Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tumepangwa Kitengenezo Kulingana na Kitabu cha Mungu

Tumepangwa Kitengenezo Kulingana na Kitabu cha Mungu

“Kwa hekima Yehova mwenyewe aliuweka msingi wa dunia. Aliziweka mbingu imara kwa utambuzi.”—MET. 3:19.

NYIMBO: 105, 107

1, 2. (a) Watu wengine wana maoni gani kuhusu wazo la kwamba Mungu ana tengenezo? (b) Tutazungumzia nini katika makala hii?

JE, MUNGU ana tengenezo? Baadhi ya watu husema kwamba hatuhitaji kuongozwa na tengenezo fulani. Wanasema kwamba tunahitaji tu kuwa na uhusiano wa kibinafsi pamoja na Mungu. Je, maoni hayo ni sahihi? Ukweli wa mambo ni nini?

2 Katika makala hii, tutachunguza mambo yanayothibitisha kwamba hakuna yeyote aliye na mpangilio kama Yehova, Mungu wa utaratibu. Tutachunguza pia jinsi tunavyopaswa kutenda tunapopokea mwongozo kutoka katika tengenezo la Yehova. (1 Kor. 14:33, 40) Katika karne ya kwanza na katika siku zetu, Biblia imesaidia sehemu ya kidunia ya tengenezo la Yehova kufanya kazi kubwa ya kuhubiri habari njema ulimwenguni pote. Kwa kuwa tunashikamana na viwango vya Biblia na kuunga mkono maagizo ya tengenezo, tunaendeleza usafi, amani, na umoja wa kutaniko la ulimwenguni pote.

YEHOVA—MUNGU MWENYE UTARATIBU

3. Ni nini kinachokuthibitishia kwamba hakuna aliye na utaratibu kama Yehova?

3 Uumbaji unathibitisha kwamba hakuna aliye na utaratibu kama Mungu. Biblia inasema hivi: “Kwa hekima Yehova mwenyewe aliuweka msingi wa dunia. Aliziweka mbingu imara kwa utambuzi.” (Met. 3:19) Tunajua tu “kingo za njia [za Mungu],” na “mnong’ono . . . wa jambo lililosikiwa juu yake.” (Ayu. 26:14) Ingawa tunajua mambo machache sana kuhusu sayari, nyota, na makundi ya nyota, tunatambua kwamba vitu vilivyo angani vimepangwa kwa utaratibu wa ajabu. (Zab. 8:3, 4) Makundi ya nyota yana mamilioni ya nyota, na zote zinasonga kwa utaratibu. Inastaajabisha sana kwamba sayari zinazunguka jua kwa mpangilio kana kwamba zinatii sheria za barabarani! Kwa kweli, mpangilio tata wa ulimwengu unatusaidia kuona kwamba Yehova, “[aliyezifanya] mbingu kwa uelewaji” pamoja na dunia, anastahili sifa, ushikamanifu, na ibada yetu.—Zab. 136:1, 5-9.

4. Kwa nini sayansi imeshindwa kujibu maswali mengi?

4 Sayansi imefunua mambo mengi kuhusu ulimwengu kwa ujumla na kuhusu dunia yetu, na imetunufaisha katika njia mbalimbali. Lakini imeshindwa kujibu maswali mengi. Kwa mfano, wataalamu wa nyota hawawezi kutuambia ulimwengu wetu ulitoka wapi au kwa nini tupo kwenye dunia, sayari pekee inayoweza kutegemeza uhai. Pia, hakuna mtu anayeweza kueleza kwa nini wanadamu wanatamani sana kuishi milele. (Mhu. 3:11) Kwa nini kuna maswali mengi sana muhimu yasiyo na majibu? Sababu moja ni kwamba wanasayansi na watu wengine wanasema hakuna Mungu na wanawafundisha watu nadharia ya mageuzi. Lakini kupitia Kitabu chake, Yehova anajibu maswali yanayowahangaisha watu kila mahali.

