Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wazazi, Je, Mnawasaidia Watoto Wenu Wafikie Hatua ya Ubatizo?

Wazazi, Je, Mnawasaidia Watoto Wenu Wafikie Hatua ya Ubatizo?

“Kwa nini unakawia? Simama, ubatizwe.”​—MDO. 22:16.

NYIMBO: 51, 135

1. Wazazi Wakristo wangependa kuhakikisha nini kabla ya watoto wao kubatizwa?

“KWA miezi mingi, niliwaambia Baba na Mama kwamba ningependa kubatizwa, nao walizungumza nami mara nyingi kuhusu jambo hilo. Walitaka kuhakikisha kwamba ninafahamu uzito wa uamuzi wangu. Hatimaye, mwezi wa Desemba 31, 1934, siku hiyo kubwa maishani mwangu ilifika.” Hivyo ndivyo Blossom Brandt alivyosimulia mambo yaliyotukia alipofanya uamuzi wa kubatizwa. Leo pia, wazazi Wakristo wangependa kuwasaidia watoto wao wafanye maamuzi kwa hekima. Kuahirisha ubatizo au kuacha wakati upite bila sababu nzuri ni jambo linaloweza kusababisha matatizo ya kiroho. (Yak. 4:17) Hata hivyo, wazazi wenye hekima watahakikisha kwamba watoto wao wako tayari kubeba jukumu la kuwa wanafunzi wa Kristo kabla ya kubatizwa.

2. (a) Baadhi ya waangalizi wa mzunguko wameripoti tatizo gani? (b) Tutachunguza nini katika makala hii?

2 Baadhi ya waangalizi wa mzunguko wameripoti kwamba kuna baadhi ya vijana walio na umri wa kati ya miaka 16 hadi 23 hivi ambao wamelelewa katika familia za Kikristo lakini bado hawajabatizwa. Katika visa vingi vijana hao huhudhuria mikutano na kushiriki katika huduma. Wao hujitambulisha kuwa Mashahidi wa Yehova. Lakini kwa sababu fulani wanasita kujiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa. Ni nini ambacho huenda kinawafanya wasite? Katika visa fulani, wazazi wao ndio waliowashauri waruhusu muda fulani upite ndipo wabatizwe. Katika makala hii, tutachunguza mambo manne ambayo yamewazuia baadhi ya wazazi Wakristo kuwasaidia watoto wao kufikia hatua ya ubatizo.

JE, MTOTO WANGU ANA UMRI WA KUTOSHA?

3. Wazazi wa Blossom walitaka kujua nini?

3 Wazazi wa Blossom, waliotajwa katika fungu la kwanza, walitaka kujua ikiwa binti yao alikuwa na umri wa kutosha kuelewa maana na uzito wa ubatizo, na hilo linaeleweka. Wazazi wanaweza kujuaje ikiwa mtoto wao yuko tayari kujiweka wakfu?

4. Amri ya Yesu iliyo katika Mathayo 28:19, 20 inaweza kuwasaidiaje wazazi wanapowafundisha watoto wao?

4 Soma Mathayo 28:19, 20. Kama tulivyoona katika makala iliyotangulia, Biblia haitaji umri hususa ambao mtu anapaswa kufikia ili abatizwe. Hata hivyo, wazazi wanaweza kunufaika kwa kufikiria kwa uzito yale yanayohusika katika kumsaidia mtu awe mwanafunzi wa Kristo. Neno la Kigiriki linalotafsiriwa ‘fanya wanafunzi’ katika Mathayo 28:19 lina maana ya kufundisha ukiwa na kusudi la kumfanya mtu awe mfuasi wa Kristo. Mwanafunzi ni yule anayejifunza na kuelewa mafundisho ya Yesu na ambaye ameazimia kuyashika. Hivyo, wazazi wote Wakristo wanapaswa kuwafundisha watoto wao tangu utotoni wakiwa na kusudi la kuwasaidia wabatizwe na kuwa wanafunzi wa Kristo. Ni kweli kwamba mtoto mchanga hawezi kutimiza matakwa ya ubatizo. Hata hivyo, Biblia inaonyesha kwamba hata watoto wenye umri mdogo wanaweza kuelewa na kuthamini kweli za Biblia.

5, 6. (a) Maelezo ya Biblia kumhusu Timotheo yanatusaidia kufikia mkataa gani kuhusu ubatizo wake? (b) Wazazi wenye utambuzi wanaweza kuwasaidiaje watoto wao kwa njia nzuri zaidi?

