Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 24

Unaweza Kutimiza Malengo Yako ya Kiroho

Unaweza Kutimiza Malengo Yako ya Kiroho

“Tusife moyo katika kufanya mema, kwa maana kwa wakati unaofaa tutavuna ikiwa hatutachoka kabisa.”​—GAL. 6:9.

WIMBO 84 Tumejitoa Kutumikia

MUHTASARI a

1. Wengi wetu tumekabili changamoto gani?

 JE, UMEWAHI kujiwekea lengo la kiroho lakini ukashindwa kulitimiza? b Ikiwa ndivyo, huko peke yako. Kwa mfano, Philip alitaka kuboresha sala zake na kusali mara nyingi zaidi, lakini ilikuwa vigumu kupata muda wa kusali. Erika alikuwa na lengo la kufika kwa wakati kwenye mkutano wa utumishi wa shambani, lakini alichelewa karibu kila mkutano. Tomáš alijaribu mara kadhaa kusoma Biblia nzima. Anasema hivi: “Sikufurahia kusoma Biblia. Nilijaribu mara tatu, lakini kila mara nilipofika kwenye kitabu cha Mambo ya Walawi sikuendelea na usomaji.”

2. Kwa nini hatupaswi kuvunjika moyo ikiwa tuna lengo la kiroho ambalo bado hatujalitimiza?

2 Ikiwa kuna lengo ambalo umeshindwa kulitimiza, usife moyo. Mara nyingi unahitaji muda na jitahidi nyingi ili kutimiza hata lengo rahisi. Kwa kuwa bado unatamani kutimiza lengo lako, hilo linaonyesha kwamba unathamini uhusiano wako pamoja na Yehova na unataka kumpa kilicho bora. Yehova anathamini jitihada zako. Bila shaka, hatarajii ufanye mambo yanayopita uwezo wako. (Zab. 103:14; Mika 6:8) Basi, unapaswa kuwa mwenye usawaziko unapojiwekea lengo, ukizingatia hali zako. Baada ya kujiwekea lengo kama hilo, unaweza kufanya nini ili kulitimiza? Acheni tuzungumzie baadhi ya mapendekezo.

KICHOCHEO NI MUHIMU

Sali ili upate kichocheo zaidi (Tazama fungu la 3 na 4)

3. Kwa nini kichocheo ni muhimu?

3 Ni muhimu sana kuwa na motisha au kichocheo ili kutimiza malengo ya kiroho. Mtu mwenye kichocheo ana sababu nzuri sana ya kutimiza lengo lake au anatamani kujitahidi kulitimiza. Tunaweza kulinganisha kichocheo na upepo unaosukuma mashua kuelekea kule inakoenda. Ikiwa upepo utaendelea kuvuma, inaelekea baharia atafika mwisho wa safari yake. Na ikiwa upepo unavuma kwa nguvu, huenda atafika upesi zaidi. Vivyo hivyo, ikiwa tunachochewa zaidi, ndivyo itakavyokuwa rahisi zaidi kutimiza malengo yetu. David, ndugu kutoka El Salvador anasema hivi: “Unapohisi umechochewa, unajitahidi hata zaidi. Unajitahidi kutoruhusu jambo lolote likuzuie kutimiza lengo lako.” Basi, unaweza kufanya nini ili uhisi umechochewa zaidi?

4. Tunaweza kumwomba Mungu atupatie nini? (Wafilipi 2:13) (Tazama pia picha.)

4 Sali ili upate kichocheo zaidi. Kupitia roho yake takatifu, Yehova anaweza kukuchochea kutimiza lengo lako. (Soma Wafilipi 2:13.) Nyakati nyingine tunajiwekea lengo kwa sababu tunajua tunapaswa kufanya hivyo, na hilo ni jambo zuri. Lakini huenda kwa kweli tusiwe na tamaa ya kutimiza lengo hilo. Hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa Dada Norina, anayeishi nchini Uganda. Alijiwekea lengo la kuongoza funzo la Biblia, lakini alikosa kichocheo kwa sababu alihisi kwamba hakuwa mwalimu mzuri. Ni nini kilichomsaidia? Anasema hivi: “Nilianza kumwomba Yehova kila siku anisaidie kuongeza tamaa yangu ya kuongoza funzo la Biblia. Na kulingana na sala zangu, nilijitahidi kuboresha uwezo wangu wa kufundisha. Baada ya miezi kadhaa, nilitambua kwamba tamaa yangu ilikuwa imeongezeka. Mwaka huohuo, nilianzisha mafunzo mawili ya Biblia.”

