Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ubatizo​—Takwa kwa Wakristo

Ubatizo​—Takwa kwa Wakristo

“Ubatizo . . . unawaokoa ninyi sasa pia.”—1 PET. 3:21.

NYIMBO: 52, 41

1, 2. (a) Baadhi ya wazazi Wakristo huhisije mtoto wao anapowaambia anataka kubatizwa? (b) Kwa nini wale wanaotaka kubatizwa huulizwa ikiwa wamejiweka wakfu kwa Yehova? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

WAZAZI Wakristo wa msichana tutakayemwita Maria mwenye umri wa miaka 9, walikuwa wakimtazama binti yao alipoinuka pamoja na wengine waliotaka kubatizwa. Kwa sauti kubwa na yenye kusikika vizuri, alijibu maswali mawili ambayo msemaji aliuliza. Muda mfupi baadaye alibatizwa.

2 Wazazi wa Maria walimwonea fahari binti yao kwa uamuzi aliofanya wa kujiweka wakfu kwa Yehova kwa moyo wote na kubatizwa. Ingawa hivyo, mwanzoni mama yake alikuwa na maswali kadhaa yaliyomhangaisha. Alijiuliza hivi: ‘Je, Maria ana umri wa kutosha kubatizwa? Je, kweli anaelewa uzito wa jambo analotaka kufanya? Je, ingekuwa bora zaidi kuruhusu muda fulani upite ndipo abatizwe?’ Hayo ni maswali ambayo wazazi wengi wenye upendo hujiuliza mtoto wao anaposema kwamba anatamani kubatizwa. (Mhu. 5:5) Na hilo linaeleweka kwa sababu wakfu na ubatizo ndizo hatua muhimu zaidi katika maisha ya Mkristo.—Tazama sanduku “ Je, Umejiweka Wakfu kwa Yehova?

3, 4. (a) Mtume Petro alitumia mfano gani kuonyesha umuhimu wa ubatizo? (b) Kwa nini ubatizo unaweza kulinganishwa na ujenzi wa safina katika siku za Noa?

3 Alipokuwa akizungumza kuhusu ubatizo, mtume Petro alirejelea ujenzi wa safina aliposema hivi: “Ubatizo, ambao unalingana na hili, unawaokoa ninyi sasa pia.” (Soma 1 Petro 3:20, 21.) Safina ilikuwa kitu halisi kilichotoa uthibitisho ulio wazi na usiopingika kwamba Noa alijitoa kabisa kufanya mapenzi ya Mungu. Noa alitimiza kwa uaminifu kazi ambayo Yehova alikuwa amempa. Naam, matendo hayo ya imani yaliyoonekana waziwazi yalimfanya Noa na familia yake waokoke Gharika. Mfano huo wa Petro unatufundisha nini?

4 Kama tu ambavyo safina ilitoa uthibitisho ulio wazi kwamba Noa alikuwa na imani, vivyo hivyo kubatizwa mbele ya watazamaji huthibitisha waziwazi kwamba mwanafunzi Mkristo amejiweka wakfu kwa Yehova kwa msingi wa imani katika Kristo aliyefufuliwa. Kama Noa, wanafunzi waliojiweka wakfu hutekeleza kwa utiifu kazi ambayo Mungu amewapa. Kama tu ambavyo Noa aliokoka Gharika, watumishi washikamanifu wa Mungu waliobatizwa wataokoka mfumo huu mwovu utakapoharibiwa. (Marko 13:10; Ufu. 7:9, 10) Hiyo ndiyo sababu inayofanya hatua ya kujiweka wakfu na kubatizwa iwe muhimu sana. Mtu anayeahirisha kubatizwa na kuacha wakati upite bila sababu nzuri anajiweka katika hatari ya kukosa uzima wa milele.

5. Tutachunguza nini katika makala hii?

5 Kwa kuwa ubatizo ni hatua nzito kadiri hiyo, tunahitaji kujiuliza maswali haya matatu. Biblia inasema nini kuhusu ubatizo? Ni hatua zipi ambazo mtu anapaswa kuchukua kabla ya kubatizwa? Kwa nini mwalimu wa Biblia anapaswa kuzingatia akilini mwake umuhimu wa ubatizo anapomfundisha mtoto wake au mwanafunzi mwingine wa Biblia?

UBATIZO UNAOTAJWA KATIKA BIBLIA

6, 7. (a) Ubatizo wa Yohana ulikuwa na maana gani? (b) Yohana alifanya ubatizo gani wa pekee?

