Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Sikiliza Nidhamu Uwe na Hekima’

‘Sikiliza Nidhamu Uwe na Hekima’

“Wanangu, . . . sikilizeni nidhamu muwe na hekima.”—MET. 8:32, 33.

NYIMBO: 56, 89

1. Tunaweza kufanya nini ili tupate hekima, na tutapata manufaa gani?

YEHOVA ndiye Chanzo cha hekima, naye huwapa wengine hekima hiyo kwa ukarimu. Andiko la Yakobo 1:5 linasema hivi: “Ikiwa yeyote kati yenu anakosa hekima, na aendelee kumwomba Mungu, kwa maana yeye huwapa wote kwa ukarimu na bila kushutumu.” Jambo moja tunaloweza kufanya ili tupate hekima kutoka kwa Mungu ni kukubali nidhamu yake. Hekima hiyo inaweza kutulinda tusipatwe na madhara ya kiadili na ya kiroho. (Met. 2:10-12) Matokeo ni kwamba “[tutajitunza] katika upendo wa Mungu . . . ili hatimaye [tupate] uzima wa milele.”—Yuda 21.

2. Ni nini kinachoweza kutusaidia kuthamini nidhamu inayotoka kwa Mungu?

2 Hata hivyo, mielekeo yetu yenye dhambi, malezi yetu, na mambo mengine yanaweza kufanya iwe vigumu kwetu kukubali nidhamu au kuwa na maoni yanayofaa kuihusu. Sisi huanza kuthamini nidhamu tunapojionea manufaa yake, na hilo hututhibitishia kwamba Mungu anatupenda. Andiko la Methali 3:11, 12 linasema hivi: “Mwanangu, usikatae nidhamu ya Yehova, . . . kwa maana Yehova huwakaripia wale anaowapenda.” Naam, tusisahau kamwe kwamba sikuzote Yehova anataka tufanikiwe. (Soma Waebrania 12:5-11.) Kwa sababu Mungu anatujua vizuri, sikuzote nidhamu yake inafaa na haipiti kiasi. Sasa tuzungumzie mambo manne kuhusiana na nidhamu: (1) jinsi tunavyoweza kujitia nidhamu, (2) nidhamu inayotolewa na wazazi, (3) nidhamu inayotolewa katika kutaniko la Kikristo, na (4) jambo ambalo ni baya zaidi kuliko maumivu ya muda mfupi ya nidhamu.

KUJITIA NIDHAMU HUONYESHA TUNA HEKIMA

3. Mtoto anaweza kukuza uwezo wake wa kujitia nidhamu jinsi gani? Toa mfano.

3 Kujitia nidhamu kunahusisha kujizuia ili tuboreshe tabia na njia yetu ya kufikiri. Hatuzaliwi tukiwa na mwelekeo wa kujitia nidhamu. Lazima tujifunze kufanya hivyo. Kwa mfano: Mtoto anapoanza kujifunza kuendesha baiskeli, kwa kawaida mzazi wake huishikilia ili mtoto asianguke. Lakini kadiri mtoto anapoanza kupata usawaziko, kwa uangalifu mzazi huiachilia baiskeli mara kwa mara. Mtoto anapofaulu kuiendesha baiskeli kwa usawaziko, mzazi huiachilia kabisa. Vivyo hivyo, wazazi wanapoendelea kuwazoeza watoto wao kwa subira “katika nidhamu na maagizo ya Yehova,” wanawasaidia kusitawisha uwezo wa kujitia nidhamu na kuwa na hekima.—Efe. 6:4.

4, 5. (a) Kwa nini kujitia nidhamu ni sehemu muhimu ya “utu mpya”? (b) Kwa nini hatupaswi kukata tamaa hata ikiwa ‘tunaanguka mara saba’?

