Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wameitwa Kutoka Gizani

Wameitwa Kutoka Gizani

“[Yehova amewaita] ninyi kutoka katika giza kuingia katika nuru yake ya ajabu.”—1 PET. 2:9.

NYIMBO: 116, 102

1. Eleza mambo yaliyotukia wakati wa uharibifu wa Yerusalemu.

KATIKA mwaka wa 607 K.W.K., jeshi kubwa la Babiloni, likiongozwa na Mfalme Nebukadneza wa Pili, lilivamia jiji la Yerusalemu. Biblia inasema hivi kuhusu mauaji ya kikatili yaliyofanyika: “[Nebukadneza] aliwaua vijana wao kwa upanga katika nyumba ya patakatifu pao, wala hakumhurumia kijana wala bikira, mzee wala mkongwe. . . . Naye akaiteketeza nyumba ya Mungu wa kweli na kuubomoa ukuta wa Yerusalemu; na minara yake yote ya makao wakaiteketeza kwa moto na pia vyombo vyake vyote vyenye kutamanika, ili kufanya uharibifu.”—2 Nya. 36:17, 19.

2. Yehova alitoa onyo gani kuhusu uharibifu wa Yerusalemu uliokuwa ukikaribia, na Wayahudi wangepatwa na nini?

2 Wakazi wa Yerusalemu hawakupaswa kushangaa jiji hilo lilipoharibiwa. Kwa miaka mingi, manabii wa Mungu walikuwa wamewaonya Wayahudi kwamba ikiwa wangeendelea kupuuza sheria za Mungu, wangetiwa mikononi mwa Wababiloni. Wayahudi wengi wangekufa kwa upanga, na wale ambao wangeokoka wangepelekwa uhamishoni Babiloni na wangeishi huko maisha yao yote. (Yer. 15:2) Maisha ya mateka hao yalikuwaje huko Babiloni? Je, utekwa wa Babiloni una ulinganifu wowote na nyakati za Kikristo? Ikiwa ndivyo, utekwa huo ulitukia lini?

MAISHA YA UHAMISHONI

3. Maisha ya Waisraeli wakiwa uhamishoni Babiloni yalitofautianaje na maisha yao wakiwa watumwa huko Misri?

3 Mambo ambayo manabii walitabiri yalitimia. Kupitia Yeremia, Yehova aliwaambia watu wake kwamba watakapotekwa wakubali hali yao mpya na wajitahidi kufurahia maisha kadiri hali ilivyoruhusu. Aliwaambia hivi: “[Mkiwa Babiloni] jengeni nyumba na kukaa ndani yake, mpande bustani na kula matunda yake. Pia, tafuteni amani kwa ajili ya jiji ambamo nimewapeleka ninyi uhamishoni, nanyi msali kwa ajili yake kwa Yehova, kwa maana katika amani ya jiji hilo kutakuwa na amani kwa ajili yenu wenyewe.” (Yer. 29:5, 7) Wale waliotii amri hiyo ya Mungu, waliishi maisha ya kawaida ingawa walikuwa utekwani. Kwa kadiri fulani, Wababiloni waliwaruhusu wafanye shughuli zao za kila siku. Hata waliruhusiwa kusafiri kwenda sehemu mbalimbali za nchi hiyo. Babiloni lilikuwa kitovu cha biashara katika ulimwengu wa kale, na hati ambazo zimechimbuliwa zinaonyesha kwamba Wayahudi wengi walijifunza ustadi wa kufanya biashara wakiwa huko, na wengine wakawa mafundi stadi. Hata baadhi ya Wayahudi walipata ufanisi wa kimwili. Maisha ya Waisraeli wakiwa uhamishoni Babiloni yalitofautiana kabisa na maisha yao wakiwa watumwa huko Misri karne nyingi zilizotangulia.—Soma Kutoka 2:23-25.

4. Mbali na Waisraeli waasi, ni nani wengine walioathiriwa na utekwa wa Babiloni, na ni mambo gani yaliwazuia kumwabudu Mungu kikamili?

4 Ingawa Wayahudi walipata mahitaji yao ya kimwili wakiwa uhamishoni, hali ilikuwaje kuhusu mahitaji yao ya kiroho? Hekalu la Yehova na madhabahu yake yalikuwa yameharibiwa na hakukuwa na mpango wa makuhani kutekeleza majukumu yao. Miongoni mwa mateka hao kulikuwa na watumishi waaminifu wa Mungu ambao hawakustahili kuadhibiwa, lakini waliteseka pamoja na taifa zima. Hata hivyo, walifanya yote waliyoweza kufuata sheria za Mungu. Kwa mfano, wakiwa Babiloni, Danieli na waandamani wake watatu, Shadraki, Meshaki, na Abednego, walikataa kula chakula ambacho Sheria ilikataza. Na tunajua kwamba Danieli aliwasiliana na Mungu kwa ukawaida kupitia sala. (Dan. 1:8; 6:10) Pamoja na hayo, bado Wayahudi waliomwogopa Mungu hawangeweza kutimiza matakwa yote ya Sheria kwa kuwa walitawaliwa na wapagani.