6 Ubatizo wa kwanza unaotajwa katika Biblia ni ule uliofanywa na Yohana Mbatizaji. (Mt. 3:1-6) Wale waliomfikia Yohana ili kubatizwa, walifanya hivyo ili kuonyesha kwamba wametubu dhambi walizotenda kwa kuvunja Sheria ya Musa. Hata hivyo, jambo la pekee ni kwamba ubatizo muhimu zaidi ambao Yohana alifanya haukuhusiana kwa vyovyote na suala la toba. Yohana alikuwa na pendeleo la pekee sana la kumbatiza Yesu, Mwana mkamilifu wa kibinadamu wa Mungu. (Mt. 3:13-17) Yesu hakuwa na dhambi, hivyo hakuhitaji kutubu. (1 Pet. 2:22) Ubatizo wake ulionyesha kwamba amejitoa mwenyewe ili kufanya mapenzi ya Mungu.—Ebr. 10:7.

7 Katika kipindi cha huduma ya Yesu duniani, wanafunzi wake pia waliwabatiza watu. (Yoh. 3:22; 4:1, 2) Kama ilivyokuwa kwa ubatizo ambao Yohana alifanya, ubatizo ambao wanafunzi wa Yesu walifanya ulionyesha kwamba wale waliobatizwa wametubu dhambi walizotenda kwa kuvunja Sheria ya Musa. Hata hivyo, baada ya Yesu kufa na kufufuliwa, ubatizo ungekuwa na maana tofauti kabisa kwa wafuasi wake.

8. (a) Baada ya kufufuliwa, Yesu aliwapa wafuasi wake amri gani? (b) Eleza maana ya ubatizo wa Kikristo.

8 Katika mwaka wa 33 W.K., baada ya kufufuliwa Yesu aliutokea umati wa zaidi ya watu 500 uliotia ndani wanaume, wanawake, na huenda hata watoto. Inaelekea alisema maneno haya katika pindi hiyo: “Basi, nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote niliyowaamuru.” (Mt. 28:19, 20; 1 Kor. 15:6) Naam, inaonekana kwamba mamia ya wafuasi wake walikuwepo Yesu alipotoa agizo la kufanya wanafunzi. Hivyo, Yesu alifunua kwamba ubatizo ungekuwa takwa kwa wale ambao wangekubali nira ya kuwa wafuasi wake. (Mt. 11:29, 30) Yeyote ambaye angependa kumtumikia Mungu kwa njia inayokubalika angehitaji kutambua na kukubali jukumu la Yesu katika kutimizwa kwa kusudi la Yehova. Baada ya kufanya mambo hayo, mtu angestahili kubatizwa. Huo ndio ubatizo pekee ambao ungekubalika mbele za Mungu. Biblia ina uthibitisho mwingi kwamba katika karne ya kwanza wanafunzi wapya wa Kristo walielewa maana ya ubatizo. Nao hawakuahirisha isivyo lazima kubatizwa.—Mdo. 2:41; 9:18; 16:14, 15, 32, 33.

USIKAWIE

9, 10. Tunaweza kujifunza nini kutokana na ubatizo wa Mwethiopia aliyegeuzwa imani na wa mtume Paulo?

9 Soma Matendo 8:35, 36. Fikiria mfano wa Mwethiopia aliyegeuzwa imani ambaye alikuwa akirudi nyumbani kutoka Yerusalemu alikokuwa ameenda kuabudu. Akiongozwa na malaika wa Yehova, Filipo alimfikia Mwethiopia huyo na “akamtangazia habari njema kumhusu Yesu.” Mwethiopia huyo aliitikiaje? Jambo alilofanya baada ya hapo lilionyesha wazi kwamba alithamini kutoka moyoni kweli alizojifunza. Alitamani kuishi kulingana na mpango wa Yehova, hivyo akabatizwa bila kukawia.

