Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 13

Tumia Uumbaji Kuwafundisha Watoto Wako Kumhusu Yehova

Tumia Uumbaji Kuwafundisha Watoto Wako Kumhusu Yehova

“Ni nani aliyeviumba vitu hivi?”​—ISA. 40:26.

WIMBO 11 Uumbaji Unamsifu Mungu

MUHTASARI a

1. Wazazi wanatamani nini kwa ajili watoto wao?

 WAZAZI, tunajua kwamba mnataka kuwasaidia watoto wenu wamjue na kumpenda Yehova. Lakini Mungu haonekani. Mnaweza kuwasaidiaje watoto wenu wamwone kuwa Mtu halisi na kumkaribia?​—Yak. 4:8.

2. Wazazi wanaweza kuwafundishaje watoto wao kuhusu sifa za Yehova?

2 Njia muhimu ya kuwasaidia watoto wako wamkaribie Yehova ni kwa kujifunza Biblia pamoja nao. (2 Tim. 3:14-17) Hata hivyo, Biblia inafunua njia nyingine ambayo watoto wanaweza kujifunza kumhusu Yehova. Kwenye kitabu cha Methali, inaonekana kuwa baba anamkumbusha mwana wake kwamba sifa za Yehova, ambazo zinaonekana kupitia uumbaji, zisiondoke machoni pake kamwe. (Met. 3:19-21) Tutachunguza baadhi ya njia ambazo wazazi wanaweza kutumia uumbaji kuwasaidia watoto wao wajifunze kuhusu utu wa Yehova.

TUMIA UUMBAJI KUWAFUNDISHA WATOTO WAKO—JINSI GANI?

3. Wazazi wanapaswa kuwasaidiaje watoto wao?

3 Biblia inasema kwamba “sifa [za Mungu] zisizoonekana, zinaonekana waziwazi tangu kuumbwa kwa ulimwengu na kuendelea, kwa sababu zinaeleweka kupitia vitu vilivyoumbwa.” (Rom. 1:20) Wazazi, inaelekea mnafurahia kutumia wakati pamoja na watoto wenu mkiwa nje. Tumia wakati huo kuwasaidia watoto wako waone uhusiano kati ya vitu vilivyoumbwa na sifa zenye kustaajabisha za Yehova. Kuhusiana na hilo, acheni tuone mambo ambayo wazazi wanaweza kujifunza kutokana na mfano wa Yesu.

4. Yesu alitumiaje uumbaji kuwafundisha wanafunzi wake? (Luka 12:24, 27-30)

4 Ona jinsi Yesu alivyotumia uumbaji kufundisha. Pindi moja, aliwaambia wanafunzi wake waangalie kunguru na mayungiyungi. (Soma Luka 12:24, 27-30.) Yesu angeweza kutaja mnyama au mmea wowote, lakini alichagua ndege na ua ambalo wanafunzi wake walifahamu vizuri. Huenda wanafunzi hao waliona kunguru wakipaa angani na maua yakichanua shambani. Je, unaweza kuwazia Yesu akivinyooshea mkono vitu hivyo alipozungumza? Na alifanya nini baada ya kutaja mifano hiyo? Aliwafundisha wanafunzi wake somo muhimu sana kuhusu ukarimu na fadhili za Baba yao wa mbinguni: Yehova atawalisha na kuwavisha watumishi wake waaminifu kama anavyofanya kwa kunguru na mayungiyungi ya shambani.

5. Ni vitu gani vinavyopatikana katika uumbaji ambavyo wazazi wanaweza kutumia kuwafundisha watoto wao kumhusu Yehova?

5 Wazazi, je, mtaiga njia ya Yesu ya kufundisha? Huenda ukamwambia mtoto wako kuhusu uumbaji fulani ambao wewe binafsi unathamini, kama vile mnyama au mmea unaopenda. Unapofanya hivyo, hakikisha unafafanua kitu hicho kinafunua nini kumhusu Yehova. Kisha unaweza kumwuliza mtoto wako kuhusu mnyama au mmea anaoupenda zaidi. Ikiwa utatumia uumbaji fulani ambao tayari anavutiwa nao, huenda atakusikiliza kwa makini hata zaidi unapozungumzia sifa za Yehova.

