Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Imba kwa Shangwe na Sauti Kubwa!

Imba kwa Shangwe na Sauti Kubwa!

“Ni vema kumpigia Mungu wetu muziki.”—ZAB. 147:1.

NYIMBO: 10, 2

1. Kuimba hutusaidia kufanya nini?

MTUNZI mmoja maarufu wa nyimbo alisema hivi pindi moja: “Maneno hufanya upate wazo fulani. Muziki hufanya upate hisia fulani. Lakini unapoimba wimbo, maneno yake hugusa moyo.” Hakuna maneno yanayoweza “kugusa” moyo kuliko maneno ya kumsifu na ya kumweleza Baba yetu wa mbinguni Yehova kwamba tunampenda! Hivyo basi, haishangazi kwamba kuimba ni sehemu muhimu ya ibada safi, iwe tunaimba tukiwa peke yetu au pamoja na kutaniko la watu wa Mungu.

2, 3. (a) Huenda baadhi ya watu wakahisije kuhusu kuimba kwa sauti kubwa kutanikoni? (b) Tutachunguza maswali gani?

2 Hata hivyo, unahisije kuhusu kuimba kwa sauti kubwa kutanikoni? Je, wewe huaibika? Katika tamaduni fulani, huenda wanaume wakaona aibu kuimba hadharani. Mtazamo huo unaweza kuathiri kutaniko lote, hasa ikiwa ndugu wanaoongoza wanajitafutia sababu za kutoimba, au wanafanya shughuli nyingine kutaniko linapoimba.—Zab. 30:12.

3 Ikiwa kwa kweli tunaona kuimba kuwa sehemu muhimu ya ibada yetu, basi hatutatoka nje au kukosa kuwepo wakati wa sehemu hiyo ya mkutano. Hivyo, kila mmoja wetu anapaswa kujiuliza hivi: ‘Nina maoni gani kuhusu kuimba katika mikutano yetu ya ibada? Ninaweza kufanya nini ili kushinda woga wowote unaonizuia kuimba kwa shangwe na sauti kubwa? Na ninaweza kufanya nini ili nitokeze kikamili hisia za nyimbo tunazoimba?’

KUIMBA NI SEHEMU MUHIMU YA IBADA YA KWELI

4, 5. Kulikuwa na mipango gani ya kuimba hekaluni katika Israeli la kale?

4 Kwa muda mrefu waabudu waaminifu wa Yehova wamekuwa wakitumia muziki kumsifu Yehova. Jambo lenye kutokeza ni kwamba Waisraeli wa kale walipokuwa wakimtumikia Yehova kwa uaminifu, kuimba kulikuwa sehemu muhimu ya ibada yao. Kwa mfano, Mfalme Daudi alipokuwa akifanya matayarisho kwa ajili ya hekalu, alipanga kikundi cha Walawi 4,000 ili wamsifu Yehova kwa muziki. Miongoni mwao kulikuwa na Walawi 288 “waliozoezwa nyimbo kwa Yehova, wote wakiwa wajuzi.”—1 Nya. 23:5; 25:7.

5 Wakati wa kuzinduliwa kwa hekalu, muziki na kuimba zilikuwa sehemu muhimu ya tukio hilo. Simulizi hilo linasema hivi: “Ikawa kwamba mara tu wapiga-tarumbeta na waimbaji walipokuwa kama mtu mmoja kwa kutokeza sauti moja isikike katika kumsifu na kumshukuru Yehova, na mara tu walipopaaza sauti kwa tarumbeta na kwa matoazi na kwa vyombo vya nyimbo na kwa kumsifu Yehova, . . . utukufu wa Yehova uliijaza nyumba ya Mungu wa kweli.” Hilo lilikuwa tukio lenye kuimarisha imani sana!—2 Nya. 5:13, 14; 7:6.

