Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

‘Mwenye Ukarimu Atabarikiwa’

‘Mwenye Ukarimu Atabarikiwa’

KWA MUDA mrefu, dhabihu zimekuwa sehemu muhimu ya ibada ya kweli. Waisraeli walitoa dhabihu za wanyama, na sikuzote Wakristo wamejulikana kwa kutoa “dhabihu ya sifa.” Hata hivyo, kuna dhabihu nyingine ambazo zinampendeza Mungu. (Ebr.  13:15, 16) Dhabihu hizo huleta shangwe na baraka kama mifano ifuatayo inavyoonyesha.

Hana, mtumishi mwaminifu wa zamani, alitamani sana kupata mwana lakini alikuwa tasa. Kupitia sala, alitoa nadhiri kwa Yehova kwamba ikiwa angepata mwana, ‘angemtoa kwa Yehova siku zote za maisha yake.’ (1 Sam. 1:10, 11) Baada ya muda, Hana alipata mimba akazaa mwana na kumwita Samweli. Baada ya Samweli kuachishwa kunyonya, Hana alimpeleka kwenye maskani, kama alivyokuwa ameahidi. Yehova alimbariki Hana kwa roho yake ya kujidhabihu. Alipata pendeleo la kuzaa watoto wengine watano, na Samweli akawa nabii na mwandikaji wa Biblia.—1 Sam. 2:21.

Kama Hana na Samweli, Wakristo leo wana pendeleo la kutumia maisha yao kumtumikia Muumba wao katika utumishi mtakatifu. Yesu aliahidi kwamba tutathawabishwa sana kwa dhabihu zozote tunazotoa tunapomtumikia Yehova.—Marko 10:28-30.

Katika karne ya kwanza, mwanamke Mkristo aliyeitwa Dorkasi alijulikana sana kwa “matendo mema na zawadi za rehema,” yaani, dhabihu alizotoa ili kuwasaidia wengine. Hata hivyo kwa kusikitisha, “alishikwa na ugonjwa akafa,” na kutaniko likahuzunika sana. Wanafunzi waliposikia kwamba Petro alikuwa katika eneo hilo, walimsihi aje mara moja. Wazia shangwe waliyopata Petro alipokuja na kumfufua Dorkasi! Huo ulikuwa ufufuo wa kwanza uliofanywa na mtume. (Mdo. 9:36-41) Mungu hakuwa amesahau dhabihu ambazo Dorkasi alikuwa ametoa. (Ebr. 6:10) Simulizi kuhusu ukarimu wake liliandikwa katika Neno la Mungu ili tuige mfano wake mzuri.

Mtume Paulo pia aliweka mfano bora wa ukarimu kwa kutumia wakati wake kuwasaidia wengine. Katika barua yake aliyowaandikia ndugu zake Wakristo huko Korintho, Paulo alisema hivi: “Kwa upande wangu mimi nitatumia kwa furaha zaidi na kutumiwa kabisa kwa ajili ya nafsi zenu.” (2 Kor. 12:15) Kupitia mambo aliyojionea, Paulo alijifunza kwamba kujidhabihu kwa ajili ya wengine hufanya mtu aridhike, na la muhimu hata zaidi, mtu hupata baraka na kibali cha Yehova.—Mdo. 20:24, 35.

Ni wazi kwamba Yehova anafurahi tunapotumia wakati na nguvu zetu kuendeleza masilahi ya Ufalme na kuwasaidia waabudu wenzetu. Lakini je, kuna njia nyingine za kuunga mkono kazi ya kuhubiri Ufalme? Ndiyo! Mbali na kutumia wakati na nguvu zetu, tunaweza kumheshimu Mungu kwa kutoa michango ya hiari. Michango hiyo hutumiwa kuendeleza kazi ya kuhubiri habari njema ulimwenguni pote, na pia kuwategemeza wamishonari na wengine walio katika utumishi wa pekee wa wakati wote. Isitoshe, michango hiyo ya hiari hutumiwa kutafsiri machapisho na kutayarisha video, kusaidia wakati wa majanga, na pia kujenga Majumba ya Ufalme. Tuna hakika kwamba ‘mwenye ukarimu atabarikiwa.’ Isitoshe, tunapompa Yehova vitu vyetu vyenye thamani, tunamheshimu Yeye.—Met. 3:9; 22:9.