Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Jinsi ya Kuzoea Kutaniko Jipya

Jinsi ya Kuzoea Kutaniko Jipya

ALLEN * anasema hivi: “Nilikuwa na wasiwasi kuhusu kuhamia kutaniko hili. Sikujua ikiwa ningepata marafiki.” Allen anajaribu kuzoea kutaniko jipya lililo kilomita zaidi ya 1,400 kutoka mahali alipokuwa akiishi.

Ikiwa umehamia kutaniko jipya huenda wewe pia una wasiwasi. Ni nini kinachoweza kukusaidia uzoee kutaniko lako jipya? Ikiwa kuzoea kutaniko jipya ni vigumu kuliko ulivyotarajia, unaweza kufanya nini? Kwa upande mwingine, wengine wanapohamia kutaniko lenu, unaweza kufanya nini ili kuwasaidia?

JINSI UNAVYOWEZA KUZOEA NA KUSITAWI KATIKA KUTANIKO JIPYA

Fikiria mfano huu: Miti huathirika inapong’olewa na kuhamishiwa eneo lingine. Mti unapong’olewa kutoka ardhini, kwa kawaida baadhi ya mizizi yake hukatwa ili iwe rahisi kuusafirisha. Mti huo unapopandwa tena, ni lazima uanze kuota mizizi mipya mara moja. Vivyo hivyo, huenda kuhamia kutaniko lingine kumekuletea mkazo. Katika kutaniko lako la awali, ulikuwa na “mizizi” kwa kuwa ulikuwa na marafiki wapendwa na ulikuwa na ratiba ya mambo ya kiroho uliyoizoea. Sasa ni lazima uote mizizi mipya ili usitawi katika kutaniko jipya. Ni nini kitakachokusaidia kufanya hivyo? Ni kutumia kanuni za Biblia. Acheni tuchunguze baadhi ya kanuni hizo.

Mtu anayesoma Neno la Mungu kwa ukawaida ni “kama mti uliopandwa kando ya vijito vya maji, ambao hutoa matunda yake katika majira yake na ambao majani yake hayanyauki, na kila jambo analofanya litafanikiwa.”Zab. 1:1-3.

Kama tu ambavyo ni lazima mti ufyonze maji kwa ukawaida ili uendelee kusitawi, ni lazima Mkristo ajilishe Neno la Mungu kwa ukawaida ili abaki akiwa imara kiroho. Hivyo, endelea kusoma Biblia kila siku na kuhudhuria mikutano ya kutaniko kwa ukawaida. Dumisha mazoea yako mazuri ya kuwa na ibada ya familia na funzo la kibinafsi. Endelea kufanya mambo yote ya kiroho uliyokuwa ukifanya katika kutaniko lako la awali.

“Anayenywesha wengine kwa ukarimu yeye mwenyewe pia atanyweshwa kwa ukarimu.”Met. 11:25.

Utaimarishwa na utazoea haraka kutaniko lako jipya ukishiriki kikamili katika huduma. Kevin, mzee Mkristo anasema hivi: “Jambo lililotusaidia sana mimi na mke wangu lilikuwa kufanya upainia msaidizi mara tu tulipofika katika kutaniko letu jipya. Baada ya muda mfupi, tuliwafahamu ndugu na dada kutanikoni, mapainia, na eneo la kutaniko hilo.” Roger, ambaye alihamia kutaniko lililokuwa zaidi ya kilomita 1,600 kutoka mahali alipokuwa akiishi alisema hivi: “Njia bora ya kuzoea kutaniko jipya ni kushiriki katika huduma ya shambani mara nyingi iwezekanavyo. Pia, wajulishe wazee kwamba uko tayari kusaidia kwa njia yoyote ile, labda kwa kusafisha Jumba la Ufalme, kujitolea kutimiza mgawo fulani kwenye mikutano, au kumsafirisha mtu kwenda mikutanoni. Ndugu na dada wanapokuona ukionyesha roho ya kujidhabihu inakuwa rahisi kwao kuanzisha urafiki pamoja nawe.”

