Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Usiruhusu Chochote Kikunyang’anye Tuzo

Usiruhusu Chochote Kikunyang’anye Tuzo

“Msiache mtu yeyote awanyang’anye tuzo.”—KOL. 2:18.

NYIMBO: 122, 139

1, 2. (a) Watumishi wa Mungu wanatazamia kwa hamu tuzo gani? (b) Ni nini kinachotusaidia kukaza macho kwenye tuzo? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

SAWA na mtume Paulo, Wakristo watiwa-mafuta leo wana tumaini zuri la kupata “tuzo la mwito wa Mungu wa kwenda juu.” (Flp. 3:14) Wanatazamia kwa hamu kutawala pamoja na Yesu Kristo katika Ufalme wake wa mbinguni na kushirikiana naye kuwasaidia wanadamu kufikia ukamilifu. (Ufu. 20:6) Huo ni mradi wenye kusisimua sana ambao watiwa-mafuta wamepewa na Mungu! Kondoo wengine wana tumaini tofauti. Wanatazamia kwa hamu kupata tuzo ya uzima wa milele duniani—na hilo ni tumaini zuri kwelikweli!—2 Pet. 3:13.

2 Ili kuwasaidia Wakristo wenzake watiwa-mafuta waendelee kuwa waaminifu na kupata tuzo, Paulo aliwahimiza hivi: “Endeleeni kukaza akili zenu juu ya mambo yaliyo juu.” (Kol. 3:2) Walipaswa kukaza akili zao kwenye tumaini zuri la kupokea urithi wao wa mbinguni. (Kol. 1:4, 5) Kwa kweli, kutafakari baraka ambazo Yehova ameweka mbele ya watu wake huwasaidia watumishi wake wote wakaze macho yao kwenye tuzo, iwe wana tumaini la kuishi mbinguni au duniani.—1 Kor. 9:24.

3. Paulo aliwatahadharisha Wakristo wenzake kuhusu hatari zipi?

3 Pia, Paulo aliwatahadharisha Wakristo wenzake kuhusu hatari ambazo zinaweza kuwafanya wakose tuzo. Kwa mfano, aliliandikia kutaniko la Kolosai kuhusu Wakristo wa uwongo waliokuwa wakijaribu kupata kibali cha Mungu kupitia kazi za Sheria badala ya kuonyesha imani katika Kristo. (Kol. 2:16-18) Pia, Paulo alizungumza kuhusu hatari zilizopo leo zinazoweza kufanya tukose tuzo. Kwa mfano, alieleza kuhusu jinsi ya kushinda tamaa ya kufanya uasherati, kushughulika na hali ya kutoelewana na waabudu wenzetu, na jinsi ya kutatua matatizo katika familia. Shauri lake kuhusu mambo hayo linafaa hata leo. Kwa hiyo, acheni tuchunguze baadhi ya maonyo hayo yenye upendo ya Paulo yanayopatikana katika barua yake kwa Wakolosai.

UENI TAMAA YA UASHERATI

4. Kwa nini tamaa ya kufanya uasherati inaweza kufanya tukose tuzo?

4 Baada ya kuwakumbusha ndugu zake kuhusu tumaini lao zuri sana, Paulo aliandika hivi: “Viueni viungo vya mwili wenu vilivyo duniani kwa habari ya uasherati, uchafu, hamu ya ngono, tamaa yenye madhara, na kutamani.” (Kol. 3:5) Tamaa ya kufanya uasherati inaweza kuwa yenye nguvu sana, nayo inaweza kufanya tupoteze uhusiano wetu pamoja na Yehova na tumaini letu la wakati ujao. Ndugu mmoja ambaye alishindwa na tamaa ya kufanya uasherati alisema hivi baada ya kurudi kutanikoni, “Nilinaswa na tamaa hiyo yenye nguvu sana hivi kwamba nilirudiwa na fahamu ilipokuwa kuchelewa mno.”

