Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 22

Boresha Mazoea Yako ya Kujifunza!

Boresha Mazoea Yako ya Kujifunza!

“Mhakikishe mambo muhimu zaidi.”​—FLP. 1:10.

WIMBO 35 “Mhakikishe Mambo Muhimu Zaidi”

MUHTASARI *

1. Kwa nini huenda ikawa vigumu kwa baadhi ya ndugu na dada kujifunza?

SIKU hizi, jitihada nyingi inahitajika ili mtu ajiruzuku. Ndugu zetu wengi hufanya kazi kwa saa nyingi ili tu kuandalia familia zao mahitaji ya lazima. Wengine wengi hutumia saa kadhaa kila siku kusafiri kwenda na kurudi kutoka kazini. Wengi wao hujitegemeza kwa kufanya kazi ngumu za mikono. Mwishoni mwa siku, ndugu na dada hao wenye bidii huwa hoi kabisa! Na kwa sababu hiyo, inakuwa vigumu sana kwa wengi wao kujifunza.

2. Wewe hujifunza wakati gani?

2 Hata hivyo, ukweli wa mambo ni kwamba ni lazima tutafute wakati wa kujifunza—kujifunza kwa kina—Neno la Mungu na machapisho yetu ya Kikristo. Ili tuwe na uhusiano mzuri pamoja na Yehova na ili tupate uzima wa milele ni lazima tuwe na mazoea mazuri ya kujifunza! (1 Tim. 4:15) Baadhi ya ndugu na dada huamka mapema kila siku ili wajifunze wakati ambapo mazingira ni matulivu na wamepumzika vya kutosha. Wengine hutenga dakika chache mwishoni mwa siku wakati ambapo kuna utulivu ili kujilisha chakula cha kiroho na kutafakari.

3-4. Ni mabadiliko gani ambayo yamefanywa kuhusu kiwango cha habari tunazopokea, na kwa nini?

3 Bila shaka unakubali kwamba ni muhimu kutafuta wakati wa kujifunza. Lakini tunapaswa kujifunza nini? Huenda ukasema, ‘Kuna mambo mengi sana ya kusoma. Ninashindwa kusoma kila kitu.’ Baadhi ya akina ndugu hufaulu kusoma habari zote zinazoandaliwa na tengenezo, lakini ndugu zetu wengi wanapambana sana ili kupata wakati wa kufanya hivyo. Baraza Linaloongoza linatambua jambo hilo. Kwa sababu hiyo, hivi karibuni mwongozo ulitolewa wa kupunguza kiwango cha habari zinazochapishwa na zinazopatikana katika mfumo wa kielektroni.

4 Kwa mfano, hatuchapishi tena Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova, kwa kuwa masimulizi mengi yenye kutia moyo yanapatikana kwenye tovuti ya jw.org/sw na pia kwenye programu za kila mwezi za JW Broadcasting®. Sasa toleo la watu wote la gazeti la Mnara wa Mlinzi na Amkeni! linachapishwa mara tatu tu kwa mwaka. Mabadiliko hayo hayakufanywa ili tuwe na muda mwingi zaidi wa kufanya shughuli nyingine za kibinafsi. Yalifanywa ili tuwe na wakati wa kutosha wa kukazia fikira “mambo muhimu zaidi.” (Flp. 1:10) Acheni tuzungumzie jinsi unavyoweza kuamua mambo ya kutanguliza na jinsi unavyoweza kunufaika kikamili unapojifunza Biblia kibinafsi.

PANGA MAMBO YA KUTANGULIZA

5-6. Ni machapisho gani tunayopaswa kuhakikisha kwamba tunajifunza kwa makini?

5 Tunapaswa kutanguliza mambo gani? Kwa hakika tunapaswa kutenga wakati fulani kila siku kujifunza Neno la Mungu. Sasa, idadi ya sura za usomaji wa Biblia wa kila juma wa kutaniko zimepunguzwa ili tuwe na muda mwingi zaidi wa kutafakari habari tunazosoma na kufanya utafiti wa ziada. Hatupaswi kuwa na lengo la kukamilisha tu sura tulizopangiwa kusoma, bali tunapaswa pia kuwa na lengo la kuruhusu ujumbe wa Biblia uguse mioyo yetu na utusaidie kumkaribia zaidi Yehova.—Zab. 19:14.

