Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Nani Ambaye Hufinyanga Njia Yako ya Kufikiri?

Ni Nani Ambaye Hufinyanga Njia Yako ya Kufikiri?

“Acheni kufinyangwa na mfumo huu wa mambo.”—ROM. 12:2.

NYIMBO: 88, 45

1, 2. (a) Yesu aliitikiaje Petro alipompa ushauri kwamba ajihurumie? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.) (b) Kwa nini Yesu aliitikia kwa njia hiyo?

WANAFUNZI wa Yesu hawakuamini walichokuwa wakisikia. Yesu, ambaye walimtarajia arudishe ufalme katika taifa la Israeli, alisema kwamba baada ya muda mfupi angeteseka na kufa. Mtume Petro alishindwa kujizuia, akamwambia, “Bwana jihurumie. Hutapatwa kamwe na mambo hayo.” Yesu akamkatiza na kusema, “Nenda nyuma yangu, Shetani! Wewe ni kikwazo kwangu, kwa sababu hufikirii mawazo ya Mungu, bali ya wanadamu.”—Mt. 16:21-23; Mdo. 1:6.

2 Kwa maneno hayo, Yesu aliweka wazi tofauti iliyopo kati ya mawazo yanayotoka kwa Mungu na mawazo ya ulimwengu huu unaoongozwa na Shetani. (1 Yoh. 5:19) Petro alionyesha mtazamo wa ulimwengu huu wa kujitendea kwa fadhili. Lakini Yesu alijua kwamba njia ya Baba yake ya kufikiri ilikuwa tofauti. Alijua kwamba Mungu alitaka awe tayari kwa ajili ya mateso na kifo kilichokuwa mbele yake. Jibu ambalo Yesu alimpa Petro, lilionyesha wazi kwamba alipinga njia ya kufikiri ya ulimwengu huu na kushikamana na njia ya Yehova ya kufikiri.

3. Kwa nini si rahisi kupinga njia ya kufikiri ya ulimwengu huu ili tupatanishe mawazo yetu na njia ya Yehova ya kufikiri?

3 Namna gani sisi? Je, sisi hufikiri kama Mungu au kama ulimwengu? Ni kweli kwamba huenda tumepatanisha mwenendo wetu na matakwa ya Mungu. Lakini vipi kuhusu njia yetu ya kufikiri? Je, tunapatanisha mawazo na njia yetu ya kuona mambo na njia ya Yehova ya kufikiri? Jitihada nyingi za kibinafsi zinahitajika ili kufanya hivyo. Kwa upande mwingine, kufyonza mawazo ya ulimwengu huu hakuhitaji jitihada yoyote. Na hali iko hivyo kwa sababu tumezungukwa kotekote na roho ya ulimwengu. (Efe. 2:2) Zaidi ya hilo, kwa kuwa roho hiyo huwachochea watu kutanguliza masilahi yao binafsi, ni rahisi kushawishiwa na njia ya kufikiri ya ulimwengu. Naam, si rahisi kufikiri kama Yehova anavyofikiri, lakini ni rahisi sana kufikiri kama ulimwengu unavyofikiri.

4. (a) Ni nini kitakachotendeka tukiruhusu ulimwengu ufinyange njia yetu ya kufikiri? (b) Makala hii itatusaidiaje?

4 Hata hivyo, tukiruhusu ulimwengu huu ufinyange au kuongoza njia yetu ya kufikiri, tutaanza kusitawisha roho ya ubinafsi na tamaa ya kujiongoza wenyewe. (Marko 7:21, 22) Hivyo, ni muhimu sana kwamba tusitawishe “mawazo ya Mungu,” badala “ya [mawazo ya] wanadamu.” Makala hii itatusaidia kufanya hivyo. Makala hii inaeleza kwa nini kupatanisha mawazo yetu na mawazo ya Yehova si jambo linalotunyima uhuru bali linalotunufaisha. Pia, inatuonyesha jinsi tunavyoweza kukataa kufinyangwa na njia ya kufikiri ya ulimwengu. Katika makala inayofuata, tutachunguza jinsi tunavyoweza kujua maoni ya Yehova kuhusu mambo mbalimbali na kufanya njia yake ya kufikiri iwe ndiyo njia yetu ya kufikiri.

