Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Endeleeni Kutiana Moyo Kila Siku

Endeleeni Kutiana Moyo Kila Siku

“Ikiwa kuna neno lolote la kitia moyo mlilo nalo kwa ajili ya watu, lisemeni.”—MDO. 13:15.

NYIMBO: 121, 45

1, 2. Eleza kwa nini ni muhimu kuwatia moyo wengine.

“SI KAWAIDA kwa wazazi wangu kunitia moyo, wao hunichambua sana. Na maneno yao yanachoma sana. Wanasema kwamba mimi hujiendesha kama mtoto, siwezi kukomaa, na kwamba mimi ni mnene. Kwa hiyo, mimi hulia mara kwa mara na kuamua kutozungumza nao. Mimi huhisi kwamba sifai.” Hayo ni maneno ya Cristina, mwenye umri wa miaka 18. [1] Maisha bila kitia moyo yanaweza kuwa yenye kuhuzunisha sana!

2 Kwa upande mwingine, tunapowatia moyo wengine tunawachochea kufanya maendeleo. Rubén anasema hivi: “Nimepambana na hisia za kujiona sifai kwa miaka mingi. Lakini siku moja, nilikuwa nikihubiri na mzee mmoja wa kutaniko na alitambua kwamba sikuwa na furaha. Nilipomweleza hisia zangu, alinisikiliza kwa huruma. Kisha akanikumbusha mambo mazuri ambayo mimi hutimiza. Alinikumbusha pia maneno ya Yesu kwamba kila mmoja wetu ni bora kuliko shomoro wengi. Mimi hukumbuka andiko hilo mara nyingi, na bado linanigusa moyo. Maneno ya mzee huyo yalinitia moyo sana.”—Mt. 10:31.

3. (a) Mtume Paulo alisema nini kuhusu kutiana moyo? (b) Tutachunguza nini katika makala hii?

3 Hatupaswi kushangaa kwamba Biblia inakazia umuhimu wa kuwatia moyo wengine kwa ukawaida. Mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo Waebrania: “Jihadharini, akina ndugu, ili moyo mwovu unaokosa imani usije ukasitawi ndani ya yeyote kati yenu kwa kujiondoa kwa Mungu aliye hai; lakini endeleeni kuhimizana kila siku, . . . ili yeyote kati yenu asije akafanywa kuwa mgumu kwa nguvu za udanganyifu za dhambi.” (Ebr. 3:12, 13) Ikiwa uliwahi kuchochewa na maneno ya kitia moyo kutoka kwa mtu fulani, bila shaka unajua umuhimu wa shauri la kuendelea kuhimizana, au kutiana moyo. Kwa hiyo, acheni tuchunguze maswali haya: Kwa nini ni muhimu kutiana moyo? Tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Yehova, Yesu, na Paulo walivyowatia moyo wengine? Na tunaweza kuwatiaje moyo wengine kwa njia itakayowagusa moyo?

SOTE TUNAHITAJI KITIA MOYO

4. Ni nani wanaohitaji kitia moyo, lakini kwa nini si rahisi kupata kitia moyo leo?

4 Sisi sote tunahitaji kitia moyo. Watoto hasa wanahitaji kutiwa moyo wanapoendelea kukua. Mwalimu mmoja anayeitwa Timothy Evans, anaeleza hivi: “Watoto . . . wanahitaji kutiwa moyo kama ambavyo mimea inahitaji maji. Mtoto anapotiwa moyo anahisi kwamba anathaminiwa.” Hata hivyo, tunaishi katika nyakati za hatari. Watu ni wenye ubinafsi, hawana upendo wa asili, na ni wachache sana ambao huwatia moyo wengine. (2 Tim. 3:1-5) Baadhi ya wazazi hawawapongezi watoto wao kwa kuwa wao wenyewe hawakuwa wakipongezwa na wazazi wao. Vilevile, wafanyakazi wengi leo hawapongezwi na hivyo wanalalamika kwamba hakuna anayemtia moyo mwenzake kazini.