5. Yehova aliwapa watu wake tumaini gani, na kwa nini ahadi hiyo ilikuwa ya pekee sana?

5 Je, Waisraeli wangeweza kupata tena uhuru wa kumwabudu Mungu kwa njia inayokubalika kabisa? Wakati huo, ilionekana kama haingewezekana. Wababiloni walikuwa na sera ya kutowaachilia mateka wao. Hata hivyo, sera hiyo haingemzuia Yehova Mungu kuchukua hatua. Alikuwa amewaahidi watu wake kwamba wangekombolewa, na kwa kweli walikombolewa. Kamwe ahadi za Mungu hazikosi kutimia.—Isa. 55:11.

JE, TUKIO HILO LINA ULINGANIFU WOWOTE LEO?

6, 7. Kwa nini inafaa tuchunguze upya uelewaji wetu wa utekwa wa Babiloni katika siku zetu?

6 Je, Wakristo wamewahi kukabili hali yoyote inayofanana na utekwa wa Babiloni? Kwa miaka mingi, gazeti hili lilisema kwamba watumishi wa kisasa wa Mungu waliingia kwenye utekwa wa Babiloni mwaka 1918, na waliachiliwa huru mwaka 1919. Hata hivyo, kama tutakavyoona kwenye makala hii na inayofuata, kuna sababu nzuri za kuchunguza upya habari hiyo.

7 Kumbuka: Babiloni Mkubwa ni milki ya ulimwenguni pote ya dini bandia. Kwa hiyo, ili watu wa Mungu wawe katika utekwa wa Babiloni mwaka 1918, hiyo ingemaanisha kwamba tayari walikuwa wametekwa na dini bandia kabla ya mwaka huo. Lakini ukweli wa mambo ni kwamba kwa miongo kadhaa kabla ya Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, watumishi wa Mungu waliotiwa mafuta walikuwa wameanza kujitenga na Babiloni Mkubwa, na hivyo walikuwa wameacha kuwa watumwa wake. Ingawa watiwa mafuta waliteswa wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, dhiki walizokabili zilisababishwa hasa na wenye mamlaka, wala si Babiloni Mkubwa. Hivyo, haielekei kwamba watu wa Yehova waliingia katika utekwa wa Babiloni Mkubwa mwaka 1918.

WATU WA MUNGU WALIINGIA KWENYE UTEKWA WA BABILONI LINI?

8. Eleza jinsi Ukristo wa kweli ulivyochafuliwa. (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

8 Katika Pentekoste ya 33 W.K., maelfu ya Wayahudi na wageuzwa imani walitiwa mafuta kwa roho takatifu. Wakristo hao wapya wakawa “jamii iliyochaguliwa, ukuhani wa kifalme, taifa takatifu, watu wa kuwa mali ya pekee.” (Soma 1 Petro 2:9, 10.) Mitume waliyachunga kwa uangalifu makutaniko ya watu wa Mungu muda wote waliokuwa hai. Hata hivyo, baada ya kifo cha mitume, watu walitokea miongoni mwao na kusema “mambo yaliyopotoka ili kuwavuta wanafunzi wawafuate wao wenyewe.” (Mdo. 20:30; 2 The. 2:6-8) Wanaume wengi kati yao walikuwa na mapendeleo makutanikoni, wakitumikia wakiwa waangalizi, lakini baadaye wakaja kuwa “maaskofu.” Jamii ya makasisi ilianza kujitokeza, ingawa Yesu alikuwa amewaambia hivi wafuasi wake: “Ninyi nyote ni ndugu.” (Mt. 23:8) Wanaume mashuhuri waliovutiwa sana na falsafa za Aristoto na Plato waliingiza mawazo ya dini za uwongo, na hatua kwa hatua yakachukua mahali pa mafundisho safi ya Neno la Mungu.