NJIA YA YEHOVA YA KUFIKIRI NI NZURI NA HUTUNUFAISHA

5. Kwa nini baadhi ya watu hawapendi kufinyangwa au kuongozwa na mtu mwingine?

5 Baadhi ya watu hawapendi mtu yeyote awaamulie jinsi wanavyopaswa kuona mambo. Wao husema, “Nitajiamulia mwenyewe.” Hata hivyo, huenda wanamaanisha kwamba watajifanyia maamuzi yao wenyewe, na hawaoni ubaya wowote wa kufanya hivyo. Hawataki kuongozwa wala hawangependa kupoteza sifa ambazo huwatofautisha na wengine. *

6. (a) Yehova ametupatia uhuru wa aina gani? (b) Je, inamaanisha kwamba uhuru huo hauna mipaka?

6 Hata hivyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba kupatanisha njia yetu ya kufikiri na njia ya Yehova ya kufikiri hakumaanishi kwamba tutapoteza sifa zinazotufanya kuwa tofauti na wengine. Kama andiko la 2 Wakorintho 3:17 linavyosema, “mahali palipo na roho ya Yehova, pana uhuru.” Kila mmoja wetu yuko huru kusitawisha sifa zinazomfanya awe tofauti na wengine. Sote tuna mambo tunayopendelea na tunaweza kuchagua mambo tunayopenda kufanya. Na kwa kweli, hivyo ndivyo Yehova alivyotuumba. Ingawa hivyo, uhuru wetu una mipaka. (Soma 1 Petro 2:16.) Inapohusu suala la kutofautisha kati ya lililo sahihi na lililo kosa, Yehova anataka tuongozwe na njia yake ya kufikiri ambayo imefunuliwa katika Neno lake. Je, kufanya hivyo hutunyima uhuru, au hutuletea manufaa?

7, 8. Kwa nini kusitawisha maoni ya Yehova kuhusu mambo hakutunyimi uhuru? Toa mfano.

7 Fikiria mfano huu. Wazazi hujitahidi kuwazoeza watoto wao kuwa na tabia nzuri. Huenda wakawafundisha kuwajali wengine, kuwa wanyoofu, na kuwa wenye bidii. Kufanya hivyo hakuwanyimi watoto wao uhuru. Badala yake, wazazi hao wanawasaidia watoto wao wafanikiwe maishani watakapokuwa watu wazima wanaojitegemea. Watoto watakapokua na kuondoka nyumbani, watakuwa huru kufanya maamuzi yao wenyewe. Ikiwa watachagua kuishi kulingana na mambo ambayo wazazi wao waliwafundisha, itakuwa rahisi kwao kufanya maamuzi ambayo hawatajutia baadaye. Hivyo, hawatapatwa na matatizo na mahangaiko ya kujiletea wenyewe.

8 Kama mzazi mzuri, Yehova anataka watoto wake wafurahie maisha bora kabisa. (Isa. 48:17, 18) Hivyo, anatufundisha kanuni za msingi zitakazotusaidia kuwa na mwenendo safi na kujua jinsi tunavyopaswa kuwatendea wengine. Anatupatia fursa ya kusitawisha maoni aliyo nayo kuhusu mambo hayo na kuwa na viwango kama vyake. Njia yake ya kufikiri haitubani, badala yake huboresha, huongeza, na kupanua uwezo wetu wa kufikiri. (Zab. 92:5; Met. 2:1-5; Isa. 55:9) Kufikiri kama Yehova hutusaidia kufanya maamuzi yatakayotuletea furaha na wakati huohuo kuturuhusu tuendelee kunawiri tukiwa mtu mmojammoja. (Zab. 1:2, 3) Naam, kuiga njia ya Yehova ya kufikiri hutunufaisha na ni jambo zuri!

NJIA YA YEHOVA YA KUFIKIRI NI BORA

9, 10. Njia ya Yehova ya kufikiri imethibitikaje kuwa bora kuliko ile ya ulimwengu?

