Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 19

“Mfalme wa Kaskazini” Katika Wakati wa Mwisho

“Mfalme wa Kaskazini” Katika Wakati wa Mwisho

“Wakati wa mwisho mfalme wa kusini atasukumana naye [mfalme wa kaskazini].”—DAN. 11:40.

WIMBO 150 Mtafute Mungu Upate Ukombozi

MUHTASARI *

1. Unabii wa Biblia unatusaidia kujua nini?

NI NINI kitakachowapata watu wa Yehova hivi karibuni? Hatuhitaji kukisia. Unabii wa Biblia unatuambia kuhusu matukio makubwa ambayo yatatugusa sisi sote. Kuna unabii mmoja hususa unaotusaidia kujua mambo fulani ambayo baadhi ya serikali zenye nguvu duniani zitafanya. Unabii huo unaopatikana kwenye Danieli sura ya 11, unaonyesha historia ya wafalme wawili wanaopingana, yaani, mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini. Tayari sehemu kubwa ya unabii huo imetimia, hivyo tunaweza kuwa na hakika kwamba sehemu iliyobaki itatimia pia.

2. Kama inavyotajwa kwenye Mwanzo 3:15 na Ufunuo 11:7 na 12:17, ni mambo gani muhimu ambayo ni lazima tukumbuke tunapojifunza unabii wa Danieli?

2 Ili kuelewa unabii wa Danieli sura ya 11, tunapaswa kukumbuka kwamba unabii huo unawahusu tu watawala na serikali ambazo zimewahi kuwaathiri watu wa Mungu moja kwa moja. Na ingawa watumishi wa Mungu ni wachache ukilinganisha na idadi ya watu duniani, kwa kawaida wao hujikuta wakiwa wamehusishwa kwa njia kubwa katika matukio makubwa ya ulimwengu. Kwa nini? Kwa sababu Shetani na mfumo wake wote una lengo moja kuu, yaani, kuwaangamiza wale wanaomtumikia Yehova na Yesu. (Soma Mwanzo 3:15 na Ufunuo 11:7; 12:17.) Pia, lazima unabii wa Danieli upatane na unabii mwingine katika Neno la Mungu. Ukweli ni kwamba tunaweza kuelewa kwa usahihi unabii wa Danieli ikiwa tu tutaulinganisha na vitabu vingine vya Biblia.

3. Tutazungumzia nini katika makala hii na ile itakayofuata?

3 Tukiwa na hayo akilini, sasa tutazungumzia Danieli 11:25-39. Tutaona ni nani aliyekuwa mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini kuanzia mwaka wa 1870 hadi 1991, na tutaona kwa nini inafaa turekebishe uelewaji wetu kuhusu sehemu fulani ya unabii huo. Katika makala itakayofuata, tutazungumzia Danieli 11:40–12:1, na tutarekebisha uelewaji wetu kuhusu mambo yanayofunuliwa na sehemu hiyo ya unabii yanayohusu kipindi cha wakati kilichoanza mwaka wa 1991 hadi wakati wa vita vya Har–Magedoni. Unapojifunza makala hizi mbili, itafaa uchunguze chati “Wafalme Wanaopingana Katika Wakati wa Mwisho.” Hata hivyo, kwanza, tunahitaji kuwatambua wafalme hao wawili katika unabii huo.

