Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 22

Endelea Kutembea Katika “Njia ya Utakatifu”

Endelea Kutembea Katika “Njia ya Utakatifu”

“Huko kutakuwa na barabara kuu, . . . Njia ya Utakatifu.”—ISA. 35:8.

WIMBO 31 Tembea Pamoja na Mungu!

MUHTASARI a

1-2. Ni uamuzi gani muhimu ambao Wayahudi walioishi Babiloni walihitaji kufanya? (Ezra 1:2-4)

 MFALME Koreshi alikuwa ametoa agizo! Wayahudi ambao walikuwa mateka huko Babiloni kwa miaka 70 hivi, walikuwa huru kurudi katika nchi yao, Israeli. (Soma Ezra 1:2-4.) Ni Yehova tu ambaye angeweza kutimiza jambo hilo. Kwa nini tunaweza kusema hivyo? Kwa kawaida Wababiloni hawakuwaweka huru mateka wao. (Isa. 14:4, 17) Lakini Babiloni lilikuwa limeshindwa, na mtawala mpya alikuwa amewaambia Wayahudi kwamba wangeweza kurudi katika nchi yao. Matokeo ni kwamba kila Myahudi, hasa vichwa vya familia, walihitaji kufanya uamuzi huu: kuondoka Babiloni au kuendelea kuishi huko. Huo haukuwa uamuzi rahisi. Kwa nini?

2 Kwa wengi waliozeeka, huenda ingekuwa vigumu kufunga safari hiyo. Na kwa kuwa Wayahudi wengi walikuwa wamezaliwa huko Babiloni, waliona nchi hiyo kuwa nyumbani kwao. Walihisi kwamba nchi ya Israeli ilikuwa nchi ya babu zao. Inaonekana kwamba baadhi ya Wayahudi walikuwa wamepata utajiri huko Babiloni, kwa hiyo huenda ilikuwa vigumu kwao kuacha nyumba zao zenye kustarehesha au biashara zao na kuanza kuishi kwenye nchi wasiyofahamu.

3. Wayahudi waaminifu ambao wangerudi katika nchi ya Israeli wangepata baraka gani?

3 Wayahudi waaminifu walijua kwamba ikiwa wangerudi katika nchi ya Israeli wangepata baraka nyingi kuliko jambo lolote ambalo wangedhabihu. Baraka kuu zaidi ilihusiana na ibada yao. Ingawa kulikuwa na zaidi ya mahekalu 50 ya kipagani huko Babiloni, hakukuwa na hekalu la Yehova katika jiji hilo. Hakukuwa na madhabahu ambayo Waisraeli wangetoa dhabihu zilizotajwa katika Sheria ya Musa, na hakukuwa na mpango wa makuhani ambao wangetoa dhabihu hizo. Isitoshe watumishi wa Yehova walikuwa wachache kwa kulinganishwa na idadi kubwa sana ya watu ambao waliabudu miungu ya uwongo, na ambao hawakumheshimu Yehova na viwango vyake. Basi, maelfu ya Wayahudi waliomwogopa Mungu, walitazamia kwa hamu kurudi katika nchi yao ambako wangerudisha ibada safi.

4. Ni msaada gani ambao Yehova aliahidi kuwapa Wayahudi waliokuwa wanarudi Israeli?

4 Safari ngumu kutoka Babiloni kwenda Israeli ingechukua miezi minne hivi, lakini Yehova aliahidi kwamba kizuizi chochote ambacho kingeonekana kuwa kinazuia safari hiyo kingeondolewa. Isaya aliandika hivi: “Fungueni njia ya Yehova! Tengenezeni barabara kuu iliyonyooka inayopitia jangwani kwa ajili ya Mungu wetu. . . . Na ardhi yenye mashimo-mashimo itasawazishwa, na ardhi yenye mawemawe itakuwa bonde tambarare.” (Isa. 40:3, 4) Wazia hali hiyo: barabara kuu inayopita jangwani na bonde tambarare lililosawazishwa. Wasafiri wangefurahia sana kupita katika barabara hiyo! Ingekuwa rahisi zaidi kwao kusafiri katika barabara kuu iliyonyooka, badala ya kupanda na kushuka au kuzunguka milima, vilima, au mabonde. Na ingechukua muda mfupi zaidi.

5. Barabara kuu ya mfano kati ya Babiloni na Israeli ilipewa jina gani?

5 Leo, barabara nyingi kuu zina majina au namba. Barabara kuu ya mfano ambayo Isaya aliandika kuihusu pia ilikuwa na jina. Aliandika hivi: “Huko kutakuwa na barabara kuu, naam, njia inayoitwa Njia ya Utakatifu. Mtu asiye safi hatasafiri kwenye njia hiyo.” (Isa. 35:8) Ahadi hiyo ilimaanisha nini kwa Waisraeli wakati huo? Na inamaanisha nini kwetu leo?

