Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Iga Haki na Rehema ya Yehova

Iga Haki na Rehema ya Yehova

“Fanyeni hukumu kwa haki ya kweli; na mtendeane kwa fadhili zenye upendo na rehema.”—ZEK. 7:9.

NYIMBO: 125, 88

1, 2. (a) Yesu alikuwa na maoni gani kuhusu Sheria ya Mungu? (b) Waandishi na Mafarisayo waliipotoshaje Sheria?

YESU aliipenda Sheria ya Musa. Na hilo halishangazi! Sheria hiyo ilitoka kwa Yehova, Baba yake—Mtu muhimu zaidi maishani mwake. Andiko la Zaburi 40:8 linaonyesha kwa njia ya kiunabii jinsi Yesu alivyoipenda sana sheria ya Mungu. Linasema hivi: “Ee Mungu wangu, nimependezwa na kufanya mapenzi yako, na sheria yako imo ndani yangu.” Kupitia maneno na matendo yake, Yesu alithibitisha kwamba Sheria ya Mungu ni kamilifu, ina manufaa, na kwa hakika itatimizwa.—Mt. 5:17-19.

2 Basi, lazima Yesu alisikitika sana kuwaona waandishi na Mafarisayo wakiipotosha Sheria ya Baba yake! Walifuatilia sana baadhi ya mambo madogo-madogo ya Sheria hiyo, na ndiyo sababu Yesu alisema: “Ninyi huitoa sehemu ya kumi ya mnanaa na dili na bizari.” Tatizo lilikuwa nini? Alisema hivi: “Lakini mmepuuza mambo mazito zaidi ya Sheria, yaani, haki na rehema na uaminifu.” (Mt. 23:23) Tofauti na Mafarisayo waliojiona kuwa waadilifu kupita kiasi, Yesu alielewa kusudi halisi la Sheria, yaani, sifa za Mungu zilizoonekana kupitia kila amri.

3. Tutazungumzia nini katika makala hii?

3 Tukiwa Wakristo, hatuko chini ya agano la Sheria. (Rom. 7:6) Hata hivyo, Yehova aliruhusu Sheria hiyo iandikwe katika Neno lake, Biblia, kwa ajili yetu. Yehova hataki tufuatilie mambo madogo-madogo ya Sheria hiyo, bali anataka tutambue na kutumia “mambo mazito,” yaani, kanuni zinazopatikana katika Sheria hiyo. Kwa mfano, ni kanuni zipi tunazoweza kujifunza kutokana na mpango wa majiji ya makimbilio? Makala iliyotangulia ilizungumzia mambo tunayojifunza kutokana na hatua ambazo mkimbizi alipaswa kuchukua. Lakini mpango huo unatufunza pia kumhusu Yehova na jinsi tunavyoweza kuiga sifa zake. Kwa hiyo, makala hii itajibu maswali matatu: Majiji ya makimbilio yanaonyeshaje rehema ya Yehova? Yanatufundisha nini kuhusu jinsi anavyouona uhai? Yanaonyeshaje haki yake kamilifu? Tunapojibu kila swali, tafuta ni katika njia zipi unaweza kumwiga Baba yako wa mbinguni.—Soma Waefeso 5:1.

MAJIJI YALIYO RAHISI KUFIKIKA YAONYESHA REHEMA YA YEHOVA

4, 5. (a) Ni mambo gani yaliyofanywa ili majiji ya makimbilio yawe rahisi kufikika, na kwa nini? (b) Hilo linatufundisha nini kumhusu Yehova?

4 Majiji sita ya makimbilio yalikuwa rahisi kufikika. Yehova aliwaamuru Waisraeli wawe na idadi sawa ya majiji ya makimbilio katika pande zote mbili za Mto Yordani. Kwa nini? Ili iwe rahisi kwa mkimbizi yeyote kukimbilia huko haraka. (Hes. 35:11-14) Njia zilizoelekea kwenye majiji ya makimbilio zilidumishwa katika hali nzuri. (Kum. 19:3) Kulingana na mapokeo ya Wayahudi, kulikuwa na alama au ishara zilizowekwa njiani ili kuwaelekeza wakimbizi kwenye majiji hayo. Kwa kuwa majiji ya makimbilio yalikuwepo, muuaji asiyekusudia hangelazimika kukimbilia nchi nyingine ambako angeshawishiwa kujiunga na ibada ya uwongo.

