Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 14

“Kwa Jambo Hili Wote Watajua Kwamba Ninyi Ni Wanafunzi Wangu”

“Kwa Jambo Hili Wote Watajua Kwamba Ninyi Ni Wanafunzi Wangu”

“Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu—mkiwa na upendo miongoni mwenu.”​—YOH. 13:35.

WIMBO 106 Kusitawisha Sifa ya Upendo

MUHTASARI a

Watu wengi ambao si Mashahidi wa Yehova wamechochewaje baada ya kujionea upendo miongoni mwa watu wa Yehova? (Tazama fungu la 1)

1. Ni nini kinachowavutia watu wengi wanapohudhuria mikutano yetu? (Tazama pia picha.)

 WAZIA wenzi wa ndoa wakihudhuria mkutano kwa mara ya kwanza katika Jumba la Ufalme la Mashahidi wa Yehova. Wanavutiwa sana na jinsi wanavyokaribishwa kwa uchangamfu na upendo ulio miongoni mwa watu kutanikoni. Wakiwa wanarudi nyumbani kutoka kwenye mkutano, mke anamwambia mume wake, ‘Kuna jambo tofauti kuhusu Mashahidi wa Yehova—nilifurahia sana kuwa pamoja nao.’

2. Kwa nini baadhi ya watu wamekwazwa?

2 Upendo uliopo miongoni mwa wale walio katika kutaniko la Kikristo ni wa pekee sana. Bila shaka, Mashahidi wa Yehova si wakamilifu. (1 Yoh. 1:8) Hivyo, kadiri tunavyozidi kuwafahamu zaidi wale walio katika kutaniko, inaelekea ndivyo tutakavyoona baadhi ya udhaifu walio nao. (Rom. 3:23) Kwa kusikitisha, baadhi ya watu wameruhusu kutokamilika kwa wengine kuwakwaze.

3. Ni nini kinachowatambulisha wafuasi wa kweli wa Yesu? (Yohana 13:34, 35)

3 Tazama tena andiko la msingi la makala hii. (Soma Yohana 13:34, 35.) Ni sifa gani inayowatambulisha wafuasi wa kweli wa Kristo? Ni upendo, si ukamilifu. Pia, ona kwamba, Yesu hakusema: ‘Kwa jambo hili mtajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu.’ Alisema: “Kwa jambo hili wote watajua kwamba ninyi ni wanafunzi wangu.” Hivyo, Yesu alionyesha kwamba si wafuasi wake tu, bali pia wale walio nje ya kutaniko la Kikristo wangetambua wafuasi wake wa kweli kupitia upendo usio na ubinafsi ulio miongoni mwao.

4. Huenda watu wengi wangetaka kujua nini kuhusu Wakristo wa kweli?

4 Watu ambao si Mashahidi wa Yehova wanaweza kujiuliza hivi: ‘Upendo unawatambulishaje wafuasi wa kweli wa Yesu? Yesu aliwaonyeshaje upendo mitume wake? Tunawezaje kuiga mfano wa Yesu leo?’ Inafaa kwa Mashahidi kutafakari majibu ya maswali hayo. Kufanya hivyo kunaweza kutusaidia kuonyesha upendo kikamili zaidi, hasa tunaposhughulika na udhaifu wa wengine.​—Efe. 5:2.

KWA NINI UPENDO UNAWATAMBULISHA KWA NJIA YA PEKEE WAFUASI WA KWELI WA YESU?

5. Fafanua maneno ya Yesu yanayopatikana katika Yohana 15:12, 13.

5 Yesu alieleza wazi kwamba upendo wa pekee ungewatambulisha wafuasi wake. (Soma Yohana 15:12, 13.) Ona kwamba Yesu aliwaamuru hivi: “Mpendane kama vile nilivyowapenda.” Hilo linamaanisha nini? Yesu aliendelea kufafanua kwamba huo ni upendo wa kujidhabihu—upendo ambao unamchochea Mkristo hata kufa kwa ajili ya mwamini mwenzake ikilazimu. b

6. Neno la Mungu linakaziaje umuhimu wa upendo?

6 Neno la Mungu linakazia sana kuhusu upendo. Ifuatayo ni baadhi ya mistari ambayo watu wengi wanaipenda zaidi: “Mungu ni upendo.” (1 Yoh. 4:8) “Lazima umpende jirani yako kama unavyojipenda mwenyewe.” (Mt. 22:39) “Upendo hufunika dhambi nyingi.” (1 Pet. 4:8) “Upendo haushindwi kamwe.” (1 Kor. 13:8) Mistari hii na mingine inaonyesha wazi kwa mtu yeyote jinsi ilivyo muhimu kusitawisha na kuonyesha sifa hii yenye kuvutia.