KUMTAMBUA MFALME WA KASKAZINI NA MFALME WA KUSINI

4. Ni mambo gani matatu yatakayotusaidia kumtambua mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini?

4 Mwanzoni, majina “mfalme wa kaskazini” na “mfalme wa kusini” yalikuwa majina yaliyotumiwa kutambulisha serikali za kisiasa zilizokuwa upande wa kaskazini na wa kusini wa nchi halisi ya Israeli. Kwa nini tunasema hivyo? Ona ujumbe huu ambao malaika alimpa Danieli: “Nimekuja kukuelewesha mambo yatakayowapata watu wako katika kipindi cha mwisho cha zile siku.” (Dan. 10:14) Kufikia Pentekoste 33 W.K., taifa halisi la Israeli ndilo lililokuwa watu wa Mungu. Hata hivyo, kuanzia wakati huo na kuendelea, Yehova alitambulisha wazi kwamba wanafunzi waaminifu wa Yesu ndio waliokuwa watu wake. Hivyo, unabii mwingi wa Danieli sura ya 11 hauhusu taifa halisi la Israeli, bali unawahusu wafuasi wa Kristo. (Mdo. 2:1-4; Rom. 9:6-8; Gal. 6:15, 16) Na kadiri muda ulivyopita, watawala au serikali tofauti-tofauti zilitambuliwa kuwa mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini. Hata hivyo, watawala hao wote walifanana kwa njia kadhaa. Kwanza, wafalme hao waliwatawala au kuwatesa watu wa Mungu. Pili, walionyesha kwamba wanamchukia Yehova, Mungu wa kweli kupitia jinsi walivyowatendea watu wa Mungu. Na tatu, wafalme hao wawili walikuwa wakipambana wao kwa wao ili kupata mamlaka.

5. Je, ingewezekana kumtambua mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini kati ya mwaka wa 100 W.K. na mwaka wa 1870? Eleza.

5 Wakati fulani katika karne ya pili W.K., Wakristo wengi wa uwongo walianza kuingia katika kutaniko la kweli la Kikristo, nao wakaanza kufundisha mafundisho ya kipagani na kuficha kweli za Neno la Mungu. Tangu wakati huo hadi kufikia mwishoni mwa karne ya 19 hakukuwa na kikundi chochote kilichopangwa cha watumishi wa Mungu duniani. Magugu ya Wakristo wa uwongo yalisitawi na ikawa vigumu kuwatambua Wakristo wa kweli. (Mt. 13:36-43) Kwa nini ni muhimu kujua jambo hilo? Kwa sababu jambo hilo linaonyesha kwamba mambo tunayosoma kuhusu mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini hayakuwahusu watawala au falme zilizokuwa zikitawala kuanzia mwaka wa 100 W.K. hadi mwaka wa 1870. Wakati huo, hakukuwa na kikundi kilichopangwa cha watu wa Mungu ambacho wangeweza kukishambulia. * Hata hivyo, muda mfupi baada ya mwaka wa 1870, ingewezekana tena kumtambua mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini. Kwa nini?

6. Ni wakati gani watu wa Mungu walianza tena kumtumikia wakiwa kikundi? Eleza.

6 Kuanzia mwaka wa 1870 na kuendelea, watu wa Mungu walianza kumtumikia wakiwa kikundi. Mwaka huo Charles T. Russell na wenzake walianzisha kikundi cha kujifunza Biblia. Ndugu Russell pamoja na wale alioshirikiana nao kwa ukaribu walitenda kama mjumbe aliyekuwa ametabiriwa ambaye ‘angefungua njia’ kabla ya Ufalme wa Kimasihi kusimamishwa. (Mal. 3:1) Kwa mara nyingine tena, kulikuwa na kikundi cha watu waliomtumikia Yehova kwa njia sahihi! Je, kulikuwa na serikali zozote za ulimwengu wakati huo ambazo ziliwatawala au kuwatesa watumishi wa Mungu? Fikiria mambo yafuatayo.

MFALME WA KUSINI NI NANI?

7. Ni nani aliyekuwa mfalme wa kusini, kufikia muda fulani baada ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu kuanza?

7 Kufikia mwaka wa 1870, tayari nchi ya Uingereza ndiyo iliyokuwa milki kubwa zaidi duniani na yenye jeshi lenye nguvu nyingi zaidi. Katika unabii wa Danieli, milki hiyo inafananishwa na pembe ndogo ambayo ilishinda pembe nyingine tatu, yaani, Ufaransa, Hispania, na Uholanzi. (Dan. 7:7, 8) Pembe hiyo ndogo ndiyo iliyokuwa mfalme wa kusini kufikia muda fulani baada ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu kuanza. Wakati huo, tayari Marekani ilikuwa nchi tajiri zaidi duniani na ilikuwa imeanza kushirikiana kwa ukaribu na Uingereza.