5 Timotheo alikuwa mwanafunzi wa Kristo aliyeifanya kweli kuwa mali yake akiwa na umri mdogo. Mtume Paulo alitaja kwamba Timotheo alijifunza kweli za Kimaandiko tangu utotoni. Hata ingawa Timotheo alilelewa katika familia iliyogawanyika kidini, mama na nyanya (bibi) yake ambao walikuwa Wayahudi, walimsaidia kuthamini Maandiko kulingana na jinsi Wayahudi walivyoyaelewa. Na hilo lilifanya imani yake iwe thabiti. (2 Tim. 1:5; 3:14, 15) Kufikia wakati alipokuwa na umri wa miaka 20 hivi, tayari Timotheo alikuwa mwanafunzi wa Kristo ambaye angeweza kupewa mapendeleo ya pekee kutanikoni.—Mdo. 16:1-3.

6 Bila shaka, kila mtoto ni tofauti na mwingine; na wote hawafikii ukomavu wa kiroho katika umri uleule. Baadhi yao huonyesha kwa kiasi fulani ukomavu wa kiakili na kihisia wakiwa wangali na umri mdogo, na hivyo hufunua tamaa yao ya kutaka kubatizwa. Na wengine huenda wasiwe tayari kubatizwa hadi umri unaposonga kidogo. Hivyo, wazazi wenye utambuzi hawawashinikizi watoto wao wabatizwe. Badala yake, wao humsaidia kila mtoto kufanya maendeleo ya kiroho kulingana na uwezo wake. Wazazi wanaweza kushangilia mtoto wao anapoonyesha kwamba anaelewa maana ya andiko la Methali 27:11. (Soma.) Hata hivyo, hawapaswi kamwe kusahau lengo walilo nalo la kuwasaidia watoto wao kuwa wanafunzi wa Kristo. Wakiwa na lengo hilo akilini, wazazi wanaweza kufikiria swali hili, ‘Je, mtoto wangu ana ujuzi wa kutosha wa kumsaidia ajiweke wakfu kwa Mungu na kubatizwa?’

JE, MTOTO WANGU ANA UJUZI WA KUTOSHA?

7. Je, ni lazima mtu ajue kila kitu kuhusu Biblia ndipo abatizwe? Eleza.

7 Wakiwa walimu katika familia, kwa kufaa wazazi wangependa kuwasaidia watoto wao kupata msingi thabiti wa ujuzi ambao unaweza kuwasaidia kujiweka wakfu. Hata hivyo, ili mtu ajiweke wakfu kwa Mungu na kubatizwa si lazima ajue kila kitu. Baada ya kubatizwa wanafunzi wote wa Kristo wanapaswa kuendelea kukua katika ujuzi sahihi. (Soma Wakolosai 1:9, 10.) Hivyo basi, mtu anapaswa kuwa na ujuzi mwingi kadiri gani kabla ya kubatizwa?

8, 9. Tunaweza kujifunza mambo gani kutokana na simulizi la Paulo na mlinzi wa jela?

8 Kisa cha familia moja katika karne ya kwanza kinaweza kuwasaidia wazazi. (Mdo. 16:25-33) Paulo alipokuwa kwenye safari yake ya pili ya umishonari, karibu mwaka wa 50 W.K., alitembelea jiji la Filipi. Akiwa huko yeye na Sila mwandamani wake walikamatwa na kufungwa gerezani kwa mashtaka ya uwongo. Wakati wa usiku, tetemeko la ardhi lilitetemesha misingi ya jela na milango yote ikafunguka. Mlinzi wa jela alikuwa karibu kujiua akidhani kwamba wafungwa walikuwa wametoroka, lakini Paulo akamzuia. Paulo na Sila walifanikiwa kumhubiria mlinzi huyo wa jela pamoja na familia yake. Kweli walizojifunza kumhusu Yesu ziliwachochea kuchukua hatua gani? Walibatizwa bila kukawia. Tunajifunza nini kutokana na simulizi hili?

9 Inaelekea mlinzi huyo alikuwa ofisa-jeshi Mroma aliyekuwa amestaafu. Hakujua Maandiko. Hivyo, ili awe na msingi imara wa ujuzi wa Maandiko, alihitaji kujifunza kweli za msingi za Biblia, kuelewa yale yanayohusika ili mtu awe mtumishi wa Mungu, na kuazimia kabisa kutii mafundisho ya Yesu. Katika kipindi kifupi cha wakati, ujuzi na uthamini aliopata kuhusu mafundisho ya msingi ya Maandiko ulimchochea abatizwe. Bila shaka aliendelea kuongeza ujuzi wake hata baada ya kubatizwa. Ukiwa na wazo hilo akilini, unaweza kufanya nini mtoto wako akionyesha kwamba anathamini kutoka moyoni mafundisho ya msingi ya Maandiko, na kwamba anaelewa maana na umuhimu wa kujiweka wakfu na kubatizwa? Ninyi wazazi Wakristo mnaweza kufikia mkataa kwamba anaweza kuzungumza na wazee wa kutaniko ili waamue ikiwa anastahili kubatizwa. * Kama ilivyo kwa wanafunzi wengine waliobatizwa, yeye pia ataendelea kuongeza ujuzi wake kuhusu kusudi la Yehova kwa muda wote wa maisha yake au hata milele.—Rom. 11:33, 34.