5. Tunaweza kujilindaje tunapokuwa katika hali hatari?

5 Ni muhimu hasa tuwe macho tunapokabili hali zinazoweza kutushawishi tuvunje viwango vya Yehova vya maadili. Kwa mfano, ni jambo la hekima kwa wale wanaochumbiana kujiwekea mipaka iliyo wazi tangu mwanzo wa uchumba kuhusu mambo kama vile kugusana, kubusiana, au kuwa peke yao faraghani. (Met. 22:3) Huenda hali zinazoweza kumshawishi Mkristo afanye uasherati zikatokea anaposafiri mbali na nyumbani kwa sababu za kikazi au Mkristo anapolazimika kufanya kazi pamoja na mtu wa jinsia tofauti. (Met. 2:10-12, 16) Ukijipata katika hali kama hiyo, jitambulishe kuwa wewe ni Shahidi wa Yehova, jiendeshe kwa njia ya heshima, na ukumbuke kwamba kuwachezea wengine kimapenzi kunaweza kuwa na matokeo mabaya sana. Huenda tukajipata katika hatari kubwa hata zaidi ikiwa tumeshuka moyo na tunahisi upweke. Wakati kama huo huenda tukatamani kupata mtu fulani atakayefanya tuhisi kwamba tunathaminiwa. Huenda tukatamani sana kutiwa moyo na hivyo tukakubali kufarijiwa na mtu yeyote. Ikiwa utapatwa na hali kama hiyo, omba msaada kutoka kwa Yehova na watu wake ili usiruhusu chochote kikunyang’anye tuzo.—Soma Zaburi 34:18; Methali 13:20.

6. Tunapaswa kuzingatia nini tunapochagua burudani?

6 Ili kuua tamaa ya kufanya uasherati, tunahitaji kuepuka burudani potovu. Burudani nyingi leo zimejaa mambo yaliyokuwa yakitendeka katika majiji ya kale ya Sodoma na Gomora. (Yuda 7) Watayarishaji wa burudani hizo huendeleza mawazo yao kuhusu maadili kwamba kufanya uasherati ni jambo la kawaida lisilo na madhara yoyote. Tunapaswa kuwa macho sikuzote. Tusikubali burudani yoyote tu. Tunapaswa kuchagua burudani ambazo hazitatuzuia kukaza macho yetu kwenye tuzo ya uzima.—Met. 4:23.

“JIVIKENI” UPENDO NA FADHILI

7. Huenda tukakabili matatizo gani katika kutaniko la Kikristo?

7 Sote tunakubali kwamba kuwa sehemu ya kutaniko la Kikristo ni baraka kwelikweli. Kujifunza Neno la Mungu katika mikutano yetu na kusaidiana kwa fadhili na upendo hutusaidia kukaza macho yetu kwenye tuzo. Hata hivyo, nyakati nyingine huenda hali ya kutoelewana ikasababisha matatizo kati ya ndugu na dada kutanikoni. Hali hiyo isiposhughulikiwa, inaweza kufanya iwe rahisi kwa ndugu na dada kuwekeana kinyongo.—Soma 1 Petro 3:8, 9.

8, 9. (a) Ni sifa gani zitakazotusaidia kushinda tuzo? (b) Ni nini kitakachotusaidia kudumisha amani Mkristo mwenzetu anapotukosea?

8 Tunaweza kufanya nini ili kinyongo kisituzuie kupata tuzo? Paulo aliwahimiza hivi Wakolosai: “Kama waliochaguliwa wa Mungu, watakatifu na wapendwa, jivikeni upendo mwororo wenye huruma, fadhili, unyenyekevu wa akili, upole, na ustahimilivu. Endeleeni kuvumiliana na kusameheana kwa hiari ikiwa yeyote ana sababu ya kulalamika juu ya mwingine. Kama vile Yehova alivyowasamehe ninyi kwa hiari, nanyi fanyeni vivyo hivyo pia. Lakini, zaidi ya mambo haya yote, jivikeni upendo, kwa maana huo ni kifungo kikamilifu cha muungano.”—Kol. 3:12-14.

9 Sifa ya upendo na fadhili zinaweza kutusaidia kusameheana. Kwa mfano, tukiumizwa na maneno au matendo ya Mkristo mwenzetu, ni vema kukumbuka pindi ambazo sisi wenyewe tulizungumza au kutenda kwa njia isiyo ya fadhili. Je, hatuthamini upendo na fadhili ambazo ndugu na dada zetu walituonyesha kwa kufunika makosa yetu? (Soma Mhubiri 7:21, 22.) Tunashukuru hata zaidi kwamba kwa fadhili Kristo anawakusanya na kuwaunganisha waabudu wa kweli. (Kol. 3:15) Sote tunampenda Mungu yuleyule, tunahubiri ujumbe uleule, na tunakabili changamoto zilezile. Tunaposameheana kwa fadhili na upendo, tunachangia umoja wa Kikristo na kuendelea kukaza macho yetu kwenye tuzo ya uzima.

