Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 12

Upendo Hutusaidia Kuvumilia Chuki

Upendo Hutusaidia Kuvumilia Chuki

“Mambo haya ninawaamuru, kwamba mpendane. Ikiwa ulimwengu unawachukia, kumbukeni kwamba umenichukia mimi kabla ya kuwachukia ninyi.”—YOH. 15:17, 18.

WIMBO 129 Tutaendelea Kuvumilia

MUHTASARI *

1. Kulingana na Mathayo 24:9, kwa nini hatupaswi kushangaa ikiwa ulimwengu unatuchukia?

YEHOVA alituumba tukiwa na uwezo wa kuonyesha upendo na tamaa ya kuonyeshwa upendo. Hivyo, mtu fulani anapotuchukia, tunaumia na huenda hata kuogopa. Kwa mfano, Georgina, dada anayeishi Ulaya anasema hivi: “Nilipokuwa na umri wa miaka 14, mama yangu alinichukia kwa sababu ya kumtumikia Yehova. Nilijihisi vibaya sana na nilihisi upweke, na nikaanza kufikiri kwamba huenda sikuwa mtu mzuri.” * Ndugu anayeitwa Danylo anaandika hivi: “Askari waliponipiga, kunitukana, na kunitishia kwa sababu nilikuwa Shahidi wa Yehova, niliogopa na kuhisi nimedhalilishwa.” Chuki ya aina hiyo huumiza, lakini haitushangazi. Yesu alitabiri kwamba tungechukiwa.—Soma Mathayo 24:9.

2-3. Kwa nini wafuasi wa Yesu wanachukiwa?

2 Ulimwengu unawachukia wafuasi wa Yesu. Kwa nini? Kwa sababu kama Yesu, sisi “si sehemu ya ulimwengu.” (Yoh. 15:17-19) Hivyo, ingawa tunazitii serikali za wanadamu, tunakataa kuziabudu au kuabudu nembo za kitaifa zinazoziwakilisha. Tunamwabudu Yehova peke yake. Tunatetea haki ya Mungu ya kuwatawala wanadamu—haki ambayo Shetani na “uzao” wake wanaipinga vikali. (Mwa. 3:1-5, 15) Tunahubiri kwamba Ufalme wa Mungu ndilo tumaini pekee kwa wanadamu na kwamba hivi karibuni Ufalme huo utawapondaponda wote wanaoupinga. (Dan. 2:44; Ufu. 19:19-21) Ujumbe huo ni habari njema kwa watu wapole, lakini habari mbaya kwa waovu.—Zab. 37:10, 11.

3 Pia, tunachukiwa kwa sababu tunaishi kulingana na viwango vya uadilifu vya Mungu. Viwango hivyo vinatofautiana kabisa na maadili mapotovu ya ulimwengu huu. Kwa mfano, watu wengi sasa wanaunga mkono waziwazi vitendo vilivyopindukia vya upotovu wa maadili ambavyo ni sawa na vile vilivyomfanya Mungu aharibu Sodoma na Gomora! (Yuda 7) Kwa sababu tunashikamana na viwango vya Biblia kuhusu mazoea hayo, watu wengi wanatudhihaki na kusema kwamba hatuna maoni yaliyosawazika.—1 Pet. 4:3, 4.

4. Ni sifa gani zinazotuimarisha tunapochukiwa na watu?

4 Ni nini kinachoweza kutusaidia kuvumilia watu wanapotuchukia na kututukana? Tunahitaji kuwa na imani yenye nguvu kwamba Yehova atatusaidia. Kama ngao, imani yetu inaweza ‘kuizima mishale yote inayowaka moto ya yule mwovu.’ (Efe. 6:16) Lakini tunahitaji mengi zaidi ya kuwa tu na imani. Tunahitaji pia upendo. Kwa nini? Kwa sababu upendo “hauchokozeki.” Upendo huhimili na kuvumilia mambo yote yenye kuumiza. (1 Kor. 13:4-7, 13) Acheni sasa tuone jinsi upendo kwa Yehova, upendo kwa waabudu wenzetu, na hata upendo kwa maadui wetu unavyotusaidia kuvumilia chuki.