6. Tunaweza kujifunza nini kutokana na kielelezo alichotuwekea mama ya Christopher?

6 Je, wazazi wanahitaji kutumia muda mwingi sana kufanya utafiti kuhusu mnyama au mmea fulani hususa kabla ya kuzungumzia uumbaji huo unafunua nini kumhusu Yehova? Si lazima. Yesu hakutoa maelezo mengi kuhusu jinsi kunguru anavyokula au kuhusu jinsi mayungiyungi yanavyokua. Ingawa huenda pindi fulani mtoto wako akafurahia mazungumzo yenye kina zaidi kuhusu uumbaji, nyakati nyingine maelezo mafupi au swali rahisi linatosha kumsaidia aelewe jambo kuu. Ona jambo ambalo ndugu anayeitwa Christopher anakumbuka alipokuwa mtoto: “Mama yangu angetoa maelezo rahisi ili kutusaidia kuthamini uumbaji unaotuzunguka. Kwa mfano, tulipokuwa karibu na eneo lenye milima, angesema hivi: ‘Angalia jinsi milima hii ilivyo mikubwa na yenye kupendeza! Yehova ni mwenye kustaajabisha, sivyo?’ Au tulipokuwa karibu na bahari angesema: ‘Angalia mawimbi hayo yalivyo na nguvu! Yehova ni Mungu mwenye nguvu sana, sivyo?’” Christopher anasema hivi: “Maelezo hayo rahisi na yenye kuchochea fikira yalitusaidia sana.”

7. Unawezaje kuwazoeza watoto wako watafakari kuhusu uumbaji?

7 Watoto wako wanapozidi kukua, unaweza kuwazoeza wafikirie zaidi kuhusu uumbaji na mambo wanayojifunza kuhusu utu wa Yehova. Unaweza kuzungumzia jambo moja kuhusu kazi za uumbaji za Mungu na kuwauliza watoto wako, “Jambo hili linakufundisha nini kumhusu Yehova?” Huenda ukashangazwa na kufurahishwa na maelezo yao.​—Mt. 21:16.

NI WAKATI GANI UNAWEZA KUTUMIA UUMBAJI KUWAFUNDISHA WATOTO WAKO?

8. Ni fursa gani ambazo wazazi Waisraeli walikuwa nazo waliposafiri “barabarani”?

8 Wazazi Waisraeli walihimizwa kuwafundisha watoto wao maneno ya amri za Yehova walipokuwa wakitembea “barabarani.” (Kum. 11:19) Katika Israeli, barabara zilifika hadi kwenye maeneo ya mashambani. Wanyama, ndege, na maua mbalimbali yaliweza kuonekana. Familia za Waisraeli ziliposafiri kwenye barabara hizo, wazazi walipata fursa za kuwasaidia watoto wao wapendezwe na uumbaji wa Yehova. Enyi wazazi, huenda ninyi pia mna fursa kama hizo za kutumia uumbaji kuwafundisha watoto wenu. Ona jinsi ambavyo baadhi ya wazazi wamefanya hivyo.

