Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 10

Kwa Nini Ubatizwe?

Kwa Nini Ubatizwe?

“Kila mmoja wenu abatizwe.”​—MDO. 2:38.

WIMBO 34 Kutembea kwa Utimilifu

MUHTASARI a

1-2. Mara nyingi ni nini ambacho hutendeka watu wanapobatizwa, na unapaswa kuchunguza nini?

 JE, UMEWAHI kukitazama kikundi cha wale wanaotaka kubatizwa? Unaweza kusikia usadikisho walio nao katika sauti zao wanapojibu yale maswali mawili kabla ya kubatizwa. Unawaona watu wa familia na marafiki wakitabasamu kwa furaha. Wale wanaobatizwa wanapoinuliwa kutoka kwenye maji, unasikia wakipigiwa makofi na unaona shangwe katika nyuso zao. Kwa wastani, kila juma maelfu ya watu wanachukua hatua hiyo, na kuwa Mashahidi wa Yehova Mungu waliojiweka wakfu na kubatizwa.

2 Namna gani wewe? Ikiwa unafikiria kuhusu kubatizwa, wewe ni mtu wa pekee sana katika ulimwengu huu mwovu kwa sababu ‘unamtafuta Yehova.’ (Zab. 14:1, 2) Makala hii imeandikwa kwa ajili yako iwe wewe ni kijana au una umri mkubwa. Lakini sisi ambao tayari tumebatizwa tunataka pia kuimarisha azimio letu la kumtumikia Yehova milele. Hivyo, acheni tuchunguze pamoja sababu tatu kati ya nyingi zilizopo za kumtumikia Yehova.

UNAPENDA UKWELI NA UADILIFU

Shetani ameliletea suto jina zuri la Yehova kwa maelfu ya miaka na anaendelea kufanya hivyo (Tazama fungu la 3 na 4)

3. Kwa nini watumishi wa Yehova wanapenda ukweli na uadilifu? (Zaburi 119:128, 163)

3 Yehova aliwaagiza watu wake ‘wapende ukweli.’ (Zek. 8:19) Yesu aliwahimiza wafuasi wake wafuatie uadilifu. (Mt. 5:6) Hilo linamaanisha kwamba tunahitaji kuwa na tamaa yenye nguvu ya kufanya yaliyo sawa, mema, na safi machoni pa Mungu. Je, unapenda ukweli na uadilifu? Tuna uhakika unapenda sifa hizo. Unachukia uwongo na mambo yote ambayo si sawa na maovu. (Soma Zaburi 119:128, 163.) Mtu anayesema uwongo anaiga utu wa Shetani, mtawala wa ulimwengu huu. (Yoh. 8:44; 12:31) Lengo moja la Shetani ni kuliletea suto jina takatifu la Yehova Mungu. Shetani amekuwa akisambaza uwongo kumhusu Mungu tangu uasi katika bustani ya Edeni. Alijaribu kumfanya Yehova aonekane kuwa Mtawala mwenye ubinafsi na asiye mnyoofu ambaye anawanyima wanadamu mema. (Mwa. 3:1, 4, 5) Uwongo wa Shetani kumhusu Yehova umeendelea kutia sumu kwenye akili na mioyo ya watu. Wanadamu wanapochagua kukataa ‘kupenda ukweli,’ Shetani anaweza kuwaongoza katika kila aina ya mwenendo usio wa uadilifu na mwovu.​—Rom. 1:25-31.

4. Yehova amethibitikaje kuwa “Mungu wa ukweli”? (Tazama pia picha.)

4 Yehova ni “Mungu wa ukweli,” na kwa ukarimu anawafundisha kweli wale wanaompenda. (Zab. 31:5) Kwa kufanya hivyo, anawaweka huru kutokana na uwongo wa Shetani. Pia, Yehova anawafundisha watumishi wake wawe wanyoofu na waadilifu. Hilo linawasaidia wajiheshimu na wawe na amani ya moyoni. (Met. 13:5, 6) Huenda Yehova alikusaidia kwa njia hizo ulipokuwa ukijifunza Biblia. Umejifunza kwamba njia za Yehova ndizo bora kwa wanadamu wote na kwako binafsi. (Zab. 77:13) Hivyo, unataka kushikamana na uadilifu wa Mungu. (Mt. 6:33) Unataka kutetea ukweli na kusaidia kuthibitisha kwamba yale ambayo Shetani alisema kumhusu Mungu wetu, Yehova, ni uchongezi. Unawezaje kufanya hivyo?

