Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, mafunjo yalitumika kutengeneza mashua nyakati za Biblia?

Mmea wa mafunjo

INAJULIKANA sana kwamba mafunjo yalitumiwa sana kutengeneza karatasi za kuandikia katika Misri ya kale. Wagiriki na pia Waroma waliandika kwenye mafunjo. * Hata hivyo, watu wengi hawajui kwamba mafunjo yalitumiwa pia kutengeneza mashua.

Mashua mbili za mafunjo zilizopatikana kwenye makaburi ya Wamisri

Zaidi ya miaka 2,500 iliyopita, nabii Isaya aliandika kwamba watu walioishi “katika eneo la mito ya Ethiopia” waliwatuma “wajumbe kupitia baharini, wanaovuka maji katika vyombo vya mafunjo.” Baadaye, nabii Yeremia alitabiri kwamba jiji la Babiloni litakapovamiwa na Wamedi na Waajemi, wangeteketeza “mashua za mafunjo” za Wababiloni ili wasitoroke.—Isa. 18:1, 2; Yer. 51:32.

Biblia imeongozwa na roho ya Mungu, hivyo wanafunzi wa Biblia hawashangai wavumbuzi wa vitu vya kale wanapopata vitu vinavyoonyesha kwamba mafunjo yalitumika kutengeneza mashua katika nyakati za Biblia. (2 Tim. 3:16) Ni mambo gani yamegunduliwa? Wavumbuzi wa vitu vya kale wamegundua habari nyingi zinazothibitisha kwamba mashua zilitengenezwa kwa mafunjo nchini Misri.

MASHUA ZA MAFUNJO ZILITENGENEZWAJE?

Kwenye makaburi ya Wamisri, kuna picha zilizochorwa na kuchongwa zinazoonyesha watu wakikusanya mafunjo na kutengenezea mashua. Watu wangekata mashina ya mafunjo, kuyafunga kwenye matita, kisha matita hayo yanafungwa pamoja. Mashina ya mafunjo yana umbo la pembe tatu. Hivyo, yanapofungwa pamoja, mashina hayo yanafanyiza fundo gumu na imara. Kulingana na kitabu A Companion to Ancient Egypt, mashua za mafunjo zingeweza kuwa na urefu wa zaidi ya futi 55 (meta 17), na kuwa na makasia 10 au 12 kila upande.

Picha ya Wamisri inayoonyesha jinsi mashua za mafunjo zilivyotengenezwa

KWA NINI WATENGENEZA MASHUA WALITUMIA MAFUNJO?

Mafunjo yalipatikana katika Bonde la Mto Nile. Zaidi ya hilo, ilikuwa rahisi kutengeneza mashua za mafunjo. Hata wakati mbao zilipoanza kutumiwa zaidi kutengeneza mashua kubwa, inaonekana wavuvi na wawindaji waliendelea kutumia mitumbwi na mashua ndogo za mafunjo.

Mashua za mafunjo ziliendelea kutumiwa kwa muda mrefu. Kulingana na mwandishi Mgiriki Plutarch, aliyeishi kati ya karne ya kwanza na karne ya pili W.K., mitumbwi ya mafunjo ilikuwa inajulikana wakati huo.

^ fu. 3 Mimea ya mafunjo inasitawi kwenye ardhi yenye majimaji na kwenye maji yasiyotembea kwa kasi. Mmea huo unaweza kuwa na urefu wa meta 5 (futi 16), na shina linaweza kuwa na upana wa sentimeta 15 (inchi 6) mahali linapoanzia.