Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

Yehova Hajawahi Kamwe Kuniacha!

Yehova Hajawahi Kamwe Kuniacha!

Nilikuwa miongoni mwa wasichana wanne wadogo waliochaguliwa kumkabidhi maua Adolf Hitler baada ya kutoa hotuba pindi moja. Kwa nini nilichaguliwa? Baba alijihusisha sana na shughuli za Wanazi na alikuwa dereva wa kiongozi fulani wa tawi la chama hicho. Mama alishikamana sana na imani ya Kikatoliki na alitaka niwe mtawa. Licha ya kulelewa katika hali hizo, sikujiunga na Wanazi wala kuwa mtawa. Acheni niwaeleze sababu.

NILILELEWA katika jiji la Graz, nchini Austria. Nilipofikisha umri wa miaka saba, nilipelekwa kwenye shule ya mazoezi ya kidini. Hata hivyo, nilishuhudia upotovu mkubwa sana wa kingono na wenye kushtua kati ya makasisi na watawa. Hivyo mwaka huohuo mama yangu aliniruhusu niondoke kwenye shule hiyo.

Familia yetu, Baba akiwa amevaa mavazi ya kijeshi

 

Baadaye, nilienda kwenye shule ya bweni. Siku moja baba alikuja shuleni na kunichukua kwa sababu jiji la Graz lilikuwa likishambuliwa vikali kwa mabomu. Tulikimbilia katika mji wa Schladming. Baada tu ya kufika katika mji huo na kuvuka daraja fulani, daraja hilo lililipuliwa. Katika pindi nyingine, ndege zilizokuwa zikipaa na kupita karibu na watu zilitufyatulia risasi mimi na Bibi (Nyanya) tulipokuwa kwenye ua wetu. Vita vilipokwisha, ilionekana kwamba kanisa na serikali vilikuwa vimetukatisha tamaa.

NAJIFUNZA KUHUSU CHANZO CHENYE KUTEGEMEKA CHA MSAADA

Katika mwaka wa 1950, Shahidi fulani wa Yehova alianza kujifunza Biblia pamoja na Mama. Nilisikiliza mazungumzo yao na hata kuhudhuria baadhi ya mikutano pamoja na Mama. Baada ya kusadiki kwamba Mashahidi wa Yehova walifundisha kweli, Mama alibatizwa mwaka wa 1952.

Katika kipindi hicho, nililiona kutaniko hilo kuwa mahali ambapo akina mama wazee-wazee walikutana. Hata hivyo baadaye, tulitembelea kutaniko fulani lililokuwa na vijana wengi—kumbe kutaniko si la akina mama wazee-wazee pekee! Niliporudi katika jiji la Graz, nilianza kuhudhuria mikutano yote, na punde si punde mimi pia nilisadiki kwamba mambo niliyokuwa nikijifunza ni kweli. Nilijifunza pia kwamba Yehova ni Mungu anayewapa watumishi wake msaada unaotegemeka sikuzote. Yeye hututegemeza hata tunapohisi ni kana kwamba tunakabili hali fulani zinazozidi uwezo wetu tukiwa peke yetu.—Zab. 3:5, 6.

Nilitaka kushiriki na wengine kweli hizo. Nilianza kuwahubiria dada zangu na kaka yangu. Tayari dada zangu wanne walikuwa wameondoka nyumbani na walikuwa walimu. Lakini niliwatembelea katika vijiji walivyoishi na kuwatia moyo wajifunze Biblia. Hatimaye, kaka na dada zangu wote walijifunza Biblia na kuwa Mashahidi wa Yehova.

Katika juma langu la pili nilipokuwa nikihubiri nyumba kwa nyumba, nilikutana na mwanamke mwenye umri wa miaka 30 na kitu, na tukaanza kujifunza Biblia. Alifanya maendeleo na kubatizwa na baadaye mume na wanaye wawili walibatizwa pia. Kujifunza naye Biblia kuliimarisha sana hali yangu ya kiroho. Kwa nini? Kwa sababu hakuna yeyote aliyekuwa ameongoza funzo rasmi la Biblia pamoja nami. Nilihitaji kujitayarisha vizuri kwa ajili ya kila somo. Kwa njia fulani, nilifanya hivyo ili kwanza nijifunze mwenyewe kisha nimfundishe mwanafunzi wangu! Kufanya hivyo kulinisaidia niielewe kweli kwa kina zaidi. Katika mwezi wa Aprili, mwaka wa 1954, nilijiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa.