5. Kitia moyo kinahusisha nini?

5 Mara nyingi, kitia moyo kinahusisha kumpongeza mtu kwa jambo zuri alilofanya. Tunaweza pia kuwatia moyo wengine kwa kuwahakikishia kwamba wana sifa nzuri, na kwa “kuzifariji nafsi zilizohuzunika.” (1 The. 5:14) Neno la Kigiriki linalotafsiriwa “kitia moyo,” linamaanisha “kumwita mtu aje upande wako.” Tunapotumikia pamoja na ndugu na dada zetu, tunaweza kupata fursa nyingi za kusema jambo lenye kutia moyo. (Soma Mhubiri 4:9, 10.) Je, tunatumia pindi zinazofaa kuwaambia wengine kwa nini tunawapenda na kuwathamini? Kabla ya kujibu swali hilo, ni vizuri tufikirie andiko hili: “Neno linalosemwa wakati unaofaa ni jema kama nini!”—Met. 15:23.

6. Kwa nini Ibilisi angependa kutuvunja moyo? Toa mfano.

6 Shetani Ibilisi angependa kutuvunja moyo kwa sababu anajua tunapovunjika moyo uhusiano wetu na Yehova unaweza kudhoofika. Methali 24:10 inasema hivi: “Je, umejionyesha kuwa umevunjika moyo siku ya taabu? Nguvu zako zitakuwa chache.” Shetani alitumia misiba na mashtaka ya uwongo kumvunja moyo mwanamume mwadilifu Ayubu, lakini njama hizo za kikatili hazikufanikiwa. (Ayu. 2:3; 22:3; 27:5) Tunaweza kushinda kazi za Ibilisi kwa kuwatia moyo washiriki wa familia zetu na ndugu na dada kutanikoni. Hilo litafanya tuhisi tukiwa wenye furaha na salama tunapokuwa nyumbani na katika Jumba la Ufalme.

MIFANO YA KUIGA KUHUSU KUWATIA MOYO WENGINE

7, 8. (a) Ni mifano gani katika Biblia inayoonyesha kwamba Yehova anaona kuwatia moyo wengine kuwa jambo muhimu? (b) Wazazi wanaweza kufanya nini ili kuiga mfano wa Yehova? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

7 Yehova. Mtunga zaburi aliimba hivi: “Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; naye huwaokoa wale waliopondwa roho.” (Zab. 34:18) Wakati fulani Yeremia alipoogopa na kuvunjika moyo, Yehova alimsaidia nabii huyo mwaminifu kupata tena ujasiri. (Yer. 1:6-10) Na hebu wazia jinsi nabii Danieli aliyekuwa amezeeka alivyotiwa moyo Mungu alipotuma malaika kumwimarisha. Malaika huyo alimwita Danieli “mtu mwenye kutamanika sana!” (Dan. 10:8, 11, 18, 19) Je, wewe pia unaweza kuwatia moyo wahubiri, mapainia, na ndugu na dada zetu waliozeeka ambao nguvu zao zimepungua na wamevunjika moyo?

8 Mungu hakuhisi kwamba kwa kuwa yeye na Mwana wake mpendwa walifanya kazi wakiwa pamoja kwa miaka mingi, hakukuwa na uhitaji wa kumpongeza au kumtia moyo alipokuwa duniani. Badala yake, katika pindi mbili, Yesu alimsikia Baba yake akizungumza kutoka mbinguni akisema hivi: “Huyu ni Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.” (Mt. 3:17; 17:5) Kwa kufanya hivyo, Mungu alimpongeza Yesu na kumhakikishia kwamba alifurahishwa na mambo aliyokuwa akitimiza. Bila shaka, Yesu alitiwa moyo aliposikia maneno hayo, kwanza mwanzoni mwa huduma yake na katika mwaka wake wa mwisho duniani. Pia, Yehova alimtuma malaika ili amtie nguvu Yesu alipokuwa katika maumivu makali usiku kabla ya kifo chake. (Luka 22:43) Ikiwa sisi ni wazazi, acheni tufuate mfano wa Yehova kwa kuwatia moyo watoto wetu kwa ukawaida na kuwapongeza wanapofanya mambo mazuri. Tunapaswa pia kuwasaidia hata zaidi utimilifu wao unapojaribiwa siku baada ya siku wakiwa shuleni.