5. Tunaweza kutafakari kuhusu nini ili tuchochewe zaidi?

5 Tafakari kuhusu mambo ambayo Yehova amekufanyia. (Zab. 143:5) Mtume Paulo alitafakari kuhusu fadhili zisizostahiliwa ambazo Yehova alimwonyesha, na hilo lilimchochea kufanya kazi ya Yehova kwa bidii. (1 Kor. 15:9, 10; 1 Tim. 1:12-14) Vivyo hivyo, kadiri unavyotafakari mambo ambayo Yehova amekufanyia, ndivyo utakavyochochewa zaidi kutimiza lengo lako. (Zab. 116:12) Fikiria jambo ambalo lilimsaidia dada mmoja nchini Honduras atimize lengo lake la kuwa painia wa kawaida. Anasema hivi: “Nilitafakari jinsi Yehova anavyonipenda sana. Alinisaidia kujiunga na watu wake. Ananijali na kunilinda. Kutafakari mambo hayo kuliimarisha upendo wangu kwake na kunichochea hata zaidi.”

6. Ni jambo gani lingine linaloweza kutusaidia tuchochewe zaidi?

6 Kazia fikira baraka za kutimiza lengo lako. Ona jambo lililomsaidia Erika, aliyetajwa mwanzoni atimize lengo lake la kufika kwa wakati. Anasema hivi: “Nilitambua kwamba nilikuwa ninakosa mengi sana kwa kuchelewa kwenda kwenye huduma. Lakini kwa kufika mapema, ningeweza kuwasalimu akina ndugu na dada na kutumia muda pamoja nao. Pia, ningeweza kusikiliza mapendekezo muhimu ambayo yangenisaidia kufurahia na kuboresha huduma yangu.” Erika alikazia fikira manufaa ya kufika kwa wakati, na akatimiza lengo lake. Unaweza kukazia fikira baraka gani? Ikiwa lengo lako linahusu kusoma Biblia au kusali, fikiria jinsi litakavyokusaidia kuimarisha urafiki wako pamoja na Yehova. (Zab. 145:18, 19) Ikiwa lengo lako ni kusitawisha sifa fulani ya Kikristo, kazia fikira jinsi sifa hiyo itakavyokusaidia kuboresha uhusiano wako pamoja na wengine. (Kol. 3:14) Kwa nini usiandike orodha ya sababu zote zinazokufanya utamani kutimiza lengo lako? Chunguza orodha hiyo tena na tena. Tomáš, aliyenukuliwa awali, anasema hivi: “Kadiri nilivyo na sababu nyingi zaidi za kutimiza lengo langu, ndivyo ninavyojitahidi zaidi kulitimiza.”

7. Ni nini kilichomsaidia Julio na mke wake kutimiza lengo lao?

7 Tumia muda pamoja na wale ambao watakuchochea. (Met. 13:20) Ona jambo lililomsaidia Julio na mke wake kutimiza lengo lao la kupanua huduma yao. Anasema hivi: “Tulichagua marafiki ambao waliunga mkono lengo letu, na tulizungumzia lengo letu pamoja nao. Tayari wengi wao walikuwa wametimiza malengo kama hayo, basi waliweza kutupatia mapendekezo muhimu. Pia, rafiki zetu walituuliza jinsi mipango yetu ilivyokuwa inaendelea, na wakatutia moyo wakati tulipohitaji.”

