Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 22

Onyesha Kwamba Unathamini Hazina Zisizoonekana

Onyesha Kwamba Unathamini Hazina Zisizoonekana

‘Kaza macho yako juu ya vitu visivyoonekana. Kwa maana vitu vinavyoonekana ni vya muda, lakini vitu visivyoonekana ni vya milele.’—2 KOR. 4:18.

WIMBO 45 Kutafakari kwa Moyo Wangu

MUHTASARI *

1. Yesu alisema nini kuhusu hazina za mbinguni?

SI HAZINA zote zinazoweza kuonekana kwa macho. Ukweli ni kwamba hazina zenye thamani zaidi ni zile zisizoonekana. Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alizungumza kuhusu hazina za mbinguni zilizo bora zaidi kuliko vitu vya kimwili. Kisha alitaja ukweli huu: “Mahali ilipo hazina yako, ndipo moyo wako utakapokuwa pia.” (Mt. 6:19-21) Moyo wetu utatuchochea tufuatilie mambo tunayoona kuwa hazina, au yenye thamani sana. Tunajiwekea “hazina mbinguni” kwa kujipatia jina zuri, au msimamo mzuri mbele za Mungu. Yesu alieleza kwamba hazina kama hizo haziwezi kuharibiwa au kuibiwa.

2. (a) Kulingana na andiko la 2 Wakorintho 4:17, 18, Paulo anatuhimiza tukazie nini? (b) Tutazungumzia nini katika makala hii?

2 Mtume Paulo anatuhimiza ‘tukaze macho yetu juu ya vitu visivyoonekana.’ (Soma 2 Wakorintho 4:17, 18.) Hazina hizo zisizoonekana zinatia ndani baraka tutakazofurahia katika ulimwengu mpya wa Mungu. Katika makala hii, tutachunguza hazina nne zisizoonekana ambazo zinaweza kutunufaisha hata sasa, yaani, urafiki wetu pamoja na Mungu, zawadi ya sala, msaada wa roho takatifu ya Mungu, na utegemezo tunaopata kutoka mbinguni ili tutimize huduma yetu. Pia, tutazungumzia jinsi tunavyoweza kuonyesha kwamba tunathamini hazina hizo zisizoonekana.

URAFIKI PAMOJA NA YEHOVA

3. Ni hazina gani yenye thamani zaidi ambayo hatuwezi kuiona kwa macho, na ni nini kinachofanya iwezekane kuwa nayo?

3 Hazina isiyoonekana yenye thamani zaidi kuliko zote ni urafiki wetu pamoja na Mungu. (Zab. 25:14) Mungu anawezaje kufanya urafiki pamoja na wanadamu wenye dhambi na bado aendelee kuwa mtakatifu? Anaweza kufanya hivyo kwa sababu dhabihu ya fidia ya Yesu ‘huondoa dhambi ya ulimwengu’ wa wanadamu. (Yoh. 1:29) Yehova alijua mapema kwamba kusudi lake la kuandaa Mkombozi kwa ajili ya wanadamu halingekosa kutimia. Hiyo ndiyo sababu Mungu angeweza kufanya urafiki pamoja na wanadamu walioishi kabla ya Kristo.—Rom. 3:25.

4. Taja baadhi ya mifano ya watu walioishi kabla ya Kristo ambao walikuwa rafiki za Mungu.

4 Wafikirie baadhi ya watu walioishi kabla ya Kristo ambao walikuwa rafiki za Mungu. Abrahamu alikuwa mwanamume aliyeonyesha imani ya pekee. Zaidi ya miaka 1,000 baada ya Abrahamu kufa, Yehova alimwita “rafiki yangu.” (Isa. 41:8) Hivyo, hata kifo chenyewe hakiwezi kumtenganisha Yehova na rafiki zake wa karibu. Abrahamu angali hai katika kumbukumbu ya Yehova. (Luka 20:37, 38) Mfano mwingine ni Ayubu. Yehova alizungumza kwa uhakika kumhusu Ayubu katika kusanyiko la malaika wote huko mbinguni. Yehova alimwita Ayubu “mtu mnyoofu na mtimilifu, anayemwogopa Mungu na kuepuka uovu.” (Ayu. 1:6-8) Na Yehova alihisije kumhusu Danieli, ambaye alimtumikia Mungu kwa uaminifu kwa miaka 80 hivi kwenye nchi ya kipagani? Malaika walimhakikishia mara tatu mwanamume huyo aliyezeeka kwamba alikuwa “mwenye thamani sana” mbele za Mungu. (Dan. 9:23; 10:11, 19) Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anatazamia kwa hamu siku atakayowafufua rafiki zake wapendwa ambao wamekufa.—Ayu. 14:15.