5. Unawezaje kuchukua msimamo wa kutetea yale yaliyo kweli na yenye uadilifu?

5 Unaweza kuchagua kuishi aina ya maisha ambayo ni kana kwamba unasema: “Ninakataa uwongo wa Shetani na ninatetea ukweli. Ninataka Yehova awe Mtawala wangu Mwenye Enzi Kuu na ninataka kufanya yale ambayo anasema ni sawa.” Unawezaje kuchukua msimamo huo? Mkaribie Yehova katika sala na ujiweke wakfu kwake, kisha uonyeshe wakfu huo hadharani kwa kubatizwa. Kupenda yaliyo kweli na yenye uadilifu ni jambo linaloweza kukuchochea kwa njia kubwa kuamua kubatizwa.

UNAMPENDA YESU KRISTO

6. Zaburi 45:4 inakupatia sababu gani za kumpenda Yesu Kristo?

6 Kwa nini unampenda Yesu Kristo? Ona sababu nzuri zinazotajwa kwenye Zaburi 45:4. (Soma.) Yesu anapenda ukweli, unyenyekevu, na uadilifu. Ikiwa unapenda ukweli na uadilifu, inaeleweka kwamba unampenda Yesu Kristo pia. Fikiria jinsi Yesu alivyotetea kwa ujasiri mambo yaliyo kweli na yenye uadilifu. (Yoh. 18:37) Hata hivyo, Yesu anaonyeshaje kwamba anapenda sifa ya unyenyekevu?

7. Ni nini kinachokuvutia kuhusu unyenyekevu wa Yesu?

7 Yesu anaonyesha anapenda sifa ya unyenyekevu kupitia mfano wake. Kwa mfano, anaelekeza utukufu wote kwa Baba yake, kamwe hajielekezei mwenyewe utukufu. (Marko 10:17, 18; Yoh. 5:19) Unahisije unapoona unyenyekevu kama huo? Je, hilo halikuchochei kumpenda na kumfuata Mwana wa Mungu? Bila shaka unachochewa kufanya hivyo. Kwa nini Yesu ni mnyenyekevu? Kwa sababu anampenda na kumwiga Baba yake ambaye ni mnyenyekevu. (Zab. 18:35; Ebr. 1:3) Je, hilo halikufanyi uvutiwe na Yesu, ambaye anaiga kikamilifu sifa za Yehova?

8. Kwa nini tunampenda Yesu akiwa Mfalme wetu?

8 Tunampenda Yesu akiwa Mfalme wetu kwa sababu yeye ni Mtawala bora. Yehova mwenyewe alimzoeza Mwana wake na kumchagua atawale. (Isa. 50:4, 5) Pia, fikiria kuhusu upendo wa kujidhabihu ambao Yesu ameonyesha. (Yoh. 13:1) Akiwa Mfalme wako, Yesu anastahili kabisa upendo wako. Alieleza kwamba wale wanaompenda kikweli—ambao anawaita rafiki zake—wanaonyesha wanampenda kwa kutii amri zake. (Yoh. 14:15; 15:14, 15) Ni pendeleo lililoje kuwa rafiki ya Mwana wa Yehova!

9. Ubatizo wa Wakristo unafananaje na ule wa Kristo?

9 Amri moja ya Yesu ni kwamba wafuasi wake wabatizwe. (Mt. 28:19, 20) Yesu alituwekea mfano. Kwa njia fulani, ubatizo wake ni tofauti na ule wa wafuasi wake. (Tazama sanduku “ Ubatizo wa Yesu Unatofautianaje na Ubatizo wa Wafuasi Wake?”) Lakini katika njia nyingine unafanana. Yesu alipobatizwa, alijitoa ili afanye mapenzi ya Baba yake. (Ebr. 10:7) Vivyo hivyo, wafuasi wa Kristo wanabatizwa ili kuonyesha hadharani kwamba wamejiweka wakfu kwa Yehova Mungu. Sasa watatanguliza maishani kufanya mapenzi yake, si yao wenyewe. Hivyo, wanafuata mfano wa Bwana wao.

10. Kwa nini kumpenda Yesu kunapaswa kukuchochea ubatizwe?

10 Unamkubali Yesu kuwa Mwana mzaliwa pekee wa Yehova na kuwa Mfalme ambaye Mungu amemchagua kututawala. Unajua kwamba Yesu ni mnyenyekevu, na anamwiga Baba yake kikamilifu. Umejifunza kwamba aliwalisha waliokuwa na njaa, aliwafariji waliovunjika moyo, na hata aliwaponya wagonjwa. (Mt. 14:14-21) Umeona jinsi anavyoongoza kutaniko lake leo. (Mt. 23:10) Na unajua kwamba atafanya mengi zaidi wakati ujao akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu. Unawezaje kuonyesha kwamba unampenda Yesu? Kwa kuiga mfano wake. (Yoh. 14:21) Unaweza kuanza kufanya hivyo kwa kujiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa.