10 Mfano wa pili ni ule wa mwanamume Myahudi aliyekuwa akiwatesa Wakristo. Alizaliwa katika taifa lililokuwa wakfu kwa Mungu. Hata hivyo, Wayahudi walikuwa wamepoteza uhusiano wao wa pekee pamoja na Yehova. Mwanamume huyo alikuwa na bidii ya kushika desturi za Kiyahudi, lakini akajifunza njia bora zaidi ya kumtumikia Mungu. Yesu Kristo aliyekuwa amefufuliwa na kupewa utukufu, alimtolea ushahidi moja kwa moja. Mwanamume huyo aliitikiaje? Alikubali kusaidiwa na mwanafunzi Mkristo aliyeitwa Anania. Biblia inatuambia hivi: “Kisha akasimama na kubatizwa.” (Mdo. 9:17, 18; Gal. 1:14) Bila shaka umetambua kwamba mwanamume huyo Myahudi ndiye ambaye baadaye alijulikana kuwa mtume Paulo. Lakini zingatia kwamba mara tu alipothamini kweli kuhusu jukumu la Yesu katika kutimizwa kwa kusudi la Mungu, Paulo alichukua hatua. Alibatizwa bila kukawia.—Soma Matendo 22:12-16.

11. (a) Leo, ni nini ambacho huwachochea wanafunzi wa Biblia wabatizwe? (b) Tunahisije tunapoona wanafunzi wapya waliojiweka wakfu wakibatizwa?

11 Hali iko hivyo pia kwa wanafunzi wa Biblia leo, iwe ni vijana au wazee. Wale walio na imani na wanaothamini kweli za Biblia kutoka moyoni hutamani sana kujiweka wakfu na kubatizwa. Hotuba ya ubatizo inayotolewa kwa ajili yao huwa pindi ya pekee katika kila kusanyiko. Mashahidi wa Yehova hushangilia mwanafunzi wa Biblia anapokubali kweli na kufanya maendeleo hadi kufikia hatua ya kubatizwa. Je, si kweli kwamba wazazi Wakristo hufurahi sana kuwaona watoto wao wakiwa miongoni mwa wanafunzi wapya watakaobatizwa? Katika mwaka wa utumishi wa 2017, watu zaidi ya 284,000 wenye “mwelekeo unaofaa” walionyesha wakfu wao kwa Yehova kwa kubatizwa. (Mdo. 13:48) Ni wazi kuwa wanafunzi hao wapya walielewa kwamba ubatizo ni takwa kwa Wakristo. Ni hatua zipi walizochukua ili wastahili kubatizwa?

12. Mwanafunzi wa Biblia anapaswa kuchukua hatua zipi kabla ya kubatizwa?

12 Kabla ya mwanafunzi kubatizwa, ni lazima asitawishe imani inayotegemea ujuzi kumhusu Mungu, kusudi Lake, na mpango Wake wa kuandaa wokovu. (1 Tim. 2:3-6) Imani hiyo humchochea mwanafunzi kukataa kabisa mwenendo unaomchukiza Mungu na kuishi kulingana na viwango vya uadilifu vya Yehova. (Mdo. 3:19) Ukweli ni kwamba mtu hawezi kudai kwamba wakfu wake ni halali ikiwa wakati uleule anajihusisha katika mwenendo ambao utamfanya asistahili kurithi Ufalme. (1 Kor. 6:9, 10) Lakini kuna mengi zaidi yanayohusika kuliko kushikamana tu na viwango vya juu vya Yehova kuhusu maadili. Mtu ambaye anafuatia uadilifu atahakikisha kwamba anahudhuria mikutano ya kutaniko na kushiriki kikamili katika kazi inayookoa uhai ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. Yesu alisema kwamba kazi hiyo ingefanywa na wale ambao kikweli ni wanafunzi wake. (Mdo. 1:8) Ni baada tu ya kuchukua hatua hizo ndipo mwanafunzi mpya anapoweza kujiweka wakfu kwa Yehova kihalali kupitia sala ya faragha, na kisha kubatizwa mbele ya watazamaji kuonyesha kwamba amejiweka wakfu.

WASAIDIE WANAFUNZI WAWE NA LENGO LA KUBATIZWA

Je, unazingatia akilini umuhimu wa ubatizo na kumsaidia mwanafunzi wako aelewe jambo hilo? (Tazama fungu la 13)

13. Kwa nini walimu wa Biblia wanapaswa kuzingatia akilini kwamba ubatizo ni takwa kwa Wakristo?

13 Tunapowasaidia watoto wetu na wanafunzi wengine wa Biblia kuchukua hatua hizo muhimu, tunapaswa kuzingatia akilini kwamba ubatizo ni hatua mojawapo ambayo mtu anapaswa kuchukua ili awe mwanafunzi wa kweli wa Kristo. Hilo likiwa wazi akilini mwetu, itakuwa rahisi zaidi kwetu kuwasaidia wanafunzi wetu kuelewa jambo hilo. Kwa wakati unaofaa, hatutasita kuzungumzia umuhimu wa kujiweka wakfu na kubatizwa. Naam, tungependa watoto wetu na wanafunzi wengine wa Biblia wafanye maendeleo na kufikia hatua ya ubatizo!

