Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 19

Upendo na Haki Katika Ulimwengu Mwovu

Upendo na Haki Katika Ulimwengu Mwovu

“Wewe si Mungu anayefurahia uovu; hakuna mtu yeyote mwovu anayeweza kukaa nawe.”​—ZAB. 5:4.

WIMBO 142 Kushikilia Tumaini Letu

MUHTASARI *

1-3. (a) Kulingana na Zaburi 5:4-6, Yehova anahisije kuhusu uovu? (b) Kwa nini tunaweza kusema kwamba kuwatendea watoto vibaya kingono ni kinyume kabisa na “sheria ya Kristo”?

YEHOVA MUNGU anachukia aina zote za uovu. (Soma Zaburi 5:4-6.) Hapana shaka kwamba anachukizwa sana watoto wanapotendewa vibaya kingono—tendo ambalo ni ovu na lenye kuchukiza sana! Kwa kuwa sisi ni Mashahidi wa Yehova, tunamwiga Yehova, na kwa sababu hiyo tunachukizwa sana na kosa la kuwatendea watoto vibaya kingono na hatuvumilii matendo hayo katika kutaniko la Kikristo.—Rom. 12:9; Ebr. 12:15, 16.

2 Kuwatendea watoto vibaya kingono kwa njia yoyote ile ni kinyume kabisa na “sheria ya Kristo”! (Gal. 6:2) Kwa nini tunasema hivyo? Kama tulivyojifunza katika makala iliyotangulia, sheria ya Kristo, yaani, mambo yote ambayo Yesu alifundisha kupitia maneno na mfano wake, hutetea haki na msingi wake ni upendo. Kwa kuwa Wakristo wa kweli wanaongozwa na sheria hiyo, wao huwatendea watoto kwa njia ambayo huwafanya wahisi wakiwa salama na wanapendwa kikweli. Lakini kumtendea mtoto vibaya kingono ni tendo la ubinafsi, lisilofaa na linalomfanya mtoto ahisi kwamba hana usalama na hapendwi.

3 Inasikitisha kwamba visa vya kuwatendea watoto vibaya kingono ni janga la ulimwenguni pote, na Wakristo wa kweli pia wamepatwa na madhara ya janga hilo. Kwa nini? “Watu waovu na wajanja” ni wengi, na huenda baadhi yao wakaingia kutanikoni. (2 Tim. 3:13) Isitoshe, baadhi ya watu waliokuwa sehemu ya kutaniko wamenaswa na tamaa zilizopotoka, nao wamewatendea watoto vibaya kingono. Acheni tuzungumzie kwa nini kuwatendea watoto vibaya kingono ni dhambi nzito sana. Kisha tutazungumzia jinsi wazee wa kutaniko wanavyoshughulikia visa vya dhambi nzito kutia ndani kuwatendea watoto vibaya kingono, na jinsi wazazi wanavyoweza kuwalinda watoto wao. *

NI DHAMBI NZITO SANA

4-5. Kwa nini kumtendea mtoto vibaya kingono ni kutenda dhambi dhidi yake?

4 Kumtendea mtoto vibaya kingono ni jambo litakalomwathiri kwa miaka mingi sana. Tendo hilo humuumiza mtoto na wale wanaompenda, yaani, watu wake wa familia na ndugu na dada zake Wakristo. Kumtendea mtoto vibaya kingono ni dhambi nzito sana.

5 Ni dhambi dhidi ya mtoto. Ni dhambi kuwasababishia wengine maumivu na mateso. Kama tutakavyoona katika makala inayofuata, hivyo ndivyo mtu anayemtendea mtoto vibaya kingono anavyofanya—anamuumiza mtoto kwa njia inayomwathiri sana. Kwa kuwa watoto huwaamini watu wazima na kuhisi wakiwa salama miongoni mwao, mtu huyo hutumia vibaya hisia hizo, na kumlazimisha mtoto apitie hali ambayo hakupaswa kamwe kupitia. Ni lazima tuwalinde watoto dhidi ya matendo maovu kama hayo, na wale waliotendewa hivyo wanahitaji faraja na msaada.—1 The. 5:14.

6-7. Kwa nini kumtendea mtoto vibaya kingono ni dhambi dhidi ya kutaniko na dhidi ya mamlaka za serikali?