9 Sababu nyingine inayowachochea waabudu wa Yehova watamani kupatanisha njia yao ya kufikiri na njia ya Mungu ya kufikiri ni kwamba njia Yake ya kufikiri ni bora kuliko ile ya ulimwengu. Nyanja mbalimbali za ulimwengu huu zimetoa ushauri kuhusu maadili, mahusiano katika familia, jinsi ya kuridhika na kazi uliyo nayo, na mambo mengine ya maisha. Ushauri mwingi unaotolewa haupatani hata kidogo na njia ya Yehova ya kufikiri. Kwa mfano, ulimwengu huwachochea watu wajione kuwa bora kuliko wengine. Pia, huwachochea watu waone kwamba kufanya uasherati ni jambo linalokubalika. Nyakati nyingine watu hushauriwa watengane au kutalikiana bila sababu za msingi na wanaambiwa kwamba kufanya hivyo kutawaletea furaha nyingi zaidi. Mashauri hayo ni kinyume kabisa na Maandiko. Lakini je, kweli kuna ushauri unaotolewa na ulimwengu unaofaa zaidi nyakati zetu?

10 Yesu alisema hivi: “Hekima huthibitishwa kuwa yenye uadilifu kupitia kazi zake.” (Mt. 11:19) Ulimwengu umepiga hatua kubwa sana kiteknolojia; hata hivyo, umeshindwa kusuluhisha matatizo makubwa yanayowafanya watu wakose furaha, kama vile vita, ubaguzi, na uhalifu. Na vipi kuhusu mtazamo wake wa kupuuza viwango vya maadili? Watu wengi wanakiri kwamba mtazamo huo haujasuluhisha matatizo, badala yake umefanya familia zivunjike, umesababisha magonjwa, na matatizo mengine. Kwa upande mwingine, Wakristo wanaositawisha maoni ya Mungu wanafurahia uhusiano mzuri katika familia zao, wana afya nzuri kwa sababu ya mwenendo safi, na wanafurahia amani miongoni mwa waabudu wenzao kotekote ulimwenguni. (Isa. 2:4; Mdo. 10:34, 35; 1 Kor. 6:9-11) Je, huo si uthibitisho wa kwamba njia ya Yehova ya kufikiri ndiyo bora kuliko ile ya ulimwengu?

11. Ni njia ya nani ya kufikiri iliyomwongoza Musa, na matokeo yalikuwa nini?

11 Waabudu wa kweli wanaotajwa katika Biblia walitambua kwamba njia ya Yehova ya kufikiri ndiyo njia bora zaidi. Kwa mfano, ingawa Musa alikuwa ameelimishwa katika “hekima yote ya Wamisri,” alimtegemea Mungu ili apate “moyo wa hekima.” (Mdo. 7:22; Zab. 90:12) Pia, alimsihi Yehova hivi: “Nifundishe njia zako.” (Kut. 33:13) Kwa kuwa aliongozwa na njia ya Yehova ya kufikiri, alishiriki kwa njia kubwa katika kutimizwa kwa kusudi la Mungu na anasifiwa katika Maandiko kwamba alikuwa mwanamume mwenye imani ya pekee.—Ebr. 11:24-27.

12. Hoja za Paulo zilitegemea nini?

12 Mtume Paulo alikuwa mtu msomi na mwenye akili nyingi, na alijua angalau lugha mbili. (Mdo. 5:34; 21:37, 39; 22:2, 3) Lakini alipohitaji kufanya maamuzi, alikataa hekima ya ulimwengu. Hoja alizotoa zilitegemea Maandiko. (Soma Matendo 17:2; 1 Wakorintho 2:6, 7, 13.) Kwa sababu hiyo, Paulo alifurahia huduma yenye matokeo mazuri na alitazamia kupokea thawabu ya milele.—2 Tim. 4:8.

13. Ni nani aliye na jukumu la kupatanisha njia yetu ya kufikiri na ile ya Yehova?

13 Ni wazi kwamba njia ya Mungu ya kufikiri ni bora kuliko ile ya ulimwengu huu. Kuishi kulingana na mawazo yake kutatuletea furaha nyingi na mafanikio. Lakini Yehova hatatulazimisha tuige njia yake ya kufikiri. “Mtumwa mwaminifu na mwenye busara” hamlazimishi yeyote afikiri kama anavyofikiri, na wazee pia hawafanyi hivyo. (Mt. 24:45; 2 Kor. 1:24) Badala yake, kila Mkristo ana jukumu la kibinafsi la kupatanisha njia yake ya kufikiri na ile ya Mungu. Tunaweza kufanyaje hivyo?