“NJIA YA UTAKATIFU”​—ZAMANI NA LEO

6. Kwa nini barabara hiyo iliitwa takatifu?

6 “Njia ya Utakatifu”​—ni jina maridadi sana la barabara kuu! Kwa nini barabara hiyo iliitwa takatifu? Mtu yeyote “asiye safi” hangeruhusiwa kuwa katika taifa la Israeli lililorudishwa, yaani, Myahudi yeyote ambaye alikuwa ameazimia kujihusisha katika ukosefu wa maadili, ibada ya sanamu, au dhambi nyingine nzito hangeruhusiwa. Wayahudi waliorudi katika nchi yao walipaswa kuwa “watu watakatifu” kwa Mungu wao. (Kum. 7:6) Hata hivyo, hilo halikumaanisha kwamba Wayahudi hao waliotoka Babiloni hawakuhitaji kufanya mabadiliko ili kumfurahisha Yehova.

7. Baadhi ya Wayahudi walihitaji kufanya mabadiliko gani? Toa mfano.

7 Kama ilivyotajwa mwanzoni, Wayahudi wengi walizaliwa huko Babiloni, na inaonekana kwamba wengi wao walikuwa wameathiriwa na njia ya kufikiri na mazoea ya Wababiloni. Miaka mingi baada ya kikundi cha kwanza cha Wayahudi kurudi Israeli, Ezra alitambua kwamba baadhi ya Wayahudi walikuwa wameoa wanawake wa kipagani. (Kut. 34:15, 16; Ezra 9:1, 2) Baadaye, Gavana Nehemia alishangaa alipotambua kwamba watoto ambao walikuwa wamezaliwa huko Israeli, hata hawakuwa wamejifunza lugha ya Kiyahudi. (Kum. 6:6, 7; Neh. 13:23, 24) Watoto hao wangewezaje kujifunza kumpenda na kumwabudu Yehova ikiwa hawangeweza kuelewa Kiebrania—lugha kuu ambayo ilitumiwa kuandika Neno la Mungu? (Ezra 10:3, 44) Basi, Wayahudi hao walihitaji kufanya mabadiliko makubwa, lakini ingekuwa rahisi zaidi kwao kufanya mabadiliko hayo wakiwa huko Israeli, ambako ibada safi ilikuwa inarudishwa hatua kwa hatua.​—Neh. 8:8, 9.

Tangu mwaka wa 1919 W.K., mamilioni ya wanaume, wanawake, na watoto wametoka katika Babiloni Mkubwa na wameanza kutembea kwenye “Njia ya Utakatifu.” (Tazama fungu la 8)

8. Kwa nini mambo yaliyotukia muda mrefu uliopita ni muhimu kwetu leo? (Tazama picha kwenye jalada.)

8 Huenda wengine wakasema hivi, ‘Mambo hayo yote yanasisimua, lakini je, mambo ambayo yaliwapata Wayahudi walioishi muda mrefu uliopita yana maana yoyote kwetu leo? Kwa kweli yana maana, kwa sababu kwa njia fulani, sisi tunatembea katika “Njia ya Utakatifu.” Iwe sisi ni watiwa-mafuta au ni “kondoo wengine,” tunapaswa kuendelea kutembea katika “Njia ya Utakatifu” inapotupitisha kwenye paradiso ya kiroho na kutuongoza kwenye baraka za wakati ujao katika Ufalme wa Mungu. b (Yoh. 10:16) Tangu mwaka wa 1919 W.K., mamilioni ya wanaume, wanawake, na watoto wametoka katika Babiloni Mkubwa, milki ya ulimwenguni pote ya dini za uwongo, na wameanza kutembea katika barabara hiyo ya mfano. Inaelekea kwamba wewe ni mmoja wao. Ingawa watu walianza kutembea katika barabara hiyo miaka 100 hivi iliyopita, kazi ya kutayarisha barabara hiyo kuu ilianza karne nyingi zilizopita.

KUITAYARISHA ILE BARABARA

9. Kulingana na Isaya 57:14, ni matayarisho gani ambayo yamekuwa yakifanywa kwenye “Njia ya Utakatifu”?

9 Wayahudi walipokuwa wakitoka Babiloni, Yehova alihakikisha kwamba vizuizi vyote viliondolewa. (Soma Isaya 57:14.) Namna gani “Njia ya Utakatifu” katika siku zetu? Kwa karne nyingi kabla ya mwaka wa 1919, Yehova alitumia wanaume waliokuwa wanamwogopa Mungu kutayarisha njia ya kutoka katika Babiloni Mkubwa. (Linganisha Isaya 40:3.) Walifanya matayarisho muhimu—kutengeneza barabara ya kiroho—ili kufanya baadaye iwezekane kwa watu wenye mioyo minyoofu kutoka katika Babiloni Mkubwa na kuingia katika paradiso ya kiroho, ambako ibada safi ya Yehova ilikuwa imerudishwa. Kazi hiyo ya “kutengeneza barabara” ilihusisha nini? Fikiria baadhi ya matayarisho yaliyofanywa.