6 Ni dhambi dhidi ya kutaniko. Mtu yeyote kutanikoni anayepatikana na hatia ya kumtendea mtoto vibaya kingono huliletea suto kutaniko. (Mt. 5:16; 1 Pet. 2:12) Ni jambo lisilo la haki hata kidogo kuwaharibia sifa Wakristo waaminifu wanaojitahidi kufanya “pigano kali kwa ajili ya imani”! (Yuda 3) Hatuwavumilii kamwe watu wanaofanya mambo maovu bila kutubu na wanaoharibu sifa nzuri ya kutaniko.

7 Ni dhambi dhidi ya mamlaka za serikali. Wakristo wanapaswa ‘kujitiisha kwa mamlaka zilizo kubwa.’ (Rom. 13:1) Tunajitiisha kwa mamlaka hizo kwa kuheshimu sheria za nchi tunamoishi. Mtu yeyote kutanikoni aliye na hatia ya kufanya kosa la jinai, kama vile kumtendea mtoto vibaya kingono, amefanya dhambi dhidi ya mamlaka za serikali. (Linganisha Matendo 25:8.) Ingawa wazee wa kutaniko hawana mamlaka ya kutekeleza sheria za nchi wanayoishi, hawamkingi mtu yeyote aliyemtendea mtoto vibaya kingono asichukuliwe hatua za kisheria kwa sababu ya matendo yake. (Rom. 13:4) Mtenda dhambi atavuna alichopanda.—Gal. 6:7.

8. Yehova anazionaje dhambi ambazo mtu anamtendea mwanadamu mwenzake?

8 Zaidi ya yote, ni dhambi dhidi ya Mungu. (Zab. 51:4) Mtu anapomtendea dhambi mwanadamu mwenzake, anamtendea dhambi Yehova pia. Kwa mfano, fikiria Sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli. Sheria ilisema kwamba ikiwa mtu alimwibia au kumlaghai jirani yake ‘alikosa uaminifu kwa Yehova.’ (Law. 6:2-4) Hivyo basi, kwa hakika mtu yeyote aliye sehemu ya kutaniko anapomtendea mtoto vibaya kingono ni kana kwamba anamwibia au anamnyang’anya haki yake ya kuhisi akiwa salama—na kwa njia hiyo anakosa uaminifu kwa Mungu. Mtu aliyetenda dhambi hiyo hulichafua sana jina la Yehova. Kwa sababu hiyo, tunapaswa kutambua kwamba kuwatendea watoto vibaya kingono ni dhambi nzito sana yenye kuchukiza mbele za Mungu, na ni lazima tuishutumu.

9. Kwa miaka mingi, tengenezo la Yehova limeandaa habari gani za Kimaandiko, na kwa nini?

9 Kwa miaka mingi, tengenezo la Yehova limechapisha habari nyingi za Kimaandiko kuhusu tatizo la kuwatendea watoto vibaya kingono. Kwa mfano, makala za Mnara wa Mlinzi na Amkeni! zimezungumzia jinsi wale waliotendewa vibaya kingono wanavyoweza kushughulika na makovu ya kihisia, jinsi wengine wanavyoweza kuwasaidia na kuwatia moyo, na jinsi wazazi wanavyoweza kuwalinda watoto wao. Wazee wa kutaniko wamepata mazoezi hususa ya Kimaandiko kuhusu jinsi ya kushughulikia visa vya watu wanaofanya dhambi ya kuwatendea watoto vibaya kingono. Bado tengenezo linaendelea kuchunguza jinsi makutaniko yanavyopaswa kushughulikia dhambi hiyo. Kwa nini? Ili kuhakikisha kwamba njia yetu ya kushughulikia visa hivyo inapatana na sheria ya Kristo.

KUSHUGHULIKIA VISA VYA DHAMBI NZITO

10-12. (a) Wazee huzingatia akilini jambo gani wanaposhughulikia visa vyovyote vya dhambi nzito, nao huhangaikia mambo gani? (b) Kulingana na Yakobo 5:14, 15, wazee hujitahidi kufanya nini?

10 Wazee wanaposhughulikia kisa chochote kinachohusisha dhambi nzito, wanazingatia akilini kwamba sheria ya Kristo inawataka walitendee kundi kwa upendo na wafanye jambo lililo sawa na la haki machoni pa Mungu. Kwa sababu hiyo, kuna mambo kadhaa ambayo wao huhangaikia wanapopokea habari kwamba mtu fulani amefanya dhambi nzito. Jambo kuu ambalo wazee wa kutaniko huhangaikia ni kutakaswa kwa jina la Mungu. (Law. 22:31, 32; Mt. 6:9) Pia, wanahangaikia sana hali ya kiroho ya ndugu na dada zao kutanikoni na wanataka kumsaidia yeyote ambaye ametendewa dhambi nzito.