5. Sisi sote hutegemea sheria za asili katika njia gani?

5 Tunategemea sheria za asili zisizobadilika na zinazotegemeka ambazo ziliwekwa na Yehova. Wataalamu kama vile mafundi wa umeme, mafundi bomba, wahandisi, marubani, madaktari wa upasuaji, hutegemea sheria hizo wanapofanya kazi zao. Kwa mfano, madaktari wa upasuaji wanajua kwamba viungo vya mwili wetu vinapatikana mahali palepale katika mwili wa mtu yeyote. Kwa hiyo, daktari wa upasuaji hahitaji kutafuta mahali moyo ulipo katika mwili wa mgonjwa. Na sisi sote hutii sheria za asili. Kwa mfano, ukikiuka sheria ya nguvu za uvutano unaweza kufa.

VITU VILIVYOPANGWA NA MUNGU

6. Kwa nini tunatazamia waabudu wa Yehova wafanye mambo kwa utaratibu?

6 Kwa kweli ulimwengu umepangwa kwa njia ya ajabu. Hivyo, tunatazamia kwamba Yehova angependa waabudu wake wafanye mambo kwa utaratibu. Ili kutimiza kusudi hilo, Mungu ametuandalia Biblia ituongoze. Kuishi bila msaada wa tengenezo la Mungu na viwango vyake kungetufanya tukose furaha na tufadhaike.

7. Ni nini kinachoonyesha kwamba Biblia ni kitabu kilichopangwa vizuri?

7 Biblia si mkusanyo tu wa vitabu tofauti-tofauti vya Kiyahudi na vya Kikristo. Badala yake, ni kitabu kilichopangwa vizuri—kazi bora na ubuni wa pekee iliyoandikwa kupitia roho ya Mungu. Vitabu vyote vya Biblia vinahusiana. Kuanzia kitabu cha Mwanzo hadi Ufunuo, kichwa kikuu cha Biblia kinaonekana wazi. Kichwa hicho ni kutetewa kwa enzi kuu ya Yehova na kutimizwa kwa kusudi lake kuelekea dunia kupitia Ufalme wake, na Kristo, “uzao” ulioahidiwa, akiwa mfalme wa Ufalme huo.—Soma Mwanzo 3:15; Mathayo 6:10; Ufunuo 11:15.

8. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Waisraeli walikuwa wamepangwa vizuri?

8 Taifa la kale la Israeli lilikuwa mfano wa watu waliopangwa kitengenezo. Kwa mfano, chini ya Sheria ya Musa kulikuwa na “wanawake ambao walifanya utumishi uliopangwa kwenye mwingilio wa hema la mkutano.” (Kut. 38:8) Pia, kambi ya Waisraeli na hema la kukutania lilihamishwa kwa utaratibu. Miaka mingi baadaye, Mfalme Daudi aliwagawa na kuwapanga Walawi na makuhani katika migawanyo mbalimbali. (1 Nya. 23:1-6; 24:1-3) Na walipomtii Yehova, Waisraeli walibarikiwa kwa kuwa na utulivu, amani, na umoja.—Kum. 11:26, 27; 28:1-14.

9. Ni nini kinachoonyesha kwamba kutaniko la karne ya kwanza la Kikristo lilikuwa limepangwa vizuri?

9 Kwa kuwa lilikuwa limepangwa vizuri, kutaniko la karne ya kwanza la Kikristo lilinufaika na mwongozo wa baraza linaloongoza ambalo mitume ndio walikuwa washiriki wa kwanza wa baraza hilo. (Mdo. 6:1-6) Baadaye, ndugu wengine waliongezwa kwenye baraza hilo. (Mdo. 15:6) Mashauri na maagizo yalitolewa kupitia barua zilizoongozwa na roho ambazo ziliandikwa na washiriki wa baraza linaloongoza la karne ya kwanza au wanaume walioshirikiana nao kwa ukaribu. (1 Tim. 3:1-13; Tito 1:5-9) Makutaniko yalinufaikaje kwa kufuata mwongozo wa baraza linaloongoza?

