Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mtumaini Yehova Uishi!

Mtumaini Yehova Uishi!

“Mtumaini Yehova kwa moyo wako wote, wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe.”MET. 3:5.

NYIMBO: 3, 8

1. Kwa nini sisi sote tunahitaji faraja?

SISI sote tunahitaji faraja. Huenda mahangaiko, mambo yenye kuvunja moyo, na mateso yamekuwa sehemu ya maisha yetu. Huenda tunateseka moyoni kwa sababu umri wetu umesonga, tuna ugonjwa fulani, au tumefiwa na mtu tunayempenda. Baadhi yetu tunakabili uhasama. Tumezungukwa na uhalifu unaozidi kuongezeka. Hatuna shaka kwamba “nyakati [hizi] za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo” ni uthibitisho wa kwamba tunaishi katika “siku za mwisho,” na kwamba kila siku inayopita inatuleta karibu zaidi na ulimwengu mpya. (2 Tim. 3:1) Hata hivyo, huenda tumekuwa tukisubiri kwa muda mrefu kuona Yehova akitimiza ahadi zake, na labda matatizo yanayotupata yanazidi kuongezeka. Hivyo basi, tunaweza kupata wapi faraja?

2, 3. (a) Tunajua nini kumhusu Habakuki? (b) Kwa nini tutachunguza kitabu cha Habakuki?

2 Ili kupata jibu la swali hilo, acheni tuchunguze kitabu cha Habakuki. Ingawa Maandiko hayaelezi mambo hususa kuhusu maisha na utendaji wa Habakuki, kitabu kinachoitwa kwa jina lake kinaweza kututia moyo sana. Huenda jina hilo linamaanisha “Kumbatio Changamfu.” Huenda linarejelea kumbatio la Yehova lenye kufariji au jinsi waabudu wake wanavyomshikilia kwa nguvu kama mtoto anavyomng’ang’ania baba yake. Habakuki alizungumza na Mungu, akiuliza maswali mazito yanayogusa hisia. Kihalisi, aliuliza maswali hayo kwa niaba yetu, kwani Yehova alimwongoza aandike mazungumzo hayo.—Hab. 2:2.

3 Mazungumzo hayo yenye hisia nyingi kati ya Yehova na mtumishi wake aliyefadhaika, ndiyo habari pekee inayofunuliwa na Maandiko kuhusu nabii huyo. Kitabu chake ni sehemu ya “mambo yote yaliyoandikwa zamani” na yaliyohifadhiwa katika Neno la Mungu, Biblia, “ili kupitia uvumilivu wetu na kupitia faraja kutoka kwa Maandiko tuwe na tumaini.” (Rom. 15:4) Sisi binafsi tunaweza kunufaikaje kwa kusoma kitabu cha Habakuki? Kinaweza kutusaidia kujua maana hasa ya kumtegemea Yehova. Zaidi ya hilo, unabii wa Habakuki unatuhakikishia kwamba inawezekana kuwa na moyo mtulivu na kudumisha hali hiyo licha ya mateso na matatizo tunayokabili. Tukiwa na hayo akilini, acheni tuchunguze kwa undani zaidi kitabu cha Habakuki.

MLILIE YEHOVA

4. Kwa nini Habakuki alifadhaika sana?

4 Soma Habakuki 1:2, 3Habakuki aliishi katika kipindi kigumu sana na kilichojaa changamoto nyingi. Alihuzunika sana kwa sababu aliishi miongoni mwa watu waovu na wakatili. Waovu hao wangefikia mwisho wao lini? Kwa nini Yehova alichukua muda mrefu hivyo kabla ya kuchukua hatua? Habakuki alipotazama kila mahali, aliona Wayahudi wenzake wakiwadhulumu na kuwakandamiza Wayahudi wenzao. Alihisi hana msaada wowote. Hivyo, katika kipindi hicho kigumu, alimlilia Yehova ili aingilie kati. Huenda Habakuki alianza kufikiri kwamba Yehova hajali. Ilionekana ni kana kwamba Mungu hangechukua hatua upesi. Je, umewahi kuhisi kama mtumishi huyo mpendwa wa Mungu alivyohisi?