10, 11. (a) Kwa nini wivu ni hatari? (b) Tunaweza kufanya nini ili wivu usituzuie kupata thawabu yetu?

10 Biblia ina mifano yenye kuonya inayotukumbusha kwamba wivu unaweza kufanya tukose tuzo. Kwa mfano, Kaini alimwonea wivu Abeli ndugu yake, naye akamuua. Kora, Dathani, na Abiramu walimwonea wivu Musa na hivyo wakampinga. Pia, Mfalme Sauli alimwonea wivu Daudi kwa sababu ya mafanikio yake, naye akajaribu kumuua. Haishangazi kwamba Neno la Mungu linasema hivi: “Mahali ambapo pana wivu na ugomvi, hapo pana machafuko na kila jambo baya.”—Yak. 3:16.

11 Ikiwa tutasitawisha upendo na fadhili mioyoni mwetu, haitakuwa rahisi kuwaonea wivu wengine. Neno la Mungu linasema hivi: “Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili. Upendo hauna wivu.” (1 Kor. 13:4) Ili kuzuia wivu usisitawi mioyoni mwetu, lazima tujitahidi kuona mambo kama Mungu anavyoyaona, na kuwaona ndugu na dada zetu kuwa viungo vya mwili uleule wa Kikristo. Kufanya hivyo kutatusaidia kuonyesha hisia-mwenzi kupatana na shauri hili lililoongozwa na roho ya Mungu: “Kiungo kimoja kikitukuzwa, vile viungo vingine vyote hushangilia pamoja nacho.” (1 Kor. 12:16-18, 26) Hivyo, badala ya kuwaonea wivu wengine, tutafurahi wanapopata baraka. Fikiria mfano wa Yonathani, mwana wa Mfalme Sauli. Hakumwonea wivu Daudi alipochaguliwa kuwa mrithi wa kiti cha ufalme. Badala yake, alimtia moyo. (1 Sam. 23:16-18) Je, tunaweza kumwiga Yonathani kwa kuwa wenye fadhili na upendo?

SHINDENI TUZO MKIWA FAMILIA

12. Ni shauri gani la Kimaandiko litakalotusaidia kushinda tuzo tukiwa familia?

12 Kutumia kanuni za Biblia kunaweza kufanya familia iwe na amani na furaha na kuisaidia ishinde tuzo. Paulo aliwapa Wakristo Wakolosai shauri gani kuhusu familia? Alisema hivi: “Enyi wake, jitiisheni kwa waume zenu, kwa kuwa inafaa katika Bwana. Enyi waume, endeleeni kuwapenda wake zenu nanyi msiwakasirikie kwa uchungu. Enyi watoto, watiini wazazi wenu katika kila jambo, kwa maana hilo linapendeza vema katika Bwana. Enyi akina baba, msiwe mkiwakasirisha watoto wenu, ili wasivunjike moyo.” (Kol. 3:18-21) Hapana shaka utakubali kwamba kutumia shauri la Paulo lililoongozwa na roho bado kunaweza kuwanufaisha waume, wake, na watoto.

13. Dada Mkristo anaweza kufanya nini ili amvute kwenye kweli mume wake ambaye si mwamini?

13 Vipi ikiwa wewe ni mke na unahisi kwamba mume wako ambaye si mwamini hakutendei kwa njia inayofaa? Je, ungeboresha hali kwa kubishana naye kuhusu tabia yake? Na hata ikiwa utafaulu kumlazimisha afanye unavyotaka, je, utamvuta kwenye kweli? Haielekei utafaulu. Lakini ikiwa utaheshimu ukichwa wa mume wako, unaweza kuchangia amani katika familia, utamtukuza Yehova, na huenda hata ukamvuta mume wako kwenye ibada ya kweli; na hivyo nyote mnaweza kupata tuzo.—Soma 1 Petro 3:1, 2.