NI ELIMU GANI ITAKAYOMNUFAISHA KIKWELI MTOTO WANGU?

10, 11. (a) Baadhi ya wazazi wamefikia mkataa gani? (b) Mzazi anapaswa kuhangaikia nini kwanza?

10 Baadhi ya wazazi wamefikia mkataa kwamba ni afadhali kwanza mwana au binti yao aahirishe kubatizwa ili aongeze elimu yake na kupata kazi nzuri. Huenda wazazi hao hawana nia mbaya wanapofikiri kwa njia hiyo, lakini je, kufanya hivyo kutamsaidia mtoto wao apate mafanikio ya kweli? Na jambo muhimu hata zaidi ni, je, uamuzi huo unapatana na Maandiko? Neno la Yehova linatutia moyo tufuatie mambo gani maishani?—Soma Mhubiri 12:1.

11 Ni muhimu kukumbuka kwamba ulimwengu huu na vyote vilivyomo vinapingana na mawazo na mambo ambayo Yehova anapenda. (Yak. 4:7, 8; 1 Yoh. 2:15-17; 5:19) Ulinzi bora zaidi ambao mtoto anaweza kuwa nao dhidi ya Shetani, ulimwengu wake, na mtazamo wake mwovu ni kuwa na uhusiano wa karibu na Yehova. Mzazi anapotanguliza na kusisitiza ufuatiaji wa miradi ya kimwili, anaweza kumchanganya mtoto na kumfanya asifuatie mambo ambayo yatamnufaisha kikweli. Mzazi Mkristo anayempenda mtoto wake, je, kweli angependa ulimwengu huu umfundishe mtoto wake kuhusu mambo anayopaswa kuyaona kuwa mafanikio ya kweli? Ukweli ni kwamba tutapata furaha na mafanikio ya kweli iwapo tu tutamtanguliza Yehova maishani.—Soma Zaburi 1:2, 3.

VIPI MTOTO WANGU AKITENDA DHAMBI?

12. Kwa nini wazazi fulani wanataka watoto wao waahirishe kubatizwa?

12 Mama mmoja Mkristo alipokuwa akieleza sababu iliyomfanya amzuie binti yake kubatizwa, alisema hivi: “Ninaaibika kusema kwamba sababu kuu iliyonifanya nimzuie kubatizwa ni mpango wa kutenga na ushirika.” Kama dada huyo, wazazi fulani hufikiri kwamba ni afadhali mtoto wao aahirishe kubatizwa hadi atakapopita umri ambao kwa kawaida watoto huwa na mwelekeo wa kutenda kipumbavu. (Mwa. 8:21; Met. 22:15) Huenda wakasema, ‘Maadamu mtoto wangu hajabatizwa, hawezi kutengwa na ushirika.’ Kwa nini kufikiri kwa njia hiyo ni kujidanganya?—Yak. 1:22.

13. Je, kuahirisha kubatizwa humfanya mtu asiwajibike mbele za Yehova? Eleza.

13 Inaeleweka kwa nini wazazi Wakristo hawangependa mtoto wao abatizwe hadi atakapokomaa vya kutosha kustahili kujiweka wakfu. Hata hivyo, lingekuwa kosa kwa mzazi kufikiri kwamba kwa kuwa mtoto wake hajabatizwa, basi hawajibiki kwa Yehova. Kwa nini? Kuwajibika mbele za Yehova hakutegemei kubatizwa. Badala yake, mtoto anawajibika mbele za Mungu anapojua yaliyo sawa na yasiyo sawa machoni pa Yehova. (Soma Yakobo 4:17.) Hivyo, badala ya kumvunja moyo mtoto asibatizwe, wazazi wenye hekima hufanya juu chini ili wao wenyewe wawe mfano mzuri. Wangependa kumsaidia mtoto wao athamini kutoka moyoni viwango vya juu vya maadili vya Yehova tangu akiwa mchanga. (Luka 6:40) Kuthamini viwango hivyo ndio ulinzi bora zaidi, kwa sababu mtoto wako atachochewa kushikamana na njia ya Yehova ya uadilifu.—Isa. 35:8.

