Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 21

Usidanganywe na “Hekima ya Ulimwengu Huu”

Usidanganywe na “Hekima ya Ulimwengu Huu”

“Hekima ya ulimwengu huu ni upumbavu kwa Mungu.”​—1 KOR. 3:19.

WIMBO 98 Maandiko​—Yaliongozwa na Roho ya Mungu

MUHTASARI *

1. Neno la Mungu hutupatia nini?

TUNAWEZA kushinda changamoto yoyote kwa sababu Yehova ni Mfundishaji wetu Mkuu. (Isa. 30:20, 21) Neno lake hutupatia kila kitu tunachohitaji ili tuwe na “uwezo kamili” na “vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.” (2 Tim. 3:17) Tunapoishi kulingana na mafundisho ya Biblia tunakuwa na hekima kuliko watu wanaoendeleza “hekima ya ulimwengu huu.”—1 Kor. 3:19; Zab. 119:97-100.

2. Tutachunguza nini katika makala hii?

2 Kama tutakavyoona, kwa kawaida hekima ya ulimwengu huvutia tamaa zetu za mwili. Hivyo, inaweza kuwa vigumu kwetu kuepuka kufikiri na kutenda kama watu wa ulimwengu huu. Hiyo ndiyo sababu Biblia husema hivi: “Jihadharini ili mtu yeyote asiwachukue mateka kupitia falsafa na udanganyifu mtupu kulingana na mapokeo ya wanadamu.” (Kol. 2:8) Katika makala hii, tutachunguza jinsi mambo mawili ya udanganyifu mtupu au uwongo yalivyoenea na kukubalika. Tunapozungumzia kila moja ya mambo hayo, tutaona kwa nini hekima ya ulimwengu huu ni upumbavu na jinsi hekima ya Neno la Mungu ilivyo bora kuliko kitu chochote ambacho ulimwengu hutoa.

KUBADILIKA KWA MAONI YA WATU KUHUSU NGONO

3-4. Kulikuwa na mabadiliko gani kuhusu ngono nchini Marekani mwanzoni mwa karne ya 20?

3 Nchini Marekani, maoni ya watu wengi kuhusu ngono yalianza kubadilika sana mwanzoni mwa karne ya 20. Awali, watu wengi waliamini kwamba ngono ilipaswa kufanywa na wale tu ambao wamefunga ndoa na kwamba haikupaswa kuzungumziwa hadharani. Lakini viwango hivyo viliporomoka, na maoni yasiyofaa kuhusu ngono yakaenea na kukubalika.

4 Miaka 30 ya kwanza ya karne ya 20 ilijulikana kuwa Miaka Iliyosheheni Anasa, nayo ilileta mabadiliko mengi na makubwa katika jamii. Mtafiti mmoja anasema kwamba “maudhui ya sinema, michezo ya kuigiza, nyimbo, vitabu vya riwaya, na matangazo ya biashara yalijaa habari za ngono ili kukidhi soko la burudani.” Katika kipindi hicho, watu wengi walianza kupenda dansi zilizosisimua kingono na pia mitindo ya mavazi iliyofunua uchi. Kama Biblia ilivyotabiri kuhusu siku za mwisho, idadi kubwa ya watu wangekuwa wenye ‘kupenda raha.’—2 Tim. 3:4.

Watu wa Yehova hawakushawishiwa na viwango vya maadili vilivyopotoka vya ulimwengu huu (Tazama fungu la 5) *

5. Maoni ya watu kuhusu maadili yamebadilikaje tangu miaka ya 1960?

5 Katika miaka ya 1960, mambo kama vile kuishi pamoja bila kufunga ndoa, ngono kati ya watu wa jinsia moja, na talaka za ovyoovyo yalianza kuwa mambo ya kawaida. Burudani nyingi zilianza kuonyesha ngono waziwazi. Katika miaka ya karibuni, matokeo mabaya ya mwenendo mchafu kingono yanaonekana waziwazi. Mwandishi mmoja aliandika kwamba kisababishi cha kuvunjika kwa familia, familia za mzazi mmoja, maumivu ya kihisia, uraibu wa ponografia, na matatizo mengine kama hayo yanahusiana na “kuzorota kwa viwango vya maadili ambavyo sasa vimebadili maoni ya watu kuhusu ngono.” Kuenea kwa magonjwa yanayoambukizwa kingono, kama vile UKIMWI, ni mojawapo ya mambo yanayoonyesha kwamba hekima ya ulimwengu huu ni upumbavu.—2 Pet. 2:19.