UPENDO KWA YEHOVA HUTUSAIDIA TUVUMILIE CHUKI

5. Upendo wa Yesu kwa Baba yake ulimwimarishaje?

5 Usiku wa mwisho kabla ya kuuawa na maadui wake, Yesu aliwaambia hivi wafuasi wake washikamanifu: “Ninampenda Baba, [hivyo] ninafanya kama vile Baba alivyoniamuru.” (Yoh. 14:31) Upendo wa Yesu kwa Yehova ulimwimarisha na kumsaidia kukabiliana na majaribu yaliyokuwa mbele yake. Upendo wetu kwa Yehova unaweza kutusaidia kwa njia hiyohiyo pia.

6. Kulingana na Waroma 5:3-5, watumishi wa Yehova wana maoni gani kuhusu kuvumilia chuki ya ulimwengu huu?

6 Sikuzote upendo kwa Mungu umewasaidia watumishi wa Yehova wavumilie mateso. Kwa mfano, mahakama kuu ya Kiyahudi yenye nguvu ilipowaamuru mitume waache kuhubiri, upendo wao kwa Mungu uliwachochea ‘wamtii Mungu kuwa mtawala badala ya wanadamu.’ (Mdo. 5:29; 1 Yoh. 5:3) Pia, upendo wa aina hiyo usioweza kuvunjwa unawaimarisha ndugu zetu leo, ambao wengi wao wanasimama imara dhidi ya serikali katili na zenye nguvu. Badala ya kuvunjika moyo, tunaliona kuwa pendeleo kubwa kuvumilia chuki ya ulimwengu.—Mdo. 5:41; soma Waroma 5:3-5.

7. Tunapaswa kutendaje watu wa familia wanapotupinga?

7 Huenda mojawapo kati ya majaribu makubwa zaidi tunayoweza kukabili likatoka kwa watu wa familia. Tunapoanza kupendezwa na kweli, huenda baadhi ya watu wa familia wakafikiri kwamba tumepotoshwa. Huenda wengine wakafikiri kwamba tumerukwa na akili. (Linganisha Marko 3:21.) Huenda hata wakatupinga vikali sana. Upinzani huo haupaswi kutushangaza. Yesu alisema: “Adui za mtu watakuwa watu wa nyumbani mwake.” (Mt. 10:36) Bila shaka, haidhuru jinsi watu wa ukoo wanavyotuona, sisi tunakataa kuwatendea kama adui. Badala yake, kadiri upendo wetu kwa Yehova unavyokua, ndivyo upendo wetu kwa watu unavyoongezeka. (Mt. 22:37-39) Lakini kamwe hatutaacha kushikamana na viwango vyetu kwa kupuuza sheria na kanuni za Biblia ili tu kumpendeza mwanadamu fulani.

Huenda tukateseka kwa kipindi fulani, lakini sikuzote Yehova atakuwa upande wetu ili kutufariji na kutuimarisha (Tazama fungu la 8 hadi 10)

8-9. Ni nini kilichomsaidia dada mmoja kusimama imara licha ya upinzani mkali?

8 Georgina, aliyetajwa awali, alifaulu kusimama imara licha ya upinzani mkali kutoka kwa mama yake. Anaeleza hivi: “Mimi na mama yangu tulianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi. Lakini miezi sita baadaye nilipotaka kuanza kuhudhuria mikutano, mtazamo wa mama ulibadilika kabisa. Niligundua kwamba alikuwa akiwasiliana na waasi-imani, na alitumia hoja zao alipozungumza nami. Pia, angenitukana, angevuta nywele zangu, angenikaba kooni, na kutupa machapisho yangu. Nilipofikisha umri wa miaka 15, nilibatizwa. Mama yangu alijaribu kunizuia kumtumikia Yehova kwa kunipeleka nikaishi kwenye nyumba ambayo matineja walioasi walikuwa wakitunzwa, na baadhi yao walitumia dawa za kulevya na kufanya uhalifu. Si rahisi kuvumilia upinzani hasa ikiwa unatoka kwa mtu anayepaswa kukupenda na kukujali.”

