Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SIMULIZI LA MAISHA

“Nimejifunza Mambo Mengi Kutoka kwa Wengine!”

“Nimejifunza Mambo Mengi Kutoka kwa Wengine!”

ULIKUWA usiku wenye giza nene kwenye milima ya Algeria, ambako kikosi cha wanajeshi wa Ufaransa kilikuwa kimepiga kambi, na vita nchini Algeria ilikuwa imepamba moto. Nilikuwa peke yangu na bunduki mkononi kwenye eneo la lindo nyuma ya mifuko ya mchanga iliyorundikwa pamoja. Ghafla, kimya kikaisha na nikasikia sauti za hatua zikinikaribia. Nikaogopa na kusimama tuli. Nilikuwa nimefikisha tu umri wa miaka ishirini na sikutaka kuua au kuuawa. Hivyo, nikamlilia Mungu anisaidie!

Tukio hilo lenye kutisha lilibadili maisha yangu kwa sababu tangu wakati huo nilianza kumtafuta Muumba. Lakini kabla sijawasimulia mambo yaliyotokea baadaye katika usiku huo wenye giza nene, nitawaeleza kuhusu malezi yangu ya utotoni yaliyoathiri njia yangu ya kufikiri, na kuutayarisha moyo wangu ili kumtafuta Mungu.

MAMBO NILIYOJIFUNZA KUTOKA KWA BABA YANGU

Nilizaliwa mwaka wa 1937, kwenye mji wenye migodi wa Guesnain, huko Kaskazini mwa Ufaransa. Nilijifunza umuhimu wa kufanya kazi kwa bidii kutoka kwa baba yangu aliyekuwa mchimba makaa ya mawe. Pia, nilijifunza kupenda haki kutoka kwake, kwa sababu alikuwa akiwatetea wachimbaji waliofanya kazi kwenye mazingira duni. Ili kuwasaidia kuboresha hali zao, Baba alijiunga kwenye vyama vya wafanyakazi na kushiriki kwenye migomo. Pia, alikasirishwa na unafiki wa makasisi. Wengi wao waliishi maisha ya anasa; lakini bado waliomba chakula na pesa kutoka kwa wachimba madini ambao walikuwa wanapambana ili kupata mahitaji yao ya kila siku. Baba alikasirishwa sana na tabia hiyo ya makasisi hivi kwamba hakunifundisha chochote kuhusu dini. Isitoshe, kamwe hatukuzungumzia chochote kumhusu Mungu.

Nilipoendelea kukua, mimi pia nilianza kuchukia ukosefu wa haki. Ukosefu huo wa haki ulitia ndani ubaguzi dhidi ya wageni walioishi nchini Ufaransa. Nilikuwa nikicheza mpira wa miguu na watoto wa wahamiaji na nilifurahia ushirika wao. Isitoshe, mama yangu hakuwa Mfaransa, alitoka Poland. Nilitamani sana kuwe na usawa na kusiwe na ubaguzi.

NILIANZA KUFIKIRIA KWA UZITO ZAIDI KUHUSU MAISHA

Nilipokuwa jeshini

Niliandikishwa jeshini mwaka wa 1957. Hivyo ndivyo nilivyojikuta kwenye milima ya Algeria katika usiku wenye giza nene nilioutaja awali. Baada ya kumlilia Mungu ili anisaidie, nilikutana uso kwa uso, si na mwanajeshi adui, bali punda wa porini! Nilishukuru sana! Lakini bado tukio hilo, na vita yenyewe, ilinifanya nifikirie kwa uzito zaidi kuhusu kusudi la maisha. Kwa nini tuko hapa duniani? Je, Mungu anatujali? Je, tutawahi kupata amani ya kudumu?