7. Kwa nini Shetani hawezi kamwe kuwaunganisha watu katika kifungo cha upendo wa kweli?

7 Watu wengi wanauliza hivi: ‘Unawezaje kutambua dini ya kweli? Dini zote zinadai zinafundisha ukweli, lakini kila moja hufundisha jambo tofauti kumhusu Mungu.’ Shetani amefaulu kuwachanganya watu kwa kutokeza mashirika mengi ya kidini ya uwongo. Lakini hawezi kamwe kutokeza undugu wa ulimwenguni pote wa Wakristo wanaopendana. Ni Yehova pekee anayeweza kufanya hivyo. Hilo linapatana na akili kwa sababu upendo wa kweli unatoka kwa Yehova—kwa kuwa na roho yake na baraka zake juu ya kikundi cha waabudu. (1 Yoh. 4:7) Hivyo, haishangazi kwamba Yesu alisema upendo usio na ubinafsi ungewatambulisha wafuasi wake wa kweli.

8-9. Watu wengi wamechochewaje na upendo walioona miongoni mwa Mashahidi wa Yehova?

8 Kama vile Yesu alivyotabiri, watu wengi wamewatambua wafuasi wa kweli kupitia upendo wa kweli ulio miongoni mwao. Kwa mfano, ndugu anayeitwa Ian anakumbuka kusanyiko la kwanza la eneo alilohudhuria, ambalo lilifanywa kwenye uwanja wa michezo karibu na nyumbani kwake. Ian alikuwa katika uwanja huo miezi michache mapema akitazama mchezo fulani. Anasema hivi: “Wakati wa kusanyiko kulikuwa na tofauti kubwa. Mashahidi walijiendesha kwa njia nzuri na walivalia nadhifu, na watoto wao walikuwa na adabu.” Anaongezea hivi: “Zaidi ya yote, watu hao walionekana kuwa wenye kuridhika na wenye amani—mambo niliyotamani. Sikumbuki hotuba yoyote iliyotolewa siku hiyo, lakini siwezi kusahau mwenendo wa Mashahidi.” c Bila shaka, mwenendo kama huo ni matokeo ya upendo wa kweli tulio nao miongoni mwetu. Kwa sababu tunawapenda ndugu na dada zetu, tunawatendea kwa fadhili na heshima.

9 Ndugu anayeitwa John alihisi vivyo hivyo alipoanza kuhudhuria mikutano ya kutaniko, anasema hivi: “Niliguswa moyo na urafiki . . . [wa] kila mtu aliyekuwa huko—walionekana kama watakatifu. Upendo wao wa kweli ulinisadikisha kwamba nilikuwa nimeipata dini ya kweli.” d Tena na tena, visa kama hivyo vinaonyesha wazi kwamba watu wa Yehova wanajithibitisha kuwa Wakristo wa kweli.

10. Ni wakati gani hasa tuna fursa ya kuonyesha upendo wa Kikristo? (Tazama pia maelezo ya chini.)

10 Kama ilivyotajwa mwanzoni, hakuna mwamini mwenzetu ambaye ni mkamilifu. Nyakati nyingine, watasema au kufanya mambo yanayotuumiza. e (Yak. 3:2) Katika pindi hizo, tuna fursa ya pekee ya kuonyesha upendo wa Kikristo kupitia jinsi tunavyotenda. Kuhusiana na jambo hilo, tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano uliowekwa na Yesu?​—Yoh. 13:15.

YESU ALIWAONYESHAJE UPENDO MITUME WAKE?

Yesu alishughulika kwa upendo na mitume wake hata ingawa walifanya makosa mengi (Tazama fungu la 11 hadi 13)

11. Yakobo na Yohana walionyesha sifa gani mbaya? (Tazama pia picha.)

11 Yesu hakutarajia ukamilifu kutoka kwa wafuasi wake. Badala yake, aliwasaidia kwa upendo kurekebisha sifa mbaya walizokuwa nazo ili wapate kibali cha Yehova. Pindi moja, mitume wawili, Yakobo na Yohana, walimtuma mama yao amwombe Yesu awapatie vyeo vikubwa katika Ufalme. (Mt. 20:20, 21) Hivyo, Yakobo na Yohana walikuwa wakionyesha sifa ya kiburi na kujitakia makuu.​—Met. 16:18.