9. Unaweza kujifunza nini kutoka kwa Punitha na Katya?

9 Mama anayeitwa Punitha, ambaye anaishi katika jiji kubwa nchini India, anasema hivi: “Tunapowatembelea watu wa familia wanaoishi kwenye maeneo ya mashambani, tunaiona hiyo kuwa fursa ya kuwasaidia watoto wetu wajifunze kuhusu uumbaji maridadi wa Yehova. Ninahisi kwamba watoto wangu wanaelewa uumbaji vizuri zaidi wanapokuwa mbali na barabara zenye watu wengi na zilizojaa magari.” Wazazi, inaelekea watoto wenu hawatasahau kamwe muda mnaotumia pamoja nao katika mandhari zenye kupendeza. Katya, dada kutoka nchini Moldova, anasema hivi: “Pindi ninazokumbuka zaidi za utotoni, ni zile tulizotumia pamoja na wazazi wangu kwenye maeneo ya mashambani. Ninawashukuru sana kwa kunifundisha tangu utotoni kutua na kuchunguza mambo ambayo Yehova ameumba na kumwona kupitia uumbaji wake.”

Hata ukiwa jijini, huenda ukaona uumbaji mbalimbali ambao unaweza kutumia kuwafundisha watoto wako kumhusu Yehova (Tazama fungu la 10)

10. Wazazi wanaweza kufanya nini ikiwa wanaona ni vigumu kusafiri nje ya mji? (Tazama sanduku “ Msaada kwa Ajili ya Wazazi.”)

10 Namna gani ikiwa haiwezekani kwenu kusafiri kwenye maeneo ya mashambani? Amol, ambaye pia anaishi nchini India, anasema hivi: “Mahali ninapoishi, wazazi wanahitaji kufanya kazi kwa saa nyingi, na safari ya kwenda kwenye eneo la mashambani inaweza kuwa na gharama kubwa. Hata hivyo, bustani ndogo au baraza lililo juu ya nyumba ni mahali panapoweza kutumiwa kutazama uumbaji na kuzungumza kuhusu sifa za Yehova.” Unapoangalia kwa makini, inaelekea utagundua mambo mengi kuhusu uumbaji ambayo unaweza kuwaonyesha watoto wako karibu na nyumba yako. (Zab. 104:24) Huenda ukapata ndege, wadudu, mimea, na mambo mengi zaidi. Karina, kutoka nchini Ujerumani, anasema hivi: “Mama yangu anapenda maua. Hivyo, nilipokuwa msichana mdogo angenionyesha maua mazuri kila wakati tulipotembea pamoja.” Wazazi, mnaweza pia kutumia video na machapisho mengi kuhusu uumbaji ambayo tengenezo letu limeandaa ili kuwafundisha watoto wenu. Naam, hata hali zako ziweje, unaweza kuwasaidia watoto wako kuchunguza uumbaji wa Mungu. Sasa, acheni tufikirie baadhi ya sifa za Yehova ambazo unaweza kukazia kwa watoto wako.

SIFA ZA YEHOVA “ZISIZOONEKANA, ZINAONEKANA WAZIWAZI”

11. Wazazi wanawezaje kuwasaidia watoto wao watambue upendo wa Yehova?

11 Ili kuwasaidia watoto wako watambue upendo wa Yehova, unaweza kukazia jinsi ambavyo kwa wororo wanyama wengi wanawatunza watoto wao. (Mt. 23:37) Pia, unaweza kukazia aina mbalimbali za uumbaji unaofurahia sana. Karina, aliyenukuliwa awali anasema hivi: “Tulipokuwa tukitembea pamoja, mama yangu alinitia moyo nitue na kuchunguza jinsi kila ua lilivyo la pekee na jinsi uzuri wake unavyoonyesha upendo wa Yehova. Miaka mingi baadaye, bado ninachunguza kwa makini maua na ninatambua jinsi yanavyotofautiana katika muundo na rangi. Yanaendelea kunikumbusha jinsi Yehova anavyotupenda sana.”