6 Ni habari gani nyingine tunayopaswa kujifunza kwa makini? Bila shaka, tungependa kutayarisha Funzo la Mnara wa Mlinzi na Funzo la Biblia la Kutaniko na pia habari nyingine tunazojifunza katika mkutano wa katikati ya juma. Vilevile, tunapaswa kusoma kila toleo la Mnara wa Mlinzi na Amkeni!

7. Je, tunapaswa kuvunjika moyo ikiwa tunashindwa kusoma au kutazama habari zote zinazopatikana kwenye tovuti yetu na kwenye JW Broadcasting?

7 Huenda ukasema, ‘Sawa, lakini vipi kuhusu habari zote zinazopatikana kwenye tovuti yetu ya jw.org/sw, na video zote zinazoonyeshwa kwenye JW Broadcasting? Ni nyingi mno!’ Fikiria mfano huu: Ndani ya mkahawa kuna meza yenye vyakula vingi vya aina mbalimbali. Wateja wanaokuja katika mkahawa huo hawawezi kula kila kitu kilichoandaliwa. Hivyo, wanachagua kula vyakula vichache tu. Vivyo hivyo, usivunjike moyo ikiwa huwezi kusoma habari zote zinazopatikana kwa njia ya kielektroni. Jitahidi kadiri uwezavyo kutazama au kusoma kiasi cha habari unachoweza. Sasa, acheni tuzungumzie maana ya kujifunza na jinsi ya kunufaika kikamili tunapojifunza.

KUJIFUNZA NI KAZI!

8. Unaweza kufuata hatua zipi unapotayarisha Funzo la Mnara wa Mlinzi, nawe utanufaikaje kwa kufanya hivyo?

8 Kujifunza ni kusoma ukiwa umekaza fikira bila kukengeuka, na ukiwa na kusudi fulani hususa. Kujifunza si kupitia tu kijuujuu habari zilizoteuliwa au kupigia mistari majibu. Kwa mfano, unapotayarisha Funzo la Mnara wa Mlinzi, kwanza soma muhtasari ulio mwanzoni mwa makala hiyo. Kisha, soma na ufikirie kuhusu kichwa cha makala hiyo, vichwa vidogo na maswali ya pitio. Halafu, soma makala hiyo polepole na kwa makini. Kazia fikira sentensi inayobeba wazo kuu la kila fungu, ambayo mara nyingi huwa sentensi ya kwanza katika fungu hilo. Kwa kawaida, sentensi hiyo itakusaidia kujua ni hoja gani itakayofafanuliwa na fungu hilo. Unapoendelea kusoma makala hiyo, fikiria jinsi kila fungu linavyounga mkono kichwa kidogo na linavyohusiana na habari kuu ya makala unayosoma. Zingatia maneno yoyote usiyoyafahamu vizuri na habari zozote ambazo ungependa kuzifanyia utafiti ili uzielewe vizuri zaidi.

9. (a) Kwa nini tunapaswa kuyafikiria kwa kina maandiko tunapotayarisha Funzo la Mnara wa Mlinzi, na tunaweza kufanya hivyo jinsi gani? (b) Kama inavyotajwa kwenye Yoshua 1:8, zaidi ya kusoma maandiko ni jambo gani lingine tunalopaswa kufanya?

9 Funzo la Mnara wa Mlinzi hutusaidia kujifunza Biblia. Kwa hiyo, yafikirie kwa kina maandiko, na hasa maandiko yatakayosomwa wakati kutaniko litakapokuwa likichunguza habari hiyo. Zingatia kwa makini jinsi maneno makuu au vifungu vya maneno katika maandiko vinavyounga mkono hoja inayozungumziwa katika fungu. Zaidi ya hilo, tumia wakati kutafakari maandiko unayosoma, na ufikirie jinsi unavyoweza kuyatumia kibinafsi maishani mwako.—Soma Yoshua 1:8.

Wazazi, wafundisheni watoto wenu jinsi ya kujifunza (Tazama fungu la 10) *

10. Kulingana na Waebrania 5:14, kwa nini wazazi wanapaswa kutumia wakati wa ibada ya familia kuwafundisha watoto wao jinsi ya kujifunza na kufanya utafiti?