11 Isitoshe, ikiwa mtenda dhambi ni sehemu ya kutaniko, wazee wa kutaniko huhangaikia jinsi ya kumsaidia ili awe tena na uhusiano mzuri na Yehova, ikiwa inawezekana. (Soma Yakobo 5:14, 15.) Mkristo anayejiruhusu ashawishiwe na kunaswa na tamaa zisizofaa na hatimaye kutumbukia kwenye dhambi nzito ni mgonjwa kiroho. Hilo linamaanisha kwamba amepoteza uhusiano mzuri pamoja na Yehova. * Kwa njia fulani, wazee wa kutaniko ni madaktari wa kiroho. Wanajitahidi ‘kumponya mgonjwa huyo,’ yaani, mtenda dhambi. Shauri lao la Kimaandiko linaweza kumsaidia awe tena na uhusiano mzuri pamoja na Mungu, lakini hilo litawezekana tu ikiwa mtenda dhambi ametubu kikweli.—Mdo. 3:19; 2 Kor. 2:5-10.

12 Ni wazi kwamba wazee wana jukumu zito. Wanalijali sana kundi ambalo Mungu amewakabidhi walitunze. (1 Pet. 5:1-3) Wangependa ndugu na dada zao wahisi wakiwa salama kutanikoni. Kwa sababu hiyo, wao huchukua hatua bila kukawia wanapopokea habari kuhusu dhambi nzito, kutia ndani dhambi ya kuwatendea watoto vibaya kingono. Fikiria kuhusu maswali yaliyo mwanzoni mwa  fungu la 13,  15, na  17.

13-14. Je, wazee hutii sheria za nchi zinazowataka raia waripoti mashtaka yanayohusu visa vya kuwatendea watoto vibaya kingono? Eleza.

 13 Je, wazee hutii sheria za nchi zinazowataka raia waripoti kwenye mamlaka za serikali mashtaka yanayohusu visa vya kuwatendea watoto vibaya kingono? Ndiyo. Katika nchi zilizo na sheria kama hizo, wazee hujitahidi kutii sheria zinazowataka watu waripoti mashtaka hayo. (Rom. 13:1) Sheria kama hizo hazipingani na sheria ya Mungu. (Mdo. 5:28, 29) Hivyo, wazee wanapopokea habari kuhusu shtaka la aina hiyo, mara moja wao hutafuta mwongozo kutoka kwa ofisi ya tawi kuhusu jinsi wanavyoweza kutii sheria za kuripoti mashtaka ya aina hiyo.

14 Wazee huwahakikishia wale waliotendewa vibaya kingono na pia wazazi wao, na wengine wanaofahamu jambo hilo kwamba wako huru kuripoti mashtaka hayo kwenye mamlaka za serikali. Lakini vipi ikiwa shtaka hilo linamhusu mtu fulani aliye sehemu ya kutaniko na kisha jambo hilo linajulikana katika jamii? Je, Mkristo aliyeripoti shtaka hilo anapaswa kuhisi kwamba ameliletea suto jina la Mungu? La. Yule aliyetenda dhambi hiyo ndiye aliyeliletea suto jina la Mungu.

15-16. (a) Kulingana na 1 Timotheo 5:19, kwa nini angalau mashahidi wawili wanahitajika kabla ya wazee kuchukua hatua yoyote ya kihukumu? (b) Wazee huchukua hatua gani wanapopata habari kwamba mtu fulani ambaye ni sehemu ya kutaniko anatuhumiwa kuwa alimtendea mtoto vibaya kingono?

 15 Kabla ya wazee kuchukua hatua ya kihukumu, kwa nini angalau mashahidi wawili wanahitajika? Takwa hilo ni mojawapo ya viwango vya juu vya Biblia kuhusu haki. Ikiwa mtenda dhambi hajakiri dhambi yake, mashahidi wawili wanahitajika ili kuthibitisha shtaka hilo na ndipo wazee wanapoweza kuchukua hatua ya kihukumu. (Kum. 19:15; Mt. 18:16; soma 1 Timotheo 5:19.) Je, hilo linamaanisha kwamba kabla ya kuripoti kwenye mamlaka za serikali shtaka la mtoto kutendewa vibaya kingono ni lazima kuwe na mashahidi wawili? Hapana. Wazee au watu wengine wanapohitaji kuripoti mashtaka ya uvunjaji wa sheria, si lazima kuwe na mashahidi wawili wa kuthibitisha jambo hilo.