10. Kulikuwa na matokeo gani makutaniko ya karne ya kwanza yaliposhika maagizo yaliyotolewa na baraza linaloongoza? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

10 Soma Matendo 16:4, 5Ndugu waliosafiri kwa niaba ya baraza linaloongoza waliyapa makutaniko “maagizo yaliyokuwa yameamuliwa na mitume na wanaume wazee waliokuwa katika Yerusalemu.” Makutaniko yaliposhika maagizo hayo, “[yaliendelea] kufanywa imara katika imani na kuongezeka hesabu siku baada ya siku.” Je, simulizi hilo la Biblia lina somo lolote tunaloweza kutumia katika tengenezo la Mungu leo?

JE, UNAFUATA MWONGOZO?

11. Wanaume waliowekwa rasmi wanapaswa kuitikiaje mwongozo wanaopokea kutoka kwenye tengenezo la Mungu?

11 Leo, washiriki wa Halmashauri za Tawi, Halmashauri za Nchi, waangalizi wa mzunguko, na wazee wa kutaniko wanapaswa kufanya nini wanapopokea mwongozo kutoka kwenye tengenezo la Mungu? Kitabu cha Mungu kinatuagiza tuwatii wanaoongoza na tujitiishe kwao. (Kum. 30:16; Ebr. 13:7, 17) Mtu mwenye roho ya uasi au ya kuwachambua wengine hana nafasi katika tengenezo la Mungu, kwa kuwa roho hiyo inaweza kuharibu upendo, amani, na umoja wa makutaniko. Bila shaka, hakuna Mkristo mshikamanifu ambaye angependa kuonyesha roho ya kukosa heshima na ushikamanifu, kama ya Diotrefe. (Soma 3 Yohana 9, 10.) Hata hivyo, tunaweza kujiuliza hivi: ‘Je, ninawachochea watu ninaoshirikiana nao waendelee kuwa na hali nzuri ya kiroho? Je, ninakubali haraka na kuunga mkono mwongozo unaotolewa na ndugu wanaoongoza?’

12. Ni badiliko gani ambalo limefanywa kuhusu jinsi ambavyo wazee na watumishi wa huduma huwekwa rasmi?

12 Fikiria uamuzi uliofanywa na Baraza Linaloongoza hivi karibuni. Makala “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Novemba 15, 2014, ilieleza badiliko la jinsi ya kuwaweka rasmi wazee na watumishi wa huduma. Makala hiyo ilionyesha kwamba katika karne ya kwanza, baraza linaloongoza liliwapa waangalizi wa mzunguko jukumu la kuwaweka rasmi ndugu hao. Kupatana na hilo, tangu Septemba 1, 2014, waangalizi wa mzunguko wamekuwa wakiwaweka rasmi wazee na watumishi wa huduma. Hivyo, mwangalizi wa mzunguko hujaribu kuwafahamu vizuri ndugu waliopendekezwa na kuhubiri pamoja nao inapowezekana. Anaichunguza pia familia ya ndugu aliyependekezwa. (1 Tim. 3:4, 5) Kisha baraza la wazee pamoja na mwangalizi wa mzunguko huchunguza kwa makini sifa za Kimaandiko ambazo Mkristo anapaswa kuwa nazo ili astahili kuwa mtumishi wa huduma au mzee.—1 Tim. 3:1-10, 12, 13; 1 Pet. 5:1-3.

13. Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunaunga mkono mwongozo tunaopokea kutoka kwa wazee?