“TUNATESWA, LAKINI HATUACHWI BILA MSAADA”

Katika mwaka wa 1955, nilihudhuria makusanyiko ya kimataifa nchini Ujerumani, Ufaransa, na Uingereza. Nilipokuwa London, nilikutana na Albert Schroeder. Alikuwa mwalimu wa Shule ya Gileadi, na baadaye alitumikia akiwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza. Tulipokuwa tukitembelea Jumba la Makumbusho la Uingereza, Ndugu Schroeder alituonyesha baadhi ya hati za zamani za Biblia. Hati hizo zilikuwa na jina la Mungu katika herufi za Kiebrania, na Ndugu Schroeder alitueleza umuhimu wa hati hizo. Jambo hilo lilinigusa moyo sana na kunichochea kiroho, nalo lilinifanya niazimie kuliko wakati mwingine wowote kutangaza kweli ya Neno la Mungu.

Nikiwa pamoja na mwandamani wangu (kulia), tukitumikia tukiwa mapainia wa pekee Mistelbach, Austria

Nilianza kutumikia nikiwa painia wa wakati wote katika mwezi wa Januari 1, 1956. Miezi minne baadaye, nilipewa mgawo wa kuwa painia wa pekee nchini Austria. Wakati huo hakukuwa na Shahidi yeyote katika mji wa Mistelbach, mji niliokuwa nimetumwa. Isitoshe, nilikabili changamoto fulani hususa. Mimi na painia mwenzangu tulikuwa tofauti sana. Nilikuwa nikikaribia kutimiza umri wa miaka 19 na nililelewa jijini; na painia mwenzangu alikuwa na umri wa miaka 25 na alilelewa kijijini. Mimi sikupenda kuamka mapema lakini yeye alipenda kuamka mapema. Jioni nilizoea kuchelewa kulala lakini yeye alipenda kulala mapema. Lakini licha ya hayo, kutumia ushauri wa Biblia kulitusaidia kushughulikia vizuri tofauti zetu na kufurahia kushirikiana pamoja tukiwa mapainia.

Kwa kweli, tulikabili changamoto nyingine kubwa. Hata tulikabili mateso fulani, lakini ‘hatukuachwa bila msaada.’ (2 Kor. 4:7-9) Siku moja tulipokuwa tukihubiri kijiji fulani cha mbali, watu waliwaachilia mbwa ili watushambulie. Muda si muda mimi na mwenzangu tulikuwa tumezingirwa na mbwa wakubwa waliokuwa wakibweka na kutukenulia meno. Tulishikana mikono, na hata nikasali nikisema, “Tafadhali Yehova, ninaomba ikiwa mbwa hawa watatushambulia tufe haraka!” Mbwa hao walipotukaribia kabisa, walisimama, wakatikisa mikia yao, na kuondoka. Tulihisi kwamba Yehova alitulinda. Baada ya hapo, tulihubiri katika kijiji hicho chote, na tulifurahi kuona kwamba watu katika kijiji hicho walitupokea vizuri sana. Huenda walishangaa kuona kwamba mbwa hawakuwa wametudhuru au kwamba baada ya tukio hilo lenye kuogopesha tuliendelea kuhubiri. Hatimaye baadhi yao walikubali kweli na kuwa Mashahidi wa Yehova.

Tulipitia kisa kingine tena chenye kuogopesha. Siku moja, mwenye nyumba alirudi nyumbani akiwa amelewa, naye alitishia kutuua akidai kwamba tulikuwa tukiwasumbua majirani. Mke wake alijaribu kumtuliza lakini hakufanikiwa. Tukiwa katika chumba chetu ghorofani, tulisikia mambo yote aliyokuwa akisema. Upesi tuliweka viti nyuma ya mlango na kuanza kufungasha mizigo yetu. Tulipofungua mlango, mwenye nyumba alikuwa amesimama kwenye ngazi ya mwisho karibu na mlango wetu akiwa na kisu kikubwa mkononi. Hivyo, tulikimbia kupitia mlango wa nyuma, tukateremka na kupita kwenye kijia kirefu kilichokuwa kwenye bustani tukiwa na mizigo yetu yote, hatukurudi tena.