16 Wazee wanapopata habari kwamba mtu fulani kutanikoni ameshtakiwa kwamba amemtendea mtoto vibaya kingono, wao hujitahidi kutii sheria zozote za nchi zinazohusu kuripoti jambo hilo kwenye mamlaka za serikali, na baada ya hapo wanafanya uchunguzi wa Kimaandiko. Mshtakiwa akikataa kwamba alifanya kosa hilo, wazee huzingatia ushahidi wa watu wengine ambao wanajua kilichotukia. Ikiwa kuna angalau mashahidi wawili, yaani, mshtaki na mtu mwingine anayeweza kuthibitisha kwamba kosa hilo au makosa mengine ya kuwatendea watoto vibaya kingono yalifanywa na mshtakiwa, basi halmashauri ya hukumu huundwa. * Kutokuwepo kwa shahidi wa pili hakumaanishi kwamba yule anayeshtaki kosa anasema uwongo. Hata ikiwa hakuna mashahidi wawili wa kuthibitisha kwamba mshtakiwa alimtendea mtoto vibaya kingono, wazee wanatambua kwamba kuna uwezekano kuwa dhambi nzito imefanywa, ambayo inawaumiza sana wengine. Wazee huendelea kumfariji na kumtegemeza mtu yeyote aliyeathiriwa na kitendo hicho. Pamoja na hilo, wazee huendelea kuwa macho kumwelekea mtuhumiwa ili kulilinda kutaniko dhidi ya hatari yoyote inayoweza kujitokeza.—Mdo. 20:28.

17-18. Fafanua jukumu la halmashauri ya hukumu.

 17 Halmashauri ya hukumu ina jukumu gani? Neno “hukumu” halimaanishi kwamba wazee huhukumu, au kuamua ikiwa yule aliyetenda dhambi anapaswa kuadhibiwa au la na wenye mamlaka kwa kuvunja sheria. Wazee hawaingilii utaratibu wowote wa kisheria; wao huacha mambo yote yanayohusu uvunjaji wa sheria mikononi mwa mamlaka za serikali. (Rom. 13:2-4; Tito 3:1) Badala yake, wazee huhukumu au kuamua ikiwa yule aliyefanya kosa anastahili kubaki katika kutaniko au la.

18 Jukumu la wazee wanaotumikia kwenye halmashauri ya hukumu linahusu tu mambo ya kiroho. Wao huongozwa na Maandiko kuamua ikiwa mtenda dhambi ametubu au la. Ikiwa hajatubu, yeye hutengwa na ushirika, na tangazo hutolewa kutanikoni. (1 Kor. 5:11-13) Ikiwa ametubu, anaweza kubaki kutanikoni. Hata hivyo, wazee watamjulisha kwamba hatastahili kupata mapendeleo yoyote kutanikoni kwa miaka mingi, au labda kwa maisha yake yote. Kwa kuwa wazee wanajali kuhusu hali njema ya watoto, wanaweza kuwatahadharisha faraghani wazazi kutanikoni kuhusu uhitaji wa kukaa macho watoto wao wanapokuwa karibu na mtu huyo. Wanapochukua hatua hizo, wazee huwa waangalifu ili wasifunue habari zozote kuhusu wale walioathiriwa na dhambi iliyotendwa.

JINSI YA KUWALINDA WATOTO WAKO

Wazazi huwalinda watoto wao wasitendewe vibaya kingono kwa kuwafundisha habari kuhusu ngono kulingana na umri wao. Wanafanya hivyo kwa kutumia habari zilizoandaliwa na tengenezo la Mungu. (Tazama fungu la 19 hadi 22)

19-22. Wazazi wanaweza kufanya nini ili kuwalinda watoto wao? (Tazama picha kwenye jalada.)

19 Ni nani aliye na jukumu la kuwalinda watoto? Ni wazazi. * Watoto wako ni amana takatifu, “urithi kutoka kwa Yehova.” (Zab. 127:3) Ni jukumu lako kuilinda amana hiyo. Unaweza kufanya nini ili uwalinde watoto wako wasitendewe vibaya kingono?