UNAMPENDA YEHOVA MUNGU

11. Ungesema sababu muhimu zaidi ya kubatizwa ni nini, na kwa nini unasema hivyo?

11 Sababu muhimu zaidi ya kubatizwa ni nini? Yesu alifunua amri ya Mungu iliyo kuu zaidi, aliposema: “Nawe lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote na kwa nguvu zako zote.” (Marko 12:30) Je, maneno hayo yanafafanua upendo wako kwa Mungu?

Yehova ndiye Chanzo cha kila kitu chema ambacho umewahi kufurahia na utakachofurahia wakati ujao (Tazama fungu la 12 na 13)

12. Kwa nini unampenda Yehova? (Tazama pia picha.)

12 Kuna sababu nyingi sana za kumpenda Yehova. Kwa mfano, umeelewa kwamba yeye ni “chanzo cha uhai” na kwamba yeye ni Mpaji wa “kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu.” (Zab. 36:9; Yak. 1:17) Kila kitu chema unachofurahia kinatoka kwa Mungu wetu mwenye ukarimu na upendo.

13. Kwa nini fidia ni zawadi nzuri sana?

13 Fidia ni zawadi nzuri sana ambayo Yehova ametupatia. Kwa nini tunaweza kusema hivyo? Fikiria uhusiano wa karibu uliopo kati ya Yehova na Mwana wake. Yesu alisema hivi: “Baba ananipenda” na “ninampenda Baba.” (Yoh. 10:17; 14:31) Uhusiano wa karibu kati yao uliimarika hata zaidi walipokuwa pamoja kwa mabilioni ya miaka. (Met. 8:22, 23, 30) Sasa, fikiria jinsi ambavyo Mungu aliumia aliporuhusu Mwana wake ateseke na kufa. Yehova anawapenda wanadamu sana—kutia ndani wewe—hivi kwamba alikuwa tayari kumtoa Mwana wake mpendwa kuwa dhabihu ili kukuwezesha wewe na wengine kuishi milele. (Yoh. 3:16; Gal. 2:20) Hiyo ndiyo sababu kuu zaidi tuliyo nayo ya kumpenda Mungu.

14. Ni lengo gani bora kabisa unaloweza kuchagua maishani?

14 Upendo wako kwa Yehova umeongezeka kadiri ulivyojifunza mengi zaidi kumhusu. Bila shaka, unataka kumkaribia zaidi sasa na milele. Na unaweza kufanya hivyo. Kwa fadhili, anakutia moyo ufanye moyo wake ushangilie. (Met. 23:15, 16) Unaweza kufanya hivyo, si kwa maneno tu, bali pia kwa matendo. Njia yako ya maisha itaonyesha kwamba kwa kweli unampenda Yehova. (1 Yoh. 5:3) Kuchagua kuishi maisha yanayompendeza Yehova ndilo lengo bora zaidi unaloweza kuchagua.

15. Unaweza kuonyeshaje kwamba unampenda Yehova?

15 Unaweza kuonyeshaje kwamba unampenda Yehova? Kwanza, ni kwa kutoa sala ya pekee ambapo unajiweka wakfu kwa Mungu wa pekee wa kweli. (Zab. 40:8) Kisha, unaonyesha hadharani wakfu wako ulioweka faraghani kwa kubatizwa. Kama tulivyozungumzia awali katika makala hii, hilo ni tukio lenye shangwe, na muhimu maishani mwako. Unaanza maisha mapya, ukiishi si kwa ajili yako mwenyewe, bali kwa ajili ya Yehova. (Rom. 14:8; 1 Pet. 4:1, 2) Uamuzi huo unaweza kuonekana kuwa uamuzi mzito, na ndivyo ilivyo. Lakini utakuwezesha kuishi maisha bora kabisa. Jinsi gani?