5 Fikiria hili: Yehova—ambaye alikuwa ameamuru kwamba wauaji wa kukusudia wapewe adhabu ya kifo—aliwapa wauaji wasiokusudia nafasi ya kutosha ya kupokea huruma na ulinzi! Msomi mmoja aliandika hivi: “Mambo yote yalikuwa wazi na rahisi kueleweka. Hivyo ndivyo Mungu anavyofanya mambo kwa neema.” Yehova si hakimu asiye na huruma anayetamani kuwaadhibu watumishi wake. Badala yake, yeye ni “tajiri katika rehema.”—Efe. 2:4.

6. Mtazamo wa Mafarisayo ulitofautianaje na rehema za Mungu?

6 Kwa upande mwingine, Mafarisayo walisita kuwaonyesha wengine rehema. Kwa mfano, kulingana na mapokeo ya Wayahudi, hawakuwa tayari kusamehe kosa lilelile zaidi ya mara tatu. Yesu alitaja waziwazi mtazamo waliokuwa nao kuelekea wakosaji aliposimulia mfano wa Farisayo fulani aliyesali hivi: “Ee Mungu, ninakushukuru ya kuwa mimi si kama wale watu wengine, wanyang’anyi, wasio waadilifu, wazinzi, au hata kama mkusanya-kodi huyu”—mkusanya-kodi ambaye alikuwa akisali kwa unyenyekevu kwamba Mungu amwonyeshe rehema. Kwa nini ilikuwa vigumu sana kwa Mafarisayo kuonyesha rehema? Biblia inasema kwamba ‘waliwaona wengine kama si kitu.’—Luka 18:9-14.

Je, unaiweka wazi “njia” itakayowawezesha wengine kukufikia ili kuomba msamaha? Wafanye wengine wahisi huru kuzungumza nawe (Tazama fungu la 4 hadi 8)

7, 8. (a) Mtu akikukosea, unaweza kumwigaje Yehova? (b) Kwa nini ni lazima tuwe wanyenyekevu ili tuwasamehe wengine?

7 Mwige Yehova, usiwaige Mafarisayo. Waonyeshe wengine huruma. (Soma Wakolosai 3:13.) Njia moja ya kufanya hivyo ni kufanya iwe rahisi kwa wengine kukuomba msamaha. (Luka 17:3, 4) Jiulize hivi: ‘Je, niko tayari kuwasamehe watu ambao wamenikosea, hata ikiwa wamefanya hivyo mara nyingi? Je, ninatamani kurudisha amani pamoja na mtu ambaye amenikosea au kuniumiza?’

8 Ni lazima tuwe wanyenyekevu ili tuwasamehe wengine. Mafarisayo hawakuwa wanyenyekevu kwa sababu waliwaona wengine kuwa duni. Hata hivyo, tukiwa Wakristo tunapaswa kuwa wanyenyekevu kwa ‘kuwaona wengine kuwa bora’ kuliko sisi, kwamba wanastahili kusamehewa. (Flp. 2:3) Je, utamwiga Yehova na kuwa mnyenyekevu? Iweke wazi “njia” itakayowawezesha wengine kukufikia ili kuomba msamaha. Uwe mwepesi wa kuonyesha rehema, usiwe mwepesi wa kuudhika.—Mhu. 7:8, 9.