9. Fafanua jinsi uasi imani wa Kikristo ulivyoungwa mkono na Serikali ya Roma. Matokeo yalikuwaje?

9 Katika mwaka wa 313 W.K., uasi imani huo wa Kikristo ulitambuliwa kisheria na Maliki Mroma Konstantino aliyekuwa mpagani. Kuanzia wakati huo, Kanisa lilianza kushirikiana kwa ukaribu na Serikali. Kwa mfano, baada ya Kongamano la Nisea, Konstantino, ambaye alikuwepo katika kongamano hilo, aliagiza Arius, kasisi aliyeasi, apelekwe uhamishoni kwa kukataa kukiri kwamba Yesu ni Mungu. Baadaye, chini ya Maliki Theodosius wa Kwanza (379-395 W.K.), Ukristo uliopotoka, ambao ulikuja kuitwa Kanisa Katoliki, ukawa dini rasmi ya Milki ya Roma. Wanahistoria wanasema kwamba Roma iliyokuwa ya kipagani, “iligeuzwa kuwa ya Kikristo” katika karne ya nne. Ukweli ni kwamba kufikia wakati huo, uasi imani wa Kikristo ulikuwa umeungana na matengenezo ya kidini yaliyokuwa ya kipagani katika Milki ya Roma, na hivyo kuwa sehemu ya Babiloni Mkubwa. Ingawa hivyo, idadi ndogo ya Wakristo watiwa mafuta, wanaofananishwa na ngano, walikuwa wakijitahidi kumwabudu Mungu kwa njia inayokubalika, lakini walikuwa wachache sana kwa kulinganishwa na Wakristo waliopotoka. (Soma Mathayo 13:24, 25, 37-39.) Ni wazi kwamba walikuwa katika utekwa wa Babiloni!

10. Ni nini kilichowasaidia watu wanyoofu waanze kutilia shaka mafundisho ya kanisa katika karne za mapema Wakati wetu wa Kawaida?

10 Hata hivyo, kwa karne chache za kwanza katika Wakati wetu wa Kawaida, watu wengi wangeweza kusoma Biblia katika Kigiriki au Kilatini. Kwa hiyo, wangeweza kulinganisha mafundisho ya Neno la Mungu na mafundisho ya kanisa. Mambo waliyojifunza katika Biblia yalifanya baadhi yao wapinge mafundisho ya kanisa. Lakini ilikuwa hatari sana kufanya hivyo kwa kuwa yeyote aliyepinga mafundisho hayo waziwazi angeweza kuuawa.

11. Makasisi walidhibiti jinsi gani matumizi ya Biblia?

11 Baada ya muda, lugha zilizotumiwa kuandika Biblia ziliacha kuzungumzwa na watu wengi, na kanisa lilipinga jitihada za kutafsiri Neno la Mungu katika lugha ambazo watu walizungumza. Kwa sababu hiyo, makasisi na watu fulani wenye elimu ndio tu wangeweza kusoma Biblia, ingawa si makasisi wote waliojua kusoma na kuandika vizuri. Mtu yeyote aliyepinga mafundisho ya kanisa angeadhibiwa vikali. Watumishi waaminifu wa Mungu waliotiwa mafuta walikutanika kisiri, na nyakati nyingine haingewezekana kabisa kukutana. Kama hali ilivyokuwa wakati wa utekwa wa Babiloni, “ukuhani wa kifalme” wa watiwa mafuta haungeweza kutekeleza majukumu yake vizuri. Ni wazi kwamba Babiloni Mkubwa alikuwa amewabana watu kwelikweli!

NURU INAANZA KUANGAZA

12, 13. Ni mambo gani mawili ambayo kwa kadiri fulani yalipunguza uvutano wa Babiloni Mkubwa? Eleza.

12 Je, Wakristo wa kweli wangeweza kupata tena uhuru wa kumwabudu Mungu kwa njia inayokubalika? Ndiyo! Miale ya nuru ya kiroho ilianza kuangaza ndani ya giza kwa sababu ya mambo mawili muhimu. Jambo la kwanza ni kuvumbuliwa kwa mashine ya kuchapisha yenye herufi za kupangwa katika miaka ya 1450. Kabla ya mashine za kuchapisha kuvumbuliwa katika nchi za Magharibi, watu walinakili Biblia kwa mkono na walifanya hivyo kwa makini sana. Nakala za Biblia zilikuwa chache na ghali sana. Inasemekana kwamba ingemchukua mwandikaji stadi miezi kumi kutokeza nakala moja tu ya Biblia! Isitoshe, ngozi zilizotumiwa ili kunakili Biblia zilikuwa ghali. Tofauti na hilo, kwa kutumia mashine inayotumia karatasi, mchapishaji stadi angeweza kutokeza kurasa 1,300 kwa siku!