“Panukeni.”2 Kor. 6:13.

Panuka katika kuwaonyesha wengine upendo wa kindugu. Baada ya Melissa na familia yake kuhamia katika kutaniko jipya, walikazia fikira kupata marafiki wapya. Melissa anasema hivi: “Tulizungumza na watu kabla na baada ya mikutano. Hilo lilitupatia wakati wa kuwajua vizuri badala ya kuwasalimia tu kijuujuu.” Jambo hilo pia lilisaidia familia hiyo ijifunze haraka majina mapya. Zaidi ya hilo, walipanuka kwa kuwakaribisha wengine nyumbani kwao, jambo lililoimarisha urafiki walioanzisha. Melissa anaongeza hivi: “Tuliwapa namba zetu za simu ili waweze kuwasiliana nasi kwa urahisi na kutuhusisha katika utendaji wa kutaniko na mambo mengine.”

Ikiwa wewe huogopa kufahamiana na kuzungumza na watu wapya, anza kwa kufanya mambo madogo-madogo. Kwa mfano, tabasamu hata ikiwa mwanzoni huhisi kufanya hivyo. Tabasamu yako itawavuta watu. Isitoshe, “mtazamo wa tabasamu huleta furaha moyoni.” (Met. 15:30, Neno Biblia) Rachel ambaye alihamia mbali na mahali alipolelewa anasema hivi: “Mimi ni mwenye haya sana. Nyakati nyingine mimi hujilazimisha kuzungumza na ndugu na dada wa kutaniko langu jipya. Mimi hutafuta mtu aliyeketi peke yake kwenye Jumba la Ufalme. Labda mtu huyo ni mwenye haya kama mimi.” Kwa nini usijiwekee lengo la kuzungumza na mtu mpya kabla au baada ya kila mkutano?

Kwa upande mwingine, huenda ukasisimka sana kukutana na watu wapya majuma machache ya kwanza. Lakini msisimko huo unaweza kufifia kadiri muda unavyopita. Unapohisi hivyo, endelea kujitahidi kupata marafiki wapya.

Miti huathirika inapong’olewa na kuhamishiwa eneo lingine, lakini inapopandwa tena, huota mizizi mipya

JIPE WAKATI WA KUTOSHA KUZOEA HALI MPYA

Baadhi ya miti huchukua muda mrefu ili mizizi yake isitawi na kuwa imara katika mazingira mapya. Vivyo hivyo, wengine huhitaji muda zaidi kuzoea kutaniko jipya. Ikiwa muda mrefu umepita tangu ulipohamia kutaniko jipya, na bado hujalizoea, unaweza kunufaika kwa kutumia kanuni zifuatazo za Biblia:

“Kwa hiyo na tusife moyo katika kufanya yaliyo mema, kwa maana katika majira yanayofaa tutavuna ikiwa hatuchoki kabisa.”Gal. 6:9.

Jipe muda zaidi wa kuzoea kutaniko lako. Kwa mfano, wamishonari wengi waliozoezwa katika Shule ya Gileadi hubaki katika mgawo wao kwa miaka kadhaa kabla ya kwenda likizo nyumbani. Kufanya hivyo huwasaidia kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na ndugu wenyeji na kuzoea utamaduni tofauti.

Alejandro ambaye amehama mara kadhaa, anajua kwamba muda unahitajika ili mtu azoee kutaniko jipya. Anasema hivi: “Mara ya mwisho tulipohama mke wangu alisema, ‘Marafiki wangu wote wako katika kutaniko letu la zamani!’” Alimkumbusha kwamba alikuwa amesema maneno hayohayo miaka miwili iliyopita walipohama kutaniko walilokuwa. Lakini katika kipindi cha miaka hiyo miwili, alikuwa mwenye urafiki na hatimaye watu ambao hakufahamiana nao wakawa marafiki wake wa karibu.

“Usiseme: ‘Kwa nini siku za zamani zilikuwa bora kuliko hizi?’ kwa maana hukuuliza hilo kwa hekima.”Mhu. 7:10.