TUNAPOKOSA KICHOCHEO

Jitahidi kutimiza lengo lako (Tazama fungu la 8)

8. Itakuwaje ikiwa tutafanyia kazi lengo letu wakati tu tunapohisi tumechochewa? (Tazama pia picha.)

8 Hata hivyo, ukweli ni kwamba kuna wakati ambapo sisi sote hukosa kichocheo. Je, hilo linamaanisha kwamba hatuwezi kujitahidi kutimiza lengo letu? Hapana. Kwa mfano, upepo unaweza kuwa kichocheo chenye nguvu kinachosukuma mashua kuelekea kule inakoenda. Hata hivyo, nguvu za upepo hubadilika-badilika, katika baadhi ya siku huenda kusiwe na upepo wowote. Je, hilo linamaanisha kwamba baharia hataendelea na safari? Si lazima iwe hivyo. Kwa mfano, baadhi ya mashua zina mota, na nyingine zina makasia. Baharia anaweza kutumia vitu hivyo ili azidi kusonga. Kichocheo chetu kinaweza kulinganishwa na upepo; huenda wakati mwingine kitapungua. Na katika baadhi ya siku, huenda tusiwe na kichocheo cha kutimiza lengo letu. Basi, ikiwa tutajitahidi tu kufanyia kazi lengo letu tunapohisi tumechochewa, huenda tusitimize kamwe lengo letu. Lakini kama vile tu baharia anavyotafuta njia nyingine za kuendelea na safari, bado tunaweza kufanyia kazi lengo letu hata tunapokosa kichocheo. Ingawa huenda isiwe rahisi kufanya hivyo, tutapata matokeo mazuri. Kabla ya kuzungumzia mambo tunayoweza kufanya, acheni tujibu swali ambalo huenda likajitokeza.

9. Je, inafaa kuendelea kufanyia kazi lengo fulani hata ikiwa hatutamani kufanya hivyo? Eleza.

9 Yehova anataka tumtumikie kwa furaha na kwa hiari. (Zab. 100:2; 2 Kor. 9:7) Hivyo je, bado tunapaswa kufanyia kazi lengo la kiroho ikiwa hatuna tamaa ya kufanya hivyo? Fikiria mfano wa mtume Paulo. Alisema hivi: “Ninaupigapiga mwili wangu na kuuongoza kama mtumwa.” (1 Kor. 9:25-27) Paulo alijilazimisha kufanya jambo lililofaa hata alipokosa tamaa ya kufanya hivyo. Je, Yehova alifurahishwa na utumishi wa Paulo? Bila shaka! Na Yehova alimbariki kwa sababu ya jitihada zake.​—2 Tim. 4:7, 8.

10. Tunanufaikaje tunapoendelea kufanyia kazi lengo letu hata tunapokosa kichocheo?

10 Vivyo hivyo, Yehova anafurahi kuona tukifanyia kazi lengo letu hata ikiwa hatuna tamaa ya kufanya hivyo. Anafurahi kwa sababu ingawa hatufanyi kila mara jambo hilo kwa sababu tunalipenda, anajua kwamba tunalifanya kwa sababu tunampenda yeye. Kama vile Yehova alivyombariki Paulo, atabariki jitihada zetu pia. (Zab. 126:5) Na tunapoona baraka za Yehova, huenda tukachochewa zaidi. Dada kutoka Poland anayeitwa Lucyna anasema hivi: “Wakati mwingine ninakosa hamu ya kwenda kwenye utumishi wa shambani, hasa ikiwa nimechoka. Ingawa hivyo, shangwe ninayopata baada ya kwenda kwenye utumishi ni zawadi yenye kustaajabisha.” Basi, acheni tuone mambo tunayoweza kufanya tunapokosa kichocheo.

11. Yehova anawezaje kutusaidia kuimarisha uwezo wetu wa kujizuia?

11 Sali ili upate sifa ya kujizuia. Sifa ya kujizuia inamaanisha uwezo wa kudhibiti hisia na matendo yetu. Mara nyingi sifa hiyo hutokeza wazo la kujizuia ili tusifanye jambo baya. Hata hivyo, pia tunahitaji sifa ya kujizuia ili tuchochewe kufanya mambo mazuri, hasa ikiwa jambo tunalofanya ni gumu au tumekosa kichocheo. Kumbuka, sifa ya kujizuia ni sehemu ya tunda la roho, basi mwombe Yehova akupatie roho takatifu ili ikusaidie kusitawisha sifa hiyo muhimu. (Luka 11:13; Gal. 5:22, 23) David, aliyetajwa awali, anaeleza jinsi sala ilivyomsaidia. Alitamani kujifunza kibinafsi kwa ukawaida zaidi. Anasema hivi: “Nilikuwa nikimwomba Yehova anisaidie kusitawisha sifa ya kujizuia. Kwa msaada wake, nilifaulu kuwa na ratiba nzuri ya kujifunza na kufanya hivyo kwa ukawaida.”

