Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Unamfanya Yehova Kuwa Kimbilio Lako?

Je, Unamfanya Yehova Kuwa Kimbilio Lako?

“Yehova anaikomboa nafsi ya watumishi wake; wala hakuna yeyote kati ya wale wanaomkimbilia atakayehesabiwa kuwa na hatia.”—ZAB. 34:22.

NYIMBO: 8, 54

1. Dhambi imesababisha hisia gani ambazo ni za kawaida miongoni mwa watumishi waaminifu wa Mungu?

“MASKINI mimi!” (Rom. 7:24) Watumishi wengi waaminifu wa Mungu wamepatwa na hisia kama hizo za mtume Paulo. Sisi sote tumerithi dhambi, na tunahuzunika sana tunapotenda mambo ambayo ni kinyume na tamaa yetu ya kumpendeza Yehova. Baadhi ya Wakristo ambao wamefanya dhambi nzito huhisi kwamba hawastahili kupata msamaha wa Mungu.

2. (a) Andiko la Zaburi 34:22 linaonyeshaje kwamba watumishi wa Mungu hawahitaji kulemewa na hatia? (b) Tutachunguza nini katika makala hii? (Tazama sanduku lenye kichwa, “ Je, Tukazie Mambo Tunayojifunza au Ufananisho wa Kiunabii?”)

2 Hata hivyo, Maandiko yanatuhakikishia kwamba wale wanaomfanya Yehova kuwa kimbilio lao hawahitaji kulemewa na hisia za hatia. (Soma Zaburi 34:22.) Kumfanya Yehova kuwa kimbilio letu kunahusisha nini? Tunapaswa kuchukua hatua gani ili tupate rehema na msamaha wa Yehova? Tutapata majibu ya maswali hayo kwa kuchunguza mpango wa majiji ya makimbilio katika Israeli la kale. Ni kweli kwamba mpango huo ulianzishwa chini ya agano la Sheria, ambalo liliondolewa Pentekoste 33 W.K. Lakini kumbuka kwamba Sheria hiyo ilitoka kwa Yehova. Hivyo, mpango wa majiji ya makimbilio unatusaidia kujua maoni ya Yehova kuhusu dhambi, watenda dhambi, na toba. Kwanza, na tuchunguze kusudi la majiji ya makimbilio na jukumu lililotimizwa na majiji hayo.

“MJIPE WENYEWE MAJIJI YA MAKIMBILIO”

3. Waisraeli walishughulikiaje visa vya watu walioua kwa kukusudia?

3 Yehova alichukua kwa uzito visa vyote vya mauaji katika Israeli la kale. Wauaji wa kukusudia waliuawa na mwanamume ambaye alikuwa mtu wa ukoo wa karibu zaidi na yule aliyeuawa. Mwanamume huyo aliitwa “mlipiza-kisasi cha damu.” (Hes. 35:19) Kufanya hivyo kulifidia damu ya mtu asiye na hatia iliyokuwa imemwagwa. Kumuua mtu huyo bila kukawia kulilinda Nchi ya Ahadi isitiwe unajisi kwa kuwa Yehova aliamuru hivi: “Nanyi msiichafue nchi mliyo ndani yake; kwa sababu [kumwaga damu ya mwanadamu ndiko kunakoichafua] nchi.”—Hes. 35:33, 34.

4. Visa vya watu walioua bila kukusudia vilishughulikiwaje katika Israeli?

4 Hata hivyo, Waisraeli walishughulikiaje visa vya watu walioua bila kukusudia? Ingawa tendo hilo lilitendwa bila kukusudia, bado muuaji huyo alikuwa na hatia ya kumwaga damu isiyo na hatia. (Mwa. 9:5) Hata hivyo, kwa rehema aliruhusiwa kumkimbia mlipiza-kisasi cha damu na kwenda kwenye mojawapo ya majiji sita ya makimbilio. Akiwa huko angeweza kuwa salama. Muuaji asiyekusudia alipaswa kubaki ndani ya jiji la makimbilio mpaka kuhani mkuu afe.—Hes. 35:15, 28.

5. Mpango wa kuwa na majiji ya makimbilio unaweza kutusaidiaje kumjua Yehova vizuri zaidi?

5 Mpango wa kuwa na majiji ya makimbilio haukutokana na wanadamu. Yehova mwenyewe alimwamuru hivi Yoshua: “Sema na wana wa Israeli, uwaambie, ‘Mjipe wenyewe majiji ya makimbilio.’” Majiji hayo yalikuwa na “hali ya utakatifu.” (Yos. 20:1, 2, 7, 8) Kwa kuwa Yehova alihusika moja kwa moja katika kuyatenga majiji hayo kwa ajili ya matumizi ya pekee, huenda tukajiuliza hivi: Mpango huo unatusaidiaje kuelewa vizuri zaidi rehema za Yehova? Nao unatusaidiaje kujua jinsi tunavyoweza kumfanya Yehova kuwa kimbilio letu leo?