10 Inaeleweka kwamba wazazi wangependa watoto wao wafurahie Ibada ya Familia ya kila juma. Hata hivyo, ingawa sikuzote wazazi wanapaswa kuwa na jambo fulani hususa akilini watakalochunguza katika ibada ya familia, hawahitaji kuhisi kwamba ni lazima wapange miradi fulani ya pekee au yenye kusisimua kila juma. Ingawa wakati wa Ibada ya Familia unaweza kutumiwa kutazama programu ya kila mwezi ya JW Broadcasting, au wakati mwingine kufanya miradi fulani ya pekee, kama vile kutengeneza mfano wa safina ya Noa, ni muhimu pia watoto wafundishwe jinsi ya kujifunza. Kwa mfano, wanahitaji kujifunza jinsi ya kutayarisha mikutano, au kufanya utafiti kuhusu jambo fulani ambalo limezuka shuleni. (Soma Waebrania 5:14.) Iwapo watatumia muda fulani kujifunza habari mbalimbali wakiwa nyumbani, itakuwa rahisi zaidi kwao kukazia fikira habari zinazozungumziwa mikutanoni na kwenye makusanyiko ya mzunguko na ya eneo, ambazo huenda zisiambatane na video. Bila shaka, urefu wa kila kipindi cha kujifunza utategemea umri na utu wa kila mtoto.

11. Kwa nini ni muhimu kuwafundisha wanafunzi wetu wa Biblia jinsi ya kujifunza kwa kina wakiwa peke yao?

11 Pia, watu tunaojifunza nao Biblia wanahitaji kujua jinsi ya kujifunza. Wanapoanza kujifunza Biblia, sisi hufurahi tunapoona wamepigia mistari majibu kwa ajili ya funzo au mikutano ya kutaniko. Lakini pia tunahitaji kuwafundisha wanafunzi wetu wa Biblia jinsi ya kufanya utafiti na jinsi ya kujifunza kwa kina wakiwa peke yao. Kwa njia hiyo, wanafunzi wetu wa Biblia watakapopatwa na matatizo, hawatawakimbilia mara moja watu wengine kutanikoni wakiomba ushauri, badala yake watajua jinsi watakavyopata mashauri yatakayowasaidia kwa kufanya utafiti kwenye machapisho yetu.

JIFUNZE UKIWA NA LENGO HUSUSA

12. Ni malengo gani tunayoweza kuwa nayo akilini tunapojifunza?

12 Ikiwa wewe si mpenzi wa kusoma, huenda ukahisi kwamba hutawahi kufurahia kujifunza. Lakini unaweza. Anza kwa vipindi vifupi vya kujifunza, kisha hatua kwa hatua ongeza muda unaotumia kujifunza. Uwe na lengo hususa akilini. Bila shaka, lengo letu kuu linapaswa kuwa kumkaribia Yehova zaidi na zaidi. Lengo lingine tunaloweza kutimiza ni kufanya utafiti ili kujibu swali ambalo mtu fulani alituuliza au kuhusu tatizo tunalokabili.

13. (a) Eleza hatua ambazo kijana anaweza kuchukua ili kutetea imani yake akiwa shuleni. (b) Unaweza kutumiaje shauri lililo kwenye Wakolosai 4:6?

13 Kwa mfano, je, wewe ni kijana aliye shuleni? Huenda wanadarasa wenzako wote wanaamini nadharia ya mageuzi. Unatamani kutetea mambo ambayo Biblia inafundisha, lakini huenda unahisi kwamba huwezi kufanya hivyo. Basi unahitaji kuweka mkakati wa kujifunza kuhusu jambo hilo! Kuna mambo mawili unayoweza kutimiza: (1) kuimarisha usadikisho wako mwenyewe kwamba Mungu aliumba vitu vyote na (2) kuboresha uwezo wako wa kuitetea kweli. (Rom. 1:20; 1 Pet. 3:15) Kwanza, unaweza kujiuliza hivi; ‘Wanadarasa wenzangu wanatumia hoja zipi kuunga mkono nadharia ya mageuzi?’ Kisha, fanya utafiti kuhusu jambo hilo ukitumia machapisho yetu. Huenda ukagundua kwamba kutetea imani yako si jambo gumu kama unavyofikiri. Watu wengi wanaamini mageuzi kwa sababu tu mtu fulani wanayemheshimu aliwaambia kuwa nadharia ya mageuzi ni ya kweli. Ukifanya utafiti na kupata angalau hoja moja au mbili unazoweza kushiriki pamoja na wengine, huenda ukamjibu kwa njia yenye kuridhisha mtu anayetamani kujua ukweli.—Soma Wakolosai 4:6.

