Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unaheshimu Sana Kitabu cha Yehova?

Je, Unaheshimu Sana Kitabu cha Yehova?

“Mlipolipokea neno la Mungu, . . . mlilikubali . . . kama vile lilivyo kwa kweli, kama neno la Mungu.”—1 THE. 2:13.

NYIMBO: 114, 113

1-3. Tunaweza kutumia mfano gani kueleza matatizo yaliyotokea kati ya Euodia na Sintike, na matatizo kama hayo yanaweza kuepukwa jinsi gani? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

WATUMISHI wa Yehova wanaiheshimu sana Biblia, kitabu kitakatifu cha Mungu. Kwa kuwa sisi si wakamilifu, tunahitaji mashauri mara kwa mara kutoka kwenye Maandiko. Tunatendaje tunaposhauriwa? Wafikirie Euodia na Sintike, Wakristo wa karne ya kwanza. Kulitokea matatizo makubwa kati ya wanawake hao watiwa mafuta. Biblia haitaji matatizo hayo, lakini acheni tuwazie jambo ambalo huenda ikawa lilitokea.

2 Tuseme Euodia aliwaalika ndugu na dada nyumbani kwake kwa ajili ya tafrija. Sintike hakualikwa, lakini alipata habari kwamba wengine walifurahia tafrija hiyo. Pengine Sintike alisema hivi: ‘Siamini Euodia hakunialika! Nilidhani sisi ni marafiki wa karibu.’ Sintike akiwa anahisi kwamba amebaguliwa, alianza kuwa na mashaka kuhusu urafiki wake na Euodia. Kwa hiyo, Sintike aliandaa tafrija na kuwaalika ndugu na dada walewale, lakini hakumwalika Euodia! Tatizo lililokuwa kati ya Euodia na Sintike lingeweza kuvuruga amani ya kutaniko lote. Biblia haituambii jinsi walivyoshughulikia hali hiyo, lakini inaelekea dada hao walikubali shauri lenye upendo kutoka kwa mtume Paulo.—Flp. 4:2, 3.

3 Hali kama hizo zinaweza kusababisha matatizo katika makutaniko ya watu wa Yehova leo. Hata hivyo, matatizo kama hayo yanaweza kutatuliwa au kuepukwa tukitumia shauri linalopatikana katika Neno la Mungu, Biblia. Na ikiwa tunaheshimu sana Kitabu cha Yehova, tutaishi kulingana na maagizo yake.—Zab. 27:11.

BIBLIA INATUFUNDISHA KUDHIBITI HISIA ZETU

4, 5. Neno la Mungu linatupatia shauri gani kuhusu kudhibiti hisia zetu?

4 Si rahisi kudhibiti hisia zetu tunapohisi kwamba tumepuuzwa au kutendewa isivyo haki. Tunaweza kuumia ikiwa tunatendewa isivyo haki kwa sababu ya kabila, rangi, au umbo letu. Na tunaumia hata zaidi ikiwa anayetutendea hivyo ni Mkristo mwenzetu! Je, Neno la Mungu lina shauri lolote linaloweza kutusaidia kukabiliana na sifa hiyo mbaya ya wanadamu wasio wakamilifu?

5 Yehova amewachunguza wanadamu tangu walipoumbwa. Anajua hisia na matendo yetu. Mawazo yetu, hasa yanayotegemea hisia kali, yanaweza kutufanya tuseme au kutenda mambo ambayo huenda tukajutia baadaye. Kwa hiyo, ni jambo la hekima kutumia shauri la Biblia kuhusu kudhibiti hisia na kuepuka kuudhika haraka! (Soma Methali 16:32; Mhubiri 7:9.) Hakuna shaka kwamba sisi sote tunahitaji kujitahidi ili tusiwe wepesi kuudhika na tuwe wenye kusamehe zaidi. Kuwasamehe wengine ni jambo muhimu sana machoni pa Yehova na Yesu. (Mt. 6:14, 15) Je, unahitaji kuwa mwenye kusamehe zaidi au kudhibiti hisia zako?

6. Kwa nini tunapaswa kuwa waangalifu tusisitawishe chuki?

6 Mara nyingi watu wanaoshindwa kudhibiti hisia zao husitawisha chuki. Kwa sababu hiyo, huenda watu wakawaepuka. Mtu mwenye chuki anaweza kuwaathiri wengine kutanikoni. Anaweza kujaribu kuficha chuki aliyo nayo, lakini mawazo yasiyofaa yaliyo moyoni mwake “[yatafunuliwa] katika kutaniko.” (Met. 26:24-26) Wazee wanaweza kuwasaidia watu kama hao kutambua kwamba chuki au kinyongo ni mambo ambayo hayakubaliki katika tengenezo la Mungu. Kitabu cha Yehova chenye thamani kinaonyesha hivyo waziwazi. (Law. 19:17, 18; Rom. 3:11-18) Je, unafuata mwongozo wa kitabu hicho?