6. Maoni ya ulimwengu kuhusu ngono hutimizaje kusudi la Shetani?

6 Maoni ya ulimwengu kuhusu ngono hutimiza kusudi la Shetani. Hapana shaka kwamba anafurahia kuwaona watu wakitumia vibaya zawadi ya ngono ambayo Mungu ametupatia, na kuvunjia heshima zawadi ya Mungu ya ndoa. (Efe. 2:2) Uasherati hauharibu tu zawadi maridadi ya kupata watoto ambayo Yehova ametupatia, bali pia unaweza kuwazuia wale wanaojihusisha nao wakose uzima wa milele.—1 Kor. 6:9, 10.

MAONI YA BIBLIA KUHUSU NGONO

7-8. Mambo ambayo Biblia inasema kuhusu ngono yanaonyeshaje kwamba Yehova anawaheshimu wanadamu?

7 Watu wanaoishi kulingana na hekima ya ulimwengu huu hudhihaki viwango vya Biblia kuhusu maadili, wakidai kwamba haiwezekani kuvifuata. Huenda watu kama hao wakauliza, ‘Kwa nini Mungu alituumba tukiwa na tamaa ya kufanya ngono na kisha kutuambia tusizitosheleze?’ Wanauliza swali hilo kwa sababu wanafikiri kimakosa kwamba mwanadamu anapaswa kutosheleza kila tamaa aliyo nayo. Lakini Biblia inasema jambo tofauti. Inafundisha kwamba Yehova amewaheshimu wanadamu kwa kuwapa uwezo wa kudhibiti tamaa zisizofaa. (Kol. 3:5) Isitoshe, Yehova ametupatia zawadi ya ndoa, na kupitia mpango huo tamaa za ngono zinaweza kutoshelezwa kwa njia yenye kuheshimika. (1 Kor. 7:8, 9) Kupitia mpango huo, mume na mke wanaweza kufurahia ngono bila kujutia chochote au kuwa na wasiwasi ambao mara nyingi watu wanaofanya uasherati huwa nao.

8 Tofauti na hekima ya ulimwengu huu, Biblia hutusaidia kujua maoni tunayopaswa kuwa nayo kuhusu ngono. Biblia inasema kwamba wenzi wa ndoa wanaweza kufurahia kufanya ngono. (Met. 5:18, 19) Hata hivyo, Biblia inasema hivi: “Kila mmoja wenu anapaswa kujua jinsi ya kuudhibiti mwili wake mwenyewe katika utakatifu na heshima, si kwa hamu yenye pupa ya ngono kama ya watu wa mataifa wasiomjua Mungu.”—1 The. 4:4, 5.

9. (a) Mapema katika karne ya 20, watu wa Yehova walitiwa moyo jinsi gani wafuate hekima iliyo bora zaidi ya Neno la Mungu? (b) Ni shauri gani lenye hekima linalopatikana kwenye 1 Yohana 2:15, 16? (c) Andiko la Waroma 1:24-27 linaorodhesha mazoea gani machafu tunayopaswa kuepuka?

9 Mapema katika karne ya 20, watu wa Yehova hawakushawishiwa na udanganyifu mtupu wa watu ambao walikuwa “wamepotoka kabisa kimaadili.” (Efe. 4:19) Walijitahidi kushikamana kabisa na viwango vya Yehova. Gazeti la Mnara wa Mlinzi la Mei 15, 1926, lilisema kwamba “mwanamume au mwanamke anapaswa kuwa safi kiadili katika mawazo na matendo, hasa inapohusu jinsi anavyoshughulika na watu wa jinsia tofauti.” Licha ya hali za ulimwengu zilizowazunguka wakati huo, watu wa Yehova waliishi kulingana na hekima iliyo bora zaidi ya Neno la Mungu. (Soma 1 Yohana 2:15, 16.) Tunashukuru sana kuwa na Neno la Mungu! Pia, tunamshukuru sana Yehova kwa kutuandalia chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa kinachotusaidia tusidanganywe na hekima ya ulimwengu huu kuhusu ngono. *Soma Waroma 1:24-27.

KUBADILIKA KWA MAONI YA WATU KUHUSU KUJIPENDA WENYEWE

10-11. Ni jambo gani ambalo Biblia ilionya kwamba lingetokea katika siku za mwisho?