13 Tunahitaji kufuata mwongozo tunaopata kutoka kwa wazee ambao unategemea Biblia. Wachungaji hao washikamanifu walio katika tengenezo la Mungu, hufuata mwongozo ‘wenye afya’ unaopatikana katika Kitabu cha Mungu. (1 Tim. 6:3) Kumbuka shauri la Paulo kuwahusu watu wanaojiendesha bila utaratibu kutanikoni. Watu fulani ‘hawakuwa wakifanya kazi hata kidogo bali walijiingiza katika mambo yasiyowahusu.’ Inawezekana walishauriwa na wazee lakini wakapuuza shauri walilopewa. Kutaniko lilipaswa kushughulikaje na mtu kama huyo? Paulo aliagiza hivi: “Mtieni alama mtu huyo, acheni kushirikiana naye.” Lakini pia Paulo aliandika kwamba mtu huyo hakupaswa kuonwa kuwa adui. (2 The. 3:11-15) Leo, wazee wanaweza kutoa hotuba ya kuonya kuhusu mtu ambaye anajiendesha kwa njia inayoharibu sifa ya kutaniko, kama vile kuwa na urafiki wa kimapenzi na mtu ambaye si mwabudu wa Yehova. (1 Kor. 7:39) Unatendaje wazee wanapotoa hotuba kama hiyo? Ikiwa unafahamu kisa kinachozungumziwa katika hotuba hiyo, je, utakuwa mwangalifu ili usishirikiane na mtu huyo? Kufanya hivyo kutaonyesha unampenda, na msimamo wako thabiti unaweza kumfanya aache mwenendo wake mbaya. [1]

DUMISHA USAFI, AMANI, NA UMOJA

14. Tunaweza kuchangiaje usafi wa kutaniko?

14 Tunaweza kuchangia usafi wa kiroho wa kutaniko kwa kufuata mwongozo wa Neno la Mungu. Fikiria hali iliyotokea katika jiji la kale la Korintho. Paulo alikuwa amejimimina katika kazi ya kuhubiri kwenye jiji hilo, na aliwapenda “watakatifu” wenzake walioishi huko. (1 Kor. 1:1, 2) Hata hivyo, mwenendo mpotovu kingono uliokuwa ukipuuzwa ndani ya kutaniko ulimhuzunisha sana mtume Paulo. Aliwaagiza wazee wamkabidhi mwasherati aliyekuwa katika kutaniko hilo kwa Shetani, yaani, wamtenge na ushirika. Ili kudumisha usafi wa kutaniko, wazee walihitaji kuondoa “chachu” iliyokuwa miongoni mwao. (1 Kor. 5:1, 5-7, 12) Tunapounga mkono uamuzi wa wazee wa kumtenga mtenda dhambi asiyetubu, tunachangia kudumisha usafi wa kutaniko na huenda tukamchochea atubu na kutafuta msamaha wa Yehova.

15. Tunaweza kudumishaje amani ndani ya kutaniko?

15 Kulikuwa na tatizo lingine lililopaswa kushughulikiwa katika kutaniko la Korintho. Baadhi ya akina ndugu walikuwa wakiwapeleka waamini wenzao mahakamani. Paulo aliwauliza swali hili lililowachochea wafikiri: “Kwa nini msiache mkosewe badala ya hivyo?” (1 Kor. 6:1-8) Hali kama hizo hutokea leo. Nyakati nyingine, amani kati ya ndugu imevurugwa kwa sababu biashara waliyofanya haikufanikiwa na hivyo kusababisha hasara, na hata mmoja wao kushtakiwa kwamba amemlaghai mwenzake. Ndugu wengine wamewapeleka waabudu wenzao mahakamani, lakini Kitabu cha Mungu kinatusaidia kuona ni afadhali kupata hasara badala ya kuliletea suto jina la Mungu au kuharibu amani ya kutaniko. [2] Ili kutatua matatizo makubwa na hali za kutoelewana, tunapaswa kutumia shauri la Yesu. (Soma Mathayo 5:23, 24; 18:15-17.) Tunapofanya hivyo, tunaendeleza umoja katika familia ya waabudu wa Yehova.

