Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Nitatembea Katika Kweli Yako”

“Nitatembea Katika Kweli Yako”

“Nifundishe, Ee Yehova, kuhusu njia yako. Nitatembea katika kweli yako.”—ZAB. 86:11.

NYIMBO: 31, 72

1-3. (a) Tunapaswa kuhisije kuhusu kweli ya Biblia? Toa mfano. (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.) (b) Tutachunguza maswali gani katika makala hii?

SIKU hizi ni jambo la kawaida kwa mtu kurudisha dukani bidhaa fulani aliyokuwa amenunua. Inakadiriwa kwamba katika nchi fulani, watu hurudisha dukani karibu asilimia 9 ya bidhaa walizonunua. Na inakadiriwa kwamba asilimia 30 ya bidhaa zilizonunuliwa mtandaoni hurudishwa baada ya kununuliwa. Huenda wateja huzirudisha kwa sababu zilikuwa na kasoro, hazikuwafurahisha, au kuwaridhisha. Hivyo, wanaamua kubadilisha bidhaa hizo na bidhaa nyingine au kuomba warudishiwe pesa zao.

2 Ingawa huenda tukaomba turudishiwe pesa za bidhaa fulani tuliyonunua, hatungependa kamwe kurudisha, au ‘kuuza’ “ujuzi sahihi” wa kweli ya Biblia ‘tunayonunua.’ (Soma Methali 23:23; 1 Tim. 2:4) Kama tulivyojifunza katika makala iliyotangulia, tulijipatia kweli kwa kutumia wakati mwingi kujifunza kweli hiyo. Isitoshe, ili kununua kweli, huenda tuliacha kazi fulani nzuri na yenye mshahara mnono, tulikabili changamoto kwa sababu uhusiano wetu na wengine ulibadilika, tulibadili mwenendo wetu na njia yetu ya kufikiri, au kuacha kabisa mazoea na desturi zisizo za Kimaandiko. Hata hivyo, gharama tuliyolipia ni ndogo ikilinganishwa na baraka ambazo tumepata.

3 Inapohusu kweli ya Biblia, hisia zetu ni kama za mwanamume ambaye Yesu alizungumza juu yake kwenye mfano mfupi aliosimulia. Ili kuonyesha jinsi kweli ya Ufalme wa Mungu ilivyo yenye thamani, Yesu alisimulia kuhusu mfanyabiashara anayesafiri ambaye alikuwa akitafuta lulu nzuri ambapo hatimaye alipata lulu moja. Kwa kweli, lulu hiyo ilikuwa na thamani kubwa sana hivi kwamba ‘aliuza mara moja’ kila kitu alichokuwa nacho na kuinunua. (Mt. 13:45, 46) Vivyo hivyo, kweli tuliyopata, inayotia ndani kweli kuhusu Ufalme wa Mungu na kweli nyinginezo zenye thamani tulizojifunza katika Neno la Mungu—ni yenye thamani sana kwetu hivi kwamba tulikuwa tayari kugharimika ili kuipata na mara moja tulichukua hatua ya kuinunua. Maadamu tunaiona kweli kuwa yenye thamani kwetu, ‘hatutaiuza kamwe.’ Hata hivyo, inasikitisha kwamba baadhi ya watu wa Mungu wameacha kuiona kweli waliyopata kuwa yenye thamani, na hata wameiuza. Tusiruhusu kamwe jambo kama hilo litupate! Ili kuonyesha kwamba tunaiona kweli kuwa yenye thamani sana na kwamba hatungependa kamwe kuiuza, ni lazima tutii himizo la Biblia linalosema, “[Endeleeni] kutembea katika kweli.” (Soma 3 Yohana 2-4.) Kutembea katika kweli kunahusisha kuishi kulingana na kweli, yaani, kuitanguliza maishani na kupatanisha mwenendo wetu na kweli hiyo. Acheni tuchunguze maswali haya: Kwa nini baadhi ya Wakristo ‘huuza’ kweli, nao hufanya hivyo jinsi gani? Tunaweza kuepukaje kufanya kosa hilo lenye kusikitisha? Tunaweza kuimarishaje azimio letu la “[kuendelea] kutembea katika kweli”?

KWA NINI WENGINE ‘HUUZA’ KWELI, NAO HUFANYAJE HIVYO?