CHOCHEA HAMU YAKO YA KUJIFUNZA

14-16. (a) Unaweza kufanya nini ili uelewe vizuri kitabu fulani cha Biblia usichokifahamu vizuri? (b) Ukitumia maandiko yaliyotajwa, eleza jinsi unavyoweza kupata picha kamili ya kitabu cha Amosi. (Tazama pia sanduku, “ Ifanye Biblia Iwe Hai!”)

14 Tuseme kwamba katika mkutano unaofuata wa kutaniko, tutachunguza kitabu cha mmoja wa wale wanaojulikana kuwa manabii wadogo, na huenda ni nabii ambaye humfahamu vizuri. Hatua ya kwanza unayoweza kuchukua ni kuchochea hamu yako ya kujua kile ambacho nabii huyo aliandika. Unaweza kufanyaje hivyo?

15 Kwanza, jiulize hivi: ‘Ninajua nini kuhusu mwandikaji wa kitabu hiki? Alikuwa nani, aliishi wapi, na alifanya kazi gani?’ Malezi ya mwandikaji huyo yanaweza pia kutusaidia kujua kwa nini alitumia maneno au mifano fulani. Unaposoma Biblia, tafuta vifungu vya maneno vinavyofunua utu wa mwandikaji huyo.

16 Vilevile, kufahamu kipindi cha wakati ambapo kitabu hicho kiliandikwa ni jambo lingine litakalokusaidia. Njia rahisi ya kufanya hivyo ni kutazama “Orodha ya Vitabu vya Biblia” iliyo upande wa nyuma wa Biblia Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Pia, unaweza kuchunguza chati ya manabii na wafalme iliyo kwenye Nyongeza A6. Ikiwa kitabu cha Biblia unachojifunza ni cha kinabii, lingekuwa jambo linalofaa kuchunguza jinsi maisha na hali za watu zilivyokuwa kilipoandikwa. Nabii huyo alitaka kurekebisha mitazamo au mazoea ya aina gani? Ni watu gani wengine walioishi kipindi kimoja cha wakati pamoja naye? Ili upate picha kamili, huenda ukahitaji kuchunguza vitabu vingine vya Biblia. Kwa mfano, utanufaika kwa kuchunguza mistari fulani ya kitabu cha 2 Wafalme na 2 Mambo ya Nyakati, inayopatikana kwenye marejezo ya pambizoni ya andiko la Amosi 1:1, ili uelewe vizuri zaidi mambo yaliyokuwa yakitendeka nabii Amosi alipokuwa hai. Unaweza pia kuchunguza kitabu cha Hosea, ambaye huenda aliishi kipindi kimoja na Amosi. Habari hizo zote zinaweza kukusaidia kuelewa jinsi maisha yalivyokuwa katika kipindi ambacho Amosi aliishi.—2 Fal. 14:25-28; 2 Nya. 26:1-15; Hos. 1:1-11; Amo. 1:1.

ZINGATIA MAMBO MADOGO-MADOGO

17-18. Ukitumia mifano iliyo katika mafungu au mfano mwingine ulio nao, onyesha jinsi kukazia fikira mambo yanayoonekana kuwa madogo kunavyoweza kufanya tufurahie zaidi kujifunza Biblia kibinafsi.

17 Ni vizuri kusoma Biblia ukiwa na hamu kubwa ya kujifunza mambo mapya. Kwa mfano, tuseme kwamba unasoma sura ya 12 ya kitabu cha unabii wa Zekaria, ambayo inatabiri kuhusu kifo cha Masihi. (Zek. 12:10) Unapofika kwenye mstari wa 12, unasoma kwamba “ukoo wa nyumba ya Nathani” ungeomboleza kwa uchungu kifo cha Masihi. Badala ya kupita wazo hilo kijuujuu tu, unatua na kujiuliza: ‘Kuna uhusiano gani kati ya nyumba ya Nathani na Masihi? Je, kuna njia nyingine ya kupata habari zaidi?’ Sasa unaamua kufanya “upelelezi” kidogo. Rejezo la pambizoni linakupeleka kwenye 2 Samweli 5:13, 14, ambapo unagundua kwamba Nathani alikuwa mwana wa Mfalme Daudi. Rejezo la pili la pambizoni, yaani, Luka 3:23, 31, linafunua kwamba Yesu alikuwa mzao wa moja kwa moja wa Nathani kupitia Maria. (Tazama Mnara wa Mlinzi, Agosti 2017, uku. 32 fu. 4.) Ghafla unasisimka! Ulijua kuwa ilitabiriwa kwamba Yesu angekuwa mzao wa Daudi. (Mt. 22:42) Lakini Daudi alikuwa na zaidi ya wana 20. Je, si jambo linalosisimua kwamba Zekaria anataja kihususa kuwa nyumba ya Nathani hasa ilikuwa na sababu ya kuomboleza kifo cha Yesu?