8. Ni nani ambaye amekuwa mfalme wa kusini katika kipindi chote cha siku za mwisho?

8 Wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, serikali ya Marekani na Uingereza ziliungana na kufanyiza jeshi lenye nguvu nyingi sana. Wakati huo, Uingereza na koloni lake la zamani, Marekani, ziliungana na kutokeza Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Uingereza na Marekani. Kama Danieli alivyotabiri, serikali hiyo ilikuwa imejikusanyia “jeshi kubwa kupita kiasi, tena lenye nguvu.” (Dan. 11:25) Katika kipindi cha siku za mwisho, muungano wa Uingereza na Marekani umekuwa ndio mfalme wa kusini. * Hata hivyo, ni nani aliyechukua nafasi ya mfalme wa kaskazini?

MFALME WA KASKAZINI AIBUKA TENA

9. Mfalme wa kaskazini aliibuka tena lini, na andiko la Danieli 11:25 lilitimizwaje?

9 Katika mwaka wa 1871, mwaka mmoja baada ya Russell na wenzake kuanzisha kikundi cha kujifunza Biblia, mfalme wa kaskazini aliibuka tena. Mwaka huo, Otto von Bismarck alichangia kwa kiwango kikubwa kuanzishwa kwa Milki ya Ujerumani. Mfalme Wilhelm wa Kwanza wa Prussia akawa maliki wa kwanza wa milki hiyo, naye akamteua Bismarck kuwa waziri mkuu wa kwanza. * Katika miaka iliyofuata, Ujerumani ikawa serikali ya kikoloni ikitawala nchi za Afrika na nchi zilizo kwenye Bahari ya Pasifiki, na ikaanza kupambana na Uingereza ili kupata mamlaka zaidi. (Soma Danieli 11:25.) Milki ya Ujerumani iliunda jeshi lenye nguvu nyingi sana na jeshi lake la majini lilikuwa la pili kwa ukubwa duniani. Ujerumani ilitumia majeshi hayo kushambulia maadui wake katika Vita vya Kwanza vya Ulimwengu.

10. Andiko la Danieli 11:25b, 26 lilitimizwaje?

10 Kisha Danieli anatabiri kuhusu kile kitakachoipata Milki ya Ujerumani na jeshi lake. Unabii huo unasema kwamba mfalme wa kaskazini “hatasimama.” Kwa nini? “Kwa sababu watapanga njama dhidi yake. Na wale wanaokula vyakula vyake bora watasababisha aanguke.” (Dan. 11:25b, 26a) Katika siku za Danieli, wale waliokula “vyakula bora ambavyo [mfalme] mwenyewe alikula” walitia ndani maofisa wa mfalme ‘waliomtumikia mfalme.’ (Dan. 1:5) Unabii huo unazungumza kuhusu nani? Unawahusu maofisa wa vyeo vya juu wa Milki ya Ujerumani—kutia ndani majenerali na washauri wa mambo ya kijeshi wa maliki—ambao hatimaye walipindua utawala wa maliki wa Ujerumani. * Unabii wa Danieli haukutabiri tu kuhusu kuanguka kwa milki hiyo, bali pia unataja matokeo ya vita kati ya mfalme wa kaskazini na wa kusini. Unabii huo unasema hivi kuhusu mfalme wa kaskazini: “Na jeshi lake litafagiliwa mbali, na wengi watauawa.” (Dan. 11:26b) Kama ilivyotabiriwa, jeshi la Ujerumani ‘lilifagiliwa mbali’ katika Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, na watu wengi ‘waliuawa.’ Watu wengi sana walikufa katika vita hivyo kuliko vita vingine vyovyote kabla ya hapo.

11. Mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini walifanya nini?

11 Andiko la Danieli 11:27, 28 linaeleza kuhusu mambo yaliyotukia kabla ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu. Unabii huo unasema kwamba mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini “wataketi kwenye meza moja wakiambiana uwongo.” Pia, unasema kwamba mfalme wa kaskazini angejikusanyia “mali nyingi.” Na hivyo ndivyo ilivyokuwa. Serikali ya Ujerumani na ya Uingereza zilisema kwamba walitaka kuwe na amani, lakini maneno yao yalithibitika kuwa ya uwongo vita vilipozuka katika mwaka wa 1914. Vilevile, kufikia mwaka wa 1914, Ujerumani ilikuwa nchi ya pili kwa utajiri duniani. Kisha, Ujerumani ikapigana vita na mfalme wa kusini lakini ikashindwa, na hivyo kutimiza unabii wa Danieli 11:29 na sehemu ya kwanza ya mstari wa 30.