5. Tunajifunza somo gani muhimu katika kitabu cha Habakuki? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

5 Je, Habakuki alikuwa ameacha kumtumaini Yehova? Je, aliacha kuamini kwamba ahadi za Mungu zingetimia? La hasha! Wazo tu la kwamba alimtwika Yehova mahangaiko na matatizo yake badala ya kuwategemea wanadamu ni uthibitisho unaoonyesha kwamba hakuwa amekata tamaa. Ni wazi alihangaika kwa sababu hakujua wakati hususa ambapo Mungu angechukua hatua au sababu iliyomfanya Yehova aruhusu apitie hali hiyo iliyomsababishia maumivu mengi. Yehova alipomwongoza Habakuki aandike kuhusu mahangaiko yake, alitufundisha somo fulani muhimu: Hatupaswi kamwe kuogopa kumweleza kuhusu wasiwasi au mahangaiko yoyote tuliyo nayo. Kwa fadhili, Yehova mwenyewe anatualika tummiminie au tummwagie moyo wetu katika sala. (Zab. 50:15; 62:8) Zaidi ya hilo, andiko la Methali 3:5 linatutia moyo ‘tumtumaini Yehova kwa moyo wetu wote na wala tusitegemee uelewaji wetu wenyewe.’ Inaelekea Habakuki alijua maneno hayo na aliishi kulingana nayo.

6. Kwa nini ni muhimu kusali?

6 Habakuki alichukua hatua ya kumkaribia Yehova, Baba yake na Rafiki yake mwenye kutegemeka. Habakuki hakuruhusu hali aliyokuwa akipitia imfanye alemewe na wasiwasi, huku akitegemea uelewaji wake mwenyewe. Badala yake, alisali kuhusu hisia zake na mahangaiko aliyokuwa nayo, na hivyo kutuwekea mfano wa kuiga. Zaidi ya hilo, Yehova, Msikiaji wa sala, anatualika tuonyeshe kwamba tunamtumaini Yeye kwa kumweleza mahangaiko yetu kupitia sala. (Zab. 65:2) Tukifanya hivyo, tutajionea jinsi Yehova anavyoitikia—atatupatia kumbatio changamfu kwa kutuandalia kwa fadhili mwongozo wake. (Zab. 73:23, 24) Atatusaidia kujua mawazo yake hata iwe tunakabili mateso ya aina gani. Sala zetu za kutoka moyoni ni mojawapo ya njia bora kabisa ya kuonyesha kwamba tunamtumaini sana Mungu wetu.

MSIKILIZE YEHOVA

7. Yehova aliitikiaje Habakuki alipomweleza kuhusu mambo yaliyomhangaisha?

7 Soma Habakuki 1:5-7. Baada ya Habakuki kumtupia Yehova wasiwasi na mahangaiko aliyokuwa nayo, huenda alijiuliza Yehova angechukua hatua gani. Kwa kuwa Yehova ni Baba mwenye huruma na anaelewa hisia zetu, hakumkemea Habakuki alipolalamika kuhusu mambo yaliyomhangaisha. Mungu alijua kwamba hicho kilikuwa kilio cha mtu anayelilia msaada kwa sababu ya maumivu na huzuni aliyo nayo. Akizungumza kuhusu Wayahudi waliokuwa wameacha njia zake, Yehova alimjulisha Habakuki mambo ambayo yangetendeka baada ya muda usio mrefu. Inawezekana kwamba Habakuki ndiye mtu wa kwanza ambaye Yehova alimjulisha kwamba mwisho wa kipindi hicho kilichojaa watu waovu ulikuwa karibu sana.