EPUKA KUFINYANGWA NA MFUMO HUU

14, 15. (a) Ili kufikiri kama Yehova anavyofikiri, ni lazima tutafakari kuhusu nini? (b) Kwa msingi wa andiko la Waroma 12:2, kwa nini ni lazima tuepuke kujilisha mawazo ya ulimwengu? Toa mfano.

14 Andiko la Waroma 12:2, linatushauri hivi: “Acheni kufinyangwa na mfumo huu wa mambo, bali mgeuzwe kwa kufanya upya akili yenu, ili mjihakikishie wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” Maneno hayo yaliyoongozwa na roho yanaonyesha kwamba hata iwe tulikuwa na njia gani ya kufikiri kabla ya kujifunza kweli, inawezekana kuipatanisha na njia ya Mungu ya kufikiri. Ni kweli kwamba njia yetu ya kufikiri imeathiriwa kwa njia fulani na sifa tulizorithi au mambo tuliyopitia zamani. Lakini akili yetu ina uwezo wa kuendelea kubadilika. Kwa kadiri kubwa, mabadiliko hayo yanategemea mambo tunayoruhusu yaingie akilini mwetu na mambo tunayotumia muda mwingi kuyafikiria. Ikiwa tutatumia muda mwingi kufikiria au kutafakari njia ya Yehova ya kufikiri, tutajithibitishia wenyewe kwamba njia yake ya kuona mambo ndiyo njia sahihi. Kisha tutatamani kutoka moyoni kupatanisha mawazo yetu na mawazo yake.

15 Hata hivyo, ona kwamba ili akili yetu ifanywe kuwa mpya na kufanana na njia ya Yehova ya kufikiri, tunahitaji “[kuacha] kufinyangwa na mfumo huu wa mambo.” Ni lazima tuache kuingiza akilini mwetu mawazo na njia ya kuona mambo inayopingana na njia ya Mungu ya kuona mambo. Tunaweza kulinganisha umuhimu wa kuchukua hatua hiyo ya kwanza na chakula. Tuseme kwamba mtu anataka kuboresha afya yake na hivyo anaanza kula chakula chenye lishe. Lakini kufanya hivyo kungekuwa na manufaa gani ikiwa mara kwa mara angejilisha chakula kilichoharibika au kuchafuliwa? Vivyo hivyo, hatutanufaika kikamili na mawazo ya Yehova ikiwa tutachafua akili yetu na mawazo ya ulimwengu.

16. Tunapaswa kujilinda dhidi ya nini?

16 Je, inawezekana kuepuka kabisa mawazo ya ulimwengu? Hapana, kwa kuwa hatuwezi kutoka kihalisi katika ulimwengu huu. Baadhi ya mawazo ya ulimwengu huu hayaepukiki. (1 Kor. 5:9, 10) Kazi ya kuhubiri yenyewe itatufanya tukutane na watu wenye imani zisizo sahihi. Hata hivyo, ikiwa haiwezekani kuepuka kabisa maoni hayo yasiyopatana na njia ya Mungu ya kufikiri, hatupaswi kamwe kuendelea kuyafikiria au kuyakubali. Kama Yesu alivyofanya, tunapaswa kukataa mara moja mawazo yanayoendeleza kusudi la Shetani. Isitoshe, tunaweza kujilinda ili tusijikute isivyo lazima katika hali inayoweza kufanya tuathiriwe na njia ya kufikiri ya ulimwengu huu.—Soma Methali 4:23.

17. Tunapaswa kuepuka mambo gani yanayoweza kufanya tuathiriwe na njia ya kufikiri ya ulimwengu?

17 Kwa mfano, tunapaswa kuwa waangalifu tunapochagua marafiki. Biblia inatuonya kwamba ikiwa tutashirikiana kwa ukaribu na watu wasiomwabudu Yehova, njia yao ya kufikiri inaweza kutuathiri. (Met. 13:20; 1 Kor. 15:12, 32, 33) Pia, tunapaswa kuwa waangalifu tunapochagua burudani. Tunapokataa burudani zinazoendeleza nadharia ya mageuzi, ukatili, au uasherati, tunalinda akili yetu isichafuliwe na mawazo yaliyo “kinyume cha ujuzi wa Mungu.”—2 Kor. 10:5.

