Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana​—Simameni Imara Mmpinge Ibilisi

Vijana​—Simameni Imara Mmpinge Ibilisi

“Vaeni mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu ili mweze kusimama imara dhidi ya matendo yenye hila ya Ibilisi.”​—EFE. 6:11.

NYIMBO: 79, 140

1, 2. (a) Kwa nini vijana Wakristo wanaendelea kushinda vita dhidi ya majeshi ya roho waovu? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.) (b) Tutachunguza nini?

MTUME Paulo alilinganisha maisha yetu tukiwa Wakristo na maisha ya wanajeshi wanaopigana vita kwa kutumia mikono. Bila shaka, tunapigana vita vya kiroho, si vita halisi. Hata hivyo, maadui wetu ni viumbe halisi. Shetani na roho waovu ni mashujaa stadi wenye uzoefu mwingi. Huenda hali yetu ikaonekana kuwa yenye kukatisha tamaa. Na vijana hasa ndio wanaoonekana kuwa rahisi kushambuliwa. Ni nini kinachoweza kuwapa uhakika kwamba wanaweza kuyashinda majeshi ya roho waovu wenye nguvu zinazopita za wanadamu? Ukweli ni kwamba vijana wanaweza kushinda, na wanaendelea kushinda! Kwa nini? Kwa sababu “[wanaendelea] kujipatia nguvu katika Bwana.” Lakini wanafanya mengi zaidi ya kutegemea nguvu kutoka kwa Mungu. Wamejivika mavazi ya vita. Kama wanajeshi waliozoezwa vizuri, vijana “[wamevaa] mavazi kamili ya silaha kutoka kwa Mungu.”—Soma Waefeso 6:10-12.

2 Paulo alipokuwa akifafanua mfano wake, huenda alikuwa akifikiria kuhusu mavazi ambayo wanajeshi Waroma walivaa. (Mdo. 28:16) Acheni tuchunguze kwa nini mfano huo ulifaa. Tunapofanya hivyo, ona yale ambayo baadhi ya vijana wanasema kuhusu changamoto na faida zinazotokana na kuvaa kila sehemu ya mavazi ya kiroho.

Je, Umevaa Mavazi Kamili ya Silaha?

“MSHIPI WA ILE KWELI”

3, 4. Ni katika njia gani kweli za Biblia ni kama mshipi uliovaliwa na mwanajeshi Mroma?

3 Soma Waefeso 6:14. Mshipi uliovaliwa na mwanajeshi Mroma ulikuwa na vipande vya chuma vilivyolinda kiuno chake. Ulitengenezwa ili utegemeze uzito wa bamba la kifuani. Pia, baadhi ya mishipi ilikuwa na vishikizo imara vilivyotumiwa kubeba upanga na kisu. Akiwa amejifunga mshipi huo vizuri, mwanajeshi angeweza kusimama vitani kwa ujasiri.

4 Vivyo hivyo, kweli tunazojifunza katika Neno la Mungu hutulinda dhidi ya madhara ya kiroho yanayosababishwa na mafundisho ya uwongo. (Yoh. 8:31, 32; 1 Yoh. 4:1) Na kadiri tunavyopenda kweli zinazotoka kwa Mungu, ndivyo inavyokuwa rahisi zaidi kwetu kubeba “bamba la kifuani,” yaani, kuishi kulingana na viwango vya Mungu vya uadilifu. (Zab. 111:7, 8; 1 Yoh. 5:3) Zaidi ya hilo, tunapoelewa vizuri kweli za Neno la Mungu, tunaweza kusimama imara na kuzitetea hata tunapopingwa.—1 Pet. 3:15.