HESHIMU UHAI, NA ‘HATIA YOYOTE YA DAMU HAITAKUJA JUU YAKO’

9. Yehova alikaziaje kwa Waisraeli kwamba uhai wa mwanadamu ni mtakatifu?

9 Kusudi kuu la majiji ya makimbilio lilikuwa kuwalinda Waisraeli wasiwe na hatia ya damu. (Kum. 19:10) Yehova anapenda uhai, naye anachukia “mikono inayomwaga damu isiyo na hatia.” (Met. 6:16, 17) Kwa kuwa yeye ni Mungu mwenye haki na mtakatifu, hawezi kamwe kupuuza hata kifo ambacho kilitokea bila kukusudiwa. Ni kweli kwamba muuaji asiyekusudia alionyeshwa rehema. Hata hivyo, alipaswa kuwasilisha kesi yake mbele ya wazee, na ikiwa wangeamua kwamba aliua bila kukusudia, alipaswa kukaa katika jiji la makimbilio mpaka kuhani mkuu alipokufa. Hilo lilimaanisha kwamba huenda angekaa huko maisha yake yote. Vizuizi hivyo vilikazia akilini mwa Waisraeli wote kwamba uhai wa mwanadamu ni mtakatifu. Ili kuonyesha kwamba wanamheshimu Mpaji wa uhai, walihitaji kufanya yote wawezayo ili wasihatarishe uhai wa mwanadamu mwenzao.

10. Maneno ya Yesu yalionyeshaje kwamba waandishi na Mafarisayo hawakujali uhai hata kidogo?

10 Tofauti na maoni ya Yehova, waandishi na Mafarisayo hawakujali uhai hata kidogo. Jinsi gani? Yesu aliwaambia hivi: “Mliuondoa ufunguo wa ujuzi; ninyi wenyewe hamkuingia, na wale wanaoingia mliwazuia!” (Luka 11:52) Walipaswa kuwafungulia watu maana ya Neno la Mungu na kuwasaidia kutembea katika barabara ya uzima wa milele. Badala ya kuwaelekeza watu kwa Yesu, “Wakili Mkuu wa uzima,” waliwaelekeza kwenye njia iliyowaongoza kwenye uharibifu wa milele. (Mdo. 3:15) Kwa sababu ya kiburi na ubinafsi, waandishi na Mafarisayo hawakujali uhai na hali njema ya wanadamu wenzao. Huo ulikuwa ukatili na ukosefu mkubwa sana wa rehema!

11. (a) Mtume Paulo alionyeshaje kwamba alikuwa na maoni kama ya Mungu kuhusu uhai? (b) Ni nini kitakachotusaidia kuwa na mtazamo kama wa Paulo kuelekea huduma?

11 Tunaweza kuepukaje mtazamo wa waandishi na Mafarisayo na hivyo kumwiga Yehova? Tunapaswa kuheshimu na kuthamini zawadi ya uhai. Mtume Paulo alifanya hivyo kwa kutoa ushahidi kamili. Kwa hiyo angeweza kusema hivi: “Mimi ni safi kutokana na damu ya watu wote.” (Soma Matendo 20:26, 27.) Hata hivyo, Paulo hakuchochewa kuhubiri kwa sababu ya kuhisi hatia au ili tu kutimiza wajibu. Badala yake, aliwapenda watu, na aliona uhai wao kuwa wenye thamani. (1 Kor. 9:19-23) Sisi pia tunapaswa kujitahidi kusitawisha maoni ya Mungu kuhusu uhai. Yehova ‘anataka wote wafikie toba.’ (2 Pet. 3:9) Vipi wewe? Utagundua kwamba ukisitawisha moyoni mwako mtazamo wa kuonyesha rehema, bidii yako katika huduma itaongezeka na utakuwa na shangwe nyingi unapofanya hivyo.

