Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Neno Lililogusa Moyo Sana!

Neno Lililogusa Moyo Sana!

“MWANAMKE.” Hivyo ndivyo Yesu aliwaita watu wa jinsia ya kike nyakati nyingine. Kwa mfano, alipokuwa akimponya mlemavu aliyekuwa amepindika vibaya kwa miaka 18, alisema hivi: “Mwanamke, umefunguliwa kutoka udhaifu wako.” (Luka 13:10-13) Yesu alitumia neno hilo hata alipozungumza na mama yake, jambo lililokuwa la kawaida na la heshima nyakati hizo. (Yoh. 19:26; 20:13) Lakini kulikuwa na neno lingine la heshima hata zaidi.

Biblia inatumia neno linaloonyesha fadhili na wororo inapozungumzia wanawake fulani. Yesu alitumia neno hilo alipozungumza na mwanamke aliyekuwa na mtiririko wa damu kwa miaka 12. Mwanamke huyo alimfikia Yesu kwa njia ambayo haikupatana na sheria ya Mungu iliyosema kwamba mtu aliye katika hali yake hakuwa safi. Tunaweza kusema kwamba hakupaswa kuwa karibu na watu kwa sababu ya hali yake. (Law. 15:19-27) Lakini alihitaji sana msaada. Kwa kweli, “alikuwa ameumizwa sana na matabibu wengi na alikuwa ametumia mali zake zote naye hakuwa amefaidika bali, badala yake, hali yake ikawa mbaya zaidi.”—Marko 5:25, 26.

Mwanamke huyo alipenya kimyakimya katikati ya umati, akamkaribia Yesu kutoka nyuma, na kugusa upindo wa vazi lake la nje. Mara moja chemchemi yake ya damu ikakauka! Mwanamke huyo alitazamia kwamba hatajulikana, lakini Yesu akauliza hivi: “Ni nani aliyenigusa?” (Luka 8:45-47) Alipoona hivyo, mwanamke huyo akiwa anatetemeka kwa woga, alianguka chini mbele ya Yesu na “akamwambia kweli yote.”—Marko 5:33.

Ili kumtuliza, Yesu alimwambia hivi kwa fadhili: “Jipe moyo, binti yangu!” (Mt. 9:22) Kulingana na wasomi wa Biblia, neno la Kiebrania na Kigiriki linalotafsiriwa “binti” linaweza kutumika kuonyesha “fadhili na wororo.” Yesu aliendelea kumtuliza kwa kumwambia hivi: “Imani yako imekuponya. Nenda kwa amani, na uwe na afya njema kutokana na ugonjwa wako wenye kuhuzunisha.”—Marko 5:34.

“Binti.” Hivyo ndivyo Mwisraeli tajiri, Boazi, alimwita Ruthu Mmoabu. Hali ya Ruthu pia ingeweza kumfanya aogope kwa sababu alikuwa akikusanya masalio ya shayiri kwenye shamba la mtu ambaye hakumjua. Boazi alimwambia hivi: “Umesikia binti yangu, sivyo?” Kisha akamhimiza Ruthu aendelee kukusanya masalio katika mashamba yake. Ruthu alianguka kifudifudi mbele ya Boazi, na kumwuliza ni kwa nini amemtendea kwa fadhili jinsi hiyo, ilhali yeye alikuwa mkaaji mgeni. Boazi alimhakikishia hivi: “Nilipewa habari kamili juu ya yote ambayo umemfanyia mama-mkwe wako [mjane Naomi] . . . Yehova na akupe thawabu kwa sababu ya jinsi unavyotenda.”—Rut. 2:8-12.

Yesu na Boazi wanawawekea wazee Wakristo mfano mzuri sana! Nyakati nyingine, wazee wawili wanaweza kupanga kuzungumza na dada Mkristo anayehitaji msaada wa Kimaandiko na kitia moyo. Baada ya kumwomba Yehova mwongozo kupitia sala na kumsikiliza dada yao kwa makini, wazee hao wanaweza kumhakikishia kwamba yeye ni mwenye thamani na kumfariji kupitia Neno la Mungu.—Rom. 15:4.