5. Kwa nini tunapaswa kusema kweli?

5 Tunapojifunga vizuri kiunoni kweli ya Biblia, tutachochewa kuishi kulingana na kweli hiyo na kusema kweli nyakati zote. Kwa nini tutaepuka kusema uwongo? Kwa sababu kusema uwongo ni mojawapo ya silaha ambazo Shetani ametumia kwa mafanikio. Kusema uwongo humdhuru yule anayeusema na anayeuamini. (Yoh. 8:44) Hivyo, ingawa sisi si wakamilifu, tunajitahidi kadiri tuwezavyo tusiseme uwongo. (Efe. 4:25) Lakini inaweza kuwa changamoto kufanya hivyo. Abigail, msichana mwenye umri wa miaka 18 anasema hivi: “Nyakati nyingine huenda ikaonekana kwamba hakuna faida ya kusema kweli, hasa ikiwa kusema uwongo kunaweza kukusaidia ujinasue kutoka katika hali fulani ngumu.” Basi kwa nini yeye hujitahidi kusema kweli nyakati zote? Anaendelea kusema hivi: “Ninaposema kweli, ninakuwa na dhamiri safi mbele za Yehova. Na wazazi wangu na rafiki zangu wanajua kwamba wanaweza kuniamini.” Victoria, msichana mwenye umri wa miaka 23, anasema hivi: “Unaposema kweli na kutetea mambo unayoamini, huenda ukadhihakiwa. Lakini unapofanya hivyo, sikuzote unanufaika kwelikweli: Unapata ujasiri, unamkaribia Yehova zaidi, na unaheshimiwa na wale wanaokupenda.” Kwa hakika, tunapata faida kubwa “[tunapojifunga] kiunoni mshipi wa ile kweli,” nyakati zote.

Mshipi wa ile kweli (Tazama fungu la 3 hadi 5)

“BAMBA LA KIFUANI LA UADILIFU”

6, 7. Kwa nini uadilifu unalinganishwa na bamba la kifuani?

6 Aina moja ya bamba la kifuani lililovaliwa na mwanajeshi Mroma wa karne ya kwanza lilikuwa na vipande vyembamba vya chuma vilivyolaliana ambavyo vilipangwa kwa urefu kutoka kushoto kwenda kulia. Vipande hivyo vilikunjwa ili vitoshane na ukubwa wa kifua chake na vilifungwa kwa kamba za ngozi zilizoshikiliwa na kulabu ndogo na vishikizo vya chuma. Pia, mabega ya mwanajeshi huyo yalifunikwa kwa vipande vyembamba vya chuma vilivyofungwa kwa kamba za ngozi. Bamba la kifuani lilimzuia kwa kiasi fulani asiweze kusonga kwa uhuru, naye alipaswa kulichunguza kwa ukawaida ili kuhakikisha kwamba vipande vyote vya chuma vimefungwa vizuri. Hata hivyo, bamba hilo lilimlinda ili moyo na viungo vingine muhimu visichomwe na ncha ya upanga au mkuki.

7 Huo ni ulinganisho unaofaa kwelikweli unaoonyesha jinsi viwango vya uadilifu vya Yehova vinavyolinda moyo wetu wa mfano! (Met. 4:23) Kama tu ambavyo mwanajeshi hangevua bamba lake la kifuani la chuma na kuvaa bamba lingine lililotengenezwa kwa madini yenye thamani ya chini, sisi pia hatungependa kamwe kuacha viwango vya Yehova kuhusu mambo yanayofaa na kufuata viwango vyetu wenyewe. Uwezo wetu wa kujiamulia yaliyo sawa na yasiyo sawa umepungukiwa sana hivi kwamba hatuwezi kuutegemea utupatie ulinzi tunaohitaji. (Met. 3:5, 6) Badala yake, tunahakikisha kwa ukawaida kwamba ‘vipande vya chuma’ ambavyo Yehova ametupatia vimefungwa vizuri ili kulinda moyo wetu.