12. Kwa nini ni muhimu kwa watu wa Mungu kuzingatia usalama?

12 Tunaonyesha kwamba tuna maoni kama ya Yehova kuhusu uhai kwa kusitawisha mtazamo unaofaa kuelekea usalama. Sikuzote, tunapaswa kuzingatia usalama tunapoendesha gari na tunapofanya kazi, kutia ndani tunapojenga au kudumisha majengo yetu ya ibada, au tunaposafiri kwenda kwenye ibada. Hatupaswi kamwe kuona kukamilisha kazi, kuokoa pesa, au kukomboa wakati kuwa muhimu kuliko usalama au afya. Sikuzote, Mungu wetu mwenye haki hutenda yaliyo sawa na yanayofaa. Tunataka kumwiga. Wazee hasa hujitahidi kuzingatia usalama wao na wa wale wanaofanya kazi pamoja nao. (Met. 22:3) Hivyo, mzee akikukumbusha kuhusu viwango na sheria za usalama, kubali shauri lake. (Gal. 6:1) Uwe na maoni kama ya Yehova kuhusu uhai, na ‘hatia yoyote ya damu haitakuja juu yako.’

‘HUKUMU KULINGANA NA HUKUMU HIZI’

13, 14. Wazee wa Israeli wangeweza kuonyeshaje kwamba wana maoni ya Yehova kuhusu haki?

13 Yehova aliwaamuru wazee wa Israeli waige viwango vyake vya juu vya haki. Kwanza, wazee walihitaji kupata habari kamili. Kisha, walipaswa kuchunguza kwa makini nia, mtazamo, na mwenendo wa zamani wa muuaji ili waamue ikiwa watamwonyesha rehema. Ili kuonyesha kwamba wana maoni ya Mungu kuhusu haki, walipaswa kuchunguza ikiwa mkimbizi alitenda kwa “chuki” na ‘ikiwa alimvizia’ mtu huyo aliyeuawa. (Soma Hesabu 35:20-24.) Ikiwa ushahidi ulihitajika, angalau mashahidi wawili wangetoa ushahidi kuthibitisha kwamba mauaji hayo yalikuwa ya kimakusudi.—Hes. 35:30.

14 Hivyo, baada ya kupata habari kamili, wazee walipaswa kufikiria jinsi mtu huyo alivyo kwa ujumla, si tu kitendo alichofanya. Walihitaji kuwa na ufahamu, yaani, uwezo wa kutambua mambo yasiyoonekana waziwazi na kuelewa hali halisi. Zaidi ya yote, walihitaji roho takatifu ya Yehova ambayo ingewawezesha kuwa na ufahamu na kuonyesha rehema na haki ya Yehova.—Kut. 34:6, 7.

15. Eleza tofauti kati ya mtazamo wa Yesu na wa Mafarisayo kuelekea watenda-dhambi.

15 Mafarisayo walikazia tu kosa la mtenda-dhambi badala ya hali yake ya moyoni. Mafarisayo walipomwona Yesu akihudhuria karamu katika nyumba ya Mathayo, waliwauliza wanafunzi wake hivi: “Kwa nini mwalimu wenu anakula pamoja na wakusanya-kodi na watenda-dhambi?” Yesu alijibu hivi: “Watu wenye afya hawahitaji tabibu, bali wenye kuugua ndio wanaomhitaji. Nendeni, basi, mkajifunze maana ya jambo hili, ‘Ninataka rehema, wala si dhabihu.’ Kwa maana nilikuja kuwaita, si watu waadilifu, bali watenda-dhambi.” (Mt. 9:9-13) Je, Yesu alikuwa akipuuza makosa mazito? La hasha. Kwa kweli, ujumbe wa msingi wa Yesu ulitia ndani kuwahimiza watu watubu dhambi zao. (Mt. 4:17) Isitoshe, kwa kutumia utambuzi, Yesu aliona kwamba baadhi ya “wakusanya-kodi na watenda-dhambi” walitaka kubadilika. Watu hao hawakuwa wamefika nyumbani kwa Mathayo ili kula tu. Badala yake, “wengi wao walimfuata” Yesu. (Marko 2:15, Biblia ya Kiafrika) Kwa kusikitisha, Mafarisayo wengi hawakuona kile ambacho Yesu aliona ndani ya watu hao. Tofauti na Mungu mwenye rehema ambaye walidai wanamwabudu, Mafarisayo waliwaona wanadamu wenzao kuwa watenda-dhambi wasioweza kubadilika.