10 Biblia ilionya kwamba katika siku za mwisho, watu wangekuwa wenye “kujipenda wenyewe.” (2 Tim. 3:1, 2) Haishangazi kwamba ulimwengu umechochea roho ya kujikweza. Kitabu kimoja cha marejeo kinasema kwamba katika miaka ya 1970, “vitabu vya kuwapa watu mashauri vilichapishwa kwa wingi.” Baadhi ya vitabu hivyo “viliwahimiza wasomaji wajijue na wajikubali na wafurahie jinsi walivyo.” Kwa mfano, fikiria maneno haya yaliyo katika mojawapo ya vitabu hivyo: “Jipende wewe mwenyewe, kwa maana wewe ndiye mtu mwenye sura nzuri zaidi, mwenye kusisimua zaidi, na anayestahili zaidi kupendwa kuliko mtu mwingine yeyote ambaye amewahi kuishi.” Kitabu hicho kinawashauri watu “wajielekezee aina fulani ya ibada ambapo mtu hujiamulia jinsi atakavyojiendesha kwa kutegemea dhamiri yake na sheria za utamaduni wake zinazomfaa yeye mwenyewe.”

11 Je, umewahi kusikia wazo kama hilo? Shetani alimtia moyo Hawa afanye jambo linalofanana na hilo. Alimwambia kwamba angeweza kuwa ‘kama Mungu, akijua mema na mabaya.’ (Mwa. 3:5) Leo, watu wengi hujikweza sana hivi kwamba kulingana na maoni yao, hakuna yeyote, hata Mungu mwenyewe, anayestahili kuwaamulia jambo wanalopaswa kufanya au wasilopaswa kufanya. Mfano wa mtazamo wa aina hiyo unaonekana wazi hasa kupitia jinsi watu wanavyoiona ndoa.

Mkristo hutanguliza mahitaji ya wengine kwanza​—hasa ya mwenzi wake wa ndoa (Tazama fungu la 12) *

12. Ulimwengu huendeleza maoni gani kuhusu ndoa?

12 Biblia inawaagiza waume na wake waheshimiane na waheshimu nadhiri zao za ndoa. Inawatia moyo wenzi wa ndoa waazimie kabisa kushikamana na kifungo chao cha ndoa inaposema: “Mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake, nao watakuwa mwili mmoja.” (Mwa. 2:24) Kinyume cha hilo, watu walioathiriwa na hekima ya ulimwengu huu huendeleza maoni tofauti, wakisema kwamba kila mtu aliyefunga ndoa anapaswa kukazia fikira mahitaji yake binafsi. Kitabu kimoja kuhusu talaka kinasema kwamba “katika baadhi ya sherehe za ndoa, kiapo cha ndoa kinachosema, ‘kwa muda wote ambao sisi wawili tutaishi’ kilibadilishwa na badala yake ahadi hii yenye masharti inayosema, ‘kwa muda wote ambao sisi wawili tutapendana’ ikaanza kutumiwa.” Mtazamo huo wa kuchukulia ndoa kivivihivi umefanya familia nyingi sana zivunjike na umesababisha maumivu mengi sana ya kihisia. Hapana shaka kwamba mtazamo wa ulimwengu wa kutoiheshimu ndoa ni upumbavu.

13. Taja sababu moja kwa nini Yehova anachukizwa na watu wenye kiburi.

13 Biblia inasema hivi: “Kila mtu mwenye kiburi moyoni humchukiza Yehova.” (Met. 16:5) Kwa nini Yehova anachukizwa na watu wenye kiburi? Sababu moja ni kwamba wale wanaositawisha na kuendeleza maoni ya kujikweza wenyewe wanaiga kiburi cha Shetani. Hebu wazia, Shetani aliamini kwamba Yesu—yule ambaye Mungu alimtumia kuumba vitu vyote—anapaswa kumsujudia na kumwabudu! (Mt. 4:8, 9; Kol. 1:15, 16) Watu walio na mtazamo wa kujiona kuwa bora kuliko wengine wanathibitisha kwamba hekima ya ulimwengu huu ni upumbavu kwa Mungu.