Tunaweza kuonyesha kwa njia zipi kwamba tunathamini hazina zisizoonekana? (Tazama fungu la 5) *

5. Tunapaswa kufanya nini ili tufurahie urafiki wa karibu pamoja na Yehova?

5 Ni wanadamu wangapi leo wasio wakamilifu ambao ni marafiki wa karibu wa Yehova? Ni mamilioni ya wanadamu. Tunajua hivyo kwa sababu kuna wanaume, wanawake, na watoto wengi duniani kote wanaothibitisha kupitia matendo yao kwamba wanataka kuwa marafiki wa Mungu. Yehova “ana urafiki wa karibu na watu wanyoofu.” (Met. 3:32) Urafiki huo unawezekana kwa sababu wana imani katika dhabihu ya fidia ya Yesu. Kwa msingi wa dhabihu hiyo, Yehova anatuonyesha fadhili kwa kuturuhusu tujiweke wakfu kwake na kubatizwa. Tunapochukua hatua hizo muhimu, tunajiunga na mamilioni ya Wakristo waliojiweka wakfu na kubatizwa ambao wanafurahia “urafiki wa karibu” pamoja na Mtu mkuu zaidi katika ulimwengu!

6. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunauthamini urafiki wetu pamoja na Mungu?

6 Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunauona urafiki wetu na Mungu kuwa hazina yenye thamani? Kama Abrahamu na Ayubu, ambao waliendelea kuwa waaminifu kwa Mungu kwa zaidi ya miaka mia moja, ni lazima tuendelee kuwa waaminifu—hata iwe tumemtumikia Yehova kwa muda mrefu kadiri gani katika mfumo huu wa zamani. Kama Danieli, ni lazima tuuone urafiki wetu pamoja na Mungu kuwa wenye thamani zaidi kuliko uhai wetu. (Dan. 6:7, 10, 16, 22) Kwa msaada wa Yehova, tunaweza kuvumilia matatizo yoyote tunayokabili na hivyo kuendelea kudumisha urafiki wetu wa karibu pamoja naye.—Flp. 4:13.

ZAWADI YA SALA

7. (a) Kulingana na Methali 15:8, Yehova anahisije kuhusu sala zetu? (b) Yehova hujibuje sala zetu?

7 Hazina nyingine isiyoonekana ni sala. Marafiki wa karibu hupenda kuelezana mawazo na hisia zao. Je, hivyo ndivyo urafiki wetu pamoja na Yehova ulivyo? Ndiyo! Yehova huzungumza nasi kupitia Neno lake, ambamo anatufunulia mawazo na hisia zake. Tunazungumza naye kupitia sala, na tunaweza kumfunulia mawazo na hisia zetu za ndani kabisa. Yehova anafurahia kusikiliza sala zetu. (Soma Methali 15:8.) Akiwa rafiki yetu mwenye upendo, Yehova hasikilizi tu sala zetu, bali pia anazijibu. Nyakati nyingine yeye hutujibu haraka. Nyakati nyingine tunahitaji kuendelea kusali kuhusu jambo fulani. Lakini bado tunaweza kuwa na uhakika kwamba atatujibu kwa wakati unaofaa na kwa njia bora kabisa. Bila shaka, huenda Mungu akatujibu kwa njia ambayo hatukutazamia. Kwa mfano, badala ya kuondoa tatizo fulani, anaweza kutupatia hekima na nguvu za ‘kulivumilia.’—1 Kor. 10:13.

(Tazama fungu la 8) *

8. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunathamini zawadi ya sala?

