yehova.’ Baada ya muda mfupi, Graham alipewa mgawo wa kuzungusha maikrofoni kwenye Jumba la Ufalme, naye alithamini sana pendeleo hilo. Mfano wake ulinifundisha kwamba mtu anapojinyenyekeza mbele za Mungu kwa kukubali nidhamu, Mungu hummiminia baraka!”

MWIGE MUNGU NA KRISTO UNAPOTOA NIDHAMU

15. Ikiwa tungependa nidhamu tunayotoa iwasaidie wengine kufanya mabadiliko, tunapaswa kufanya nini?

15 Ili tuwe walimu wazuri, ni lazima kwanza tuwe wanafunzi wazuri. (1 Tim. 4:15, 16) Vivyo hivyo, ni lazima wale ambao Mungu amewapa jukumu la kutoa nidhamu waendelee kujinyenyekeza kwa kupenda chini ya mwongozo wa Yehova. Wanapojitiisha kwa unyenyekevu chini ya mwongozo Wake, inakuwa rahisi kwa wengine kuwaheshimu, pia wanakuwa na uhuru wa usemi wanapowazoeza au kuwarekebisha wengine. Fikiria mfano wa Yesu.

16. Tunaweza kujifunza mambo gani kutoka kwa Yesu kuhusu nidhamu inayofaa na jinsi ya kuwafundisha wengine kwa njia itakayowagusa moyo?

16 Sikuzote Yesu alimsikiliza na kumtii Baba yake hata ilipokuwa vigumu kufanya hivyo. (Mt. 26:39) Pia, Yesu alimpa Baba yake utukufu kwa mambo aliyofundisha na hekima aliyokuwa nayo. (Yoh. 5:19, 30) Unyenyekevu na utii wa Yesu uliwavuta watu wanyoofu kwake, na ulimfanya awe mwalimu mwenye huruma na neema. (Soma Mathayo 11:29.) Maneno yake yenye fadhili yaliwafariji sana wale ambao kwa njia ya mfano walikuwa kama tete lililovunjika au utambi wa taa uliokuwa karibu kuzimika. (Mt. 12:20) Hata katika hali ambayo ingeonekana kuwa vigumu kuonyesha subira, Yesu alikuwa mwenye fadhili na upendo. Hilo lilionekana wazi alipowarekebisha mitume wake kwa sababu ya kuonyesha roho ya ubinafsi na kutaka makuu.—Marko 9:33-37; Luka 22:24-27.

17. Ni sifa gani zenye kuvutia zitakazowasaidia wazee wawe wachungaji wazuri wa kondoo wa Mungu?

17 Wale ambao Mungu amewapa jukumu la kutoa nidhamu wataonyesha wana hekima wanapoiga mfano wa Kristo. Kwa kweli, wanapofanya hivyo wanaonyesha kwamba wanatamani kuongozwa na Mungu na Mwana wake. Mtume Petro aliandika hivi: “Lichungeni kundi la Mungu lililo chini ya utunzaji wenu, mkiwa waangalizi, si kwa kulazimishwa, bali kwa hiari mbele za Mungu; si kwa kupenda pato lisilo la haki, bali kwa hamu; si kupiga ubwana juu ya wale ambao ni urithi wa Mungu, bali kuwa vielelezo kwa kundi.” (1 Pet. 5:2-4) Kwa hakika, waangalizi wanaojitiisha kwa shangwe kwa Mungu na kwa Kristo ambaye ndiye kichwa cha kutaniko, hunufaika kwa kufanya hivyo na huwanufaisha pia wale walio chini ya uangalizi wao.—Isa. 32:1, 2, 17, 18.

18. (a) Yehova anataka wazazi wafanye nini? (b) Mungu huwasaidiaje wazazi kutimiza majukumu yao?

18 Mambo tuliyozungumzia kuhusu nidhamu na kuwazoeza wengine kwa njia itakayowagusa moyo yanaweza kutumika pia katika familia. Vichwa vya familia wanahimizwa hivi: “Msiwe mkiwakasirisha watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na maagizo ya Yehova.” (Efe. 6:4) Jambo hilo ni zito kadiri gani? Andiko la Methali 19:18 linasema hivi: “Mtie nidhamu mtoto wako wakati bado kuna tumaini, nawe usiwajibike kwa kifo chake.” Naam, wazazi Wakristo watawajibika mbele za Yehova ikiwa hawatawapa watoto wao nidhamu inayohitajiwa! (1 Sam. 3:12-14) Hata hivyo, Yehova huwapa wazazi hekima na uwezo wanaohitaji ikiwa watamsihi kwa unyenyekevu kupitia sala na kutegemea mwongozo wa Neno lake na roho yake takatifu.—Soma Yakobo 1:5.

JIFUNZE JINSI YA KUISHI MILELE KWA AMANI

19, 20. (a) Tutapata baraka gani kwa kukubali nidhamu kutoka kwa Mungu? (b) Tutachunguza nini katika makala inayofuata?

19 Si rahisi kuorodhesha baraka zote tunazopata kwa kukubali nidhamu kutoka kwa Mungu, na kwa kumwiga Yehova na Yesu tunapowapa wengine nidhamu. Mojawapo ya baraka tutakazofurahia ni amani katika familia zetu na katika makutaniko. Pia, kila mmoja wetu atahisi kwamba anapendwa kikweli, anathaminiwa, na kuhisi akiwa salama—mambo ambayo ni kionjo tu cha baraka za wakati ujao. (Zab. 72:7) Kwa kweli, si kutilia chumvi kusema kwamba nidhamu inayotoka kwa Yehova hutufundisha jinsi ya kuishi pamoja milele kwa amani na umoja kama familia chini ya utunzaji wa Baba yetu. (Soma Isaya 11:9.) Tunapokuwa na maoni kama hayo kuhusu nidhamu inayotoka kwa Mungu, inaelekea tutakuwa tayari zaidi kutambua kwamba nidhamu ni uthibitisho wenye kuvutia sana wa upendo usio na kifani ambao Mungu anao kutuelekea.

20 Katika makala inayofuata, tutajifunza mengi zaidi kuhusu nidhamu katika familia na kutanikoni. Pia, tutazungumza kuhusu kujitia nidhamu na vilevile tutazungumzia jambo ambalo ni baya zaidi kuliko maumivu yoyote ya muda mfupi yanayoweza kuletwa na nidhamu.