4 Ndivyo ilivyo pia kwa wale wanaojifunza kumhusu Yehova wakiwa watu wazima. Ni kweli kwamba huenda tayari wana uwezo wa kujitia nidhamu kwa kadiri fulani. Hata hivyo, inapohusu mambo ya kiroho, Mkristo aliyebatizwa karibuni huwa bado hajakomaa kiroho. Lakini hatua kwa hatua, anaweza kukomaa kiroho kwa kujifunza kuvaa “utu mpya” ulio kama wa Kristo. (Efe. 4:23, 24) Kujitia nidhamu ni sehemu muhimu ya ukuzi huo. Tunapojitia nidhamu tunajifunza “kukataa matendo yasiyompendeza Mungu na tamaa za ulimwengu na kuishi kwa utimamu wa akili, uadilifu, na ujitoaji-kimungu katika mfumo huu wa mambo.”—Tito 2:12.

5 Ingawa hivyo, sisi sote tuna mwelekeo wa kufanya dhambi. (Mhu. 7:20) Hata hivyo, kuanguka katika dhambi hakumaanishi kwamba tumeshindwa kabisa kujitia nidhamu au tuna tatizo kubwa sana inapohusu kujitia nidhamu. Andiko la Methali 24:16 linasema hivi: “Mwadilifu anaweza kuanguka mara saba, lakini atainuka tena.” Ni nini kitakachomsaidia afanikiwe? Si jitihada zake mwenyewe, bali roho ya Mungu. (Soma Wafilipi 4:13.) Mojawapo ya sifa ya tunda la roho ni kujizuia, sifa inayohusiana kwa ukaribu na kujitia nidhamu.

6. Tunaweza kufanya nini ili tuwe wanafunzi wazuri zaidi wa Neno la Mungu? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

6 Mambo mengine muhimu yatakayotusaidia kukuza uwezo wetu wa kujitia nidhamu ni kusali kutoka moyoni, kujifunza Biblia, na kutafakari. Lakini vipi ikiwa unaona kujifunza Neno la Mungu kuwa jambo gumu? Labda unahisi wewe si mpenzi wa kusoma. Hata hivyo, kumbuka kwamba Yehova atakusaidia ikiwa utakuwa tayari kukubali msaada wake. Anaweza kukusaidia ‘kukuza hamu’ ya kujifunza Neno lake. (1 Pet. 2:2) Kwanza, mwombe Yehova akusaidie ujitie nidhamu itakayokusaidia kujifunza Neno lake. Kisha, tenda kulingana na sala zako, labda kwa kujifunza kwa vipindi vifupi. Baada ya muda, itakuwa rahisi zaidi kwako kujifunza na utafurahia zaidi kufanya hivyo! Kwa hakika, utatambua kwamba unaanza kufurahia zaidi pindi unazotumia kutafakari na kuzama katika mawazo ya Yehova yenye thamani.—1 Tim. 4:15.

7. Zoea la kujitia nidhamu linaweza kutusaidiaje kufikia malengo ya kiroho?

7 Zoea la kujitia nidhamu hutusaidia kufikia malengo ya kiroho. Fikiria mfano wa ndugu mmoja aliye na familia ambaye alihisi kwamba bidii yake ilikuwa ikipungua. Kwa kuwa alihangaishwa na hali hiyo, alijiwekea lengo la kuwa painia wa kawaida na kusoma makala zilizozungumzia upainia wa kawaida katika magazeti yetu. Mambo hayo pamoja na sala yalimjenga na kumwimarisha kiroho. Pia, alifanya mipango atumikie akiwa painia msaidizi alipopata fursa ya kufanya hivyo. Alipata matokeo gani? Licha ya vipingamizi, alikaza macho yake kwenye lengo lake la kuwa painia wa kawaida na hatimaye akalifikia.

WALEE WATOTO KATIKA NIDHAMU YA YEHOVA

Watoto hawazaliwi wakijua lililo sawa na lililo kosa; wanahitaji kuzoezwa (Tazama fungu la 8)

8-10. Ni nini kinachoweza kuwasaidia wazazi Wakristo wafanikiwe kuwalea watoto wao ili wawe watumishi wa Yehova? Toa mfano.