18 Fikiria mfano mwingine. Katika sura ya kwanza ya kitabu cha Luka, tunasoma kwamba malaika Gabrieli alimtembelea Maria na kumwambia hivi kuhusu mwana ambaye angezaa: “Huyo atakuwa mkuu naye ataitwa Mwana wa Aliye Juu Zaidi, na Yehova Mungu atampa kiti cha ufalme cha Daudi baba yake naye atatawala akiwa Mfalme juu ya nyumba ya Yakobo milele.” (Luka 1:32, 33) Huenda tukakazia zaidi sehemu ya kwanza ya ujumbe wa Gabrieli kwamba Yesu ataitwa “Mwana wa Aliye Juu Zaidi.” Lakini Gabrieli alitabiri pia kwamba Yesu “atatawala akiwa Mfalme.” Hivyo tunajiuliza, Maria aliyaelewaje maneno ya Gabrieli? Je, alielewa kwamba maneno ya Gabrieli yalimaanisha kwamba Yesu angekuwa mtawala badala ya Mfalme Herode—au angechukua mahali pa mmoja wa warithi wa Herode akiwa mtawala wa Israeli? Ikiwa Yesu angekuwa mfalme, Maria angekuwa mama malkia, na familia yake ingeishi katika makao ya mfalme. Hata hivyo, hatusomi popote kamwe kwamba Maria alimtajia Gabrieli jambo kama hilo au kwamba aliomba kuwa na cheo cha pekee katika Ufalme, kama walivyofanya wanafunzi wawili wa Yesu. (Mt. 20:20-23) Jambo hilo dogo linatusadikisha kwamba Maria alikuwa mwanamke mnyenyekevu sana!

19-20. Kama inavyoelezwa kwenye Yakobo 1:22-25 na 4:8, tunapaswa kuwa na malengo gani tunapojifunza?

19 Acheni tukumbuke kwamba lengo letu kuu la kujifunza Neno la Mungu na machapisho yetu ya Kikristo ni kumkaribia Yehova zaidi. Pia, tungependa kuona wazi zaidi ‘jinsi tulivyo’ na ni mabadiliko gani tunayohitaji kufanya ili kumpendeza Mungu. (Soma Yakobo 1:22-25; 4:8.) Hivyo, kila mara tunapojifunza tunapaswa kuanza kwa kumwomba Yehova atupatie roho yake. Tunapaswa kumsihi atusaidie kunufaika kikamili na habari tutakayojifunza na atusaidie kujiona kama anavyotuona.

20 Acheni sisi sote tuwe kama mtu wa Mungu anayefafanuliwa hivi na mtunga zaburi: “Anapendezwa na sheria ya Yehova, naye huisoma sheria Yake kwa sauti ya chini mchana na usiku. . . . Kila jambo analofanya litafanikiwa.”—Zab. 1:2, 3.

WIMBO 88 Nijulishe Njia Zako

^ fu. 5 Akichochewa na ukarimu, Yehova anatupatia kwa wingi habari nyingi za kutazama, kusoma, na kujifunza. Makala hii itakusaidia ujue jinsi unavyoweza kuamua habari utakazojifunza, na inatoa mapendekezo mazuri yatakayokusaidia unufaike kikamili unapojifunza.

^ fu. 61 MAELEZO YA PICHA: Wazazi wakiwaonyesha watoto wao jinsi ya kutayarisha funzo la kila juma la Mnara wa Mlinzi.

^ fu. 63 MAELEZO YA PICHA: Ndugu akifanya utafiti kuhusu mwandikaji wa Biblia, Amosi. Picha zilizo nyuma yake zinaonyesha mambo ambayo ndugu huyo anawazia anaposoma masimulizi ya Biblia na kuyatafakari.