8. Kwa nini jibu la Yehova lilimshangaza Habakuki?

8 Yehova alimwonyesha Habakuki kwamba alikuwa tayari kuchukua hatua. Hukumu dhidi ya kizazi hicho kilichojaa watu waovu na wakatili ilikuwa karibu sana. Maneno “katika siku zenu,” ambayo Yehova alimwambia Habakuki, yanaonyesha kwamba hukumu yake ingekuja katika siku zake au katika kipindi cha watu walioishi katika siku zake. Habakuki hakutarajia jibu ambalo Yehova alitoa. Je, kweli jibu ambalo Yehova alitoa lilikuwa ndilo suluhisho la kilio chake cha kumwomba achukue hatua bila kukawia? Kwa kweli, mambo ambayo Yehova alimwambia yalimaanisha kwamba mateso yangeongezeka kotekote katika nchi ya Yuda. Wakaldayo (Wababiloni) walikuwa watu wakatili na wauaji, hata kuliko watu wa taifa la Habakuki mwenyewe, ambao angalau walijua viwango vya Yehova. Kwa nini Yehova aliamua kutumia taifa hilo lisilomjua kuwaletea msiba watu wake? Wewe ungehisije baada ya kusikia jibu hilo kutoka kwa Mungu?

9. Huenda Habakuki alijiuliza maswali gani?

9 Soma Habakuki 1:12-14, 17. Habakuki alielewa kwamba Yehova angewatumia Wababiloni kuleta hukumu yake na kuwaadhibu watu waovu waliomzunguka, lakini bado jambo hilo lilimtatanisha. Hata hivyo, alimweleza Yehova kwa unyenyekevu kwamba ataendelea kumtumaini akiwa “Mwamba” wake. (Kum. 32:4; Isa. 26:4) Habakuki aliazimia kuendelea kuwa mwenye subira na kutumaini kwamba Yehova angethibitika kuwa Mungu mwenye upendo na fadhili. Kwa kuwa aliazimia hivyo, nabii huyo alipata ujasiri wa kumlilia Yehova kwa mara nyingine. Kwa nini Mungu angeruhusu hali nchini Yuda ziwe mbaya hata zaidi? Kwa nini hangechukua hatua mara moja? Kwa nini Mweza-Yote angevumilia kuona matatizo yakizidi kuongezeka? Kwa nini angeendelea “kunyamaza” wakati uovu unazidi kuongezeka? Yeye ni “Mtakatifu”; na “macho [yake] ni safi sana yasiweze kutazama uovu.”

10. Kwa nini nyakati nyingine huenda tukahisi kama Habakuki?

10 Nyakati nyingine, huenda sisi pia tukahisi kama Habakuki. Ni kweli kwamba tunamsikiliza Yehova. Na kwa kuwa tunamtumaini kikamili, tunasoma na kujifunza Neno lake, jambo ambalo hutupatia tumaini. Tunajifunza kuhusu ahadi zake kupitia mafundisho tunayopata katika tengenezo lake. Lakini bado huenda tukajiuliza, ‘Mateso yetu yatakwisha lini?’ Tunaweza kujifunza nini kutokana na hatua inayofuata ambayo Habakuki alichukua?

MNGOJEE YEHOVA

11. Habakuki aliazimia kufanya nini baada ya kumsikiliza Yehova?

11 Soma Habakuki 2:1. Mazungumzo ambayo Habakuki alifanya pamoja na Yehova yalimsaidia awe na utulivu moyoni. Hivyo, aliazimia kuendelea kumngojea Yehova akiwa na uhakika kwamba angechukua hatua. Hakuamua kufanya hivyo kwa sababu ya msisimko wa muda mfupi, kwa kuwa baadaye alirudia kutaja tena azimio lake aliposema kwamba “[angengojea] kimyakimya ile siku ya taabu.” (Hab. 3:16) Vilevile, watumishi wengine waaminifu wa Mungu walionyesha kwamba wangeendelea kumtumaini Yehova kwa subira, na mfano wao unatutia moyo tusikate tamaa tunapoendelea kumngojea Yehova achukue hatua.—Mika 7:7; Yak. 5:7, 8.