9. Tunaweza kujifunza nini kutokana na jinsi Yesu alivyowatendea mitume wake?

9 Yesu. Usiku ambao alianzisha Ukumbusho wa kifo chake, Yesu alitambua kwamba bado mitume wake walikuwa na kiburi. Kwa unyenyekevu, Yesu aliwaosha miguu, lakini waliendelea kubishana kuhusu ni nani kati yao aliyekuwa mkuu zaidi; naye Petro alijiamini kupita kiasi. (Luka 22:24, 33, 34) Hata hivyo, bado Yesu aliwapongeza mitume wake kwa kushikamana naye wakati wa majaribu. Alitabiri kwamba wangefanya kazi kubwa kuliko alizofanya, na akawahakikishia kwamba Mungu anawapenda. (Luka 22:28; Yoh. 14:12; 16:27) Ikiwa tuna watoto, tunaweza kujiuliza hivi: ‘Je, sipaswi kumwiga Yesu kwa kuwapongeza watoto wangu na watu wengine kwa mambo mazuri wanayotimiza badala ya kukazia fikira udhaifu wao?’

10, 11. Mtume Paulo alionyeshaje kwamba aliona umuhimu wa kuwatia moyo wengine?

10 Mtume Paulo. Katika barua zake, Paulo aliwasifu sana Wakristo wenzake. Alisafiri na baadhi yao kwa miaka mingi na bila shaka alijua udhaifu wao, lakini bado alisema mambo mazuri kuwahusu. Kwa mfano, Paulo alisema kwamba Timotheo alikuwa “mtoto [wake] mpendwa na mwaminifu katika Bwana,” ambaye angejali kwa unyoofu mambo ya Wakristo wenzake. (1 Kor. 4:17; Flp. 2:19, 20) Mtume huyo alimsifu Tito alipoandikia kutaniko la Korintho kwa kumwita “mshiriki pamoja nami na mfanyakazi mwenzangu kwa ajili ya faida yenu.” (2 Kor. 8:23) Bila shaka, Timotheo na Tito walitiwa moyo sana walipojua maoni ya Paulo kuwahusu!

11 Paulo na Barnaba walihatarisha uhai wao kwa kurudi mara kadhaa katika miji ambayo walishambuliwa. Kwa mfano, walirudi Listra ili wawatie moyo wanafunzi wapya wabaki katika imani ingawa walikabili upinzani mkali wakiwa huko. (Mdo. 14:19-22) Huko Efeso, Paulo alikabili umati wenye hasira. Andiko la Matendo 20:1, 2 linasema hivi: “Sasa baada ya ghasia . . . kutulia, Paulo akatuma watu wawaite wanafunzi, na alipokuwa amewatia moyo na kuwaaga, akasafiri na kuingia Makedonia. Baada ya kupitia sehemu hizo na kuwatia moyo wale walio huko kwa maneno mengi, akaingia Ugiriki.” Ni wazi kwamba Paulo aliona kuwatia moyo wengine kuwa jambo muhimu sana.