8 Wazazi Wakristo wana pendeleo lenye thamani—pendeleo la kuwalea watoto wao “katika nidhamu na maagizo ya Yehova.” (Efe. 6:4) Hiyo ni kazi ngumu sana hasa katika ulimwengu wa leo. (2 Tim. 3:1-5) Ni wazi kwamba watoto hawazaliwi wakijua lililo sawa na lililo kosa. Wao huzaliwa wakiwa na dhamiri, lakini dhamiri hiyo inahitaji kuzoezwa au kutiwa nidhamu. (Rom. 2:14, 15) Kitabu kimoja cha marejeo ya Biblia kinadokeza kwamba neno la Kigiriki linalotafsiriwa “nidhamu” linaweza kumaanisha “ukuzi wa mtoto.”

9 Kwa kawaida, watoto wanaotiwa nidhamu kwa upendo huhisi wakiwa salama. Wao hujifunza kwamba uhuru una mipaka na kwamba sikuzote maamuzi na matendo ya mtu huwa na matokeo fulani—iwe ni matokeo mazuri au mabaya. Hivyo basi, ni jambo la muhimu sana kwa wazazi Wakristo kumtegemea Yehova awape mwongozo. Usisahau kwamba njia na mbinu za kuwalea watoto hutofautiana kutoka tamaduni moja hadi nyingine na kutoka kizazi kimoja hadi kingine. Wazazi wanaotegemea hekima kutoka kwa Mungu, hawahitaji kukisia ni njia gani inayofaa ya kuwalea watoto wao, au kutegemea uzoefu au maoni ya wanadamu.

10 Kwa mfano, fikiria mfano wa Noa. Yehova alipomwambia ajenge safina, Noa hakuwa na uzoefu wowote kwa sababu hakuwa amewahi kujenga safina. Hivyo basi, alihitaji kumtegemea Yehova, ili afanye kama Yehova alivyokuwa amemwagiza. “Hivyo ndivyo alivyofanya.” (Mwa. 6:22) Ikawaje? Ingawa ilikuwa mara ya kwanza kujenga safina, Noa hakukosea. Na kwa kweli hakupaswa kukosea! Pia, Noa alifanikiwa kutimiza vizuri jukumu lake akiwa kichwa cha familia kwa sababu ya jambo lilelile lililomsaidia kujenga safina, yaani, kutegemea hekima kutoka kwa Mungu. Hivyo, aliwafundisha watoto wake vizuri na kuwawekea mfano mzuri, jambo ambalo halikuwa rahisi kufanya katika ulimwengu huo mwovu wa kabla ya Gharika.—Mwa. 6:5.

11. Mfano wa wazazi ni muhimu kadiri gani inapohusu kuwazoeza watoto?

11 Biblia inasema hivi kumhusu Noa: “Hivyo ndivyo alivyofanya.” Tukiwa wazazi, tunawezaje kumwiga? Msikilize Yehova. Mruhusu akufundishe jinsi ya kuwalea watoto wako kwa kutumia Neno lake na mwongozo tunaopokea kutoka katika tengenezo lake. Baada ya muda, huenda watoto wako wakakushukuru kwa kufanya hivyo! Ndugu mmoja aliandika hivi: “Ninashukuru sana jinsi wazazi wangu walivyonilea. Walifanya yote waliyoweza ili kufikia moyo wangu. Wazazi wangu walikuwa na mchango mkubwa katika kunisaidia kufanya maendeleo ya kiroho.” Hata hivyo, licha ya jitihada nyingi za wazazi, baadhi ya watoto humwacha Yehova. Ingawa hivyo, wazazi ambao wamejitahidi kadiri wawezavyo kukazia kweli katika moyo wa mtoto wao huwa na dhamiri safi. Wanaweza kutarajia kwamba siku moja mtoto huyo aliyeasi atamrudia Yehova.

12, 13. (a) Mtoto akitengwa na ushirika, wazazi Wakristo wataonyeshaje kwamba wanamtii Mungu? (b) Familia moja ilinufaikaje kwa sababu wazazi walimtii Yehova?

12 Mojawapo ya majaribu makubwa zaidi ambayo baadhi ya wazazi hukabili ni jinsi ya kushughulika na mtoto aliyetengwa na ushirika. Fikiria mfano wa mama mmoja ambaye binti yake aliyetengwa na ushirika aliondoka nyumbani. Mama huyo anakiri hivi: “Nilitafuta katika machapisho yetu visingizio vya kushirikiana na binti yangu pamoja na mjukuu wangu.” Anaendelea kusema, “Lakini kwa fadhili mume wangu alinisaidia kutambua kwamba mtoto wetu hakuwa chini ya utunzaji wetu tena na kwamba tulipaswa kuwa washikamanifu kwa Yehova kwa kuunga mkono nidhamu aliyopewa.”