‘NAYE ATASEMA MANENO YAKE MASIKIONI MWA WANAUME WAZEE’

6, 7. (a) Eleza jukumu la wazee katika kuamua kesi ya muuaji asiyekusudia. (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.) (b) Kwa nini lilikuwa jambo la hekima kwa mkimbizi kwenda kwa wazee?

6 Baada ya kumuua mtu bila kukusudia, mkimbizi alipaswa kwanza “kusema maneno yake masikioni mwa wanaume wazee” katika lango la jiji alilokimbilia. Alipaswa kupokelewa vizuri. (Yos. 20:4) Baada ya muda fulani, alipelekwa kwa wazee wa jiji ambalo mauaji yalifanyika, nao walisikiliza kesi hiyo. (Soma Hesabu 35:24, 25.) Ni baada tu ya kuthibitisha kwamba kifo hicho kilitokea bila kukusudia, ndipo mkimbizi huyo aliporuhusiwa kurudi katika jiji la makimbilio.

7 Kwa nini wazee walihusishwa? Walihusishwa ili kudumisha kutaniko la Israeli likiwa safi na kumsaidia muuaji asiyekusudia anufaike na rehema ya Yehova. Msomi mmoja wa Biblia aliandika kwamba ikiwa mkimbizi angepuuza kwenda kwa wazee, “angekuwa akihatarisha uhai wake mwenyewe.” Aliongeza hivi: “Damu yake ingekuwa juu ya kichwa chake mwenyewe, kwa sababu alipuuza mpango wa ulinzi ambao Mungu alikuwa amemwandalia.” Kulikuwa na mpango wa kumsaidia muuaji asiyekusudia, lakini alipaswa kuutafuta na kuukubali msaada huo. Ikiwa hangekimbilia katika mojawapo ya majiji ambayo Yehova alikuwa ameteua, mtu wa karibu zaidi wa ukoo wa aliyeuawa aliruhusiwa kumuua.

8, 9. Kwa nini Mkristo aliyetenda dhambi nzito anapaswa kutafuta msaada wa wazee?

8 Leo, Mkristo aliyetenda dhambi nzito anahitaji kutafuta msaada wa wazee wa kutaniko ili arudie hali nzuri ya kiroho. Kwa nini hilo ni muhimu sana? Kwanza, kama inavyoonyeshwa katika Neno lake, ni mpango wa Yehova kwamba wazee washughulikie visa vya dhambi nzito. (Yak. 5:14-16) Pili, mpango huo huwasaidia watenda dhambi waliotubu kubaki chini ya utunzaji wa Mungu na kuepuka mazoea ya kutenda dhambi. (Gal. 6:1; Ebr. 12:11) Tatu, wazee wamezoezwa na kupewa kazi ya kuwafariji watenda dhambi waliotubu na kuwasaidia kutuliza maumivu na hisia zao za hatia. Yehova anawaita wanaume hao wazee “mahali pa kujificha kutokana na dhoruba ya mvua.” (Isa. 32:1, 2) Je, hukubali kwamba mpango huo unaonyesha kwamba Mungu ni mwenye rehema?

9 Watumishi wengi wa Mungu wamepata kitulizo kwa sababu wametafuta na kupokea msaada kutoka kwa wazee. Kwa mfano, ndugu anayeitwa Daniel alitenda dhambi nzito, lakini kwa miezi kadhaa alisita kwenda kuwaambia wazee. Anakiri hivi: “Kwa kuwa muda mrefu ulikuwa umepita, nilihisi kwamba hakuna jambo lolote ambalo wazee wangeweza kufanya ili kunisaidia. Lakini sikuzote nilikuwa na wasiwasi mwingi nikisubiri matokeo mabaya ya dhambi yangu. Na niliposali kwa Yehova, nilihisi ninahitaji kuomba msamaha kwanza kabla ya kusali kuhusu jambo lolote lile.” Hatimaye, Daniel alitafuta msaada wa wazee. Anapokumbuka wakati huo, anasema hivi: “Kwa kweli niliogopa kwenda kuwaambia wazee. Lakini baadaye nilihisi kana kwamba nimetua mzigo mzito sana. Sasa, ninahisi kwamba ninaweza kumkaribia Yehova bila kizuizi chochote.” Leo, Daniel ana dhamiri safi, na aliwekwa kuwa mtumishi wa huduma hivi karibuni.