16. Kama Zaburi 41:12 inavyoonyesha, Yehova atawathawabishaje wale wanaotoa maisha yao ili kumtumikia?

16 Yehova ndiye Mtu mkarimu zaidi. Hata umpatie nini, sikuzote atakupatia mengi zaidi ya uliyotoa. (Marko 10:29, 30) Atakupatia maisha yenye kufurahisha, yenye kuthawabisha, na yenye kuridhisha zaidi, hata sasa kwenye ulimwengu huu mwovu unaokaribia mwisho wake. Na huo ni mwanzo tu. Safari yako inayoanza unapobatizwa haihitaji kufika mwisho. Unaweza kuendelea kumtumikia Baba yako mpendwa milele. Upendo ulio kati yako na Baba yako utaendelea kuongezeka, na kwa kweli utaishi kwa muda mrefu kama yeye anavyoishi, yaani, kwa umilele wote.​—Soma Zaburi 41:12.

17. Ni nini unachoweza kumpatia Yehova ambacho bado hana?

17 Unapochukua hatua ya kujiweka wakfu na kubatizwa, unakuwa na pendeleo la kumpatia Baba yako kitu chenye thamani sana. Amekupatia kila kitu chema, kila pindi yenye furaha, ambayo umewahi kufurahia. Nawe unaweza kumpatia Mmiliki wa mbingu na dunia kitu ambacho bado hana, yaani, utumishi wako mshikamanifu na wa hiari. (Ayu. 1:8; 41:11; Met. 27:11) Kwa hakika, hiyo ndiyo njia bora zaidi ya maisha! Bila shaka, upendo wako kwa Yehova ndiyo sababu bora ya kuamua kubatizwa.

JE, UKO TAYARI KUBATIZWA?

18. Ni maswali gani unayoweza kujiuliza?

18 Basi, ungejibuje swali, Je, utabatizwa? Ni wewe pekee unayeweza kujibu swali hilo. Lakini huenda ikafaa ujiulize, ‘Je, niko tayari kubatizwa?’ (Mdo. 8:36) Kumbuka sababu tatu za kubatizwa ambazo tumechunguza. Kwanza, unapenda ukweli na uadilifu. Jiulize, ‘Je ninataka kuona siku ambayo kila mtu atasema ukweli na kufanya yaliyo sawa?’ Pili, unampenda Yesu Kristo. Jiulize, ‘Je, ninataka Mwana wa Mungu awe Mfalme wangu, na je, ninataka kufuata mfano wake?’ Tatu, zaidi ya yote, unampenda Yehova. Jiulize, ‘Je, ninataka kufanya moyo wa Yehova ushangilie kwa kumtumikia akiwa Mungu wangu?’ Ikiwa majibu ya maswali hayo ni ndiyo, basi kwa nini usibatizwe? Kwa nini ukawie?​—Mdo. 16:33.

19. Kwa nini hupaswi kusitasita kubatizwa? Toa mfano. (Yohana 4:34)

19 Ikiwa unasitasita kubatizwa, fikiria mfano ambao Yesu alitumia. (Soma Yohana 4:34.) Ona kwamba Yesu alilinganisha kufanya mapenzi ya Baba yake na chakula. Kwa nini? Chakula kinatunufaisha. Yesu alijua kwamba kila jambo ambalo Yehova anatuomba tufanye ni kwa faida yetu. Yehova hataki tufanye jambo lolote ambalo litatudhuru. Je, mapenzi ya Yehova kukuelekea yanatia ndani kubatizwa? Ndiyo. (Mdo. 2:38) Hivyo, unaweza kuwa na uhakika kwamba kutii amri ya kubatizwa kutakunufaisha. Ikiwa hutasita kufurahia mlo mzuri sana, kwa nini usite kubatizwa?

20. Tutachunguza nini katika makala inayofuata?

20 Kwa nini wengine wanakawia kubatizwa? Huenda wengi wakajibu, “Kwa sasa siko tayari.” Ukweli ni kwamba uamuzi wa kujiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa ndio uamuzi muhimu zaidi utakaowahi kufanya. Hivyo, ili uwe tayari unahitaji muda, unahitaji kutafakari kwa makini, na kutia bidii. Lakini ikiwa kwa unyoofu unatamani kuchukua hatua hiyo ya kubatizwa, unaweza kufanya nini sasa ili ujitayarishe? Tutajibu swali hilo katika makala inayofuata.

WIMBO 28 Kuwa Rafiki ya Yehova

a Ubatizo ni hatua muhimu kwa kila mwanafunzi wa Biblia. Ni nini kinachoweza kumchochea mwanafunzi achukue hatua hiyo? Kwa ufupi, ni upendo. Lakini upendo kuelekea nini na kwa nani? Katika makala hii, tutatafuta majibu ya maswali hayo na tutazungumzia aina ya maisha tunayoweza kutarajia tukiwa Wakristo waliobatizwa.