6. Eleza kuhusu mipango ya pekee ya uimbaji ambayo Nehemia alifanya alipokuwa gavana jijini Yerusalemu.

6 Nehemia alipowaongoza Waisraeli waaminifu kufanya kazi ya kujenga upya kuta za Yerusalemu, alipanga pia kuwe na Walawi walioimba na kupiga ala za muziki. Wakati wa kuzinduliwa kwa kuta hizo, kulikuwa na uimbaji wa pekee uliochangia sana shangwe ya tukio hilo. Wakati huu, kulikuwa na “makundi mawili makubwa ya waimbaji ya kutoa shukrani.” Kikundi kimoja kilielekea upande wa kulia na kikundi kingine kikaelekea upande wa kushoto na kukutana juu ya ukuta ulio karibu na eneo la hekalu ili kutokeza sauti ambayo ingeweza kusikika mbali sana. (Neh. 12:27, 28, 31, 38, 40, 43) Bila shaka, Yehova alifurahi kusikia waabudu wake wakimwimbia nyimbo za sifa kwa uchangamfu.

7. Yesu alionyeshaje umuhimu wa kuimba katika ibada ya Kikristo?

7 Kutaniko la Kikristo lilipoanzishwa, muziki uliendelea kuwa sehemu muhimu ya ibada ya kweli. Kwenye usiku muhimu zaidi katika historia ya wanadamu, baada ya kuanzisha Mlo wa Jioni wa Bwana, Yesu pamoja na wanafunzi wake waliimba nyimbo.—Soma Mathayo 26:30.

8. Wakristo wa karne ya kwanza walituwekea kielelezo gani cha kuimba katika ibada?

8 Wakristo wa karne ya kwanza walituwekea kielelezo cha kumsifu Mungu kwa nyimbo. Ingawa mara nyingi walikutana katika nyumba za watu binafsi ambazo hazikuwa za kifahari, hilo halikupunguza bidii yao ya kumwimbia Yehova. Akiongozwa na roho ya Mungu, mtume Paulo aliwahimiza hivi ndugu zake Wakristo: “Endeleeni kufundishana na kuonyana kwa zaburi, sifa kwa Mungu, nyimbo za kiroho kwa neema.” (Kol. 3:16) Kwa kweli, nyimbo zilizo katika kitabu chetu cha nyimbo ni “nyimbo za kiroho” zinazopaswa kuimbwa kwa shukrani. Nyimbo hizo ni sehemu ya chakula cha kiroho kinachoandaliwa na “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.”—Mt. 24:45.

KUSHINDA WOGA WA KUIMBA

9. (a) Ni nini kinachoweza kuwazuia baadhi ya watu kuimba kwa shangwe na sauti kubwa katika mikutano na makusanyiko? (b) Tunapaswa kumwimbia Yehova sifa jinsi gani, na ni nani wanaopaswa kuwa mstari wa mbele kuimba? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

9 Vipi ikiwa kuimba si jambo la kawaida katika familia, utamaduni, au mazingira yenu? Teknolojia imefanya iwe rahisi kufurahia kuwasikiliza waimbaji stadi wakiimba. Hata hivyo, unapolinganisha sauti yako na sauti ya waimbaji katika ulimwengu wa burudani, huenda ukaaibika au kuvunjika moyo. Lakini hilo halipaswi kukuzuia kutimiza jukumu lako la kumwimbia Yehova sifa. Badala yake, inua juu kitabu chako cha nyimbo, inua kichwa chako, na uimbe kutoka moyoni! (Ezra 3:11; soma Zaburi 147:1.) Leo, katika Majumba mengi ya Ufalme, maneno ya nyimbo huonyeshwa kwenye skrini, jambo ambalo hutusaidia kuimba kwa sauti kubwa. Pia, inapendeza kwamba sasa kuimba nyimbo za Ufalme ni sehemu ya mtaala wa Shule ya Huduma ya Ufalme kwa ajili ya wazee. Hilo linakazia kwamba wazee wanapaswa kuwa mstari wa mbele inapohusu kuimba kutanikoni.

10. Tunapaswa kukumbuka nini ikiwa woga unatuzuia kuimba kwa sauti kubwa?

10 Jambo moja linalofanya watu wengi wasiimbe kwa sauti kubwa ni woga. Huenda wanaogopa kwamba wataimba kwa sauti kubwa sana au hawataimba vizuri. Hata hivyo, tunapaswa kukumbuka kwamba “sisi sote hujikwaa mara nyingi” tunapozungumza. (Yak. 3:2) Lakini hilo halitufanyi tuache kuzungumza. Hivyo basi, kwa nini turuhusu sauti zetu zisizo kamilifu zituzuie kumsifu Yehova kwa nyimbo?