Kwa karne nyingi, wanaume waliomwogopa Mungu walisaidia kutayarisha njia ya kuondoka katika Babiloni Mkubwa (Tazama fungu la 10 na 11)

10-11. Kuchapishwa na kutafsiriwa kwa Biblia kumechangiaje kuenea kwa ujuzi wa Biblia? (Tazama pia picha.)

10 Uchapishaji. Kufikia katikati ya karne ya 15, Biblia ilikuwa inanakiliwa kwa mkono. Kazi hiyo ilichukua muda mrefu, na nakala za Biblia zilikuwa chache na za bei ghali. Lakini mashine ya kuchapisha kurasa ilipovumbuliwa, sasa ilikuwa rahisi zaidi kutokeza na kusambaza Biblia.

11 Kutafsiri. Kwa karne nyingi, Biblia ilipatikana hasa katika lugha ya Kilatini, ambayo ingeweza kueleweka hasa na watu wenye elimu. Lakini kazi ya uchapishaji ilipozidi kuenea, watu waliomwogopa Mungu waliongeza bidii ya kutafsiri Biblia katika lugha zilizozungumzwa na watu wa kawaida. Sasa wasomaji wa Biblia wangeweza kulinganisha mambo ambayo makasisi walikuwa wakiwafundisha na kile ambacho hasa Biblia ilikuwa inafundisha.

Wanaume waliomwogopa Mungu walisaidia kutayarisha njia ya kuondoka katika Babiloni Mkubwa (Tazama fungu la 12 hadi 14) c

12-13. Toa mfano wa jinsi wanafunzi wanyoofu wa Biblia katika karne ya 19 walivyoanza kufunua mafundisho ya uwongo ya kidini.

12 Machapisho ya kujifunzia Biblia. Wale waliojifunza Biblia kwa makini, walijifunza mengi kutokana na yale waliyosoma katika Neno la Mungu. Lakini makasisi walikasirika kwa sababu wanafunzi hao wa Biblia walianza kuwaambia wengine mambo waliyojifunza. Kwa mfano, katika karne ya 19, baadhi ya wanaume wanyoofu walianza kuchapisha trakti ambazo zilifunua mafundisho ya uwongo ya kidini yaliyofundishwa katika makanisa.

13 Karibu mwaka wa 1835, Henry Grew, mwanamume aliyemwogopa Mungu alichapisha trakti iliyozungumzia hali ya wafu. Katika trakti hiyo, alithibitisha kutoka katika Maandiko kwamba kutoweza kufa ni zawadi kutoka kwa Mungu, na si hali ambayo sisi sote tunazaliwa tukiwa nayo, kama makanisa mengi yalivyofundisha. Mwaka wa 1837, mhudumu wa kidini aliyeitwa George Storrs alipata nakala ya trakti hiyo alipokuwa akisafiri kwenye garimoshi. Aliisoma na akasadiki kwamba alikuwa ameupata ukweli muhimu. Aliamua kuwaambia watu wengine mambo aliyojifunza. Mwaka wa 1842 alitoa mfululizo wa hotuba zilizokuwa na kichwa hiki chenye kusisimua, “Uchunguzi—Je, Waovu Wana Hali ya Kutoweza Kufa?” Maandishi ya George Storrs yalimchochea mwanamume kijana aliyeitwa Charles Taze Russell.

14. Ni kwa njia gani Ndugu Russell na wale walioshirikiana pamoja naye walinufaika na kazi ya kutengeneza barabara ya kiroho iliyofanywa kabla ya wakati wao? (Tazama pia picha.)

14 Ni kwa njia gani Ndugu Russell na wale walioshirikiana naye walinufaika na kazi ambayo ilikuwa imefanywa mapema ya kutengeneza barabara ya kiroho? Walipokuwa wakijifunza, walichunguza kamusi za Biblia, konkodansi, na tafsiri mbalimbali za Biblia, na machapisho hayo yote yalikuwa yametayarishwa kabla wao hawajaanza kazi yao. Pia, walinufaika na utafiti wa Biblia ambao ulikuwa umefanywa na wanaume kama vile Henry Grew, George Storrs, na wengine. Ndugu Russell na wale walioshirikiana pamoja naye walichangia katika kazi ya kutengeneza barabara hiyo ya kiroho kwa kutokeza kwa wingi vitabu na trakti zilizozungumzia Biblia.