8 Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunathamini zawadi yenye thamani ya sala? Njia moja ni kwa kutii shauri la Mungu la ‘kusali bila kuacha.’ (1 The. 5:17) Yehova hatulazimishi tusali kwake. Badala yake, anaheshimu uhuru wetu wa kuchagua na anatuhimiza ‘tudumu katika sala.’ (Rom. 12:12) Hivyo, tunaweza kuonyesha kwamba tunaithamini zawadi hiyo kwa kusali kwa ukawaida mara kwa mara kila siku. Na bila shaka, tunapaswa pia kumshukuru na kumsifu Yehova katika sala zetu.—Zab. 145:2, 3.

9. Ndugu mmoja anahisije kuhusu sala, na wewe unahisije kuihusu?

9 Kadiri tunavyomtumikia Yehova kwa muda mrefu na kujionea njia anazotumia kujibu maombi yetu, ndivyo tunavyopaswa kuthamini hata zaidi zawadi ya sala. Fikiria mfano wa Chris, ndugu ambaye amekuwa katika utumishi wa wakati wote kwa miaka 47. Anaeleza hivi: “Inafurahisha sana kuamka asubuhi na mapema ili nitumie wakati fulani kusali kwa Yehova. Inaburudisha sana kuzungumza na Yehova huku miale ya kwanza ya jua ikichomoza na kusababisha umande umetemete! Jambo hilo hunichochea nimshukuru kwa zawadi zake zote, kutia ndani pendeleo la sala. Kisha ninaposali kwake mwishoni mwa siku, ninafurahi sana kwa sababu ninalala nikiwa na dhamiri safi.”

ZAWADI YA ROHO TAKATIFU

10. Kwa nini tunapaswa kuithamini roho takatifu ya Mungu?

10 Nguvu ya utendaji ya Mungu ni zawadi nyingine isiyoonekana tunayopaswa kuithamini. Yesu alituhimiza tuendelee kusali ili tupate roho takatifu. (Luka 11:9, 13) Kupitia roho yake, Yehova hutupatia nguvu, naam, hata “nguvu zinazopita zile za kawaida.” (2 Kor. 4:7; Mdo. 1:8) Kwa msaada wa roho ya Mungu, tunaweza kuvumilia matatizo yoyote tunayokabili.

(Tazama fungu la 11) *

11. Roho takatifu inaweza kutusaidiaje?

11 Roho takatifu inaweza kutusaidia tutimize migawo yetu katika utumishi wa Mungu. Roho ya Mungu inaweza kuboresha au kukuza vipawa na uwezo tulio nao. Inatusaidia tutekeleze majukumu yetu ya Kikristo. Kwa unyoofu tunaweza kusema kwamba mafanikio tunayopata hayatokani na uwezo wetu wenyewe, bali tunapata msaada kutoka kwa roho ya Mungu.

12. Kulingana na Zaburi 139:23, 24, tunaweza kusali ili roho takatifu itusaidie kufanya nini?

12 Njia nyingine tunayoweza kuonyesha kwamba tunaithamini roho takatifu ya Mungu ni kwa kusali ili itusaidie kutambua mawazo au tamaa yoyote isiyofaa ndani ya moyo wetu. (Soma Zaburi 139:23, 24.) Ikiwa tutasali kuhusu jambo hilo, Yehova anaweza kutumia roho yake kutusaidia tutambue mawazo au mwelekeo wowote usiofaa tulio nao. Na tunapotambua kwamba tuna mawazo au tamaa yoyote isiyofaa, tunapaswa kusali ili roho ya Mungu itupatie nguvu ya kupinga mawazo au tamaa hiyo isiyofaa. Kwa njia hiyo, tutaonyesha kwamba tumeazimia kuepuka kufanya jambo lolote ambalo linaweza kumfanya Yehova aache kutusaidia kupitia roho yake takatifu.—Efe. 4:30.

13. Tunaweza kuongezaje kina cha uthamini wetu kwa roho takatifu?

13 Tunaweza kuongeza kina cha uthamini wetu kwa roho takatifu kwa kutafakari kuhusu mambo ambayo roho hiyo imetimiza katika nyakati zetu. Kabla ya Yesu kurudi mbinguni, aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Roho takatifu itakapokuja juu yenu mtapokea nguvu, nanyi mtakuwa mashahidi wangu . . . mpaka sehemu ya mbali zaidi ya dunia.” (Mdo. 1:8) Maneno hayo yanatimizwa kwa njia yenye kustaajabisha leo. Kwa utegemezo wa roho takatifu, waabudu wa Yehova wapatao milioni nane na nusu wamekusanywa kutoka katika kila pembe ya dunia. Pia, tunafurahia paradiso ya kiroho kwa sababu roho ya Mungu inatusaidia tusitawishe sifa maridadi, kama vile, upendo, shangwe, amani, subira, fadhili, wema, imani, upole, na kujizuia. Sifa hizo ndizo zinazofanyiza “tunda la roho.” (Gal. 5:22, 23) Kwa kweli, roho takatifu ni zawadi yenye thamani sana!