WAFALME HAO WAPAMBANA NA WATU WA MUNGU

12. Wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini walifanya nini?

12 Tangu mwaka wa 1914 na kuendelea, wafalme hao wawili wamezidisha mashambulizi kati yao na dhidi ya watu wa Mungu. Kwa mfano, katika Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, serikali ya Ujerumani na serikali ya Uingereza ziliwatesa watumishi wa Mungu waliokataa kwenda vitani. Nayo serikali ya Marekani ikawatupa gerezani wale waliokuwa wakisimamia kazi ya kuhubiri. Mateso hayo yalitimiza unabii wa Ufunuo 11:7-10.

13. Mfalme wa kaskazini alifanya nini katika miaka ya 1930 na wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu?

13 Kisha, katika miaka ya 1930 na hasa wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu, mfalme wa kaskazini aliwashambulia watu wa Mungu bila huruma. Halafu chama cha Nazi kilipochukua mamlaka nchini Ujerumani, Hitler na wafuasi wake walipiga marufuku kazi ya watu wa Mungu. Wapinzani hao waliwaua mamia ya watu wa Yehova na kuwapeleka maelfu zaidi kwenye kambi za mateso. Danieli alikuwa ametabiri kuhusu matukio hayo. Mfalme wa kaskazini alifanikiwa ‘kupachafua patakatifu’ na “kuondoa ile dhabihu inayotolewa daima” kwa kuwawekea watu wa Mungu vizuizi vikali ili wasilisifu jina la Yehova hadharani. (Dan. 11:30b, 31a) Hata Hitler aliyekuwa kiongozi wao aliapa kuwafutilia mbali watu wa Mungu nchini Ujerumani.

MFALME MPYA WA KASKAZINI AIBUKA

14. Ni nani aliyekuwa mfalme wa kaskazini baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu? Eleza.

14 Baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu, serikali ya Kikomunisti ya Muungano wa Sovieti ilianza kutawala maeneo makubwa iliyokuwa imeshinda kutoka kwa Ujerumani, nayo ikawa mfalme wa kaskazini. Kama ilivyokuwa kwa utawala wa kimabavu wa Wanazi, Muungano wa Sovieti uliwatesa sana wale wote waliotanguliza ibada yao kwa Mungu wa kweli, badala ya kujitiisha kikamili kwa serikali.

15. Baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu kuisha, mfalme wa kaskazini alifanya nini?

15 Muda mfupi baada ya Vita vya Pili vya Ulimwengu kuisha, mfalme mpya wa kaskazini, yaani, Muungano wa Sovieti na nchi zilizounga mkono muungano huo, alianza kuwatesa vikali watu wa Mungu. Kama unabii wa Ufunuo 12:15-17 ulivyokuwa umeonyesha, mfalme huyo alipiga marufuku kazi yetu ya kuhubiri na kuwapeleka maelfu ya watu wa Yehova uhamishoni. Isitoshe, katika kipindi chote cha siku za mwisho, mfalme wa kaskazini ametapika “mto” wa mateso ili asimamishe kazi ya watu wa Mungu, lakini hajafanikiwa. *

16. Muungano wa Sovieti ulitimizaje andiko la Danieli 11:37-39?

16 Soma Danieli 11:37-39. Unabii huo ulitimia mfalme wa kaskazini alipokosa ‘kumjali Mungu wa baba zake.’ Jinsi gani? Muungano wa Sovieti ulikuwa na lengo la kufutilia mbali dini, hivyo ulijaribu kuyanyang’anya mashirika ya kidini mamlaka yao. Ili kutimiza lengo hilo, tayari mwaka wa 1918 serikali ya Sovieti ilikuwa imetoa agizo ambalo liliweka msingi wa kuwafundisha wanafunzi shuleni wazo la kutokuwepo kwa Mungu. Mfalme huyo wa kaskazini ‘alimpaje utukufu mungu wa ngome’? Muungano wa Sovieti ulitumia pesa nyingi sana kuimarisha jeshi lake na kutengeneza maelfu ya silaha za nyuklia ili kuimarisha mamlaka yake. Mwishowe, mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini walijikusanyia silaha za kutosha na zenye nguvu zinazoweza kuangamiza mabilioni ya watu!