Unaweza kukazia jinsi mwili wetu ulivyoumbwa kwa njia yenye kustaajabisha ili kumfundisha mtoto wako kuhusu hekima ya Yehova (Tazama fungu la 12)

12. Wazazi wanawezaje kuwasaidia watoto wao watambue hekima ya Mungu? (Zaburi 139:14) (Tazama pia picha.)

12 Wasaidie watoto wako watambue hekima ya Mungu. Bila shaka, Yehova ana hekima nyingi sana kuliko sisi. (Rom. 11:33) Kwa mfano, unaweza kukazia jinsi maji yanayotengeneza mawingu yanavyoelea kwa urahisi kutoka sehemu moja hadi nyingine. (Ayu. 38:36, 37) Pia, unaweza kukazia jinsi mwili wa mwanadamu ulivyoumbwa kwa njia yenye kustaajabisha. (Soma Zaburi 139:14.) Fikiria jinsi baba anayeitwa Vladimir alivyofanya hivyo. Anasema hivi: “Siku moja mwana wetu alianguka kutoka kwenye baiskeli na akajijeruhi. Baada ya siku chache, jeraha hilo lilipona. Mimi na mke wangu tulimfafanulia kwamba Yehova aliumba seli za mwili wetu zikiwa na uwezo wa kujirekebisha zenyewe. Tulimweleza kwamba hatuoni jambo kama hilo katika vitu ambavyo wanadamu wanatengeneza. Kwa mfano, gari halijirekebishi lenyewe baada ya aksidenti. Jambo hilo lilimsaidia mwana wetu aelewe hekima ya Yehova.”

13. Wazazi wanawezaje kuwasaidia watoto wao watambue nguvu za Mungu? (Isaya 40:26)

13 Yehova anatualika tuinue macho yetu mbinguni na kufikiria kuhusu jinsi ambavyo nguvu zake zenye kustaajabisha zinahakikisha nyota zote ziko mahali sahihi. (Soma Isaya 40:26.) Unaweza kuwatia moyo watoto wako walitazame anga na kutafakari kuhusu mambo wanayoona. Ona jambo ambalo Tingting, dada kutoka Taiwan, anakumbuka alipokuwa mtoto: “Pindi moja tulienda na mama kupiga kambi kwenye mahema nje ya mji, na tulitazama anga la usiku na kuona nyota nyingi kwa sababu tulikuwa mbali na taa za jijini. Pindi hiyo nilikuwa na wasiwasi kuhusu kushinikizwa na wanafunzi wenzangu na nilijiuliza ikiwa nitaweza kumtumikia Yehova kwa uaminifu. Mama yangu alinitia moyo nifikirie kuhusu nguvu ambazo Yehova alitumia alipoumba nyota hizo zote na nikumbuke kwamba kwa hakika anaweza kutumia nguvu hizo kunisaidia kukabiliana na jaribu lolote. Baada ya kuchunguza uumbaji kwenye safari hiyo, nilichochewa kumjua Yehova vizuri zaidi na niliimarisha azimio langu la kumtumikia.”

14. Wazazi wanawezaje kutumia uumbaji kuwasaidia watoto wao wamwone Yehova kuwa Mungu mwenye furaha?

14 Uumbaji wa Yehova unamwonyesha kuwa Mungu mwenye shangwe na mwenye ucheshi. Wanasayansi wameona kwamba wanyama wengi wanapenda kucheza, kutia ndani ndege na samaki. (Ayu. 40:20) Je, watoto wako wamewahi kucheka walipomwona mnyama fulani akicheza? Labda wamewahi kuona mtoto wa paka akicheza na uzi wa kufumia au watoto wa mbwa wakicheza mieleka. Pindi nyingine watoto watakapocheka wanapotazama michezo ya wanyama, kwa nini usiwakumbushe kwamba tunamtumikia Mungu mwenye furaha?​—1 Tim. 1:11.

