Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Kwa nini mwanamume aliyeitwa “Fulani wa fulani” alisema kwamba urithi wake ‘ungeharibiwa’ ikiwa angemwoa Ruthu? (Ruthu 4:1, 6)

Katika nyakati za Biblia, ikiwa mwanamume aliyeoa angekufa bila kupata mtoto, maswali fulani yangehitaji kujibiwa: Ingekuwaje kwa ardhi yoyote aliyomiliki? Je, jina la familia yake lingepotea milele? Sheria ya Musa ilijibu maswali hayo.

Ingekuwaje kwa ardhi ya mwanamume aliyekufa au aliyekuja kuwa maskini na kuuza ardhi yake? Ndugu yake au mtu wake wa karibu wa ukoo angeweza kukomboa ardhi hiyo. Hivyo ingebaki katika familia.​—Law. 25:23-28; Hes. 27:8-11.

Jina la familia ya mwanamume aliyekufa lingehifadhiwaje? Kupitia ndoa ya ndugu mkwe, ambayo ilitumiwa katika kisa cha Ruthu. Mwanamume angemwoa mjane wa ndugu yake ili kutokeza mrithi ambaye angeendeleza jina la mwanamume aliyekufa na kurithi mali yake. Mpango huo wenye upendo pia ulimtunza mjane.​—Kum. 25:5-7; Mt. 22:23-28.

Fikiria mfano wa Naomi. Alikuwa ameolewa na mwanamume aliyeitwa Elimeleki. Mume wake na wana wake wawili walipokufa, aliachwa bila mwanamume wa kumwandalia mahitaji yake. (Rut. 1:1-5) Aliporudi Yuda, Naomi alimwongoza Ruthu, binti mkwe wake, amwombe Boazi awe mkombozi na anunue ardhi yao. Boazi alikuwa mtu wa karibu wa ukoo wa Elimeleki. (Rut. 2:1, 19, 20; 3:1-4) Lakini Boazi alimfahamu mtu mwingine wa ukoo, ambaye Biblia inamwita “Fulani wa fulani,” aliyekuwa mtu wa karibu zaidi wa ukoo. Hivyo, alikuwa na fursa ya kwanza ya kuchagua ikiwa angetaka kuwa mkombozi.​—Rut. 3:9, 12, 13.

Mwanzoni, “Fulani wa fulani” alikuwa tayari kusaidia. (Rut. 4:1-4) Ingawa ingehusisha gharama fulani, alitambua kwamba Naomi hangeweza kuzaa mtoto ambaye angeweza kurithi ardhi ya Elimeleki. Kimsingi ardhi hiyo ingeongezwa kwenye urithi wa ardhi ya Fulani wa fulani, hivyo lingeonekana kuwa jambo ambalo lilimnufaisha.

Lakini Fulani wa fulani alibadili uamuzi wake alipotambua kwamba angehitaji kumwoa Ruthu. Alisema hivi: “Siwezi kulikomboa [shamba] kwa maana huenda nikaharibu urithi wangu mwenyewe.” (Rut. 4:5, 6) Kwa nini alibadili uamuzi wake?

Ikiwa Fulani wa fulani au mtu mwingine angemwoa Ruthu na angepata mwana, mwana huyo angerithi ardhi ya Elimeleki. Hilo ‘lingeharibu’ jinsi gani “urithi” wa Fulani wa fulani? Biblia haisemi, lakini huenda ni kwa njia zifuatazo.

  • Kwanza, pesa ambazo angetumia zingepotea, kwa sababu mwishowe asingemiliki ardhi ya Elimeleki. Mwana wa Ruthu angeirithi.

  • Pili, angekuwa na jukumu la kumlisha na kumtunza Naomi pamoja na Ruthu.

  • Tatu, ikiwa Ruthu angepata watoto wengine na Fulani wa fulani, wangegawana urithi na watoto wengine wowote ambao Fulani wa fulani alikuwa nao.

  • Nne, ikiwa Fulani wa fulani hakuwa na watoto wengine wa kwake mwenyewe, mwana ambaye Ruthu angezaa angekuwa na haki ya kurithi ardhi ya Elimeleki na ya Fulani wa fulani. Baada ya kifo chake, ardhi yake ingeenda kwa mwana ambaye alikuwa na jina la Elimeleki, na si lake. Fulani wa fulani hakuwa tayari kuhatarisha urithi wake ili amsaidie Naomi. Aliamua kumruhusu Boazi, mkombozi aliyefuata, achukue hilo jukumu. Boazi alichukua jukumu hilo kwa sababu alitaka “kurudisha jina la mwanamume huyo aliyekufa katika urithi wake.”​—Rut. 4:10.

Inaonekana kwamba Fulani wa fulani alikazia fikira zaidi kudumisha jina na urithi wake mwenyewe. Ubinafsi ulitawala njia yake ya kufikiri. Lakini badala ya kuhifadhi jina lake, jina la Fulani wa fulani hata halijulikani kabisa leo. Pia, alikosa pendeleo la pekee ambalo Boazi alipata, la kuorodheshwa kwenye ukoo ambao ulimtokeza Masihi, Yesu Kristo. Hayo ni matokeo yenye kusikitisha sana kwa Fulani wa fulani kwa sababu kwa ubinafsi alikataa fursa ya kumsaidia mtu mwenye uhitaji!—Mt. 1:5; Luka 3:23, 32.