KUMBUKA JINSI YEHOVA ANAVYOTUONGOZA

7, 8. (a) Yehova anaongozaje sehemu ya kidunia ya tengenezo lake? (b) Taja baadhi ya miongozo tunayopata katika Neno la Mungu. Kwa nini tunapaswa kutii miongozo hiyo?

7 Yehova anawaongoza na kuwalisha watu walio sehemu ya kidunia ya tengenezo lake kupitia “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” akiongozwa na Kristo, ambaye ndiye “kichwa cha kutaniko.” (Mt. 24:45-47; Efe. 5:23) Kama baraza linaloongoza la karne ya kwanza lilivyokuwa likifanya, mtumwa huyo anakubali na kutii Neno la Mungu, au ujumbe ulioongozwa na roho na kuuheshimu sana. (Soma 1 Wathesalonike 2:13.) Biblia ina miongozo na maagizo gani yanayoweza kutunufaisha?

8 Biblia inatuagiza tuhudhurie mikutano kwa ukawaida. (Ebr. 10:24, 25) Inatuhimiza tudumishe umoja wa mafundisho. (1 Kor. 1:10) Neno la Mungu linatuambia tutangulize Ufalme maishani mwetu. (Mt. 6:33) Maandiko pia yanakazia jukumu na pendeleo letu la kuhubiri nyumba kwa nyumba, hadharani, na isivyo rasmi. (Mt. 28:19, 20; Mdo. 5:42; 17:17; 20:20) Kitabu cha Mungu kinawaagiza wazee wadumishe tengenezo lake likiwa safi. (1 Kor. 5:1-5, 13; 1 Tim. 5:19-21) Na Yehova anawaagiza wote katika tengenezo lake wawe safi kimwili na kiroho.—2 Kor. 7:1.

9. Ni njia gani pekee ambayo Yesu anatumia kutusaidia kuelewa Neno la Mungu?

9 Huenda watu fulani wakahisi kwamba hawahitaji msaada ili waielewe Biblia. Hata hivyo, Yesu anamtumia “mtumwa mwaminifu” akiwa njia pekee ya kutoa chakula cha kiroho kwa watu wake. Tangu mwaka 1919, Yesu Kristo akiwa mfalme amekuwa akimtumia mtumwa huyo kuwasaidia wafuasi wake waelewe Kitabu cha Mungu na kutii miongozo yake. Tunapotii miongozo inayopatikana katika Biblia, tunaendeleza usafi, amani, na umoja ndani ya kutaniko. Inafaa kila mmoja wetu ajiulize hivi, ‘Je, ninashikamana na njia ambayo Yesu anatumia kuongoza watu wake leo?’

GARI LA YEHOVA LIKO MWENDONI!

10. Sehemu ya kimbingu ya tengenezo la Yehova inafafanuliwaje katika kitabu cha Ezekieli?

10 Neno la Yehova linatueleza kuhusu sehemu ya kimbingu ya tengenezo lake. Kwa mfano, nabii Ezekieli alipata maono ya sehemu ya kimbingu ya tengenezo la Mungu linalowakilishwa na gari la Yehova. (Eze. 1:4-28) Yehova ndiye anayeendesha gari hilo, nalo linaenda mahali popote ambapo roho yake inalielekeza. Kisha, sehemu ya kimbingu ya tengenezo la Mungu inaongoza sehemu ya kidunia. Bila shaka, gari hilo limekuwa mwendoni! Fikiria mabadiliko mengi ambayo tengenezo limefanya katika miaka kumi iliyopita, na ukumbuke kwamba Yehova ndiye ameleta mabadiliko hayo. Kwa kuwa hivi karibuni Kristo na malaika watakatifu wataharibu ulimwengu huu mwovu, gari la Yehova linasonga kwa kasi ili enzi yake kuu itetewe na jina lake takatifu litakaswe!

Tunawathamini sana wajitoleaji wengi wanaofanya kazi bila kuchoka katika miradi ya ujenzi! (Tazama fungu la 11)

11, 12. Tengenezo la Yehova limekuwa likitimiza mambo gani?

11 Fikiria mambo ambayo sehemu ya kidunia ya tengenezo la Mungu imekuwa ikitimiza katika siku hizi za mwisho. Ujenzi. Mamia ya wajitoleaji walifanya kazi kwa bidii kujenga makao makuu mapya ya Mashahidi wa Yehova yaliyoko Warwick, New York, Marekani. Chini ya mwongozo wa Idara ya Ulimwenguni Pote ya Usanifu-Majengo na Ujenzi, maelfu ya wajitoleaji ulimwenguni pote wanajitolea kwa bidii kujenga Majumba ya Ufalme na kupanua majengo ya ofisi za tawi. Tunawathamini sana wajitoleaji wengi wanaofanya kazi kwa hiari bila kuchoka katika miradi kama hiyo! Kumbuka kwamba Yehova anawabariki wahubiri wa Ufalme ulimwenguni pote ambao kwa unyenyekevu na ushikamanifu, wanatoa michango ili kutegemeza miradi hiyo.—Luka 21:1-4.