Epuka kulinganisha kutaniko lako jipya na kutaniko lako la zamani. Kwa mfano, huenda ndugu katika kutaniko lako jipya ni wakimya au ni wazungumzaji sana tofauti na ulivyozoea. Kazia fikira sifa zao nzuri kama ambavyo ungependa wakazie fikira sifa zako nzuri. Baada ya kuhamia kutaniko jipya, baadhi ya akina ndugu na dada wamelazimika kujiuliza swali hili ambalo hawakufikiri wangejiuliza, ‘Je, ninaupenda kikweli “ushirika mzima wa akina ndugu”?’—1 Pet. 2:17.

“Endeleeni kuomba, nanyi mtapewa.” Luka 11:9.

Endelea kumwomba Yehova akusaidie. David, ambaye ni mzee wa kutaniko alisema hivi: “Usivumilie hali hiyo kwa nguvu zako mwenyewe. Mambo mengi ambayo tunaweza kufanya, yanawezekana tu kwa msaada wa Yehova. Sali kuhusu jambo hilo!” Rachel, aliyenukuliwa katika makala hii, anakubaliana na jambo hilo. Anasema hivi: “Mimi na mume wangu tunapohisi hatuna uhusiano wa karibu na kutaniko letu, sisi husali kihususa kwa Yehova na kumwomba, ‘Tafadhali tusaidie kutambua ikiwa kuna jambo ambalo tunafanya linalosababisha iwe vigumu kwa akina ndugu kutukaribia.’ Kisha tunajaribu kutumia muda mwingi zaidi na akina ndugu na dada.”

Wazazi, ikiwa watoto wenu wanaona ni vigumu kuzoea kutaniko jipya, salini pamoja nao kuhusu jambo hilo. Wasaidieni kupata marafiki wapya kwa kupanga kuwe na fursa za kufurahia ushirika mchangamfu pamoja na wengine.

WASAIDIE WAPYA WAHISI WAMEKARIBISHWA

Unaweza kufanya nini ili kuwasaidia wale waliohamia kutaniko lenu? Jitahidi tangu mwanzoni kuwa rafiki wa kweli. Ili ufaulu kufanya hivyo, jaribu kuwazia ni mambo gani ambayo ungependa kutendewa ikiwa wewe ndiye uliyehamia kutaniko fulani, kisha ufanye mambo hayo. (Mt. 7:12) Je, ndugu na dada hao wanaweza kujiunga nanyi kwa ajili ya ibada ya familia au kutazama programu ya kila mwezi ya JW Broadcasting? Je, unaweza kuwaalika ili wahubiri pamoja nawe? Ukiwakaribisha kwa ajili ya chakula chepesi, watakumbuka ukarimu wako kwa muda mrefu. Ni jambo gani lingine unaloweza kufanya ili kuwasaidia ndugu na dada wageni?

Carlos anasema hivi: “Tulipohamia kutaniko jipya, dada mmoja alitupatia orodha ya maduka yanayouza bidhaa kwa bei nafuu. Hilo lilitusaidia sana.” Wale wanaohamia katika maeneo yaliyo na hali ya hewa tofauti na waliyozoea, huenda watathamini sana kujua jinsi ya kuvalia kulingana na hali ya hewa ya eneo jipya. Pia, unaweza kuwasaidia wapate matokeo mazuri katika huduma kwa kuwasimulia historia ya eneo lenu au kuwaeleza kuhusu imani za kidini za watu wa eneo lenu.

JITIHADA ZAKO ZITATHAWABISHWA

Allen, ambaye ametajwa mwanzoni mwa makala hii, amekuwa katika kutaniko lake jipya kwa zaidi ya mwaka mmoja. Anakumbuka hivi: “Mwanzoni ilibidi nijilazimishe kuwajua ndugu na dada. Lakini sasa ninawaona kama watu wa familia, na nina furaha.” Allen ametambua kwamba kuhama hakukumfanya apoteze marafiki. Badala yake alipata marafiki wapya ambao huenda wakawa marafiki wa kudumu.

^ fu. 2 Baadhi ya majina yamebadilishwa.