Tulifika kwenye hoteli moja na kukodi chumba. Ilitukia kwamba tulikaa kwenye hoteli hiyo kwa mwaka mmoja hivi, jambo ambalo mwishowe lilikuwa na manufaa katika huduma yetu. Jinsi gani? Hoteli hiyo ilikuwa katikati ya mji, na baadhi ya wanafunzi wetu wa Biblia walikuja ili kujifunza. Muda si muda, tulianza kufanya mkutano wa Funzo la Kitabu na Funzo la Mnara wa Mlinzi kila juma katika chumba chetu cha hoteli, na watu 15 hivi walikuwa wakihudhuria.

Tulikaa katika mji wa Mistelbach kwa zaidi ya mwaka mmoja. Kisha nikapewa mgawo wa kwenda katika mji wa Feldbach, ulio kusini mashariki ya jiji la Graz. Nilipata mwandamani mpya, na katika mji huo pia hakukuwa na kutaniko. Tuliishi katika chumba kidogo kilichokuwa kwenye ghorofa ya pili kwenye nyumba iliyotengenezwa kwa mbao. Upepo ulivuma na kupenya katikati ya mianya ya mbao hizo, hivyo tulijaribu kuziba mianya hiyo kwa magazeti. Pia, tulilazimika kuchota maji kisimani. Lakini hatujuti kamwe. Baada ya miezi michache, kikundi kilianzishwa. Hatimaye, watu 30 wa familia moja niliyojifunza nayo Biblia walikubali kweli!

Mambo hayo niliyojionea yalifanya nithamini zaidi msaada wenye kutegemeka ambao Yehova huwapa wale wanaofuatia masilahi ya Ufalme. Hata ikiwa hakuna mwanadamu anayeweza kutusaidia, sikuzote Yehova yuko pamoja nasi ili kutusaidia.—Zab. 121:1-3.

TWATEGEMEZWA NA ‘MKONO WA KUUME WA MUNGU WA UADILIFU’

Mwaka wa 1958, mpango ulifanywa ili kuwe na kusanyiko la kimataifa katika uwanja wa Yankee Stadium na Polo Grounds, jijini New York City. Nilijiandikisha ili nihudhurie, lakini ofisi ya tawi ya Austria ikaniuliza ikiwa ningependa kuhudhuria darasa la 32 la Shule ya Gileadi. Kwa kweli ningewezaje kukataa pendeleo kama hilo? Mara moja nilijibu, “Ndiyo!”

Darasani katika Shule ya Gileadi, niliketi kando ya Martin Poetzinger. Alikuwa amevumilia mateso makali katika kambi za mateso za Wanazi. Baadaye, yeye pia alitumikia akiwa mshiriki wa Baraza Linaloongoza. Tukiwa darasani, Martin angeninong’oneza hivi: “Erika, ungesemaje hilo katika Kijerumani?”

Katikati ya mtaala wa masomo, Nathan Knorr alitujulisha migawo yetu. Nilipewa mgawo wa kwenda Paraguai. Kwa kuwa nilikuwa na umri mdogo sana, nilihitaji kibali cha Baba ili niingie nchini humo. Baada ya kupata kibali hicho, nilisafiri na kuwasili nchini Paraguai mwezi wa Machi mwaka wa 1959. Mimi pamoja na mwandamani wangu mpya tuliishi kwenye nyumba ya wamishonari katika jiji la Asunción.

Baada ya muda mfupi, nilikutana na Walter Bright, mmishonari aliyekuwa amehitimu darasa la 30. Hatimaye, tulifunga ndoa na sasa tungeweza kukabiliana na changamoto za maisha tukiwa pamoja. Kila tulipokabili tatizo fulani lililojaribu imani yetu, tulisoma ahadi ya Yehova inayopatikana kwenye andiko la Isaya 41:10: “Usiogope, kwa maana mimi niko pamoja nawe. Usihangaike, kwa maana mimi ni Mungu wako. Nitakutia nguvu.” Hilo lilituhakikishia kwamba maadamu tunaendelea kujitahidi kuwa waaminifu kwa Mungu na kutanguliza Ufalme wake, hawezi kamwe kututamausha.