Je, tunawasaidia watoto wetu wakatae burudani zenye kudhuru? (Tazama fungu la 18 na 19)

18, 19. (a) Kwa nini ni lazima tuwe macho tusiathiriwe na maoni ya ulimwengu yanayoendelezwa kwa njia iliyofichika? (b) Tunapaswa kujiuliza maswali gani, na kwa nini?

18 Pia, ni jambo linalofaa kutambua na kupinga mawazo yaliyojificha yanayoendeleza njia ya kufikiri ya ulimwengu huu. Kwa mfano, taarifa fulani ya habari inaweza kuwasilishwa kwa njia inayopendelea sera fulani za kisiasa. Habari fulani kuhusu maisha ya mtu inaweza kutumiwa kuendeleza maoni ya ulimwengu kuhusu malengo na mafanikio. Baadhi ya sinema na vitabu huendeleza falsafa ya “mimi kwanza” na “familia yangu kwanza,” na hivyo kuwafanya watu waone kuwa falsafa hizo ni nzuri, zinavutia, na hakuna ubaya wa kuzifuata. Njia hiyo ya kuona mambo haizingatii maoni ya Maandiko kwamba ili familia zetu zisitawi na tuwe na maoni yanayofaa kujihusu, ni lazima tumpende Yehova kuliko vitu vingine vyote maishani. (Mt. 22:36-39) Pia, baadhi ya hadithi za watoto ambazo huenda zinakubalika zinaweza, kwa njia iliyofichika, kupanda mawazo ya kwamba kufanya uasherati ni jambo linalokubalika.

19 Hilo halimaanishi kwamba ni kosa kufurahia burudani zinazofaa. Hata hivyo, inafaa tujiulize maswali haya: ‘Je, tunatambua mawazo ya ulimwengu, hata kama yanaendelezwa kwa njia iliyofichika? Je, tunadhibiti vipindi vya televisheni au vitabu na magazeti ambayo watoto wetu, au hata sisi wenyewe, tunatazama au kusoma? Watoto wetu wanaposikia au kuona jambo fulani linaloendeleza njia ya kufikiri ya ulimwengu, je, sisi huwasaidia mara moja kwa kupanda akilini mwao mawazo ya Yehova kuhusu jambo hilo?’ Ikiwa tutatambua tofauti iliyopo kati ya njia ya Mungu ya kufikiri na ile ya ulimwengu, tutaepuka “kufinyangwa na mfumo huu wa mambo.”

NI NANI ANAYEKUFINYANGA SASA?

20. Ni nini kitakachotusaidia kujua ikiwa tunaongozwa na njia ya Mungu ya kufikiri au ile ya ulimwengu?

20 Kumbuka kwamba watu hujifunza mambo mbalimbali kutoka katika vyanzo viwili vikuu, yaani, Yehova au ulimwengu unaoongozwa na Shetani. Wewe binafsi unafinyangwa na nani? Inategemea ni chanzo gani kinachokuelimisha. Tukijilisha mawazo ya ulimwengu, mawazo hayo yatafinyanga njia yetu ya kufikiri na kutuongoza tuwe na maoni na tabia zinazochochewa na tamaa za kimwili. Hiyo ndiyo sababu ni muhimu tuwe waangalifu kuhusu mambo tunayotumia wakati mwingi kuyafikiria.

21. Ni jambo gani muhimu litakalozungumziwa katika makala inayofuata?

21 Kama tulivyojifunza awali, ili tusitawishe njia ya Yehova ya kufikiri, ni lazima tufanye mengi zaidi ya kuepuka tu mambo yanayoweza kuchafua akili yetu. Pia, ni lazima tujilishe mawazo ya Mungu tukiwa na lengo la kuyafanya yawe mawazo yetu. Makala inayofuata itazungumzia zaidi jinsi tunavyoweza kufanya hivyo.

^ fu. 5 Kihalisi, hata watu wanaojulikana kuwa na msimamo thabiti kimawazo hawawezi kuepuka kuathiriwa na wengine. Iwe wanadamu wanachanganua mambo mazito kama vile chanzo cha uhai au kufikiria tu ni mavazi gani watakayovaa, kwa kiwango fulani kila mtu huathiriwa na maoni ya watu wengine. Ingawa hivyo, tunaweza kuamua ni nani atakayefinyanga njia yetu ya kufikiri.