“NAYE ATAKIMBILIA MOJA LA MAJIJI HAYO”

10. Ili apokee rehema, muuaji asiyekusudia alipaswa kuchukua hatua gani bila kukawia?

10 Muuaji asiyekusudia alipaswa kuchukua hatua ili aonyeshwe rehema. Alipaswa kukimbilia jiji la makimbilio lililo karibu naye. (Soma Yoshua 20:4.) Hatuwezi kuwazia mkimbizi huyo akionyesha mtazamo wa kutojali. Ili aendelee kuishi alipaswa kufika katika jiji hilo haraka iwezekanavyo na kubaki humo! Hivyo, alihitaji kujidhabihu. Alihitaji kuacha kazi aliyofanya awali, nyumba yake, na kupoteza uhuru wa kusafiri—mpaka kuhani mkuu atakapokufa. * (Hes. 35:25) Lakini kudhabihu mambo hayo kulimnufaisha sana. Ikiwa angeondoka katika jiji la makimbilio, mkimbizi angekuwa akionyesha mtazamo mbaya sana wa kutojali kuelekea damu aliyomwaga, na maisha yake yangekuwa hatarini.

11. Mkristo aliyetubu anaweza kufanya nini ili kuonyesha kwamba hachukulii kivivihivi rehema za Mungu?

11 Leo, ni lazima watenda dhambi wanaotubu wachukue hatua ili wanufaike na rehema za Mungu. Ni lazima tuache kabisa mazoea ya kufanya dhambi, yaani, tuache kutenda dhambi nzito, na vilevile dhambi ndogo-ndogo ambazo mara nyingi huongoza kwenye dhambi nzito. Mtume Paulo aliongozwa na roho kuandika hivi kuhusu Wakristo waliotubu huko Korintho: “Jambo hili, kule kuhuzunishwa kwenu kwa njia ya kimungu, kulitokeza katika ninyi hali ya bidii kubwa kama nini, ndiyo, kujiondolea wenyewe hatia, ndiyo, ghadhabu, ndiyo, woga, ndiyo, kutamani, ndiyo, bidii, ndiyo, kurekebisha kosa!” (2 Kor. 7:10, 11) Jitihada za kuacha mazoea ya dhambi zinamwonyesha Yehova kwamba tunachukua mambo kwa uzito, na kwamba hatuchukulii rehema zake kivivihivi.

12. Huenda Mkristo akahitaji kudhabihu mambo gani ili aendelee kupokea rehema za Mungu?

12 Huenda Mkristo akahitaji kuacha mambo gani ili aendelee kupokea rehema za Mungu? Anapaswa kuwa tayari kudhabihu hata mambo anayopenda sana ikiwa yatamfanya atumbukie kwenye hatari ya kutenda dhambi. (Mt. 18:8, 9) Ikiwa baadhi ya marafiki wako wanakushawishi ufanye mambo yasiyompendeza Yehova, je, utaacha kushirikiana nao? Ikiwa unapambana ili usinywe pombe kupita kiasi, je, uko tayari kuepuka hali zozote zinazoweza kukushawishi unywe kupita kiasi? Ikiwa unapambana na tamaa ya upotovu wa maadili kingono, je, unaepuka sinema, tovuti, au mambo mengine yanayoweza kuchochea mawazo machafu? Kumbuka, jitihada zako za kujidhabihu ili udumishe utimilifu wako kwa Yehova si za bure. Hakuna jambo linaloumiza kuliko kuhisi kwamba Yehova amekuacha. Wakati huohuo, hakuna jambo linaloridhisha kuliko kuhisi “fadhili [zake] zenye upendo [za] mpaka wakati usio na kipimo.”—Isa. 54:7, 8.

“NAYO YATAKUWA KWENU MAKIMBILIO”

13. Eleza kwa nini mkimbizi angeweza kuhisi akiwa salama na mwenye furaha akiwa katika jiji la makimbilio.

13 Akiwa katika jiji la makimbilio, mkimbizi alikuwa salama. Yehova alisema hivi kuhusu majiji hayo ya makimbilio: “Nayo yatakuwa kwenu makimbilio.” (Yos. 20:2, 3) Yehova hakutaka muuaji ahukumiwe tena kwa kosa lilelile; wala mlipiza-kisasi cha damu hakuruhusiwa kuingia katika jiji la makimbilio ili kumuua muuaji. Hivyo, mkimbizi hakuhitaji kuogopa kwamba angeuawa na mlipiza-kisasi cha damu. Akiwa humo, angekuwa salama salimini chini ya ulinzi wa Yehova. Jiji la makimbilio halikuwa gereza la makimbilio. Mkimbizi angeweza kufanya kazi, kuwasaidia wengine, na kumtumikia Yehova kwa amani. Naam, angeweza kufurahia maisha yenye kuridhisha!