TUTIANE MOYO

12. Mikutano yetu inatusaidiaje kuendelea kutiana moyo?

12 Kwa fadhili, Baba yetu wa mbinguni ametuandalia mikutano ili tutiane moyo. (Soma Waebrania 10:24, 25.) Kama wafuasi wa mapema wa Yesu walivyokuwa wakifanya, sisi pia hukutana pamoja ili kujifunza na kutiwa moyo. (1 Kor. 14:31) Cristina, aliyetajwa mwanzoni mwa makala hii, anasema hivi: “Jambo ninalopenda zaidi kuhusu mikutano ni upendo na kitia moyo ninachopata nikiwa huko. Nyakati nyingine, mimi huwa nimeshuka moyo ninapofika kwenye Jumba la Ufalme. Lakini akina dada hunisalimu, hunikumbatia, na kuniambia kwamba ninapendeza. Wao huniambia kwamba wananipenda na wanapendezwa na maendeleo yangu ya kiroho. Kitia moyo chao hunifanya nijihisi vizuri sana!” Inaburudisha sana kila mmoja wetu anapotimiza sehemu yake katika “ubadilishanaji wa kitia-moyo”!—Rom. 1:11, 12.

13. Kwa nini watumishi wakomavu wa Mungu wanahitaji kutiwa moyo?

13 Hata watumishi wakomavu wa Mungu wanahitaji kutiwa moyo. Mfikirie Yoshua. Alikuwa amemtumikia Mungu kwa uaminifu kwa miaka mingi. Lakini bado Yehova alimwambia Musa amtie moyo, aliposema hivi: “Nawe umpe Yoshua utume na kumtia moyo na kumwimarisha, kwa maana yeye ndiye atakayevuka mbele ya watu hawa naye ndiye atakayewafanya warithi nchi utakayoiona.” (Kum. 3:27, 28) Yoshua alikuwa karibu kuanza mgawo mzito wa kuwaongoza Waisraeli kupigana na adui zao ili wamiliki Nchi ya Ahadi. Angekabili changamoto mbalimbali, zilizohusisha kushindwa vitani angalau katika pigano moja. (Yos. 7:1-9) Haishangazi kwamba Yoshua alihitaji kutiwa moyo na kuimarishwa! Kwa hiyo, acheni tuwatie moyo wazee, kutia ndani waangalizi wa mzunguko, ambao wanafanya kazi kwa bidii kulichunga kundi la Mungu. (Soma 1 Wathesalonike 5:12, 13.) Mwangalizi mmoja wa mzunguko alisema hivi: “Nyakati fulani akina ndugu hutuandikia barua za shukrani na kusema kwamba walifurahia sana ziara yetu. Sisi huhifadhi barua hizo na kuzisoma tunapovunjika moyo. Barua hizo hututia moyo sana.”

Watoto wetu watakuwa na shangwe na furaha tunapowatia moyo kwa uchangamfu (Tazama fungu la 14)

14. Ni nini kinachoonyesha kwamba shauri linakuwa na matokeo mazuri linapotolewa pamoja na pongezi na kitia moyo?

14 Wazee Wakristo na wazazi wamegundua kwamba inakuwa rahisi zaidi kukazia shauri la Kimaandiko wanapowapongeza na kuwatia moyo wengine. Paulo alipowapongeza Wakorintho kwa kufuata shauri lake, ni wazi kwamba walitiwa moyo kuendelea kufanya yaliyo sawa. (2 Kor. 7:8-11) Andreas, ambaye ana watoto wawili, anasema hivi: “Kuwatia moyo watoto huwasaidia kukua kiroho na kihisia. Shauri huwa na matokeo zaidi linapotolewa pamoja na pongezi. Ingawa watoto wetu wanajua mambo yaliyo sawa, kufanya mambo hayo huwa sehemu ya maisha yao tunapowatia moyo kwa ukawaida.”