12. Je, ni Yakobo na Yohana tu walioonyesha sifa mbaya? Eleza.

12 Si Yakobo na Yohana pekee walioonyesha sifa mbaya katika pindi hiyo. Ona jinsi mitume wengine walivyotenda: “Wale wengine kumi waliposikia jambo hilo, wakawakasirikia hao ndugu wawili.” (Mt. 20:24) Tunaweza kuwazia jinsi Yakobo, Yohana, na mitume wengine walivyorushiana maneno makali. Huenda wale mitume wengine walisema jambo kama hili: ‘Mnafikiri ninyi ni nani hata mwombe vyeo vikubwa katika Ufalme? Si ninyi pekee mliofanya kazi kwa bidii pamoja na Yesu. Kama tu vile ninyi, sisi pia tunastahili kupokea mapendeleo ya pekee!’ Vyovyote vile, kwa muda mfupi mitume waliruhusu hali hiyo iwazuie kuonyeshana upendo wa kindugu.

13. Yesu alitendaje alipoona udhaifu wa mitume wake? (Mathayo 20:25-28)

13 Yesu alishughulikiaje hali hiyo? Hakukasirika. Hakusema kwamba angeenda kutafuta mitume wanaofaa zaidi, wanaume waliokuwa wanyenyekevu zaidi na ambao sikuzote wangetendeana kwa upendo. Badala yake, Yesu alizungumza na wanaume hao wanyoofu kwa subira. (Soma Mathayo 20:25-28.) Aliendelea kushughulika nao kwa upendo, hata ingawa hiyo haikuwa mara ya kwanza wala ya mwisho kwa mitume hao kujaribu kuamua ni nani miongoni mwao alikuwa mkuu zaidi.​—Marko 9:34; Luka 22:24.

14. Mitume wa Yesu walilelewa katika mazingira ya aina gani?

14 Bila shaka, Yesu alifikiria malezi ya mitume wake. (Yoh. 2:24, 25) Walilelewa katika mazingira ambayo viongozi wa kidini walikazia sana umashuhuri na vyeo vikubwa. (Mt. 23:6; linganisha video The Front Seats in the Synagogue kwenye nwtsty habari za utafiti Mathayo 23:6.) Pia, viongozi wa dini ya Kiyahudi walijiona kuwa waadilifu kupita kiasi. f (Luka 18:9-12) Yesu alielewa kwamba mazingira kama hayo yanaweza kuathiri maoni ya mitume kujihusu na kuwahusu wengine. (Met. 19:11) Alikuwa mwenye usawaziko kuhusu yale aliyotarajia kutoka kwa wanafunzi wake na alionyesha subira walipokosea. Alijua kwamba walikuwa na nia nzuri, hivyo kwa subira aliwasaidia kushinda sifa ya kiburi na kujitakia makuu, na kuwasaidia waonyeshane upendo.

TUNAWEZAJE KUIGA MFANO WA YESU?

15. Tunaweza kujifunza nini kutokana na kisa cha Yakobo na Yohana?

15 Tunaweza kujifunza mengi kutokana na kisa cha Yakobo na Yohana. Walikosea walipoomba vyeo vikubwa katika Ufalme. Lakini pia, mitume wengine walikuwa wamekosea waliporuhusu hali hiyo ivuruge umoja wao. Hata hivyo, Yesu, alishughulika na mitume wote 12 kwa njia yenye fadhili na upendo. Tunajifunza nini? Jambo muhimu si tu yale ambayo wengine wanafanya, lakini pia jinsi sisi tunavyotenda kuelekea makosa na udhaifu wao. Ni nini kinachoweza kutusaidia kutenda kwa njia nzuri? Mwamini mwenzetu anapotukosea, tunaweza kujiuliza hivi: ‘Kwa nini ninasumbuliwa sana na jambo ambalo amenitendea? Je, hilo linafunua sifa fulani mbaya ambayo ninahitaji kufanyia kazi? Je, inawezekana kwamba mtu aliyeniumiza anakabiliana na matatizo fulani? Hata ikiwa ninahisi kwamba nina haki ya kukasirika, je, ninaweza kuonyesha upendo usio na ubinafsi kwa kuachilia kosa?’ Kadiri tunavyoshughulika na wengine kwa njia ya upendo, ndivyo tutakavyothibitisha kwamba sisi ni wafuasi wa kweli wa Yesu.

16. Tunaweza kujifunza jambo gani lingine kutokana na mfano wa Yesu?

16 Pia, mfano wa Yesu unatufundisha kwamba tunapaswa kujitahidi kuwaelewa waamini wenzetu. (Met. 20:5) Yesu aliweza kusoma mioyo. Sisi hatuwezi kufanya hivyo. Lakini tunaweza kuonyesha subira kuelekea udhaifu wa ndugu na dada zetu. (Efe. 4:1, 2; 1 Pet. 3:8) Ni rahisi zaidi kufanya hivyo ikiwa tutajifunza kuhusu malezi yao. Fikiria mfano mmoja.