Baadaye, nilipokuwa nimewatembelea wazazi wangu, nilikutana na Shahidi wa Yehova. Alinipatia nakala ya La Sainte Bible, Biblia ya Kikatoliki iliyotafsiriwa katika Kifaransa, ambayo nilianza kuisoma baada ya kurudi nchini Algeria. Andiko lililonigusa sana ni Ufunuo 21:3, 4. Linasema hivi: “Hema la Mungu liko pamoja na wanadamu . . . Naye atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.” * Maneno hayo yalinishangaza sana. Nilijiuliza, ‘Je, maneno hayo yanaweza kuwa ya kweli?’ Wakati huo, nilikuwa sijui chochote kumhusu Mungu na Biblia.

Nilipomaliza utumishi wangu wa kijeshi mwaka wa 1959, nilikutana na Shahidi aliyeitwa François aliyenifundisha kweli nyingi za Biblia. Kwa mfano, alinionyesha katika Biblia kwamba Mungu ana jina la kibinafsi, Yehova. (Zab. 83:13). Pia, François alinieleza kwamba Yehova ataleta haki duniani, atabadili dunia kuwa paradiso, na kutimiza maneno ya Ufunuo 21:3, 4.

Mafundisho hayo yalipatana na akili na yaligusa moyo wangu. Lakini pia, niliwakasirikia sana makasisi na nilitaka kuwashutumu kwa kufundisha mambo ambayo hayapo kwenye Biblia! Inaonekana kwamba bado nilikuwa nimeathiriwa na maoni ya baba yangu, na sikuwa na subira. Nilitaka kusuluhisha mambo haraka!

François na marafiki wangu wengine ambao ni Mashahidi walinisaidia kutuliza hasira yangu. Walinieleza kwamba kazi yetu tukiwa Wakristo si kuhukumu, bali kutoa tumaini kupitia habari njema za Ufalme wa Mungu. Hiyo ndiyo kazi ambayo Yesu alifanya na aliyowapatia wafuasi wake waifanye. (Mt. 24:14; Luka 4:43) Pia, nilihitaji kujifunza kuzungumza na watu kwa fadhili na busara, haidhuru imani yao. Biblia inasema: “Mtumwa wa Bwana hahitaji kupigana, bali anahitaji kuwa mpole kwa wote.”—2 Tim. 2:24.

Nilifanya mabadiliko yanayohitajiwa na nilibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova mwaka wa 1959 kwenye kusanyiko la mzunguko. Kusanyikoni nilikutana na dada kijana anayeitwa Angèle, ambaye nilivutiwa naye. Nilianza kutembelea kutaniko alilokuwa akihudhuria, na tukafunga ndoa mwaka wa 1960. Ni mwanamke bora, mke wa pekee, na zawadi yenye thamani kutoka kwa Yehova.—Met. 19:14.

Siku ya ndoa yetu

NILIJIFUNZA MAMBO MENGI KUTOKA KWA WANAUME WENYE HEKIMA NA UZOEFU

Kwa miaka mingi, nimejifunza mambo mengi muhimu kutoka kwa wanaume wenye hekima na uzoefu. Jambo muhimu zaidi kati ya mambo niliyojifunza ni: Ili tufanikiwe katika mgawo wowote wenye changamoto, tunahitaji kuwa wanyenyekevu na kutumia ushauri wenye hekima unaopatikana katika andiko la Methali 15:22, linalosema: “Mambo hufanikiwa kupitia washauri wengi.”

Nilipokuwa nikizungukia makutaniko nchini Ufaransa, 1965

Mwaka wa 1964, nilianza kujionea ukweli wa maneno hayo yaliyoongozwa na roho ya Mungu. Mwaka huo, nilianza kutumikia nikiwa mwangalizi wa mzunguko nikitembelea makutaniko ili kuwatia moyo akina ndugu na kuwaimarisha kiroho. Hata hivyo, nilikuwa na umri wa miaka 27 wakati huo na sikuwa na uzoefu. Hivyo, nilifanya makosa mengi. Lakini nilijitahidi kujifunza kutokana na makosa hayo. Zaidi ya yote, nilijifunza mambo mengi muhimu kutoka kwa “washauri” wenye uwezo na wazoefu.