20 Kwanza, jielimishe kuhusu jinsi ya kuwalinda watoto wako ili wasitendewe vibaya kingono. Jifunze kuhusu aina ya watu wanaowatendea watoto vibaya kingono na mbinu wanazotumia ili kuwadanganya. Uwe macho kuhusu hali zinazoweza kuhatarisha usalama wao. (Met. 22:3; 24:3) Kumbuka kwamba katika visa vingi, mtu anayemtendea mtoto vibaya kingono ni mtu ambaye tayari mtoto anamfahamu na anamwamini.

21 Pili, uwe na mazoea ya kuzungumza waziwazi na watoto wako na uwatie moyo wazungumze nawe kwa uhuru. (Kum. 6:6, 7) Hilo linatia ndani kuwa msikilizaji mzuri. (Yak. 1:19) Kumbuka kwamba watoto huogopa kusema kwamba walitendewa vibaya kingono. Huenda wakaogopa kwamba wengine watafikiri kuwa wanasema uwongo, au huenda yule aliyewatendea hivyo amewatisha kwamba ikiwa watamwambia mtu jambo hilo atawafanyia jambo fulani baya. Ukihisi kwamba mtoto wako ametendewa vibaya kingono, kwa upole muulize maswali yatakayomsaidia kujieleza, kisha sikiliza kwa subira chochote atakachokuambia.

22 Tatu, waelimishe watoto wako. Wafundishe mambo wanayohitaji kujua kuhusu ngono kulingana na umri wao. Wafundishe jambo wanalopaswa kusema na kutenda mtu fulani akijaribu kuwagusa kwa njia isiyofaa. Tumia habari zilizochapishwa na tengenezo la Mungu kuhusu jinsi ya kuwalinda watoto wako.​—Tazama sanduku, “ Jielimishe na Uwaelimishe Watoto Wako.”

23. Tuna maoni gani kuhusu kuwatendea watoto vibaya kingono, na makala inayofuata itajibu swali gani?

23 Tukiwa Mashahidi wa Yehova, tunaona kuwatendea watoto vibaya kingono kuwa dhambi nzito sana na yenye kuchukiza. Kwa kuwa tunaongozwa na sheria ya Kristo, makutaniko yetu hayawakingi wale waliowatendea watoto vibaya kingono wasipatwe na matokeo ya dhambi zao. Hata hivyo, tunaweza kufanya nini ili kuwasaidia wale waliotendewa vibaya kingono? Makala inayofuata itajibu swali hilo.

WIMBO 103 Wachungaji—Zawadi Katika Wanadamu

^ fu. 5 Makala hii itazungumzia jinsi watoto wanavyoweza kulindwa ili wasitendewe vibaya kingono. Tutajifunza jinsi wazee wanavyotenda kwa niaba ya kutaniko na jinsi wazazi wanavyoweza kuwalinda watoto wao.

^ fu. 3 UFAFANUZI WA MANENO: Mwanamume au mwanamke aliye mtu mzima anapomtumia mtoto kutosheleza tamaa zake za kingono anasemwa kwamba amemtendea vibaya kingono. Hilo linatia ndani kufanya ngono na mtoto; ngono ya kinywa au ya mkundu; kupapasa-papasa viungo vyake vya uzazi, matiti, au matako; au matendo mengine yaliyopotoka. Ni muhimu kutambua kwamba mtoto aliyetendewa vibaya kingono ameumizwa kihisia na kimwili na amedhulumiwa haki zake, na hapaswi kulaumiwa kwa jambo lililotendeka. Ingawa idadi kubwa ya wale wanaotendewa vibaya kingono ni wasichana, wavulana wengi pia hutendewa hivyo. Ingawa idadi kubwa ya watu wanaowatendea watoto vibaya kingono ni wanaume, baadhi ya wanawake pia hufanya hivyo.

^ fu. 11 Kuwa mgonjwa kiroho si kisingizio cha kufanya dhambi nzito. Mtenda dhambi anawajibika kikamili mbele za Yehova kwa maamuzi na matendo mabaya aliyofanya.—Rom. 14:12.

^ fu. 16 Mtoto hapaswi kulazimika kamwe kuwepo wazee wanapozungumza na mtuhumiwa aliyemtendea vibaya kingono. Mzazi au mtu mwingine mzima ambaye mtoto anamwamini anaweza kuwaeleza wazee kuhusu kilichotukia ili kuepuka kumsababishia mtoto maumivu zaidi ya kihisia.

^ fu. 19 Habari hii inawahusu pia walezi wanaotambulika kisheria au wengine ambao wana jukumu la kumlea mtoto.