12. Tunajifunza mambo gani kutoka kwa Habakuki?

12 Tunajifunza nini kutokana na azimio ambalo Habakuki alikuwa nalo? Kwanza, hatupaswi kamwe kuacha kusali kwa Yehova, hata majaribu ya aina gani yatupate. Pili, tunahitaji kutii mambo ambayo Yehova anatuambia kupitia Neno lake na tengenezo lake. Tatu, tunapaswa kumngojea Yehova kwa subira, tukitumaini kikamili kwamba ataondoa maumivu yetu kwa wakati unaofaa. Ikiwa tutaendelea kumweleza Yehova hisia zetu kutoka moyoni na kumsikiliza tukiwa na mtazamo wa kumngojea kama Habakuki alivyofanya, sisi pia tutapata utulivu moyoni mwetu utakaotusaidia kuendelea kuvumilia. Tumaini letu litatusaidia tuendelee kuwa na subira, nayo subira itatusaidia kushangilia licha ya matatizo yoyote ambayo huenda tukakabili. Tumaini hutupatia uhakika kwamba Baba yetu wa mbinguni atachukua hatua.—Rom. 12:12.

13. Andiko la Habakuki 2:3 linatuhakikishia nini?

13 Soma Habakuki 2:3. Bila shaka Yehova alifurahishwa na uamuzi wa Habakuki wa kumngojea. Mweza-Yote alielewa kikamili hali ngumu ambazo Habakuki alikuwa akipitia. Hivyo, Mungu alimfariji nabii huyo kwa kumhakikishia kwa upendo na upole kwamba angepata majibu ya maswali yake ya unyoofu. Baada ya muda si mrefu, angepata kitulizo cha mahangaiko yake yote. Ni kana kwamba Mungu alikuwa akimwambia hivi Habakuki: “Uwe na subira, nitumaini. Nitakujibu hata ikionekana ni kana kwamba ninachelewa!” Yehova alimkumbusha kwamba ameweka wakati hususa wa kutimiza ahadi Zake. Alimshauri Habakuki aendelee kumngojea atimize ahadi Zake. Na bila shaka hangetamaushwa.

Kwa nini tumeazimia kumtumikia Yehova kwa uwezo wetu wote? (Tazama fungu la 14)

14. Tunapaswa kuazimia kufanya nini tunapokumbwa na hali ngumu?

14 Kumngojea Yehova kwa subira na kuzingatia kwa makini mambo anayotuambia kutatuondolea wasiwasi na kutusaidia kuwa na utulivu moyoni licha ya matatizo na hali zozote ngumu zinazoweza kutupata. Yesu alituhakikishia kwamba tunaweza kumtumaini Yehova, Mtunza-Wakati Mkuu, badala ya kuhangaikia “nyakati au majira” ambayo Mungu hajatufunulia bado. (Mdo. 1:7) Basi, na tusife moyo, bali tumngojee Yehova kwa unyenyekevu, imani, na subira, tukitumia vizuri wakati tulio nao kumtumikia Yehova kwa uwezo wetu wote.—Marko 13:35-37; Gal. 6:9.

KUMTUMAINI YEHOVA KUTATUSAIDIA KUPATA UZIMA NA WAKATI UJAO WENYE FANAKA

15, 16. (a) Ni ahadi gani zenye kugusa moyo zilizo kwenye kitabu cha Habakuki? (b) Tunajifunza nini kutokana na ahadi hizo?

15 Yehova anawaahidi hivi watu waadilifu wanaomtumaini: “Mwadilifu ataishi kwa uaminifu wake,” na “dunia itajaa ujuzi wa utukufu wa Yehova.” (Hab. 2:4, 14) Naam, wale wote wanaoendelea kumtumaini Mungu kwa subira watathawabishwa kwa kupewa uzima.