8. Kwa nini kushikamana na viwango vya Yehova kuna faida kubwa?

8 Je, nyakati nyingine wewe huhisi kwamba viwango vya uadilifu vya Yehova vinakulemea au vinakunyima uhuru? Daniel, mwenye umri wa miaka 21 anasema hivi: “Walimu na wanafunzi wenzangu walinicheka kwa sababu ninaishi kulingana na viwango vya Biblia. Kwa kipindi fulani, nilipoteza ujasiri na kushuka moyo.” Ni nini kilichomsaidia kurudia hali nzuri? Anasema, “Hatimaye, nilijionea manufaa ya kuishi kulingana na viwango vya Yehova. Baadhi ya wale niliowaita marafiki wangu walianza kutumia dawa za kulevya na wengine wakaacha shule. Nilisikitika kuona jinsi maisha yao yalivyobadilika. Kwa kweli Yehova anatulinda sana.” Madison, msichana mwenye umri wa miaka 15, anasema hivi: “Ni changamoto kubwa sana kwangu kushikamana na viwango vya Yehova na kuepuka kushawishiwa kufanya mambo ambayo vijana wenzangu wanaona kuwa sawa au yenye kufurahisha.” Anakabilianaje na hali hiyo? “Mimi hujikumbusha kwamba ninalibeba jina la Yehova na kwamba vishawishi ni njia ya Shetani ya kunishambulia. Ninaposhinda kishawishi fulani, ninajihisi vizuri sana.”

Bamba la kifuani la uadilifu (Tazama fungu la 6 hadi 8)

“MKIWA MMEVAA VIATU MIGUUNI TAYARI KUTANGAZA HABARI NJEMA YA AMANI”

9-11. (a) Wakristo huvaa viatu gani vya mfano? (b) Ni nini kinachoweza kutusaidia kutangaza habari njema bila wasiwasi?

9 Soma Waefeso 6:15. Mwanajeshi Mroma ambaye hakuwa amevaa viatu hakuwa tayari kwenda vitani. Viatu vyake vilitengenezwa kwa safu tatu za ngozi ambazo ziliunganishwa ili vimsaidie kutembea vizuri. Vilitengenezwa kwa njia ambayo vingedumu na havingemuumiza.

10 Viatu halisi vilivyovaliwa na wanajeshi Waroma viliwasaidia kwenda kupigana vitani, kinyume cha hilo viatu vya mfano ambavyo Wakristo huvaa huwasaidia kupeleka ujumbe wa amani. (Isa. 52:7; Rom. 10:15) Hata hivyo, ujasiri unahitajika ili tuhubiri fursa inapojitokeza. Bo, mwanamume kijana mwenye umri wa miaka 20 anasema hivi: “Niliogopa kuwahubiria wanafunzi wenzangu. Niliaibika kuwahubiria. Ninapokumbuka wakati huo, sioni sababu iliyonifanya niaibike. Sasa ninafurahia kuwahubiria vijana wenzangu.”

11 Vijana wengi wametambua kwamba inakuwa rahisi zaidi kwao kutangaza habari njema ikiwa wamejitayarisha vizuri. Unaweza kujitayarisha jinsi gani? Julia, msichana mwenye umri wa miaka 16 anasema, “Mimi huweka machapisho ndani ya mkoba wangu wa shule, nami husikiliza wanafunzi wenzangu wanapoeleza maoni yao na mambo wanayoamini. Kwa kufanya hivyo, ninaweza kujua jinsi ya kuwasaidia. Wakati ambapo nimejitayarisha, ninaweza kuzungumza nao kuhusu mambo hususa ambayo yatawasaidia.” Makenzie, msichana mwenye umri wa miaka 23 anasema hivi: “Ukitenda kwa fadhili na kuwa msikilizaji mzuri, utajua matatizo ambayo vijana wenzako wanapitia. Mimi huhakikisha kwamba nimesoma machapisho yote yaliyoandaliwa kwa ajili ya vijana. Kufanya hivyo huniwezesha kuwasomea vijana wenzangu mstari fulani wa Biblia au kuwaelekeza kwenye habari fulani iliyo kwenye Tovuti ya jw.org ambayo itawasaidia.” Kama maelezo hayo yanavyoonyesha, kadiri unavyojitayarisha vizuri kuhubiri ndivyo viatu vyako vya mfano vitakavyokutoshea vizuri.

Viatu vikiwa tayari miguuni (Tazama fungu la 9 hadi 11)

“NGAO KUBWA YA IMANI”

12, 13. Taja baadhi ya ‘mishale inayowaka moto’ ya Shetani.