Baada ya muda fulani, tulipewa mgawo mwingine kwenye eneo lililokuwa karibu na mpaka wa nchi ya Brazili. Huko, makasisi waliwachochea vijana kuitupia mawe nyumba ya wamishonari tuliyokuwa tukiishi, ambayo tayari haikuwa katika hali nzuri. Kisha Walter akaanza kujifunza Biblia na mkuu wa polisi. Mkuu huyo wa polisi alihakikisha kwamba maofisa wa polisi walisimama karibu na nyumba yetu kwa juma moja, na watu hao wasumbufu hawakutuhangaisha tena. Muda mfupi baada ya hapo, tulihamishiwa katika makao bora zaidi yaliyokuwa ndani ya nchi ya Brazili karibu na mpaka. Kuhamia huko kulikuwa na manufaa kwa kuwa tungeweza kufanya mikutano nchini Paraguai na Brazili. Kabla ya kuondoka katika mgawo huo, makutaniko mawili madogo yalikuwa yameanzishwa.

Nikiwa pamoja na mume wangu, Walter, tulipokuwa wamishonari Asunción, Paraguai

YEHOVA ANAENDELEA KUNITEGEMEZA

Madaktari walikuwa wameniambia kwamba singeweza kupata watoto, hivyo katika mwaka wa 1962 nilishangaa sana kwamba nilikuwa mjamzito! Mwishowe tulienda kuishi Hollywood, Florida, karibu na familia ya Walter. Kwa miaka kadhaa, hali zetu hazikuturuhusu kuwa mapainia. Tulihitaji kutunza familia. Lakini bado tuliendelea kutanguliza masilahi ya Ufalme.—Mt. 6:33.

Tulipofika Florida mwezi wa Novemba mwaka wa 1962, tulishangaa kujua kwamba akina ndugu weusi walilazimika kufanya mikutano na kuhubiri katika maeneo tofauti na akina ndugu weupe kwa sababu ya hisia za watu za ubaguzi. Lakini Yehova hana ubaguzi, na punde si punde akina ndugu weusi na weupe walianza kushirikiana pamoja makutanikoni. Mkono wa Yehova ulionekana wazi katika mpango huo kwa kuwa sasa kuna makutaniko mengi katika eneo hilo.

Kwa kusikitisha, Walter alikufa kwa sababu ya kansa ya ubongo mwaka wa 2015. Alikuwa mume mzuri kwa miaka 55 tuliyokuwa pamoja, naye alimpenda Yehova na kuwasaidia ndugu wengi. Ninatazamia kwa hamu kumwona tena akiwa na afya nzuri atakapofufuliwa.—Mdo. 24:15.

Ninafurahi kwamba nimekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa zaidi ya miaka 40, nami nimepata shangwe na thawabu nyingi. Kwa mfano, mimi na Walter tumeshuhudia watu 136 tuliojifunza nao Biblia wakibatizwa. Bila shaka tulikabili matatizo. Lakini hatukuona matatizo hayo kuwa sababu ya kuacha kumtumikia Mungu wetu mwaminifu. Badala yake, tulimkaribia zaidi, tukitumaini kwamba atasuluhisha matatizo hayo kwa wakati wake na kwa njia yake. Naye amekuwa akifanya hivyo!—2 Tim. 4:16, 17.

Ninamkosa sana Walter, lakini upainia unanisaidia kukabiliana na hali hiyo. Nimejionea kwamba ninanufaika ninapowafundisha wengine, na hasa ninapowaeleza kuhusu tumaini la ufufuo. Kwa kweli, siwezi kuhesabu mara ambazo Yehova amenitegemeza. Kulingana na ahadi yake, Yehova amenitegemeza, ameniimarisha, na kuushika kwelikweli mkono wangu kwa “mkono [wake] wa kuume wa uadilifu.”—Isa. 41:10.