14. Mume Mkristo anaweza kufanya nini ikiwa mke wake ambaye si mwamini hamheshimu?

14 Vipi ikiwa wewe ni mume na unahisi kwamba mke wako ambaye si mwamini hakuheshimu? Je, ungemlazimisha akuheshimu kwa kumfokea ili kumwonyesha kwamba wewe ndiye kichwa? La hasha! Mungu anatazamia utumie ukichwa kwa upendo kwa kumwiga Yesu. (Efe. 5:23) Yesu akiwa kichwa huongoza kutaniko kwa upendo na subira. (Luka 9:46-48) Kwa kuiga kielelezo cha Yesu, mume anaweza kumvuta mke wake kwenye ibada ya kweli.

15. Mume Mkristo huonyeshaje kwamba anampenda mke wake?

15 Waume wanaambiwa hivi: “Endeleeni kuwapenda wake zenu nanyi msiwakasirikie kwa uchungu.” (Kol. 3:19) Mume mwenye upendo humheshimu mke wake kwa kusikiliza maoni yake na kwa kumhakikishia kwamba anayathamini. (1 Pet. 3:7) Ingawa hatafuata maoni ya mke wake nyakati zote, mara nyingi mume atafikia uamuzi mzuri zaidi kwa kusikiliza maoni ya mke wake. (Met. 15:22) Mume mwenye upendo hamlazimishi mke wake amheshimu, bali matendo yake ndiyo yatakayomchochea amheshimu. Mume anayempenda mke wake na watoto atakuwa na familia inayomtumikia Yehova kwa furaha na watashinda tuzo ya uzima.

Tunaweza kufanya nini ili matatizo katika familia yasituzuie kupata tuzo? (Tazama fungu la 13 hadi 15)

VIJANA—MSIRUHUSU CHOCHOTE KIWANYANG’ANYE TUZO!

16, 17. Ikiwa wewe ni kijana, unaweza kufanya nini ili uepuke kuwakasirikia wazazi wako kupita kiasi?

16 Vipi ikiwa wewe ni tineja na unahisi kwamba wazazi wako Wakristo hawakuelewi na wanakuwekea vizuizi? Hilo linaweza kukuvunja moyo sana na kukufanya utilie shaka ikiwa kumtumikia Yehova ndiyo njia bora ya maisha. Lakini ukiruhusu hilo likufanye uache kumtumikia Yehova, mwishowe utagundua kwamba hakuna mtu mwingine anayekujali kikweli kuliko wazazi wako wanaomwogopa Mungu na kutaniko lako.

17 Ikiwa wazazi wako hawana zoea la kukutia nidhamu, je, usingeshuku ikiwa kwa kweli wanakujali? (Ebr. 12:8) Lakini huenda njia ambayo wazazi wako wanatumia kukutia nidhamu ndiyo inayokukasirisha. Badala ya kuruhusu hilo likukasirishe, jaribu kuelewa kwamba huenda kuna sababu inayowafanya watende kwa njia hiyo. Hivyo, uwe mtulivu na ujitahidi kabisa kuepuka kukasirika kupita kiasi unapokosolewa. Neno la Mungu linasema hivi: “Yeyote anayezuia maneno yake ana ujuzi, na mtu mwenye utambuzi ana roho ya utulivu.” (Met. 17:27) Jiwekee lengo la kuwa mtu mkomavu ambaye anaweza kukubali shauri kwa utulivu na kunufaika nalo bila kuhangaikia sana jinsi lilivyotolewa. (Met. 1:8) Kuwa na wazazi Wakristo wanaompenda Yehova kikweli ni baraka. Kwa hakika, wangependa kukusaidia ushinde tuzo ya uzima.

18. Kwa nini umeazimia kukaza macho yako kwenye tuzo?

18 Tuzo iliyo mbele yetu—iwe ni uhai usioweza kufa mbinguni au uzima wa milele katika dunia Paradiso—ni thawabu tunayotazamia kwa hamu. Tuzo hiyo ni tumaini hakika linalotegemea ahadi ya Muumba wetu mwenyewe. Mungu anasema hivi kuhusu dunia itakayokuwa paradiso: “Dunia hakika itajawa na kumjua Yehova.” (Isa. 11:9) Wakati huo, kila mtu duniani atafundishwa na Mungu. Kwa hakika, tunapaswa kufanya yote tuwezayo kupata tuzo hiyo. Kwa hiyo, kaza akili yako kwenye ahadi za Yehova, na usiruhusu chochote kikunyang’anye tuzo!