USHIRIKIANO USIO WA KAWAIDA

17. ‘Kile kitu chenye kuchukiza sana kinachosababisha ukiwa’ ni nini?

17 Mfalme wa kaskazini amemuunga mkono mfalme wa kusini katika jambo moja muhimu; ‘walisimamisha kile kitu chenye kuchukiza sana kinachosababisha ukiwa.’ (Dan. 11:31) ‘Kitu hicho chenye kuchukiza sana’ ni shirika la Umoja wa Mataifa.

18. Kwa nini shirika la Umoja wa Mataifa linatajwa kuwa ‘kitu chenye kuchukiza sana’?

18 Shirika la Umoja wa Mataifa linatajwa kuwa ‘kitu chenye kuchukiza sana’ kwa sababu linadai kwamba linaweza kufanya jambo ambalo Ufalme wa Mungu pekee ndio unaoweza kufanya, yaani, kuleta amani duniani. Na unabii wa Danieli unataja kwamba kitu hicho chenye kuchukiza sana ‘kinasababisha ukiwa’ kwa sababu shirika la Umoja wa Mataifa litashambulia dini zote za uwongo na kuziangamiza.—Tazama chati “Wafalme Wanaopingana Katika Wakati wa Mwisho.”

KWA NINI TUNAHITAJI KUJUA HISTORIA HIYO?

19-20. (a) Kwa nini tunahitaji kuijua historia hiyo? (b) Tutajibu swali gani katika makala inayofuata?

19 Tunahitaji kujua historia hiyo kwa sababu inathibitisha kwamba kuanzia miaka ya 1870 hadi mwanzoni mwa miaka ya 1990, unabii wa Danieli kuhusu mfalme wa kaskazini na mfalme wa kusini umetimizwa. Hivyo, tunaweza kuwa na imani kwamba sehemu iliyobaki ya unabii huo itatimia pia.

20 Mwaka wa 1991, Muungano wa Sovieti ulianguka. Basi mfalme wa kaskazini ni nani leo? Makala inayofuata inajibu swali hilo.

WIMBO 128 Kuvumilia Mpaka Mwisho

^ fu. 5 Tunajionea uthibitisho kwamba unabii wa Danieli kuhusu “mfalme wa kaskazini” na “mfalme wa kusini” unaendelea kutimia. Tunawezaje kuwa na uhakika kuhusu jambo hilo? Na kwa nini tunahitaji kuelewa mambo yanayohusu unabii huo?

^ fu. 5 Hivyo, kutokana na maelezo hayo isingefaa kusema kwamba Maliki Mroma Aurelian (270-275 W.K.) alikuwa “mfalme wa kaskazini” au kwamba Malkia Zenobia (267-272 W.K.) alikuwa “mfalme wa kusini.” Ufafanuzi huo unarekebisha uelewaji uliochapishwa kwenye sura ya 13 na ya 14 ya kitabu Sikiliza Unabii wa Danieli!

^ fu. 9 Mwaka wa 1890, Maliki Wilhelm wa Pili alimwondoa Bismarck madarakani.

^ fu. 10 Walifanya mambo mengi yaliyosababisha milki yao ianguke haraka. Kwa mfano, waliacha kumsaidia maliki, walivujisha siri kuhusu habari nyeti za vita, na kumlazimisha maliki ajiuzulu.

^ fu. 15 Kama andiko la Danieli 11:34 linavyoonyesha, Wakristo walioishi chini ya mfalme wa kaskazini walipata kiasi fulani cha utulivu kutokana na mateso waliyokuwa nayo. Kwa mfano, hilo lilitukia Muungano wa Sovieti ulipoanguka mwaka wa 1991.