14. Kwa nini hatupaswi kumshinikiza yeyote abatizwe?

14 Bila shaka hakuna mtu anayepaswa kushinikizwa na yeyote abatizwe, iwe ni mzazi wake, mwalimu wa Biblia, au mtu mwingine yeyote kutanikoni. Hiyo si njia ya Yehova ya kufanya mambo. (1 Yoh. 4:8) Badala yake, tunapowafundisha wanafunzi wetu wa Biblia, tunapaswa kuwasaidia waone umuhimu wa kusitawisha uhusiano wa kibinafsi pamoja na Mungu. Mwanafunzi anapothamini kutoka moyoni kweli anazojifunza na anapotamani kubeba nira ya kuwa mwanafunzi wa Kristo, atachochewa kubatizwa.—2 Kor. 5:14, 15.

15, 16. (a) Je, kuna umri hususa ambao mtu anapaswa kufikia ili abatizwe? Eleza. (b) Kwa nini ni lazima mwanafunzi wa Biblia abatizwe na kuwa Shahidi wa Yehova hata ikiwa awali alikuwa amebatizwa katika dini nyingine?

15 Hakuna umri hususa ambao mtu anapaswa kufikia ili abatizwe. Kila mwanafunzi wa Biblia hutofautiana inapohusu ukuzi na ukomavu wa kiroho. Watu wengi hubatizwa wangali na umri mdogo, nao hudumu wakiwa waaminifu kwa Yehova. Wanafunzi wengine wa Biblia hujifunza kweli za Biblia na kuona umuhimu wa kubatizwa umri wao ukiwa umesonga—baadhi yao wakiwa na umri wa miaka zaidi ya 100!

16 Mwanafunzi mmoja wa Biblia aliyezeeka alimuuliza mwalimu wake ikiwa kulikuwa na haja ya kubatizwa tena kwa sababu miaka iliyopita alikuwa amebatizwa katika dini tofauti-tofauti. Mwanafunzi huyo na mwalimu wake walichunguza tena Maandiko yaliyozungumzia jambo hilo. Mwanafunzi huyo akaelewa vizuri takwa hilo la Kimaandiko, na muda mfupi baadaye akabatizwa. Ingawa alikuwa na umri unaokaribia miaka 80, hakuhisi kwamba ubatizo ni jambo lisilo la lazima kwake. Naam, msingi wa ubatizo halali ni ujuzi sahihi kuhusu mapenzi ya Mungu. Hivyo, ni lazima wanafunzi wapya wabatizwe hata ikiwa awali walibatizwa katika dini nyingine.—Soma Matendo 19:3-5.

17. Mtu anapaswa kutafakari kuhusu nini katika siku yake ya kubatizwa?

17 Siku ya ubatizo huwa siku yenye shangwe kwelikweli. Pia, ni wakati wa kutafakari kwa uzito kuhusu wakfu na ubatizo na yale yanayohusika. Kuishi kupatana na wakfu wetu huhusisha jitihada nyingi. Hiyo ndiyo sababu Yesu alilinganisha kuwa mwanafunzi wa Kristo na kubeba nira. Ni lazima wanafunzi wa Yesu “wasiishi tena kwa ajili yao wenyewe, bali kwa ajili ya yule aliyekufa kwa ajili yao na kufufuliwa.”—2 Kor. 5:15; Mt. 16:24.

18. Tutachunguza maswali gani katika makala inayofuata?

18 Mama ya Maria alikuwa akifikiria kuhusu mambo hayo alipojiuliza maswali yaliyotajwa kwenye utangulizi. Ikiwa wewe ni mzazi huenda umejiuliza hivi: ‘Je, kweli mtoto wangu yuko tayari kubatizwa? Je, ana ujuzi wa kutosha wa kumsaidia kujiweka wakfu kihalali? Ana malengo gani kuhusu elimu na kazi? Vipi ikiwa mtoto wangu anabatizwa na kisha anatumbukia katika dhambi nzito?’ Katika makala inayofuata, tutazungumzia mambo hayo na jinsi wazazi Wakristo wanavyoweza kudumisha maoni yenye usawaziko kuhusu ubatizo.