12. Kanuni iliyo kwenye Mhubiri 11:4, inahusianaje na malengo ya kiroho?

12 Usisubiri mpaka hali ziwe nzuri kabisa. Katika ulimwengu huu, inaelekea kwamba hatutakuwa kamwe na hali zinazofaa kabisa. Ikiwa tutasubiri hali zinazofaa, huenda tusitimize kamwe lengo letu. (Soma Mhubiri 11:4.) Ndugu anayeitwa Dayniel anasema hivi: “Huwezi kupata hali bora kabisa. Tunatengeneza hali bora tunapoanza kufanya kazi.” Ndugu kutoka Uganda anayeitwa Paul alitaja sababu nyingine inayoonyesha kwa nini hatupaswi kuahirisha mambo: “Tunapofanya jambo licha ya changamoto, tunampa Yehova sababu ya kutubariki.”​—Mal. 3:10.

13. Kuna manufaa gani ya kuanza na malengo madogo?

13 Anza na mambo madogo. Huenda tukakosa kichocheo kwa sababu inaonekana kwamba ni vigumu sana kutimiza lengo letu. Ikiwa unakabili hali hiyo, je, unaweza kugawa lengo lako ili liwe malengo madogo-madogo? Ikiwa una lengo la kusitawisha sifa fulani, kwa nini usianze kujitahidi kuionyesha kwa njia ndogo? Ikiwa lengo lako ni kusoma Biblia nzima, je, unaweza kuanza kwa kupanga vipindi vifupi zaidi vya kusoma? Tomáš, aliyetajwa awali, alikabili changamoto katika lengo lake la kusoma Biblia nzima kwa mwaka mmoja. Anasema hivi: “Nilitambua kwamba nilikuwa nimechagua mwendo wa kusoma wa kasi kuliko uwezo wangu. Basi niliamua kujaribu tena, lakini wakati huu, nilipanga kusoma mafungu machache kila siku na kutafakari kuyahusu. Matokeo ni kwamba nilianza kufurahia usomaji wangu.” Tomáš alipozidi kufurahia, alianza kusoma kwa vipindi virefu zaidi. Mwishowe, aliisoma Biblia nzima. c

USIVUNJWE MOYO NA VIPINGAMIZI

14. Huenda tukakabili vipingamizi gani?

14 Inasikitisha kwamba hata tuwe tumechochewa au tuna nidhamu kadiri gani, bado huenda tutakabili vipingamizi vinavyofanya iwe vigumu kufikia malengo yetu. Kwa mfano, “matukio yasiyotarajiwa” yanaweza kuchukua muda tunaohitaji ili tufanyie kazi lengo letu. (Mhu. 9:11) Huenda tukakabili hali ngumu ambayo itatuacha tukiwa tumevunjika moyo na kuishiwa nguvu. (Met. 24:10) Kwa kuwa hatajukamilika, huenda tukafanya makosa ambayo yatafanya iwe vigumu kutimiza lengo letu. (Rom. 7:23) Au huenda tukahisi tu kwamba tumechoka. (Mt. 26:43) Ni nini kinachoweza kutusaidia kushinda vipingamizi au hali ngumu?