12 Elimu. Fikiria shule mbalimbali zinazotoa elimu ya Kimaandiko. (Isa. 2:2, 3) Tuna Shule ya Utumishi wa Painia, Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme, Shule ya Gileadi, Shule ya Wanabetheli Wapya, Shule ya Waangalizi wa Mzunguko na Wake Zao, Shule ya Wazee wa Kutaniko, Shule ya Huduma ya Ufalme, na Shule ya Washiriki wa Halmashauri ya Tawi na Wake Zao. Ni wazi kwamba Yehova anapenda sana kuwaelimisha watu wake! Tovuti yetu ya jw.org inayopatikana katika lugha nyingi inachangia pia kutoa elimu ya Biblia. Tovuti hiyo ina sehemu za pekee kwa ajili ya watoto na familia, na vilevile sehemu ya habari zinazowahusu Mashahidi wa Yehova. Je, unatumia jw.org katika huduma yako na katika ibada ya familia?

UWE MSHIKAMANIFU KWA YEHOVA NA UUNGE MKONO TENGENEZO LAKE

13. Tuna wajibu gani tukiwa waabudu washikamanifu wa Yehova?

13 Ni heshima kubwa sana kuwa sehemu ya tengenezo la Yehova! Kwa kuwa tuna ujuzi wa matakwa na viwango vya Mungu, tuna wajibu wa kufanya yaliyo sawa na kutetea enzi yake kuu. Kadiri ulimwengu huu unavyozidi kupotoka, tunapaswa “[kuchukia] yaliyo mabaya,” kama Yehova anavyoyachukia. (Zab. 97:10) Tunakataa kuwaiga watu wasiomwogopa Mungu ambao wanasema hivi: “Wema ni ubaya na ubaya ni wema.” (Isa. 5:20) Kwa kuwa tunataka kumpendeza Mungu, tunajitahidi kudumisha usafi wa kimwili, kiadili, na kiroho. (1 Kor. 6:9-11) Na kwa sababu tunampenda Yehova na tunamtegemea, tunachagua kuwa washikamanifu kwake kwa kuishi kupatana na viwango vilivyoonyeshwa waziwazi kwenye Kitabu chake chenye thamani. Pia, tunajitahidi kufuata viwango hivyo iwe tuko nyumbani, kutanikoni, kazini, au shuleni. (Met. 15:3) Acheni tuchunguze njia nyingine za kuthibitisha kwamba sisi ni washikamanifu kwa Mungu.

14. Wazazi Wakristo wanaweza kuonyeshaje kwamba wao ni washikamanifu kwa Mungu?

14 Kulea watoto. Wazazi Wakristo wanaonyesha kwamba wao ni washikamanifu kwa Yehova wanapowalea watoto wao kulingana na Neno lake. Wazazi wanaomwogopa Mungu hawaongozwi na utamaduni wa nchi zao wanapowalea watoto wao. Familia ya Kikristo haipaswi kuongozwa na roho ya ulimwengu. (Efe. 2:2) Baba Mkristo hatajiambia, ‘Katika nchi yetu, kazi ya kuwafundisha watoto ni ya wanawake.’ Biblia inatoa mwongozo ulio wazi kuhusu jambo hilo inaposema hivi: “Akina baba, . . . endeleeni kuwalea [watoto wenu] katika nidhamu na mwongozo wa akilini wa Yehova.” (Efe. 6:4) Wazazi wanaomwogopa Yehova wangependa watoto wao wawe kama Samweli, kwa kuwa Yehova alikuwa pamoja naye alipoendelea kukua.—1 Sam. 3:19.

15. Tunaweza kuonyeshaje kwamba sisi ni washikamanifu kwa Yehova tunapofanya maamuzi mazito?

15 Kufanya maamuzi. Njia moja ya kuonyesha kwamba sisi ni washikamanifu kwa Mungu ni kwa kutafuta mwongozo wa Neno lake na tengenezo lake tunapofanya maamuzi mazito maishani. Ili tuelewe umuhimu wa kufanya hivyo, fikiria suala fulani linalowaathiri wazazi wengi. Baadhi ya wahamiaji wana zoea la kuwapeleka watoto wao katika nchi zao wakatunzwe na watu wa familia ili wazazi waendelee kufanya kazi na kutafuta pesa katika nchi ya kigeni. Ni kweli kwamba huo ni uamuzi wa kibinafsi, lakini tunapaswa kukumbuka kwamba tunawajibika mbele za Mungu kwa maamuzi tunayofanya. (Soma Waroma 14:12.) Je, lingekuwa jambo la hekima kufanya maamuzi muhimu kuhusu familia au kazi yetu bila kutafuta kwanza mwongozo wa Biblia? La hasha! Tunahitaji msaada wa Baba yetu wa mbinguni kwa sababu hatuwezi kuongoza hatua zetu wenyewe.—Yer. 10:23.