11, 12. Unaweza kutumia mapendekezo gani ili kuboresha jinsi unavyoimba?

11 Huenda tukaogopa kuimba kwa sababu hatujui jinsi ya kuimba. Hata hivyo, tunaweza kuboresha uimbaji wetu kwa kufuata mapendekezo fulani ya msingi. *

12 Unaweza kujifunza kuimba kwa sauti kubwa yenye nguvu kwa kupumua vizuri. Sawa tu na jinsi umeme unavyowasha taa, kupumua vizuri hufanya sauti yako iwe na nguvu unapozungumza au kuimba. Unapaswa kuimba kwa sauti kubwa kama unayotumia unapozungumza au hata kubwa zaidi. (Tazama mapendekezo yanayopatikana katika kitabu Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, ukurasa wa 181 hadi 184, chini ya kichwa kidogo “Pumua Vizuri.”) Nyakati nyingine Maandiko yanapozungumza kuhusu kuimba sifa, yanawaagiza waabudu wa Yehova ‘wapige vigelegele vya shangwe,’ yaani, wapaze sauti kwa shangwe.—Zab. 33:1-3.

13. Eleza jinsi tunavyoweza kuimba kwa ujasiri.

13 Wakati wa ibada ya familia au ukiwa peke yako, jaribu kufanya mambo yafuatayo: Chagua wimbo mmoja unaoupenda kutoka katika kitabu chetu cha nyimbo. Soma maneno yake kwa sauti kubwa yenye nguvu. Kisha, kwa sauti hiyohiyo, soma maneno ya mstari mmoja (mshororo) bila kuvuta pumzi. Kisha imba mstari huo kwa sauti hiyohiyo yenye nguvu. (Isa. 24:14) Sauti yako itakuwa yenye nguvu, na hilo ni jambo zuri. Usiogope wala kuaibika!

14. (a) Kufungua mdomo wazi kabisa kunaweza kutusaidiaje tunapoimba? (Tazama pia sanduku “ Jinsi ya Kuboresha Uimbaji Wako.”) (b) Wewe binafsi unaweza kutumia mapendekezo gani ili kushinda mambo yanayokuzuia usiimbe vizuri?

14 Ili uimbe kwa sauti yenye nguvu, lazima ufungue mdomo wako kabisa. Kwa hiyo, unapoimba fungua mdomo wako wazi zaidi ya unavyoufungua unapozungumza. Unapaswa kufanya nini ikiwa unahisi kuwa sauti yako ni dhaifu au ni nyembamba sana? Unaweza kupata mapendekezo kuhusu matatizo hayo katika kitabu Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi, ukurasa wa 184, kwenye sanduku lenye kichwa “Kushinda Matatizo Fulani Hususa.”

IMBA SIFA KUTOKA MOYONI

15. (a) Ni tangazo gani lililotolewa kwenye mkutano wa kila mwaka wa 2016? (b) Kwa nini kitabu kipya cha nyimbo kilitolewa?

15 Kulikuwa na msisimko kwenye mkutano wa kila mwaka wa Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania wa mwaka wa 2016, Ndugu Stephen Lett wa Baraza Linaloongoza alipotangaza kwamba kitabu kipya cha nyimbo cha Kiingereza chenye kichwa ‘Mwimbieni Yehova kwa Shangwe,’ kingeanza kutumiwa kwenye mikutano baada ya muda mfupi. Ndugu Lett alieleza kwamba sababu moja ya kurekebisha kitabu cha nyimbo ni ili kukipatanisha na Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya iliyorekebishwa. Maneno ya nyimbo fulani yaliondolewa au kurekebishwa kwa sababu hayatumiwi tena katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya toleo la 2013. Isitoshe, nyimbo mpya kuhusu kazi yetu ya kuhubiri na nyimbo zinazoonyesha shukrani zetu kwa ajili ya fidia zimeongezwa. Pia, kwa sababu nyimbo ni sehemu muhimu ya ibada yetu, Baraza Linaloongoza lilitaka kuchapisha kitabu cha nyimbo chenye ubora wa hali ya juu, chenye jalada linalofanana na la Tafsiri ya Ulimwengu Mpya iliyorekebishwa.