MAONI YA BIBLIA KUHUSU KUJIPENDA WENYEWE

14. Andiko la Waroma 12:3 linatusaidiaje kuwa na maoni yanayofaa kujihusu?

14 Biblia hutusaidia tuwe na maoni yanayofaa kujihusu. Inasema wazi kwamba ni jambo linalofaa kujipenda kwa kiwango kinachofaa. Yesu alisema: “[Mpende] jirani yako kama unavyojipenda mwenyewe,” na maneno hayo yanaonyesha kwamba tunapaswa kuyapa uangalifu wa kutosha mahitaji yetu. (Mt. 19:19) Hata hivyo, Biblia haifundishi kwamba tunapaswa kujiona kuwa bora kuliko watu wengine. Badala yake, inasema hivi: “Msifanye jambo lolote kwa ugomvi au kwa kujisifu, bali kwa unyenyekevu mwaone wengine kuwa bora kuliko ninyi.”—Flp. 2:3; soma Waroma 12:3.

15. Kwa nini unafikiri kwamba shauri la Biblia kuhusu kutojiona kuwa bora kuliko wengine linafaa?

15 Leo, watu wengi wanaoonwa kuwa wenye hekima wanadhihaki ushauri wa Biblia kuhusu maoni tunayopaswa kuwa nayo kujihusu. Wanasema kwamba kuwaona wengine kuwa bora kuliko wewe kutakufanya uonekane kuwa mnyonge, na kwamba wengine watakutumia kwa faida zao wenyewe. Hata hivyo, mtazamo huo wa ubinafsi unaoendelezwa na ulimwengu wa Shetani umekuwa na matokeo gani? Wewe umejionea nini? Je, watu wabinafsi ni wenye furaha? Je, familia zao ni zenye furaha? Je, wana marafiki wa kweli? Je, wana urafiki wa karibu pamoja na Mungu? Kutokana na mambo uliyojionea, ni hekima gani inayotokeza matokeo mazuri, je, ni hekima ya ulimwengu huu au hekima iliyo katika Neno la Mungu?

16-17. Ni sababu gani inayotufanya tuwe wenye shukrani, na kwa nini?

16 Watu wanaofuata ushauri wa wale wanaoonwa na ulimwengu huu kuwa wenye hekima ni sawa na mtalii anayemwomba mtalii mwenzake amwonyeshe njia ilhali wote wawili wamepotea. Yesu alisema hivi kuhusu wanaume walioonwa kuwa wenye hekima katika siku zake: “Wao ni viongozi vipofu. Basi, kipofu akimwongoza kipofu, wote wawili watatumbukia ndani ya shimo.” (Mt. 15:14) Kwa kweli, hekima ya ulimwengu huu ni upumbavu kwa Mungu.

Watumishi wa Mungu wanakumbuka kwa furaha maisha yao katika utumishi wa Yehova (Tazama fungu la 17) *

17 Sikuzote shauri la Biblia limethibitika kuwa “lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kurekebisha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu.” (2 Tim. 3:16, maelezo ya chini) Tunamshukuru sana Yehova kwamba kupitia tengenezo lake, ametulinda tusiathiriwe na hekima ya ulimwengu huu! (Efe. 4:14) Chakula cha kiroho ambacho ametuandalia hutupatia nguvu za kushikamana na viwango vya Neno lake. Ni pendeleo kubwa sana kuongozwa na hekima inayopatikana katika Biblia, hekima inayotegemeka zaidi kuliko nyingine yoyote!

WIMBO 54 “Hii Ndiyo Njia”

^ fu. 5 Makala hii itatusaidia kuimarisha usadikisho wetu kwamba Yehova pekee ndiye Chanzo kinachotegemeka cha mwongozo. Pia, itatusaidia kujua kwamba ikiwa tutafuata hekima ya ulimwengu huu tutapata madhara makubwa, lakini tutapata manufaa kwa kutumia hekima ya Neno la Mungu.

^ fu. 9 Kwa mfano, tazama kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi Buku la 1, sura ya 24 hadi 26, na Buku la 2, sura ya 4 na 5.

^ fu. 50 MAELEZO YA PICHA: Tunaona baadhi ya pindi katika maisha ya wenzi fulani wa ndoa Mashahidi. Hapa, wenzi hao wanaonekana wakishiriki katika kazi ya kuhubiri mwishoni mwa miaka ya 1960.

^ fu. 52 MAELEZO YA PICHA: Katika miaka ya 1980, mume akimtunza mke wake mgonjwa huku binti yao akitazama.

^ fu. 54 MAELEZO YA PICHA: Leo, wenzi hao wa ndoa wanakumbuka kwa furaha maisha yao katika utumishi wa Yehova. Binti yao ambaye sasa ni mtu mzima, anafurahi pamoja nao.