13 Miaka kadhaa baadaye, binti huyo alirudishwa kutanikoni. Mama yake anasema hivi: “Sasa yeye hunipigia simu au kunitumia ujumbe karibu kila siku! Naye ananiheshimu sana mimi pamoja na baba yake kwa sababu anajua kwamba tulimtii Mungu. Sasa uhusiano wetu ni mzuri sana.” Ikiwa mtoto wako ametengwa na ushirika, je, ‘utamtumaini Yehova kwa moyo wako wote, na kutotegemea uelewaji wako mwenyewe’? (Met. 3:5, 6) Kumbuka, nidhamu ambayo Yehova anatoa hufunua hekima na upendo wake usio na kifani. Usisahau kamwe kwamba alimtoa Mwana wake kwa ajili ya watu wote, kutia ndani mtoto wako. Mungu hataki yeyote aangamizwe. (Soma 2 Petro 3:9.) Hivyo, uwe na imani kwamba nidhamu na mwongozo kutoka kwa Yehova huwa na manufaa sikuzote. Mzazi, hata ikiwa nidhamu na mwongozo kutoka kwa Yehova unakuumiza, endelea kushikamana nao. Naam, unga mkono nidhamu kutoka kwa Mungu, na usiipinge.

NIDHAMU KATIKA KUTANIKO

14. Tunanufaikaje na mafundisho ya Yehova tunayopokea kupitia “msimamizi mwaminifu”?

14 Yehova ameahidi kulitunza, kulilinda, na kuliongoza kutaniko la Kikristo. Anatumia njia mbalimbali kutimiza mambo hayo. Kwa mfano, ameliweka kutaniko chini ya uangalizi wa Mwana wake, ambaye amemweka “msimamizi mwaminifu” ili aandae chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa. (Luka 12:42) Chakula hicho kinachopatikana katika njia mbalimbali, hutupatia mafundisho yenye thamani, au nidhamu. Jiulize, ‘Ni mara ngapi hotuba au makala katika mojawapo ya machapisho yetu imenichochea nifanye mabadiliko katika njia yangu ya kufikiri au mwenendo wangu?’ Ikiwa umefanya mabadiliko, shangilia kwa sababu unamruhusu Yehova akufinyange, au akutie nidhamu kwa faida yako.—Met. 2:1-5.

15, 16. (a) Tunaweza kunufaikaje na ‘wanaume waliotolewa kuwa zawadi’ kutanikoni? (b) Tunaweza kufanya nini ili wazee wafurahie zaidi kazi yao?

15 Pia, Kristo ametupatia “wanaume kuwa zawadi” katika kutaniko—wazee ambao hulichunga kundi la Mungu. (Efe. 4:8, 11-13) Tunaweza kunufaikaje na zawadi hizo zenye thamani? Njia moja ni kwa kuiga imani ya wazee hao na vilevile mfano wao mzuri. Njia nyingine ni kutii mashauri yao yanayotegemea Biblia. (Soma Waebrania 13:7, 17.) Kumbuka, wazee wanatupenda na wanataka tukomae kiroho. Kwa mfano, wakitambua kwamba tunakosa mikutano au bidii yetu inafifia, bila shaka watatusaidia bila kukawia. Watatusikiliza na watajitahidi kututia moyo ili kutuimarisha na kutupatia mashauri yanayofaa ya Kimaandiko. Je, unauona msaada wa aina hiyo kuwa ishara ya kwamba Yehova anakupenda?