Ninakumbuka kisa kimoja kilichotokea baada tu ya kuwekwa kuwa mwangalizi. Baada ya kutembelea kutaniko moja jijini Paris, ndugu fulani aliye mkomavu kiroho aliniomba tuzungumze faraghani. Nikamwambia, “Sawa.”

Aliniuliza hivi, “Louis, daktari humsaidia nani, mgonjwa au mtu mwenye afya?”

Nikamjibu, “Mgonjwa.”

Akasema: “Ni kweli. Lakini nimegundua kwamba unatumia muda wako mwingi na wale ambao hali yao ya kiroho ni nzuri, kama vile mwangalizi wa kutaniko. Kutaniko letu lina ndugu na dada wengi ambao wamevunjika moyo, ni wapya, au wenye haya. Watathamini sana ikiwa utatumia muda pamoja nao, hata kwenda nyumbani kwao kwa ajili ya mlo.”

Shauri la ndugu huyo mpendwa lilifaa na nililithamini sana. Upendo wake kwa kondoo za Yehova uligusa moyo wangu. Ingawa haikuwa rahisi kukubali kwamba nilikosea, mara moja nilianza kutumia ushauri alionipatia. Ninamshukuru Yehova kwa ndugu kama hao.

Mwaka wa 1969 na 1973, nilipewa mgawo wa kusimamia Idara ya Huduma ya Chakula kwenye makusanyiko mawili ya kimataifa yaliyofanywa Colombes, Paris. Kwenye kusanyiko la mwaka 1973, watu 60,000 hivi walihitaji kulishwa chakula kwa siku tano! Nilihofu sana, sikujua ningetimizaje jukumu hilo. Lakini kwa mara nyingine tena, ili nifanikiwe nilihitaji kutumia kanuni ya Methali 15:22—kutafuta ushauri kutoka kwa wenye hekima. Nilitafuta ushauri kutoka kwa wanaume walio wakomavu kiroho ambao walikuwa na uzoefu katika masuala ya chakula. Walitia ndani wauza nyama, wakulima wa mboga, wapishi, na wanunuzi. Kwa pamoja, tulifaulu kutimiza mgawo uliokuwa kama mlima.

Mwaka wa 1973, mimi na mke wangu tulialikwa kutumikia katika Betheli ya Ufaransa. Mgawo wangu wa kwanza pia haukuwa rahisi. Nilihitaji kuwapelekea machapisho ndugu zetu waliokuwa Kamerun, nchi iliyoko Afrika, ambako kazi yetu ilikuwa imepigwa marufuku kati ya mwaka wa 1970 na 1973. Kwa mara nyingine tena, nilihisi nimelemewa. Huenda akiwa ametambua hilo, ndugu aliyekuwa akisimamia kazi nchini Ufaransa alinitia moyo, akisema: “Ndugu zetu nchini Kamerun wana uhitaji mkubwa wa chakula cha kiroho. Tunahitaji kuwalisha!” Na kwa kweli tuliwalisha.

Kwenye mkutano wa pekee nchini Nigeria pamoja na Mashahidi kutoka Kamerun, 1973

Nilifanya safari kadhaa kwenye nchi zinazopakana na Kamerun ili kukutana na wazee wa makutaniko kutoka katika nchi hiyo. Wanaume hao jasiri na wenye busara walinisaidia kufanya mipango iliyohitajika ili kupeleka kwa ukawaida chakula cha kiroho nchini Kamerun. Yehova alibariki jitihada zetu. Isitoshe, kwa miaka ishirini hivi, watu wake katika nchi hiyo hawakuwahi kukosa hata toleo moja la gazeti la Mnara wa Mlinzi na chapisho la kila mwezi la wakati huo lililoitwa Utumishi Wetu wa Ufalme.