12 Soma Waefeso 6:16. “Ngao kubwa” iliyobebwa na mwanajeshi Mroma ilikuwa na umbo la mstatili, nayo ilimfunika kuanzia kwenye mabega mpaka kwenye magoti. Ilimkinga asifikiwe na silaha au mishale iliyorushwa.

13 Baadhi ya ‘mishale inayowaka moto’ ambayo huenda Shetani akakurushia ni uwongo kumhusu Yehova kwamba hakujali na kwamba hawezi kukupenda. Ida, msichana mwenye umri wa miaka 19, anapambana sana na hisia za kujiona hafai. Anasema, “Mara kwa mara mimi huhisi kwamba Yehova yuko mbali nami na hataki kuwa Rafiki yangu.” Anakabilianaje na shambulizi hilo la Shetani? Ida anasema, “Mikutano huimarisha sana imani yangu. Nilizoea tu kunyamaza bila kutoa maelezo yoyote, nikifikiri kwamba hakuna aliyetaka kusikia maelezo yangu. Hata hivyo, sasa mimi hujitayarisha kwa ajili ya mikutano na kutoa maelezo angalau mara mbili au tatu. Si rahisi lakini ninajihisi vizuri zaidi ninapofanya hivyo. Na ndugu na dada hunitia moyo sana. Sikuzote mimi hutoka mikutanoni nikihisi kwamba Yehova ananipenda.”

14. Kisa cha Ida kinakazia ukweli gani muhimu?

14 Kisa cha Ida kinakazia ukweli huu muhimu: Ngao halisi ambayo mwanajeshi alipewa ilikuwa na ukubwa usioweza kubadilika, lakini ukubwa wa ngao yetu ya imani unaweza kuongezeka au kupungua. Uamuzi ni wetu. (Mt. 14:31; 2 The. 1:3) Hivyo, ni muhimu sana tujenge imani yetu!

Ngao kubwa ya imani (Tazama fungu la 12 hadi 14)

“KOFIA YA CHUMA YA WOKOVU”

15, 16. Tumaini letu ni kama kofia ya chuma katika njia gani?

15 Soma Waefeso 6:17. Kofia ya chuma ambayo mwanajeshi Mroma aliyetembea kwa miguu alivaa ilitengenezwa kwa njia ambayo ingemkinga asijeruhiwe na mashambulizi yaliyolenga kichwa, shingo, na uso wake. Baadhi ya kofia zilikuwa na kishikio ambacho mwanajeshi angetumia kuibeba mkononi.

16 Kama tu ambavyo kofia ya chuma ililinda ubongo wa mwanajeshi, “tumaini [letu] la wokovu” hulinda akili yetu, yaani, uwezo wetu wa kufikiri. (1 The. 5:8; Met. 3:21) Tumaini hutufanya tuendelee kukazia fikira ahadi za Mungu na kutusaidia tuwe na mtazamo unaofaa kuhusu matatizo. (Zab. 27:1, 14; Mdo. 24:15) Lakini ikiwa tunataka “kofia [yetu] ya chuma” itusaidie kikamili, ni lazima tuivae kichwani na si kuibeba mkononi.

17, 18. (a) Shetani anaweza kutushawishi jinsi gani tuvue kofia yetu? (b) Tunaweza kuonyeshaje kwamba hatujapumbazwa na uwongo wa Shetani?

17 Shetani anaweza kutushawishi jinsi gani tuvue kofia yetu? Fikiria jinsi alivyoshughulika na Yesu. Bila shaka, Shetani alijua kwamba Yesu alikuwa na tumaini la kuwa mtawala juu ya wanadamu. Hata hivyo, Yesu angehitaji kusubiri hadi wakati uliowekwa na Yehova. Na kabla ya wakati huo angeteseka na kufa. Hivyo, Shetani alimpa Yesu fursa ya kuona tumaini lake likitimia bila kusubiri kwa muda mrefu. Shetani alimwambia Yesu kwamba ikiwa angefanya tendo moja la ibada mbele yake, Yesu angepata mamlaka yote, tena papo hapo. (Luka 4:5-7) Vivyo hivyo, Shetani anajua kwamba Yehova ameahidi kutupatia baraka za kimwili katika ulimwengu mpya. Lakini tunahitaji kusubiri, na huenda kwa sasa tukalazimika kukabili hali ngumu. Shetani anatushawishi kwa kutupatia fursa za kufurahia maisha hayo mazuri sasa. Anataka tufuatie vitu vya kimwili, tujipatie vyote tunavyotaka, tena sasa hivi. Shetani anatuhimiza tutangulize mambo yetu na Ufalme uwe sehemu ya pili maishani.—Mt. 6:31-33.