FURAHIENI UUMBAJI WA YEHOVA MKIWA FAMILIA

Huenda watoto wako wakahisi wamestarehe zaidi na wakawa tayari zaidi kuzungumzia hisia zao wanapokuwa wakifurahia uumbaji pamoja nawe (Tazama fungu la 15)

15. Ni nini kinachoweza kuwasaidia wazazi kuteka mawazo ya watoto wao? (Methali 20:5) (Tazama pia picha.)

15 Nyakati nyingine, huenda wazazi wakaona ni vigumu kwa watoto wao kuzungumzia matatizo wanayokabili. Ikiwa unakabili hali hiyo, huenda ukahitaji kuteka mawazo ya watoto wako. (Soma Methali 20:5.) Baadhi ya wazazi wanaona ni rahisi zaidi kufanya hivyo wanapokuwa wakifurahia uumbaji pamoja na watoto wao. Kwa nini? Sababu moja ni kwamba hakuna vikengeusha fikira vingi kwa watoto na kwa wazazi. Masahiko, baba anayeishi Taiwan, anataja sababu nyingine: “Tunapotumia muda nje pamoja na watoto wetu—kupanda milima au kutembea kwenye ufuo wa bahari—kwa kawaida wanajihisi wamestarehe. Kwa hiyo, katika pindi hizo tunaona ikiwa rahisi zaidi kuteka mawazo yao na kujua kile kilicho akilini mwao.” Katya, aliyenukuliwa awali, anasema hivi: “Baada ya shule, mama yangu angenipeleka kwenye bustani maridadi. Katika mazingira hayo yenye kustarehesha, ilikuwa rahisi zaidi kumweleza ni nini kilichotokea shuleni au jambo lililonihangaisha.”

16. Familia zinawezaje kupumzika na kustarehe pamoja wanapofurahia uumbaji wa Yehova?

16 Pia, uumbaji wa Yehova unaweza kutoa fursa kwa familia kupumzika na kufurahi pamoja, na hivyo kuimarisha upendo katika familia. Biblia inasema kwamba kuna “wakati wa kucheka” na “wakati wa kurukaruka.” (Mhu. 3:1, 4, maelezo ya chini) Kupitia kazi ya mikono yake, Yehova ametupatia mandhari maridadi ili tufurahie utendaji wenye kuburudisha. Familia nyingi zinapenda kuwa pamoja katika hifadhi za wanyama, maeneo ya mashambani, milimani, au katika ufuo wa bahari. Baadhi ya watoto wanapenda kukimbia na kucheza katika bustani, kuangalia wanyama, kuogelea mtoni, ziwani, au baharini. Tuna nafasi nzuri sana za kufanya tafrija kwenye maeneo ya nje, tukiwa tumezungukwa na vitu ambavyo Yehova ameumba!

17. Kwa nini wazazi wanapaswa kuwasaidia watoto wao wafurahie uumbaji wa Mungu?

17 Katika ulimwengu mpya wa Mungu, wazazi na watoto watafurahia uumbaji wa Yehova kuliko wakati mwingine wowote. Tofauti na leo, hatutakuwa na sababu ya kuwaogopa wanyama; nao hawatatuogopa. (Isa. 11:6-9) Tutakuwa na wakati usio na kikomo wa kufurahia vitu ambavyo Yehova ameumba. (Zab. 22:26) Lakini wazazi, msisubiri hadi wakati huo kuwasaidia watoto wenu waanze kufurahia uumbaji. Unapotumia uumbaji kuwafundisha watoto wako kumhusu Yehova, inaelekea watakubaliana na kile ambacho Mfalme Daudi alisema: “Ee Yehova, hakuna kazi zilizo kama kazi zako.”​—Zab. 86:8.

WIMBO 134 Watoto—Amana Kutoka kwa Mungu

a Ndugu na dada wengi wana kumbukumbu nzuri za wakati waliotumia kufurahia uumbaji pamoja na wazazi wao Wakristo. Hawajasahau jinsi wazazi wao walivyotumia pindi hizo kuwafundisha kuhusu utu wa Yehova. Ikiwa una watoto, unawezaje kutumia uumbaji kuwafundisha kuhusu sifa za Mungu? Makala hii itajibu swali hilo.