KUWATIA MOYO WENGINE KWA NJIA INAYOWAGUSA MOYO

15. Tunaweza kuchukua hatua gani ili kuwatia moyo wengine?

15 Onyesha kwamba unathamini jitihada na sifa nzuri za waabudu wenzako. (2 Nya. 16:9; Ayu. 1:8) Yehova na Yesu wanathamini sana mambo ambayo sote tunafanya ili kutegemeza masilahi ya Ufalme, hata ikiwa hali zetu zinatuzuia kutoa michango au kushiriki kwa kiwango kikubwa zaidi. (Soma Luka 21:1-4; 2 Wakorintho 8:12.) Kwa mfano, baadhi ya ndugu na dada zetu wapendwa ambao wamezeeka wanajitahidi sana kuhudhuria na kushiriki kwa ukawaida katika mikutano na huduma. Je, hatupaswi kuwapongeza na kuwatia moyo?

16. Kwa nini hatupaswi kamwe kusita kuwatia moyo wengine?

16 Tumia kila fursa kuwatia moyo wengine. Mtu anapofanya jambo linalostahili pongezi, kwa nini usimpongeze? Fikiria kilichotokea Paulo na Barnaba walipokuwa Antiokia ya Pisidia. Wasimamizi wa sinagogi wa jiji hilo waliwaambia hivi: “Wanaume, akina ndugu, ikiwa kuna neno lolote la kitia moyo mlilo nalo kwa ajili ya watu, lisemeni.” Kisha Paulo alitoa hotuba nzuri sana. (Mdo. 13:13-16, 42-44) Ikiwa tuna neno lolote la kitia moyo, kwa nini tusiliseme? Inaelekea kwamba tukiwa na zoea la kuwatia moyo wengine, wao pia watatutia moyo.—Luka 6:38.

17. Tunaweza kufanya nini ili maneno yetu yawaguse moyo wengine tunapowapongeza?

17 Uwe mnyoofu na utaje mambo hususa. Ni vizuri kuwatia moyo na kuwapongeza wengine kwa mambo mazuri wanayotimiza. Hata hivyo, ujumbe wa Yesu kwa Wakristo wa Thiatira unaonyesha kwamba kutaja mambo hususa huwa na matokeo mazuri zaidi. (Soma Ufunuo 2:18, 19.) Kwa mfano, ikiwa sisi ni wazazi, tunaweza kuwaambia watoto wetu mambo tunayothamini kuhusu maendeleo ya kiroho ambayo wamefanya. Tunaweza kumwambia dada anayelea watoto bila mume, kinachotuvutia kuhusu jinsi anavyowalea watoto wake licha ya changamoto anazokabili. Kuwapongeza na kuwatia moyo kwa njia hiyo kunaweza kuwachochea sana.

18, 19. Tunaweza kuwaimarishaje wale wanaohitaji kitia moyo?

18 Ni kweli kwamba Yehova hatatuambia tumtie moyo mtu fulani hususa kama alivyomwambia Musa amtie moyo na kumwimarisha Yoshua. Hata hivyo, Mungu anafurahi tunapowatia moyo waabudu wenzetu na watu wengine. (Met. 19:17; Ebr. 12:12) Kwa mfano, tunaweza kumwambia ndugu aliyetoa hotuba jinsi hotuba yake ilivyotupatia shauri tulilohitaji au ilivyotusaidia kuelewa andiko fulani. Dada mmoja alimwandikia hivi msemaji aliyewatembelea: “Ingawa tulizungumza kwa dakika chache, ulitambua kwamba nilikuwa nimehuzunika, ukanifariji na kunitia nguvu. Ningependa ujue kwamba maneno yako ya fadhili, ukiwa jukwaani na tulipozungumza ana kwa ana, yalifanya nihisi kuwa nimepokea zawadi kutoka kwa Yehova.”

19 Inaelekea tutapata fursa nyingi za kuwaimarisha wengine kiroho tukiazimia kutumia shauri hili la Paulo: “Endeleeni kufarijiana na kujengana, kama vile mnavyofanya.” (1 The. 5:11) Bila shaka, sote tutamfurahisha Yehova ikiwa tutaendelea kutiana moyo kila siku.

^ [1] (fungu la 1) Baadhi ya majina yamebadilishwa.