18 Kama ilivyo kwa vijana wengi Wakristo, msichana anayeitwa Kiana mwenye umri wa miaka 20, hajapumbazwa na uwongo huo. Anasema hivi: “Ninajua kwamba tumaini pekee la utatuzi wa matatizo yetu yote ni Ufalme wa Mungu.” Tumaini hilo thabiti linachocheaje mawazo na matendo yake sasa? Anaendelea kusema, “Tumaini la kuishi katika Paradiso hunisaidia kuweka malengo ya kimwili mahali panapofaa maishani. Situmii vipawa nilivyo navyo kujitafutia pesa wala sijikakamui ili nipandishwe daraja kazini. Badala yake, ninatumia wakati na nguvu zangu kufuatia malengo ya kiroho.”

Kofia ya chuma ya wokovu (Tazama fungu la 15 hadi 18)

NENO LA MUNGU, “UPANGA WA ROHO”

19, 20. Tunaweza kuboreshaje ustadi wetu wa kutumia Neno la Mungu?

19 Paulo alipoandika barua yake, upanga uliotumiwa na wanajeshi Waroma waliotembea kwa miguu ulikuwa na urefu wa sentimita 50 hivi na ulitumiwa katika mapambano ya ana kwa ana. Sababu moja iliyofanya wanajeshi Waroma wawe stadi vitani ni kwamba walifanya mazoezi kila siku kwa kutumia silaha zao.

20 Paulo analinganisha Neno la Mungu na upanga. Yehova ndiye aliyetupatia upanga huo. Hata hivyo, ni lazima tujifunze jinsi ya kuutumia kwa ustadi tunapotetea mambo tunayoamini au tunaporekebisha njia yetu ya kufikiri. (2 Kor. 10:4, 5; 2 Tim. 2:15) Unaweza kuboreshaje ustadi wako? Sebastian, kijana mwenye umri wa miaka 21, anasema hivi: “Nimekuwa nikiandika mstari mmoja kutoka katika kila sura ninayosoma katika usomaji wangu wa Biblia. Ninakusanya orodha ya maandiko ninayopenda zaidi. Kwa kufanya hivyo, ninahisi kwamba njia yangu ya kufikiri inazidi kupatana na njia ya Yehova ya kufikiri.” Daniel, aliyenukuliwa awali, anasema hivi: “Ninapofanya usomaji wangu wa Biblia, mimi huchagua mistari ambayo ninahisi kwamba itawasaidia watu ninaokutana nao katika huduma. Nimetambua kwamba watu huitikia vizuri wanapoona ukizungumzia habari za Biblia kwa shauku na unapofanya yote unayoweza kuwasaidia.”

Upanga wa roho (Tazama fungu la 19 na 20)

21. Kwa nini hakuna haja ya kumwogopa Shetani na roho waovu?

21 Kama maelezo ya vijana waliotajwa katika makala hii yanavyoonyesha, hakuna haja ya kumwogopa Shetani na roho waovu. Ni maadui wenye nguvu sana, lakini tunaweza kuwashinda. Na wanaweza kufa. Hivi karibuni wakati wa Utawala wa Miaka Elfu Moja wa Kristo, watawekwa katika hali itakayowazuia kabisa kutenda, na baada ya hapo wataangamizwa. (Ufu. 20:1-3, 7-10) Tunamjua adui yetu, tunajua mbinu zake, na tunajua nia yake. Kwa msaada wa Yehova tunaweza kusimama imara na kumpinga!