16. Mwanamke mmoja alihitaji kufanya uamuzi gani, na ni nini kilichomsaidia kufanya uamuzi unaofaa?

16 Alipokuwa akiishi kwenye nchi ya kigeni, mwanamke mmoja alijifungua mtoto wa kiume, na akataka kumpeleka mtoto wake kwenye nchi ya kwao akatunzwe na babu na nyanya yake. Muda mfupi baada ya kujifungua, mwanamke huyo alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Alifanya maendeleo na akajifunza kwamba Mungu amempa wajibu wa kumlea mtoto wake awe mwabudu wa Yehova. (Zab. 127:3; Met. 22:6) Mwanamke huyo alimmiminia Yehova moyo wake, kama ambavyo Maandiko hutuambia tufanye. (Zab. 62:7, 8) Pia, alimweleza mwalimu wake wa Biblia kuhusu mahangaiko yake na akazungumza na wengine kutanikoni kuhusu tatizo hilo. Ingawa watu wa ukoo na marafiki walimshinikiza ampeleke mtoto wake nyumbani, mwanamke huyo aliamua kwamba hatafanya hivyo. Mume wake alivutiwa sana na jinsi kutaniko lilivyomtunza mke na mtoto wake hivi kwamba akaanza kujifunza Biblia na kuhudhuria mikutano pamoja nao. Je, unafikiri mama huyo alihisi kwamba Yehova amejibu sala yake ya kutoka moyoni? Hakuna shaka kwamba alihisi hivyo.

17. Tumepata mwongozo gani kuhusu wanafunzi wetu wa Biblia?

17 Kufuata mwongozo. Njia moja muhimu ya kuonyesha kwamba sisi ni washikamanifu kwa Mungu ni kwa kufuata mwongozo wa tengenezo lake. Kwa mfano, fikiria mapendekezo tuliyopewa kuhusu wanafunzi wetu wa Biblia. Tumependekezewa kwamba baada tu ya kuanza kujifunza na mwanafunzi kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?, tutumie dakika chache kumsaidia alifahamu tengenezo la Yehova. Tunaweza kutumia video Ni Nini Hutendeka Katika Jumba la Ufalme? na broshua Ni Nani Wanaofanya Mapenzi ya Yehova Leo? Baada ya kumaliza kujifunza kitabu Biblia Inafundisha na mwanafunzi anayefanya maendeleo, tumetiwa moyo kujifunza kitabu Jitunzeni Katika Upendo wa Munguna mwanafunzi huyo, hata ikiwa tayari amebatizwa. Tengenezo limetoa mwongozo huo ili wanafunzi wapya ‘waimarishwe katika imani.’ (Kol. 2:7) Je, unafuata mapendekezo hayo kutoka kwenye tengenezo la Yehova?

18, 19. Tuna sababu gani za kumshukuru Yehova?

18 Tuna sababu nyingi za kumshukuru Yehova! Maisha yetu yanamtegemea, kwa kuwa kama si yeye tusingekuwa hai. (Mdo. 17:27, 28) Pia, ametupatia Biblia ambayo ni zawadi yenye thamani sana. Tumekubali Biblia kuwa ujumbe kutoka kwa Mungu, kama Wakristo wa Thesalonike walivyolipokea Neno la Mungu na kulikubali.—1 The. 2:13.

19 Kuwa na Neno la Mungu kumetusaidia kumkaribia Yehova, naye ametukaribia pia. (Yak. 4:8) Baba yetu wa mbinguni ametupatia heshima kubwa sana ya kuwa sehemu ya tengenezo lake. Tunathamini sana baraka hizo! Mtunga zaburi alionyesha jinsi alivyothamini baraka za Yehova alipoimba hivi: “Mshukuruni Yehova, kwa maana ni mwema: kwa maana fadhili zake zenye upendo ni za mpaka wakati usio na kipimo.” (Zab. 136:1) Maneno haya yanarudiwa mara 26 katika Zaburi ya 136: “Fadhili zake zenye upendo ni za mpaka wakati usio na kipimo.” Tukiwa washikamanifu kwa Yehova na tengenezo lake, tutajionea uhalisi wa maneno hayo yanayotia moyo kwa sababu tutaishi milele!