15. Ni jambo gani muhimu lililotokea mwaka wa 1919?

15 Mwaka wa 1919, watu wa Mungu waliwekwa huru kutoka katika Babiloni Mkubwa. Mwaka huo, “mtumwa mwaminifu na mwenye busara” alianza kufanya kazi ili watu wenye mioyo minyoofu waanze kutembea katika ‘Njia hiyo mpya ya Utakatifu’ iliyofunguliwa. (Mt. 24:45-47) Kazi iliyofanywa na “watengeneza-barabara” waliotangulia, iliwasaidia wale walioanza kutembea katika barabara hiyo kuu wajifunze mengi zaidi kumhusu Yehova na makusudi yake. (Met. 4:18) Pia, wangeweza kupatanisha maisha yao na viwango vya Yehova. Yehova hakutarajia watu wake wafanye marekebisho yote yaliyohitajika kwa wakati mmoja. Badala yake, amekuwa akiwasafisha watu wake hatua kwa hatua. (Tazama sanduku “ Yehova Anawasafisha Watu Wake Hatua kwa Hatua.”) Tutafurahi sana wakati ambapo tutaweza kumfurahisha Mungu wetu katika kila jambo tunalofanya!—Kol. 1:10.

“NJIA YA UTAKATIFU” BADO IKO WAZI

16. Tangu mwaka wa 1919, ni kazi gani ya udumishaji ambayo imekuwa ikifanywa katika “Njia ya Utakatifu”? (Isaya 48:17; 60:17)

16 Kila barabara inahitaji kudumishwa kwa ukawaida. Tangu mwaka wa 1919, kazi ya kutengeneza “Njia ya Utakatifu” imekuwa ikiendelea, ili kufanya iwezekane kwa watu wengi zaidi kuondoka katika Babiloni Mkubwa. Baada ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara kuwekwa rasmi alianza kazi, na mwaka wa 1921, walichapisha kitabu cha kujifunzia Biblia kilichokusudiwa kuwasaidia wapya wajifunze kweli za Biblia. Mwishowe, nakala milioni sita hivi za kitabu hicho, The Harp of God, zilichapishwa katika lugha 36, na kuwasaidia wengi wajifunze kweli. Hivi karibuni, tumepata chapisho zuri la kuongoza mafunzo ya Biblia, Furahia Maisha Milele! Katika kipindi chote cha siku za mwisho, Yehova ametumia tengenezo lake kuendelea kuandaa chakula cha kiroho ili kutusaidia sisi sote tuendelee kutembea katika “Njia ya Utakatifu.”​—Soma Isaya 48:17; 60:17.

17-18. “Njia ya Utakatifu” inaongoza wapi?

17 Tunaweza kusema kwamba kila mara mtu anapokubali kujifunza Biblia, anapata nafasi ya kutembea katika “Njia ya Utakatifu.” Baada ya kutembea kwa muda mfupi, baadhi yao huacha kutembea katika barabara hiyo kuu. Wengine wameazimia kuendelea kutembea katika barabara hiyo hadi watakapofika mwisho wa safari yao. Mwisho huo wa safari ni nini?

18 Kwa wale ambao wana tumaini la kwenda mbinguni, “Njia ya Utakatifu” inaongoza kwenye “paradiso ya Mungu” huko mbinguni. (Ufu. 2:7) Kwa wale walio na tumaini la kuishi duniani, barabara hiyo kuu itaongoza kwenye ukamilifu mwishoni mwa ile miaka 1,000. Ikiwa leo unatembea katika barabara hiyo kuu, usitazame nyuma. Na usiondoke kwenye barabara hiyo hadi utakapomaliza safari yako na kuingia katika ulimwengu mpya! Tunakutakia “safari njema.”

WIMBO 24 Njooni Kwenye Mlima wa Yehova

a Yehova aliita barabara ya mfano iliyotoka Babiloni kwenda Israeli kuwa “Njia ya Utakatifu.” Katika nyakati zetu, je, pia Yehova amewatayarishia watu wake njia? Ndiyo! Tangu mwaka wa 1919 W.K., mamilioni ya watu wametoka katika Babiloni Mkubwa na wameanza kutembea kwenye “Njia ya Utakatifu.” Sisi sote tunapaswa kuendelea kutembea katika barabara hiyo mpaka tufike mwisho wa safari yetu.

b Tazama kitabu Unabii wa Isaya—Nuru kwa Wanadamu Wote II, uku. 56-57.

c MAELEZO YA PICHA: Ndugu Russell na wale walioshirikiana naye walitumia machapisho ya kujifunzia Biblia yaliyokuwa yametayarishwa kabla ya wakati wao.