Mwaka wa 1977, mimi na Angèle tulifurahia kwenda Nigeria ili kuwatembelea waangalizi wa mzunguko na wake zao waliotoka Kamerun

NILIJIFUNZA MAMBO MENGI KUTOKA KWA MKE WANGU MPENDWA

Tangu mwanzoni mwa uchumba wetu nilitambua sifa nzuri za kiroho za Angèle. Sifa hizo zimeonekana wazi katika maisha yetu ya ndoa. Isitoshe, jioni ileile ya siku yetu ya harusi, aliniomba nisali kuhusu tamaa yetu ya kumtumikia Yehova kikamili tukiwa wenzi wa ndoa. Yehova alijibu sala hiyo.

Pia, Angèle amenisaidia kumtumaini kikamili zaidi Yehova. Kwa mfano, mwaka wa 1973 tulipoalikwa tukatumikie Betheli, nilisita kwa sababu nilipenda kazi ya kuzungukia makutaniko. Lakini Angèle alinikumbusha kwamba tulikuwa tumeweka wakfu maisha yetu kwa Yehova. Je, hatupaswi kufanya chochote ambacho tengenezo lake linatuambia tufanye? (Ebr. 13:17) Ningewezaje kupinga hilo? Hivyo, tukaenda Betheli. Katika kipindi chote cha maisha yetu pamoja, busara, utimamu wa akili, na mtazamo wa kiroho wa mke wangu umeimarisha ndoa yetu na kutusaidia kufanya maamuzi mazuri.

Nikiwa na Angèle katika bustani ya Betheli ya Ufaransa

Ingawa umri wetu umesonga, Angèle ameendelea kuwa mke bora anayenisaidia sana. Kwa mfano, ili tuhudhurie shule za kitheokrasi ambazo nyingi zinafanywa kwa Kiingereza, mimi na Angèle tulijitahidi kuboresha Kiingereza chetu. Hilo lilihusisha kujiunga na kutaniko la Kiingereza, hata ingawa tulikuwa na umri wa miaka 75 hivi. Kwa sababu ya majukumu yangu nikiwa mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Ufaransa, kujifunza lugha nyingine ilikuwa changamoto. Lakini mimi na Angèle tulisaidiana. Na sasa tuna miaka 80 hivi na tunaendelea kuandaa mikutano kwa Kiingereza na Kifaransa. Pia, tunajitahidi kushiriki mara nyingi kadiri tunavyoweza katika mikutano na huduma pamoja na kutaniko letu. Yehova amebariki jitihada zetu za kujifunza Kiingereza.

Tulipata baraka moja ya pekee mwaka wa 2017. Mimi na Angèle tulipata pendeleo la kuhudhuria Shule ya Washiriki wa Halmashauri ya Tawi na Wake Zao, inayofanyika kwenye Kituo cha Elimu cha Watchtower Patterson, New York.

Kwa kweli Yehova ndiye Mfundishaji Mkuu. (Isa. 30:20) Hivyo haishangazi kwamba watu wake—wazee kwa vijana—wanapata elimu bora zaidi! (Kum. 4:5-8) Kwa kweli, nimejionea kwamba vijana wanaomsikiliza Yehova na ndugu na dada wenye uzoefu huwa na maendeleo mazuri kiroho na kuwa watu wazima waliofanikiwa. Methali 9:9 inatukumbusha hivi: “Mfundishe mwenye hekima, naye atazidi kuwa na hekima. Mfundishe mwadilifu, naye atazidi kuelimika.”

Pindi fulani, ninakumbuka ule usiku wenye kutisha kwenye milima ya Algeria miaka  60 hivi iliyopita. Usiku huo sikujua kwamba ningekuja kuwa na maisha mazuri hivi. Nimejifunza mambo mengi sana kutoka kwa wengine! Kwa kweli, Yehova ametupatia mimi na Angèle maisha yenye kuthawabisha na kuridhisha. Hivyo, tumeazimia kutoacha kujifunza kutoka kwa Baba yetu wa mbinguni na kutoka kwa ndugu na dada wenye uzoefu na hekima ambao wanampenda.

^ fu. 11 Biblia TakatifuTafsiri ya Ulimwengu Mpya.