15. Tunapokabili kipingamizi, je, hilo linamaanisha kwamba tumeshindwa? Eleza. (Zaburi 145:14)

15 Kumbuka, kipingamizi hakimaanishi kwamba umeshindwa. Biblia inasema kwamba huenda tukakabili tena na tena matatizo au hali ngumu. Hata hivyo, pia inataja wazi kwamba tunaweza kusimama tena, hasa kwa msaada wa Yehova. (Soma Zaburi 145:14.) Ndugu anayeitwa Philip, aliyetajwa awali, anatumia njia ifuatayo kupima mafanikio yake, anasema hivi: “Mafanikio yangu hayategemei mara ambazo nimeanguka. Badala yake, yanategemea mara ambazo nimesimama tena na kuendelea.” David, aliyenukuliwa awali, anasema hivi: “Ninajitahidi kuona vipingamizi au hali ngumu, si kama vizuizi, bali kama nafasi za kumwonyesha Yehova jinsi ninavyompenda sana.” Naam, ukisonga mbele licha ya vipingamizi, unamthibitishia Yehova kwamba unataka kumfurahisha. Bila shaka, Yehova anafurahi sana anapoona ukijitahidi kutimiza lengo lako!

16. Tunaweza kujifunza nini tunaposhindwa kutimiza lengo?

16 Ona kipingamizi kuwa fursa ya kujifunza. Fikiria jambo lililosababisha kipingamizi hicho kikuzuie kutimiza lengo lako, na ujiulize hivi: ‘Je, kuna jambo ambalo ninaweza kubadilisha ili niepuke kipingamizi kingine?’ (Met. 27:12) Lakini ikiwa wakati mwingine ni vigumu sana kwako kutimiza lengo lako, huenda ulijiwekea lengo ambalo huwezi kutimiza. Ikiwa unahisi kwamba hali iko hivyo kuhusu lengo lako, chunguza tena lengo hilo ili uone kama kweli wewe unaweza kulitimiza. d Yehova hataona kwamba umeshindwa kwa kukosa kutimiza lengo ambalo linapita uwezo wako.​—2 Kor. 8:12.

17. Kwa nini tunapaswa kukumbuka mambo ambayo tayari tumetimiza?

17 Kumbuka mambo ambayo tayari umetimiza. Biblia inasema hivi: “Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi [yako].” (Ebr. 6:10) Basi wewe pia hupaswi kusahau. Fikiria kuhusu mambo ambayo tayari umetimiza—iwe ni kusitawisha urafiki pamoja na Yehova, kuwaambia wengine kumhusu, au kubatizwa. Kama vile ulivyofanya maendeleo na kutimiza malengo ya kiroho wakati uliopita, unaweza kuendelea kufanya maendeleo ili kutimiza lengo lako sasa.​—Flp. 3:16.

Furahia safari (Tazama fungu la 18)

18. Tunapaswa kukumbuka kufanya nini tunapojitahidi kutimiza lengo letu? (Tazama pia picha.)

18 Kwa msaada wa Yehova unaweza kutimiza lengo lako, kama vile tu baharia anavyofurahia kufika mwisho wa safari yake. Lakini kumbuka kwamba mabaharia wengi pia hufurahia safari yenyewe. Vivyo hivyo, unapoendelea kufanyia kazi lengo lako la kiroho, usisahau kufurahia kuona jinsi Yehova anavyokusaidia na kukubariki unapojitahidi kutimiza lengo lako. (2 Kor. 4:7) Usipokufa moyo, utapata baraka kubwa hata zaidi.​—Gal. 6:9.

WIMBO 126 Uwe Macho, Simama Imara, Uwe na Nguvu

a Mara kwa mara tunatiwa moyo tujiwekee malengo ya kiroho. Vipi ikiwa tayari tumejiwekea lengo linalofaa lakini tunashindwa kulitimiza? Makala hii itazungumzia mapendekezo mbalimbali yanayoweza kutusaidia kutimiza malengo yetu.

b UFAFANUZI WA MANENO: Lengo la kiroho linaweza kutia ndani jambo lolote unalojitahidi kuboresha au kutimiza ili umtumikie Yehova kikamili zaidi na kumfurahisha. Kwa mfano, unaweza kujiwekea lengo la kusitawisha sifa fulani ya Kikristo au kuboresha sehemu fulani ya ibada yako, kama vile kusoma Biblia, kujifunza kibinafsi, au huduma ya shambani.

c Tazama kitabu Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, uku. 10-11, fu. 4.

d Kwa habari zaidi, ona makala “Uwe na Matarajio Yenye Usawaziko, na Uwe Mwenye Shangwe” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Julai 15, 2008.