9 Ni nini kilichomsaidia Georgina kuvumilia? Anasema hivi: “Siku ambayo mama yangu alinigeuka, nilikuwa nimetoka tu kumaliza kusoma Biblia nzima. Wakati huo, nilikuwa nimesadiki kabisa kwamba nimeipata kweli, na nilihisi nikiwa karibu sana na Yehova. Nilisali kwake mara nyingi, naye alinisikiliza. Nilipokuwa nikiishi kwenye ile nyumba, dada fulani alinialika nyumbani kwake na tulijifunza Biblia pamoja. Katika kipindi hicho chote, niliimarishwa na ndugu na dada kwenye Jumba la Ufalme. Walifanya niwe sehemu ya familia zao. Nilijionea waziwazi kwamba Yehova ana nguvu kuliko wapinzani wetu, haijalishi wao ni nani.”

10. Tunaweza kuwa na uhakika gani katika Yehova Mungu wetu?

10 Mtume Paulo aliandika kwamba hakuna kitu kinachoweza “kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.” (Rom. 8:38, 39) Hata ingawa huenda tukateseka kwa muda fulani, sikuzote Yehova atakuwa upande wetu ili kutufariji na kutuimarisha. Na kama simulizi la Georgina linavyoonyesha, Yehova anatusaidia pia kupitia familia yetu ya kiroho yenye thamani.

UPENDO KWA WAABUDU WENZETU HUTUSAIDIA KUVUMILIA CHUKI

11. Upendo ambao Yesu aliuzungumzia kwenye Yohana 15:12, 13 uliwasaidiaje wanafunzi wake? Toa mfano.

11 Usiku uliotangulia kifo chake, Yesu aliwakumbusha wanafunzi wake wapendane. (Soma Yohana 15:12, 13.) Alijua kwamba upendo wa kujidhabihu ungewasaidia waendelee kuwa na umoja na wavumilie chuki ya ulimwengu huu. Fikiria mfano wa kutaniko la Thesalonike. Tangu lilipoanzishwa, washiriki wake waliteswa. Hata hivyo, ndugu na dada wa kutaniko hilo walikuja kuwa kielelezo kizuri cha utimilifu na upendo. (1 The. 1:3, 6, 7) Paulo aliwatia moyo waendelee kuonyesha upendo ‘kwa ukamili hata zaidi.’ (1 The. 4:9, 10) Upendo ungewachochea wawafariji walioshuka moyo na kuwategemeza walio dhaifu. (1 The. 5:14) Walifuata maagizo ya Paulo, ndiyo sababu katika barua ya pili aliyowaandikia mwaka moja hivi baadaye, Paulo aliweza kuwaambia hivi: “Upendo wa kila mmoja wenu unaongezeka kati yenu.” (2 The. 1:3-5) Upendo wao uliwasaidia kuvumilia hali ngumu na mateso.

Upendo wa Kikristo unaweza kutusaidia kuvumilia chuki (Tazama fungu la 12) *

12. Katika nchi fulani, ndugu na dada walionyeshanaje upendo wakati wa vita?

12 Fikiria kisa cha ndugu aliyetajwa awali anayeitwa Danylo, na mke wake. Vita ilipoenea katika mji wao, waliendelea kuhudhuria mikutano, kuhubiri kadiri walivyoweza, na kushiriki chakula walichokuwa nacho pamoja na ndugu na dada zao. Kisha siku moja, wanajeshi wenye silaha walimfuata Danylo nyumbani. Danylo anasema hivi: “Waliniamuru niikane imani yangu. Nilipokataa, walinipiga na kujifanya wananipiga risasi, wakifyatua risasi juu ya kichwa changu. Kabla hawajaondoka, walitishia kwamba watarudi kumbaka mke wangu. Lakini ndugu zetu walitusafirisha haraka kwa treni kwenda kwenye mji mwingine. Sitasahau kamwe upendo wa ndugu hao wapendwa. Na tulipowasili kwenye mji huo mpya, ndugu wenyeji walitupatia chakula na kunisaidia kupata kazi na nyumba! Hivyo, sisi pia tuliweza kuwaandalia mahali pa kuishi Mashahidi wengine waliokuwa wakikimbia eneo la vita.” Visa kama hivyo vinatuonyesha kwamba upendo wa Kikristo unaweza kutusaidia kuvumilia chuki.