16 Kumbuka kwamba nyakati nyingine si rahisi kwa wazee kutufikia ili kutushauri. Kwa mfano, wazia jinsi ilivyokuwa vigumu kwa nabii Nathani kuzungumza na Mfalme Daudi ambaye alijaribu kuficha dhambi nzito aliyotenda! (2 Sam. 12:1-14) Vivyo hivyo, hapana shaka kwamba mtume Paulo alihitaji kuwa na ujasiri ili kumrekebisha Petro, aliyekuwa mmoja wa wale mitume 12, kwa kuwaonyesha upendeleo ndugu zake Wayahudi. (Gal. 2:11-14) Hivyo, unaweza kufanya nini ili kuwarahisishia kazi wazee wa kutaniko lako? Uwe mnyenyekevu, mwenye kufikika, na mwenye shukrani. Uone msaada wao kuwa ishara ya kwamba Mungu anakupenda. Kufanya hivyo kutakunufaisha wewe, nao pia watapata shangwe nyingi wanapofanya kazi yao.

17. Dada mmoja alinufaikaje na msaada wenye upendo ambao wazee wa kutaniko lake walimpa?

17 Kwa sababu ya mambo aliyopitia zamani, dada mmoja alihisi ni vigumu kumpenda Yehova. Anasema hivi: “Mambo na hali nyingine nilizopitia zamani ziliponifanya nishuke moyo, nilijua kwamba sikuwa na budi kuzungumza na wazee. Hawakunikemea wala kunichambua, lakini walinitia moyo na kuniimarisha. Licha ya shughuli nyingi walizokuwa nazo, baada ya kila mkutano angalau mmoja wao alinifikia na kuniuliza ninaendeleaje. Kwa sababu ya mambo niliyopitia zamani, nilihisi kwamba sistahili kupendwa na Mungu. Hata hivyo, mara kwa mara Yehova ametumia kutaniko lake na wazee kunithibitishia kwamba ananipenda. Ninasali kwamba nisimwache kamwe.”

JAMBO BAYA ZAIDI KULIKO MAUMIVU YA NIDHAMU

18, 19. Ni jambo gani baya zaidi kuliko maumivu tunayoweza kupata kwa kukubali nidhamu? Toa mfano.

18 Ingawa huenda nidhamu ikasababisha maumivu, kuna jambo ambalo ni baya zaidi kuliko maumivu hayo—madhara yanayoweza kutokea kwa sababu ya kukataa kukubali nidhamu. (Ebr. 12:11) Fikiria mifano miwili—mfano wa Kaini na Mfalme Sedekia. Kaini alipositawisha chuki kali ya kutaka kumuua Abeli, Mungu alimshauri hivi: “Kwa nini umekasirika sana na kusononeka? Ukitenda mema, je, hutapata kibali tena? Lakini usipotenda mema, dhambi inakunyemelea mlangoni, nayo inatamani sana kukutawala; lakini je, utaishinda?” (Mwa. 4:6, 7) Kaini hakusikiliza. Kisha dhambi ikamzidi nguvu. Kaini alijiletea maumivu na mateso mengi yasiyo ya lazima! (Mwa. 4:11, 12) Maumivu ambayo angepata kwa kukubali karipio la Yehova hayangekuwa makali kama aliyopata alipolikataa.

19 Sedekia, mfalme mwovu na asiye thabiti alitawala wakati ambapo jiji la Yerusalemu lilikaribia kuangamizwa. Nabii Yeremia alimhimiza Sedekia tena na tena aache njia zake mbaya, lakini mfalme huyo alikataa kukubali nidhamu. Kwa mara nyingine tena, matokeo yalikuwa mabaya sana. (Yer. 52:8-11) Yehova anatamani sana kutuepusha na mateso kama hayo yasiyo ya lazima!—Soma Isaya 48:17, 18.

20. Watu wanaokubali nidhamu kutoka kwa Mungu na wale wanaoikataa watapatwa na nini wakati ujao?

20 Katika ulimwengu wa leo, mara nyingi watu hudharau nidhamu, kutia ndani wazo la kujitia nidhamu. Lakini hivi karibuni, watu waovu watajionea madhara ya mtazamo huo wa kipumbavu. (Met. 1:24-31) Hivyo, acheni ‘tusikilize nidhamu ili tuwe na hekima.’ Na kama andiko la Methali 4:13 linavyosema, “shika kabisa nidhamu; usiiache. Ilinde, kwa maana ni uzima wako.”