16. Halmashauri ya hukumu hujitahidi kutambua nini?

16 Leo, wazee wanapaswa kuhakikisha kwamba wanamwiga Yehova, Mungu “mpenda-haki.” (Zab. 37:28) Kwanza, wanapaswa “kupeleleza na kuuliza habari kabisa” ili kuhakikisha kwamba kosa limefanywa. Ikiwa kosa limefanywa, basi watalishughulikia kwa kufuata mwongozo wa Kimaandiko. (Kum. 13:12-14) Wanapokuwa kwenye halmashauri ya hukumu, wanapaswa kuchunguza kwa makini ili wajue ikiwa Mkristo aliyetenda dhambi nzito ametubu. Si rahisi nyakati zote kutambua ikiwa mtu ametubu au hajatubu. Toba inahusisha mtazamo na mwelekeo wa mtu kuelekea dhambi aliyofanya na hali yake ya moyoni. (Ufu. 3:3) Ni lazima mtenda-dhambi atubu ili aonyeshwe rehema. *

17, 18. Wazee wanaweza kutambuaje toba ya kweli? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

17 Tofauti na Yehova na Yesu, wazee hawawezi kusoma mioyo. Hivyo basi, ikiwa wewe ni mzee, unaweza kufanya nini ili uweze kutambua toba ya kweli? Kwanza, sali upate hekima na utambuzi. (1 Fal. 3:9) Pili, chunguza Neno la Mungu na machapisho ya mtumwa mwaminifu ili yakusaidie kutofautisha kati ya “huzuni ya ulimwengu” na “huzuni kwa njia ya kimungu,” yaani, toba ya kweli. (2 Kor. 7:10, 11) Chunguza mifano ya Kimaandiko ya watu waliotubu kikweli na wale ambao hawakuonyesha toba ya kweli. Biblia inafafanuaje hisia, mtazamo, na mwenendo wao?

18 Mwishowe, jaribu kutambua jinsi mtu huyo alivyo kwa ujumla. Zingatia malezi, nia, na udhaifu wa mtenda-dhambi. Biblia ilitabiri hivi kumhusu Yesu, kichwa cha kutaniko la Kikristo: “Hatahukumu kulingana na sura inayoonekana kwa macho yake tu, wala kukaripia kulingana tu na jambo lililosikiwa na masikio yake. Naye atawahukumu kwa uadilifu watu wa hali ya chini, atakaripia kwa unyoofu kwa ajili ya watu wapole wa dunia.” (Isa. 11:3, 4) Enyi wazee, ninyi ni wachungaji mlio chini ya usimamizi wa Yesu, naye atawasaidia kuhukumu kama anavyohukumu. (Mt. 18:18-20) Je, hatufurahi kwamba tuna wazee wenye kujali wanaojitahidi kumwiga Yesu? Tunathamini sana jinsi wanavyojitahidi sikuzote kuonyesha rehema na haki katika makutaniko yetu!

19. Ni mambo gani uliyojifunza kuhusu majiji ya makimbilio unayopanga kutumia maishani?

19 Sheria ya Musa ilitoa “picha ya ujuzi na ya ile kweli” kumhusu Yehova na kanuni zake za uadilifu. (Rom. 2:20) Kwa mfano, majiji ya makimbilio yanawafundisha wazee jinsi ya ‘kufanya hukumu kwa haki ya kweli,’ nayo yanatufundisha sisi sote jinsi ya ‘kutendeana kwa fadhili zenye upendo na rehema.’ (Zek. 7:9) Hatuko tena chini ya Sheria ya Musa. Hata hivyo, Yehova habadiliki, na bado anaona sifa ya haki na rehema kuwa muhimu machoni pake. Ni pendeleo kubwa sana kumwabudu Mungu ambaye alituumba kwa mfano wake, Mungu ambaye tunaweza kuiga sifa zake, na ambaye tunaweza kumfanya kuwa kimbilio letu!

^ fu. 16 Tazama makala yenye kichwa “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Septemba 15, 2006, ukurasa wa 30.