UTEGEMEZO TUNAOPATA KUTOKA MBINGUNI ILI KUTIMIZA HUDUMA YETU

14. Tunapata msaada gani tusioweza kuuona tunaposhiriki katika huduma?

14 Tuna hazina isiyoonekana ya ‘kufanya kazi pamoja’ na Yehova, Yesu, na malaika. (2 Kor. 6:1) Tunafanya kazi pamoja nao wakati wowote tunaposhiriki katika huduma. Paulo alisema hivi kujihusu na kuwahusu wale wanaoshiriki kazi hiyo: “Sisi ni wafanyakazi wenzi wa Mungu.” (1 Kor. 3:9) Tunaposhiriki katika huduma ya Kikristo, sisi pia ni wafanyakazi wenzi wa Yesu. Kumbuka kwamba baada ya Yesu kuwaamuru wafuasi wake ‘wakafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote,’ aliwaambia hivi: “Mimi nipo pamoja nanyi.” (Mt. 28:19, 20) Na vipi kuhusu malaika? Tunashukuru sana kwamba malaika wanatuongoza tunapoendelea kutangaza “habari njema ya milele . . . kwa wale wanaokaa duniani”!—Ufu. 14:6.

15. Simulia mfano katika Biblia unaoonyesha fungu muhimu ambalo Yehova anatimiza kuhusiana na huduma yetu.

15 Tunatimiza nini kwa sababu ya utegemezo huo tunaopata kutoka mbinguni? Tunapoendelea kupanda mbegu za ujumbe wa Ufalme, baadhi ya mbegu hizo huanguka kwenye mioyo mizuri na kukua. (Mt. 13:18, 23) Ni nani anayesababisha mbegu hizo za kweli zikue na kuzaa matunda? Yesu anaeleza kwamba hakuna mtu anayeweza kuwa mfuasi wake isipokuwa “Baba . . . amvute.” (Yoh. 6:44) Biblia ina mfano hususa kuhusu jambo hilo. Je, unakumbuka wakati ambapo Paulo aliwatolea ushahidi kikundi cha wanawake waliokuwa nje ya jiji la Filipi? Ona kile ambacho Biblia inasema kumhusu Lidia, aliyekuwa miongoni mwa wanawake hao: “Yehova akaufungua moyo wake wazi ili asikilize kwa makini mambo ambayo Paulo alikuwa akisema.” (Mdo. 16:13-15) Kama Lidia, mamilioni ya watu wamevutwa na Yehova.

16. Ni nani anayepaswa kutukuzwa tunapopata mafanikio yoyote katika huduma?

16 Ni nani kwa kweli anayestahili kutukuzwa tunapopata mafanikio yoyote katika huduma? Paulo alijibu swali hilo alipoliandikia hivi kutaniko la Korintho: “Mimi nilipanda, Apolo akatia maji, lakini Mungu akaendelea kuikuza, hivi kwamba anayepanda si kitu wala anayetia maji, bali Mungu anayeikuza.” (1 Kor. 3:6, 7) Kama Paulo, sikuzote tunapaswa kumtukuza Yehova tunapopata mafanikio yoyote katika huduma.

17. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunathamini ‘kufanya kazi pamoja’ na Mungu, Kristo, na malaika?

17 Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunalithamini pendeleo la ‘kufanya kazi pamoja’ na Yehova, Yesu, na malaika? Tunaweza kufanya hivyo kwa kutafuta kwa bidii fursa za kuwaambia wengine habari njema. Kuna njia nyingi za kufanya hivyo, kama vile kwa kutoa ushahidi “hadharani na nyumba kwa nyumba.” (Mdo. 20:20) Ndugu na dada wengi pia hufurahia kuhubiri isivyo rasmi. Wanapokutana na mtu wasiyemjua, wao humsalimu kwa urafiki na kujaribu kuanzisha mazungumzo pamoja naye. Ikiwa mtu huyo anaitikia vizuri, wao huzungumzia pamoja naye ujumbe wa Ufalme kwa njia ya busara.