Uvumbuzi wa mashine za kuchapisha na ujasiri wa watafsiri wa Biblia ulisaidia kupunguza uvutano wa Babiloni Mkubwa (Tazama fungu la 12 na la 13)

13 Jambo la pili lenye kutokeza ni uamuzi ambao wanaume wachache jasiri walifanya mwanzoni mwa karne ya 16; walitafsiri Neno la Mungu katika lugha ambazo watu wengi walizungumza. Watafsiri wengi walihatarisha maisha yao kwa kufanya kazi hiyo. Kanisa liliogopa sana. Viongozi wa dini walihisi kwamba kumpa mtu aliyemwogopa Mungu Biblia ni kama kumpa silaha hatari! Na kadiri Biblia ilivyopatikana kwa urahisi, watu waliendelea kuisoma. Na walipoisoma waliuliza maswali kama vile: ‘Ni wapi katika Neno la Mungu ambapo toharani pametajwa, kulipia Misa kwa ajili ya wafu, au mapapa na makadinali?’ Kwa maoni ya kanisa, hilo lilikuwa jambo lenye kughadhabisha sana. Watu hawakupaswa kutilia shaka viongozi wa kanisa hata kidogo! Kanisa nalo likalipiza kisasi. Wanaume na wanawake walihukumiwa kuwa waasi kwa sababu walikataa mafundisho ya kanisa. Baadhi ya mafundisho hayo yalitegemea falsafa za Aristoto na Plato, watu walioishi kabla ya Yesu Kristo kuzaliwa. Kanisa lilitoa hukumu ya kifo, nayo Serikali ikatekeleza hukumu hiyo. Lengo lilikuwa kuwavunja moyo watu wasiisome Biblia na hivyo kutilia shaka kanisa. Njama hiyo ilifanikiwa kwa kiwango kikubwa. Hata hivyo, watu wachache jasiri walikataa kuogopeshwa na Babiloni Mkubwa. Walikuwa wameonja Neno la Mungu na sasa walitaka kuendelea kujifunza. Sasa njia ya kukombolewa kutoka dini za uwongo ikaanza kupatikana.

14. (a) Ni hali gani zilizowasaidia watu kuelewa kweli ya Biblia vizuri zaidi katika mwaka wa 1870? (b) Eleza jinsi Ndugu Russell alivyoitafuta kweli.

14 Watu wengi waliokuwa na kiu ya ukweli wa Biblia walikimbilia nchi ambazo hazikuwa na uvutano mkubwa wa kanisa. Walitaka kusoma, kujifunza, na kuzungumzia Biblia wakiwa huru kutokana na mafundisho ya kanisa. Katika mwaka wa 1870, Charles Taze Russell na wenzake, walianza kujifunza Biblia kwa makini wakiwa Marekani, moja ya nchi ambazo hazikuwa na uvutano mkubwa wa kanisa. Mwanzoni, lengo la Ndugu Russell lilikuwa kuchunguza ikiwa kuna dini inayofundisha kweli. Alikuwa amelinganisha kwa uangalifu kile ambacho Biblia inasema na mafundisho ya dini tofauti-tofauti, hata dini ambazo si za Kikristo. Haikumchukua muda mrefu kutambua kwamba hakukuwa na dini yoyote iliyoshikamana kikamili na Neno la Mungu. Wakati fulani, Russell alikutana na makasisi kadhaa akitumaini kwamba wangekubali kweli ambazo yeye na wenzake walikuwa wamejifunza katika Biblia, na kwamba wangewafundisha washiriki wa dini zao kweli hizo. Makasisi hawakupendezwa na wazo hilo. Wanafunzi wa Biblia walilazimika kukubali ukweli huu: Haingewezekana kushirikiana na watu ambao wameazimia kushikamana na dini za uwongo.—Soma 2 Wakorintho 6:14.

15. (a) Wakristo waliingia katika utumwa wa Babiloni Mkubwa lini? (b) Ni maswali gani tutakayochunguza katika makala inayofuata?

15 Kufikia sasa tumeona kwamba Wakristo wa kweli waliingia kwenye utekwa wa Babiloni muda mfupi baada kifo cha mtume wa mwisho. Hata hivyo, jambo hilo linatokeza maswali kadhaa: Kuna uthibitisho gani zaidi kwamba katika miongo iliyotangulia mwaka 1914, watiwa mafuta walikuwa wameanza kutoka kwenye uvutano wa Babiloni Mkubwa, na hivyo kuacha kuwa watumwa wake? Je, ni kweli kwamba watumishi wa Yehova walipoteza kibali chake kwa sababu walipunguza bidii yao ya kuhubiri wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu? Na je, ni kweli kwamba baadhi ya ndugu zetu walivunja msimamo wao wa kutounga mkono upande wowote katika kipindi hicho cha vita, na hivyo kupoteza kibali cha Yehova? Na la mwisho ni, ikiwa Wakristo waliingia katika utekwa wa dini za uwongo kuanzia karne ya pili W.K., waliachiliwa huru lini? Hayo ni maswali mazuri sana. Yatajibiwa katika makala inayofuata.