UPENDO KWA ADUI ZETU HUTUSAIDIA KUVUMILIA CHUKI

13. Roho takatifu inatusaidiaje kuvumilia katika utumishi wetu kwa Yehova hata watu wanapotuchukia?

13 Yesu aliwaambia wafuasi wake wawapende adui zao. (Mt. 5:44, 45) Je, ni rahisi kufanya hivyo? La hasha! Lakini inawezekana kwa msaada wa roho takatifu ya Mungu. Sifa za tunda la roho zinatia ndani upendo na pia subira, fadhili, upole, na kujizuia. (Gal. 5:22, 23) Sifa hizo zinatusaidia kuvumilia chuki. Wapinzani wengi wamebadili maoni yao kwa sababu mume, mke, mtoto, au jirani ambaye ni Shahidi alionyesha sifa hizo zinazompendeza Mungu. Wapinzani wengi hata wamekuwa ndugu na dada zetu wapendwa. Hivyo, ikiwa unaona ni vigumu kuwapenda wale wanaokuchukia kwa sababu tu unamtumikia Yehova, sali ili upate roho takatifu. (Luka 11:13) Na uwe na uhakika kabisa kwamba sikuzote njia ya Yehova ndiyo njia bora zaidi.—Met. 3:5-7.

14-15. Andiko la Waroma 12:17-21 lilimsaidiaje Yasmeen kumwonyesha upendo mume wake licha ya upinzani wake mkali?

14 Fikiria mfano wa Yasmeen, anayeishi Mashariki ya Kati. Alipokuwa Shahidi wa Yehova, mume wake alifikiri kwamba ametoposhwa, naye alijaribu kumzuia kumtumikia Mungu. Alimtukana na kuwahimiza ndugu zake na pia kasisi na mlozi wamtishie na kumshtumu kwamba anavunja familia yake. Mume wake hata aliwatukana akina ndugu kwa sauti kubwa wakati wa mkutano wa kutaniko! Mara nyingi Yasmeen alilia kwa sababu hakutendewa kwa fadhili.

15 Kwenye Jumba la Ufalme, familia ya kiroho ya Yasmeen ilimfariji na kumwimarisha. Wazee walimtia moyo atumie maneno yanayopatikana kwenye Waroma 12:17-21. (Soma.) Yasmeen anasema hivi: “Haikuwa rahisi. Lakini nilimwomba Yehova anisaidie, na nikafanya yote niliyoweza ili kutumia mambo ambayo Biblia inasema. Hivyo, kwa chuki mume wangu alipotupa uchafu jikoni, nilisafisha. Aliponitukana, nilijibu kwa upole. Na alipokuwa mgonjwa, nilimtunza.”

Tunapowaonyesha upendo wale wanaotutesa, huenda tukalainisha mioyo yao (Tazama fungu la 16 na 17) *

16-17. Unajifunza nini kutokana na mfano wa Yasmeen?

16 Yasmeen alithawabishwa kwa kumwonyesha upendo mume wake. Anasema hivi: “Mume wangu alianza kunitumaini zaidi kwa sababu alijua kwamba siku zote ningesema kweli. Alianza kunisikiliza kwa heshima nilipozungumza kuhusu dini, na alikubali kudumisha amani nyumbani. Siku hizi yeye huniambia nifurahie mikutano ya kutaniko. Uhusiano wangu na mume wangu umekuwa mzuri sana, na tunafurahia amani ya kweli. Tumaini langu ni kwamba mume wangu atakubali kweli na kujiunga nami katika kumtumikia Yehova.”