(Tazama fungu la 18) *

18-19. (a) Tunatiaje maji mbegu za kweli? (b) Simulia kisa kinachoonyesha jinsi Yehova alivyomsaidia mwanafunzi mmoja wa Biblia.

18 Tukiwa “wafanyakazi wenzi wa Mungu,” hatupaswi tu kupanda mbegu za kweli bali pia tunapaswa kuzitia maji. Mtu anapoonyesha kwamba anapendezwa, tunataka kufanya yote tunayoweza ili kufuatia upendezi huo, au kufanya mipango na mtu mwingine ili aweze kuwasiliana na mtu huyo, lengo likiwa kuanzisha funzo la Biblia. Mtu huyo anapoendelea kujifunza Biblia, tunashangilia tunapoona jinsi Yehova anavyofinyanga moyo na akili yake.

19 Mfikirie Raphalalani, mganga wa kienyeji kutoka Afrika Kusini. Alipenda mambo aliyojifunza katika funzo lake la Biblia. Lakini ilikuwa vigumu kwake kukubaliana na mambo ambayo Neno la Mungu linasema kuhusu kuwasiliana na mababu waliokufa. (Kum. 18:10-12) Hatua kwa hatua, alimruhusu Mungu afinyange njia yake ya kufikiri. Na baada ya muda, aliacha kazi yake ya uganga wa kienyeji, ingawa hilo lilimaanisha kupoteza kazi iliyokuwa ikimruzuku. Raphalalani, ambaye sasa ana umri wa miaka 60, anaeleza hivi: “Ninawashukuru sana Mashahidi wa Yehova kwa kunisaidia katika njia nyingi sana, kama vile kunisaidia kupata kazi. Zaidi ya yote, ninamshukuru sana Yehova kwa kunisaidia nisafishe maisha yangu, hivi kwamba sasa ninaweza kushiriki katika huduma nikiwa mmoja wa Mashahidi wake waliobatizwa.”

20. Umeazimia kufanya nini?

20 Katika makala hii, tumechunguza hazina nne zisizoonekana kwa macho. Hazina kubwa kati ya zote ni pendeleo la kuwa marafiki wa karibu zaidi wa Yehova. Tunapokuwa marafiki wa karibu wa Yehova, tunaweza kufaidika kutokana na hazina nyingine ambazo hatuzioni kwa macho. Kwa mfano, tunaweza kusali kwa Yehova, tunaweza kujionea jinsi roho yake takatifu inavyotusaidia, na tunaweza kupata msaada kutoka mbinguni ili tutimize huduma yetu. Acheni tuazimie kuimarisha kina cha uthamini wetu kwa hazina hizo zisizoonekana kwa macho. Na tusiache kamwe kumshukuru Yehova kwa kuwa Rafiki yetu bora.

WIMBO 145 Ahadi ya Mungu ya Paradiso

^ fu. 5 Katika makala iliyotangulia, tulizungumzia hazina kadhaa kutoka kwa Mungu zinazoonekana kwa macho. Katika makala hii tutakazia kuhusu hazina ambazo hatuwezi kuziona kwa macho na jinsi tunavyoweza kuonyesha kwamba tunazithamini. Pia, makala hii itaongeza uthamini wetu kwa Yehova Mungu ambaye ndiye Chanzo cha hazina hizo.

^ fu. 58 MAELEZO YA PICHA: (1) Dada anatafakari kuhusu urafiki wake pamoja na Yehova, huku akifurahia uumbaji wa Yehova.

^ fu. 60 MAELEZO YA PICHA: (2) Dada huyohuyo anasali kwa Yehova ampe nguvu ya kutoa ushahidi.

^ fu. 62 MAELEZO YA PICHA: (3) Roho takatifu inamsaidia dada huyo apate ujasiri wa kutoa ushahidi isivyo rasmi.

^ fu. 64 MAELEZO YA PICHA: (4) Dada huyo anajifunza Biblia na mtu ambaye alimhubiria isivyo rasmi. Dada huyo anafanya kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi kwa msaada wa malaika.