16, 17. Ni marekebisho gani yaliyofanywa katika kitabu kipya cha nyimbo?

16 Ili kufanya iwe rahisi zaidi kutumia kitabu ‘Mwimbieni Yehova kwa Shangwe,’ nyimbo zimepangwa kulingana na habari kuu. Kwa mfano, nyimbo 12 za kwanza ni kuhusu Yehova, nyimbo 8 zinazofuata ni kuhusu Yesu na fidia, na kadhalika. Kuna fahirisi ambayo inaweza kuwasaidia akina ndugu wanapochagua nyimbo kwa ajili ya hotuba za watu wote.

17 Ili kuwasaidia wote waimbe kutoka moyoni, baadhi ya maneno yamerekebishwa ili ujumbe wa wimbo uwe wazi na maneno ambayo hayatumiwi tena yameondolewa. Kwa mfano, kichwa “Ustahimilivu” kimebadilishwa na kuwa “Iweni na Subira,” na maneno ya wimbo huo yamebadilishwa ili yapatane na kichwa. Uamuzi wa kurekebisha kichwa “Linda Moyo Wako” kuwa “Tuulinde Moyo Wetu” ulifaa sana. Kwa nini? Miongoni mwa wale wanaohudhuria mikutano na makusanyiko yetu kuna wapya, wanaopendezwa, watoto, na akina dada ambao hawangehisi huru kuimba maneno ya wimbo huo kwani kufanya hivyo kungekuwa sawa na kuwaambia wengine jambo la kufanya. Kwa sababu hiyo, kichwa na maneno ya wimbo yalirekebishwa.

Fanyeni mazoezi ya kuimba wakati wa ibada ya familia (Tazama fungu la 18)

18. Kwa nini tunapaswa kujua vizuri nyimbo zilizo katika kitabu chetu kipya cha nyimbo? (Tazama maelezo ya chini.)

18 Nyimbo nyingi katika kitabu ‘Mwimbieni Yehova kwa Shangwe,’ zimetungwa katika mtindo wa sala. Kupitia nyimbo hizo, unaweza kumweleza Yehova hisia zako za ndani. Nyimbo nyingine ‘zitatuchochea katika upendo na matendo mazuri.’ (Ebr. 10:24) Bila shaka tungependa kujua vizuri muziki, mdundo, na maneno ya nyimbo zetu. Ukijizoeza kuimba nyimbo hizo nyumbani, utajifunza kuimba kwa ujasiri na kutoka moyoni. *

19. Ni njia gani ya moja kwa moja ambayo wote kutanikoni wanaweza kushiriki kumwabudu Yehova?

19 Kumbuka kwamba kuimba ni sehemu muhimu ya ibada yetu. Ni njia bora sana ya kuonyesha kwamba tunampenda na kumshukuru Yehova. (Soma Isaya 12:5.) Pia, unapoimba kwa shangwe na sauti kubwa, utawatia moyo wengine waimbe kwa ujasiri. Kwa hakika, wote kutanikoni—vijana, wazee, na wapya—wanaweza kushiriki katika njia hii ya moja kwa moja ya kumwabudu Yehova. Hivyo, usiogope kuimba kwa hisia. Badala yake, tii mwongozo huu ulio wazi wa mtunga zaburi aliyeongozwa na roho: “Mwimbieni Yehova!” Naam, imba kwa shangwe na sauti kubwa!—Zab. 96:1.

^ fu. 11 Kwa maelezo zaidi kuhusu jinsi ya kuboresha sauti yako, tazama programu ya JW Broadcasting ya mwezi wa Desemba 2014 ya Kiingereza (kwenye sehemu ya video, tafuta chini ya FROM OUR STUDIO).

^ fu. 18 Ili kututayarisha kwa ajili ya kuimba, kila kipindi cha programu ya kusanyiko huanza kwa video ya muziki ya dakika kumi. Muziki huo wa ala umetungwa kwa njia ambayo itatayarisha moyo na akili yetu kwa ajili ya programu itakayofuata. Kwa hiyo, tunatiwa moyo tuwe tumeketi programu hizo za muziki zinapoanza na kuzisikiliza kwa makini.