WENGINE WANAWEZA KUKUSAIDIA

14. Wazee wanaweza kuungaje mkono jitihada za wazazi za kuwasaidia watoto wao wafikie ubatizo?

14 Wakiwa wachungaji wa kiroho, wazee wanaweza kuunga mkono jitihada za wazazi kwa kusema mambo mazuri kuhusu malengo ya kiroho. Dada mmoja ambaye alitumikia akiwa painia kwa zaidi ya miaka 70, anakumbuka jinsi mazungumzo yake pamoja na Ndugu Charles T. Russell yalivyomchochea alipokuwa na umri wa miaka sita tu. Anaeleza hivi: “Alizungumza nami kwa dakika 15 kuhusu malengo yangu ya kiroho.” Naam, maneno yenye kujenga yanaweza kumchochea mtu kwa muda mrefu sana. (Met. 25:11) Pia, wazee wanaweza kuwahusisha wazazi pamoja na watoto wao kwenye kazi mbalimbali katika Jumba la Ufalme, na kuwapa vijana kazi zinazolingana na umri na uwezo wao.

15. Wengine katika kutaniko wanaweza kuwatia moyo vijana katika njia zipi?

15 Washiriki wa kutaniko wanaweza kuwasaidia wazazi kwa kupendezwa kibinafsi na vijana. Hilo linatia ndani kuwa macho ili kutambua ishara yoyote ya maendeleo ya kiroho. Je, kijana fulani ametoa maelezo yanayotoka moyoni, yaliyotayarishwa vizuri au kutoa sehemu katika mkutano wa katikati ya juma? Je, kuna kijana ambaye ameshinda jaribu la utimilifu au kutumia vizuri fursa aliyopata kutoa ushahidi shuleni? Usikawie kuwapongeza kwa unyoofu. Unaonaje ukijiwekea lengo la kuzungumza na kijana mmoja—kabla au baada ya mkutano—na kumwonyesha kwamba unapendezwa naye kikweli? Mambo kama hayo na mengine, yanaweza kuwafanya vijana watambue kwamba wao ni sehemu ya “kutaniko kubwa.”—Zab. 35:18.

MSAIDIE MTOTO WAKO AFIKIE UBATIZO

16, 17. (a) Ubatizo unahusianaje na tumaini la wakati ujao la kila mmoja wetu? (b) Wazazi wote Wakristo hujitahidi kupata shangwe gani? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

16 Kumlea mtoto katika “nidhamu na maagizo ya Yehova” ni mojawapo ya mapendeleo makubwa zaidi ambayo mzazi Mkristo anaweza kuwa nayo. (Efe. 6:4; Zab. 127:3) Tofauti na watoto waliozaliwa katika taifa la kale la Israeli, watoto wa wazazi Wakristo hawazaliwi wakiwa wakfu kwa Yehova. Isitoshe, mtu hawezi kurithi kumpenda Mungu na kweli ya Biblia. Tangu mtoto anapozaliwa, wazazi wanapaswa kuwa na nia ya kumfanya awe mwanafunzi wa Kristo kwa kumsaidia awe mtumishi wa Yehova aliyejiweka wakfu na kubatizwa. Bila shaka, hakuna jambo lingine muhimu zaidi ya hilo. Ukweli wa mambo ni kwamba jambo litakalomsaidia mtu kuokoka dhiki kuu inayokaribia ni wakfu na ubatizo wake pamoja na kumtumikia Mungu kwa uaminifu.—Mt. 24:13.

Wazazi wanapaswa kuwa na lengo la kumsaidia mtoto wao awe mwanafunzi wa Kristo (Tazama fungu la 16 na 17)

17 Blossom Brandt alipoamua kwamba alitaka kubatizwa, wazazi wake waliomwogopa Mungu walitaka kuhakikisha kwamba alikuwa tayari kuchukua hatua hiyo muhimu zaidi maishani mwake. Walipokuwa na uhakika kwamba alikuwa tayari, waliunga mkono uamuzi wake. Usiku uliotangulia siku ya ubatizo wake, baba yake alifanya jambo fulani linalovutia. Blossom anaeleza hivi: “Alituomba sote tupige magoti, kisha akatoa sala. Alimwambia Yehova kwamba alikuwa amefurahi sana kwa sababu ya uamuzi ambao binti yake mdogo alikuwa amefanya wa kujiweka wakfu Kwake.” Zaidi ya miaka 60 hivi baadaye, Blossom anasema, “Kwa hakika, sitasahau kamwe usiku huo maisha yangu yote!” Wazazi, na mpate shangwe na furaha inayotokana na kuwaona watoto wenu wakiwa watumishi wa Yehova waliojiweka wakfu na kubatizwa.

^ fu. 9 Wazazi wanaweza kuzungumzia pamoja na watoto wao habari zinazopatikana kwenye kitabu, Maswali Ambayo Vijana Huuliza​—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 2, uku. 304-310. Tazama pia “Sanduku la Swali” kwenye Huduma Yetu ya Ufalme, ya Aprili 2011, uku. 2.