16. Kwa nini tunatarajia watu wa Mungu wawe na umoja?

16 Kitabu cha Yehova kinaonyesha ni kwa nini tunatarajia watu wake wawe na umoja. Mtunga zaburi aliimba hivi: “Tazama! Jinsi ilivyo vyema na jinsi inavyopendeza ndugu kukaa pamoja kwa umoja!” (Zab. 133:1) Waisraeli walipomtii Yehova, walifanya mambo kwa mpangilio na wakaunganishwa kwa umoja. Alipotabiri hali ya wakati ujao ya watu wake, Mungu alisema hivi: “Nitawaunganisha, kama kundi zizini.” (Mika 2:12) Zaidi ya hayo, Yehova alitabiri hivi kupitia nabii Sefania: “[Nitabadilisha] lugha ya vikundi vya watu na kuwapa lugha safi [ya kweli ya Biblia], ili wote waliitie jina la Yehova, wamtumikie bega kwa bega,” au wamwabudu kwa umoja. (Sef. 3:9) Tunafurahia sana pendeleo la kumwabudu Yehova kwa umoja!

Wazee hujitahidi kumsaidia mtu ambaye amejikwaa katika kosa fulani (Tazama fungu la 17)

17. Ili kudumisha umoja na usafi wa kutaniko, wazee wanapaswa kufanya nini Mkristo anapotenda dhambi?

17 Ili kudumisha umoja na usafi wa kutaniko, wazee wanapaswa kushughulikia mambo ya kihukumu haraka iwezekanavyo na kwa njia ya upendo. Paulo alijua kwamba upendo wa Mungu hauongozwi na hisia, na Mungu hapuuzi dhambi. (Met. 15:3) Kwa hiyo, Paulo hakusita kuwaandikia Wakorintho barua yake ya kwanza iliyokuwa na maneno thabiti lakini yenye upendo. Barua ya pili kwa Wakorintho, iliyoandikwa miezi kadhaa baadaye, ilionyesha kwamba walikuwa wamefanya maendeleo kwa sababu wazee walifuata mwongozo wa Paulo. Mkristo akijikwaa katika kosa fulani kabla ya yeye kulijua, wanaume wenye sifa za kustahili kiroho wanapaswa kujaribu kumrekebisha upya katika roho ya upole.—Gal. 6:1.

18. (a) Shauri la Neno la Mungu lilisaidia makutaniko ya karne ya kwanza katika njia gani? (b) Tutazungumzia nini katika makala inayofuata?

18 Ni wazi kwamba shauri linalopatikana katika Kitabu cha Mungu, liliwasaidia Wakristo wa karne ya kwanza walioishi Korintho na Wakristo walioishi katika maeneo mengine kudumisha usafi, amani, na umoja katika makutaniko yao. (1 Kor. 1:10; Efe. 4:11-13; 1 Pet. 3:8) Kwa sababu hiyo, ndugu na dada zetu wa nyakati hizo walitimiza mengi katika huduma. Hiyo ndiyo sababu Paulo alisema kwamba habari njema “ilihubiriwa katika uumbaji wote ulio chini ya mbingu.” (Kol. 1:23) Leo, jitihada za wahubiri walio sehemu ya tengenezo lililounganishwa kwa umoja, zimechangia kuenezwa kwa ujuzi kuhusu kusudi la Mungu la wakati ujao duniani pote. Makala inayofuata itaonyesha uthibitisho zaidi kwamba wahubiri hao wanaiheshimu sana Biblia, na wameazimia kumheshimu Bwana Mwenye Enzi Kuu, Yehova.—Zab. 71:15, 16.

^ [1] (fungu la 13) Tazama kitabu Tengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova, ukurasa wa 134-136.

^ [2] (fungu la 15) Kwa habari zaidi kuhusu hali zinazoweza kumfanya Mkristo aamue kuchukua hatua za kisheria dhidi ya Mkristo mwenzake, tazama maelezo ya chini kwenye kitabu Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu,” ukurasa wa 223.