Uwe na uhakika katika msamaha wa Yehova (Tazama fungu la 14 hadi 16)

14. Mkristo aliyetubu anaweza kuwa na uhakika gani?

14 Baadhi ya watu wa Mungu waliotenda dhambi nzito sana lakini wakatubu, wamehisi ni kana kwamba wako “gerezani” kwa sababu ya hisia za hatia, hata wamehisi kwamba Yehova hatasahau kamwe kwamba walitenda dhambi nzito. Ikiwa unahisi hivyo, uwe na hakika kwamba Yehova anapokusamehe, anasamehe kabisa! Daniel, aliyetajwa mapema, alijionea ukweli wa jambo hilo. Baada ya kurekebishwa na wazee na kusaidiwa kupata tena dhamiri safi, alisema hivi: “Nilihisi kwamba sasa ninaweza kupumua tena. Baada ya tatizo hilo kushughulikiwa kwa njia nzuri, sikuwa na sababu ya kuhisi hatia tena. Dhambi zako zinapofutwa, haziendelei kuwapo. Kama Yehova alivyosema, anaondoa mizigo yako na kuiweka mbali sana nawe. Hutaiona tena kamwe.” Akiwa katika jiji la makimbilio, mkimbizi hakuhitaji kuendelea kuwa na wasiwasi kuhusu mlipiza-kisasi cha damu. Vivyohivyo, Yehova anapotusamehe dhambi zetu, hatuhitaji kuogopa kwamba anatafuta sababu ya kuzikumbuka au kutuhukumu kwa sababu ya dhambi hizo.—Soma Zaburi 103:8-12.

15, 16. Jukumu la Yesu la kulipa fidia na vilevile la kuwa Kuhani Mkuu linaweza kuimarishaje uhakika wako katika rehema za Mungu?

15 Kwa kweli, tunapojilinganisha na Waisraeli, sisi tuna sababu kubwa hata zaidi ya kuwa na uhakika katika rehema za Yehova. Baada ya Paulo kueleza kuhusu hisia zake za huzuni kwa sababu ya kushindwa kumtii Yehova kikamili, alisema hivi: “Shukrani kwa Mungu kupitia Yesu Kristo Bwana wetu!” (Rom. 7:25) Naam, licha ya kupambana na dhambi na matendo yake mabaya ya zamani ambayo alikuwa ametubu, Paulo alikuwa na uhakika kwamba Mungu amemsamehe kupitia Yesu. Kupitia fidia, Yesu husafisha dhamiri zetu na kutupatia amani ya akili. (Ebr. 9:13, 14) Akiwa Kuhani wetu Mkuu, “anaweza pia kuwaokoa kwa ukamili wale wanaomkaribia Mungu kupitia yeye, kwa sababu yeye yuko hai sikuzote ili kuwaombea.” (Ebr. 7:24, 25) Ikiwa jukumu la kuhani mkuu liliwahakikishia Waisraeli kwamba dhambi zao zingesamehewa, je, utumishi wa Kuhani wetu Mkuu, Yesu, haupaswi kutuhakikishia hata zaidi kwamba “[tutapokea] rehema na kupata fadhili zisizostahiliwa kuwa msaada kwa wakati unaofaa”?—Ebr. 4:15, 16.

16 Hivyo basi, ili kumfanya Yehova kuwa kimbilio lako, onyesha kwamba una imani katika dhabihu ya Yesu. Badala ya kuona tu kwamba fidia inawahusu watu wote kwa ujumla, uwe na imani kwamba fidia inakuhusu wewe binafsi. (Gal. 2:20, 21) Uwe na imani kwamba fidia ndiyo msingi wa msamaha wa dhambi zako. Uwe na imani kwamba fidia inakupa wewe tumaini la uzima wa milele. Dhabihu ya Yesu ni zawadi ambayo Yehova amekupa wewe.

17. Kwa nini ungependa kumfanya Yehova kuwa kimbilio lako?

17 Majiji ya makimbilio yanatusaidia kuelewa vizuri rehema ya Yehova. Kupitia mpango huo, Mungu hakukazia tu jinsi uhai ulivyo mtakatifu bali alionyesha pia jinsi wazee wanavyotusaidia, mambo yanayohusika katika toba ya kweli, na kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kabisa katika msamaha wa Yehova. Je, unamfanya Yehova kuwa kimbilio lako? Hakuna mahali pengine pa kukimbilia palipo salama zaidi! (Zab. 91:1, 2) Katika makala inayofuata, tutaona jinsi majiji ya makimbilio yanavyotusaidia kuiga mfano bora wa Yehova wa kuonyesha haki na rehema.

^ fu. 10 Kulingana na vitabu vya marejeo vya Wayahudi, inaelekea kwamba familia ya muuaji asiyekusudia ilijiunga naye katika jiji la makimbilio.