17. Mwangalizi mmoja anayesafiri alinufaikaje kwa kumfahamu vizuri zaidi mwamini mwenzake?

17 Mwangalizi anayesafiri anayetumikia Afrika Mashariki anamkumbuka ndugu fulani ambaye alihisi kwamba hakuwa mwenye fadhili. Mwangalizi huyo wa mzunguko alitendaje? Anasema hivi: “Badala ya kumwepuka ndugu huyo, niliazimia kumjua vizuri zaidi.” Kwa kufanya hivyo, mwangalizi huyo alijifunza baadhi ya mambo kuhusu malezi ya ndugu huyo ambayo yalikuwa yameathiri utu wake. Mwangalizi huyo anaendelea kusema hivi: “Nilipoelewa jinsi ndugu huyo alivyopambana sana ili kushinda athari za malezi yake na maendeleo makubwa aliyofanya, nilimthamini zaidi. Tukawa marafiki wazuri.” Kwa hakika, tunapojitahidi kuwaelewa ndugu na dada zetu, mara nyingi inakuwa rahisi zaidi kuwaonyesha upendo.

18. Tunaweza kujiuliza maswali gani ikiwa tumekosewa na mwamini mwenzetu? (Methali 26:20)

18 Huenda nyakati nyingine tukahitaji kuzungumza na mwamini mwenzetu ambaye ametukosea. Hata hivyo, kwanza, ni vema kujiuliza maswali kama: ‘Je, nina habari kamili?’ (Met. 18:13) ‘Je, inawezekana kwamba hakukusudia kunikosea?’ (Mhu. 7:20) ‘Je, nimewahi kufanya kosa kama hilo?’ (Mhu. 7:21, 22) ‘Je, kwa kuzungumza na mtu huyo, nitafanya tatizo liwe kubwa zaidi kuliko lile ninalojaribu kutatua?’ (Soma Methali 26:20.) Tunapotenga wakati kufikiria maswali hayo, huenda tukafikia mkataa kwamba upendo wetu kwa ndugu yetu unaweza kutuchochea kuachilia tu kosa.

19. Umeazimia kufanya nini?

19 Wakiwa kikundi, Mashahidi wa Yehova wamethibitika kuwa wafuasi wa kweli wa Yesu. Tukiwa mtu mmoja-mmoja tunathibitisha kwamba sisi ni wafuasi wa kweli wa Yesu tunapoonyesha upendo usio na ubinafsi kuwaelekea ndugu na dada zetu licha ya udhaifu wao. Tunapofanya hivyo, huenda tukawasaidia wengine watambue dini ya kweli na wajiunge nasi katika kumwabudu Yehova, Mungu wa upendo. Acheni tuazimie kuendelea kuonyesha upendo ambao unawatambulisha Wakristo wa kweli.

WIMBO 17 “Nataka”

a Watu wengi wanavutiwa na kweli kwa sababu ya upendo wa kweli ambao wanaona miongoni mwetu. Hata hivyo, sisi si wakamilifu, hivyo nyakati nyingine huenda ikawa vigumu kushughulika na mwamini mwenzetu kwa njia ya upendo. Acheni tuchunguze kwa nini upendo ni sifa muhimu sana na jinsi tunavyoweza kuiga kielezo cha Yesu tunaposhughulika na udhaifu wa wengine.

b Ona kitabu ‘Njoo Uwe Mfuasi Wangu,’ sura ya 17, fungu la 10-11.

c Ona makala “Hatimaye, Maisha Yangu Yana Kusudi,” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi, Novemba 1, 2012, uku. 13-14.

d Ona makala “Maisha Yangu Yalionekana Kuwa Mazuri,” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi, Mei 1, 2012, uku. 18-19.

e Makala hii haizungumzii dhambi nzito ambazo zinapaswa kushughulikiwa na wazee, kama zile zinazotajwa kwenye 1 Wakorintho 6:9, 10.

f Inaripotiwa kwamba muda mrefu baadaye rabi fulani alisema hivi: “Duniani kuna wanaume wasiopungua thelathini walio waadilifu kama Abrahamu. Ikiwa wako thelathini, mimi na mwana wangu ni wawili kati yao; ikiwa wako kumi, mimi na mwana wangu ni wawili kati yao; ikiwa wako watano, mimi na mwana wangu ni wawili kati yao; ikiwa wako wawili, ni mimi na mwana wangu; ikiwa yuko mmoja tu, ni mimi.”