17 Mfano wa Yasmeen unaonyesha kwamba upendo “huhimili mambo yote, . . . hutumaini mambo yote, huvumilia mambo yote.” (1 Kor. 13:4, 7) Chuki inaweza kuwa na nguvu na inaweza kuumiza, lakini upendo una nguvu kuliko chuki. Unaweza kuwafanya watu wabadili maoni yao. Na unaufanya moyo wa Yehova ushangilie. Lakini hata ikiwa wapinzani wataendelea kutuchukia, bado tunaweza kuwa na furaha. Jinsi gani?

WENYE FURAHA TUNAPOCHUKIWA

18. Kwa nini tunaweza kuwa na furaha tunapochukiwa?

18 Yesu alisema hivi: “Wenye furaha ni ninyi watu wanapowachukia.” (Luka 6:22) Hatuchagui kuchukiwa. Hatujaribu kuwa wafia-imani. Basi, kwa nini tunaweza kuwa na furaha tunapochukiwa? Fikiria sababu hizi tatu. Kwanza, tunapovumilia tunapata kibali cha Mungu. (1 Pet. 4:13, 14) Pili, imani yetu inakuwa na thamani kubwa zaidi na inakuwa imara zaidi. (1 Pet. 1:7) Na tatu, tutapokea thawabu ambayo thamani yake haiwezi kulinganishwa na chochote, yaani, uzima wa milele.—Rom. 2:6, 7.

19. Kwa nini mitume walikuwa na furaha baada ya kupigwa viboko?

19 Muda mfupi baada ya Yesu kufufuliwa, mitume walijionea furaha ambayo Yesu alikuwa ameizungumzia. Baada ya kupigwa viboko na kuagizwa waache kuhubiri, walishangilia. Kwa nini? “Kwa sababu walikuwa wamestahili kuvunjiwa heshima kwa ajili ya jina [la Yesu].” (Mdo. 5:40-42) Walimpenda Bwana wao zaidi ya walivyoogopa kuchukiwa na maadui zao. Na walionyesha upendo wao kwa kutangaza habari njema “bila kuacha.” Ndugu zetu wengi leo wanaendelea kutumikia kwa uaminifu licha ya hali ngumu wanazopitia. Wanajua kwamba Yehova hatasahau kazi yao na upendo wao kwa ajili ya jina lake.—Ebr. 6:10.

20. Tutachunguza nini katika makala inayofuata?

20 Ulimwengu utatuchukia maadamu mfumo huu unaendelea kuwepo. (Yoh. 15:19) Lakini hatuhitaji kuwa na hofu. Kama tutakavyoona katika makala inayofuata, Yehova “atawaimarisha na kuwalinda” washikamanifu wake. (2 The. 3:3) Hivyo, acheni tuendelee kumpenda Yehova, kuwapenda ndugu na dada zetu, na kuwapenda hata adui zetu. Tunapofuata shauri hilo, tutaendelea kuwa na umoja na kuwa imara kiroho, tutamletea heshima Yehova, na tutathibitisha kwamba upendo una nguvu zaidi kuliko chuki.

WIMBO 106 Kusitawisha Sifa ya Upendo

^ fu. 5 Katika makala hii, tutaona jinsi upendo kwa Yehova, upendo kwa waamini wenzetu, na hata upendo kwa maadui wetu unavyotusaidia kuvumilia chuki ya ulimwengu huu. Pia, tutaona kwa nini Yesu alisema kwamba tunaweza kuwa na furaha tunapochukiwa.

^ fu. 1 Majina yamebadilishwa.

^ fu. 58 MAELEZO YA PICHA: Baada ya wanajeshi kumtishia Danylo, akina ndugu walimsaidia yeye na mke wake wahamie mji mwingine, na akina ndugu wa huko waliwakaribisha kwa uchangamfu.

^ fu. 60 MAELEZO YA PICHA: Mume wa Yasmeen alimpinga, lakini wazee walimpa Yasmeen ushauri mzuri. Alithibitika kuwa mke mzuri na alimtunza mume wake alipokuwa mgonjwa.