16 Kwa kutazama kijuujuu, ahadi inayopatikana kwenye Habakuki 2:4 inaweza kuonekana kama taarifa ya ujumla tu. Lakini mtume Paulo aliyaona maneno hayo ya Yehova yenye uhakikisho kuwa ya pekee sana hivi kwamba alinukuu mstari huo mara tatu! (Rom. 1:17; Gal. 3:11; Ebr. 10:38) Hata mwadilifu akabili matatizo ya aina gani, imani na tumaini lake kwa Mungu litamwezesha kuishi na kujionea ahadi za Mungu zikitimia. Yehova anatuambia tukazie macho yetu kwenye mambo yajayo.

17. Kitabu cha Habakuki kinatuhakikishia nini?

17 Kitabu cha Habakuki kinatufundisha somo muhimu sana sisi tunaoishi katika siku hizi za mwisho. Yehova anaahidi kumpa uzima mtu yeyote mwadilifu anayemwamini na kumtumaini. Acheni tuendelee kuimarisha imani yetu kwa Mungu na kuendelea kumtumaini, hata iwe tunakabili matatizo au mikazo gani maishani. Kupitia nabii Habakuki, Yehova anatuhakikishia kwamba atatutegemeza na kutuokoa. Kwa fadhili, anatusihi tumtumaini na kungojea kwa subira wakati wake uliowekwa, ambapo chini ya Ufalme wake dunia nzima itajawa na waabudu wake wenye furaha na wenye sifa ya upole.—Mt. 5:5; Ebr. 10:36-39.

MTUMAINI YEHOVA UKIWA NA SHANGWE

18. Maneno ya Yehova yalimwimarishaje Habakuki?

18 Soma Habakuki 3:16-19. Maneno ya Yehova yalimwimarisha sana Habakuki. Alitafakari kuhusu matendo yenye kustaajabisha ambayo Yehova alifanya wakati uliopita kwa niaba ya watu wake. Sasa alipata sababu nzuri ya kumtumaini Yehova hata zaidi. Alijua kwamba punde, Yehova angechukua hatua! Jambo hilo lilimfariji nabii huyo, hata ingawa alijua kwamba angeendelea kuteseka kwa muda fulani. Ingawa mwanzoni Habakuki hakuwa na uhakika kwamba Yehova angechukua hatua, hatimaye mtazamo wake ulibadilika na kwa shangwe akatumaini bila kuyumbayumba nguvu za Yehova za kuokoa. Huenda maneno yenye uhakika aliyosema ni kati ya maneno yanayokumbukwa zaidi ambayo yamewahi kusemwa na mwanadamu. Wasomi fulani wanasema kwamba kihalisi mstari wa 18 unamaanisha, “Nitaruka kwa shangwe katika Bwana; nitajizungusha-zungusha kwa sababu ninamfurahia Mungu.” Maneno hayo yanatupatia sisi sote uhakika wenye nguvu sana! Yehova hajatuahidi tu mambo yenye kusisimua, bali pia ametuhakikishia kwamba yuko mbioni kutekeleza kusudi lake kuu.

19. Tunaweza kupataje faraja kama ile ambayo Habakuki alipata?

19 Hapana shaka kwamba ujumbe muhimu ulio katika kitabu cha Habakuki ni kumtumaini Yehova. (Hab. 2:4) Tunaweza kumtumaini Yehova na kuendelea kufanya hivyo ikiwa tutaimarisha uhusiano wetu pamoja naye kwa kufanya mambo yafuatayo: (1) kwa kudumu katika sala na kumweleza Yehova kuhusu wasiwasi wetu na mambo yanayotuhangaisha; (2) kwa kuzingatia kwa uangalifu Neno la Mungu na mwongozo wowote tunaopokea kupitia tengenezo lake; na (3) kwa kumngojea Yehova kwa uaminifu na subira. Hivyo ndivyo Habakuki alivyofanya. Ingawa mwanzoni mwa kitabu chake Habakuki alianza kwa maneno yenye huzuni, alimalizia kwa maneno yenye uhakika na msisimko wa shangwe. Acheni tuige kielelezo chake chenye kuchochea ili sisi pia tuhisi kumbatio la Yehova, Baba yetu! Je, kuna faraja yoyote tunayoweza kupata katika ulimwengu huu wenye giza inayozidi faraja hiyo?