4. Katika karne ya kwanza, kwa nini baadhi ya watu ‘waliuza’ kweli?

4 Katika karne ya kwanza, baadhi ya watu ambao mwanzoni walikubali mafundisho ya Yesu, hawakuendelea kutembea katika kweli. Kwa mfano, baada ya umati mkubwa wa watu kulishwa na Yesu kimuujiza, umati huo ulimfuata ng’ambo ile nyingine ya Bahari ya Galilaya. Huko, Yesu alisema jambo fulani lililowashtua: “Msipokula mwili wa Mwana wa binadamu na kunywa damu yake, hamna uzima ndani yenu.” Badala ya kumwomba Yesu afafanue alichomaanisha, walikwazwa na maneno yake na kusema hivi: “Maneno hayo yanashtua; ni nani anayeweza kuyasikiliza?” Kwa sababu hiyo, “wengi kati ya wanafunzi wake wakarudi kwenye mambo yaliyo nyuma nao hawakumfuata tena.”—Yoh. 6:53-66.

5, 6. (a) Katika nyakati za hivi karibuni, kwa nini baadhi ya watumishi wa Mungu wameshindwa kushikamana na kweli? (b) Mtu anawezaje kuiacha kweli hatua kwa hatua?

5 Inasikitisha kwamba baadhi ya watumishi wa Mungu wameshindwa kushikamana na kweli. Baadhi yao walikwazika baada ya kupokea uelewaji mpya wa mistari fulani ya Biblia au kwa sababu ya jambo fulani ambalo ndugu anayefahamika alisema au kutenda. Wengine hawakufurahishwa na shauri fulani la Kimaandiko walilopewa, au waliacha kweli kwa sababu ya mkwaruzano baina yao na Mkristo mwenzao. Na wengine waliwaunga mkono waasi imani na wapinzani wengine waliosema mambo yasiyo ya kweli kuhusu yale tunayoamini. Kwa sababu hiyo, baadhi yao walianza ‘kujiondoa’ kimakusudi kutoka kwa Yehova na kutaniko lake. (Ebr. 3:12-14) Hali ingekuwa bora zaidi ikiwa wangeendelea kushika imani na kuweka uhakika wao katika Yesu, kama mtume Petro alivyofanya! Yesu alipowauliza mitume wake ikiwa walitaka kumwacha, mara moja Petro alimjibu hivi: “Bwana, tutaenda kwa nani? Wewe una maneno ya uzima wa milele.”—Yoh. 6:67-69.

6 Wengine wameacha kweli hatua kwa hatua, labda hata bila kutambua. Mtu anayeacha kweli hatua kwa hatua ni kama mashua inayosukumwa pole kwa pole mbali na ukingo wa mto. Biblia inaiita hali hiyo inayotokea pole kwa pole kuwa ‘kupeperushwa.’ (Ebr. 2:1) Tofauti na mtu anayejiondoa kimakusudi kutoka kwenye kweli, mtu anayepeperuka mbali na kweli hafanyi hivyo kimakusudi. Ingawa hivyo, mtu huyo anafanya uhusiano wake pamoja na Mungu uzorote na yuko katika hatari ya kuupoteza. Tunaweza kuepukaje kupatwa na hali kama hiyo inayoweza kutusababishia msiba mkubwa?

TUNAWEZA KUFANYA NINI ILI TUSIIUZE KWELI?

7. Ni hatua gani ya kwanza tunayopaswa kuchukua ili tusiiuze kweli?

7 Ili tutembee katika kweli, ni lazima tukubali na kutii mambo yote ambayo Yehova anatuambia. Ni lazima tutangulize kweli maishani mwetu na kuishi kulingana na kanuni za Biblia. Mfalme Daudi alisali hivi kwa Yehova: “Nitatembea katika kweli yako.” (Zab. 86:11) Daudi alikuwa ameazimia kuendelea kutembea katika kweli. Sisi pia tunapaswa kuazimia kwa dhati kuendelea kutembea katika kweli ya Mungu. Ikiwa hatujaazimia kwa dhati, ni rahisi kuanza kuhisi kwamba gharama tuliyolipa ili kupata kweli ni kubwa sana na hata labda kuanza kutamani baadhi ya vitu tulivyoacha ili kuinunua. Badala ya kufanya hivyo, tunaendelea kushikamana na kweli yote kwa umakini. Tunatambua kwamba hatuwezi kujichagulia ni kweli gani tutakazokubali na ni zipi tutakazopuuza. Ukweli ni kwamba ni lazima tutembee katika “kweli yote.” (Yoh. 16:13) Acheni tuchunguze mambo matano ambayo huenda tuligharimika ili kununua kweli. Kufanya hivyo kutatusaidia kuimarisha azimio letu la kutonaswa na mtego wa kutamani hata sehemu ndogo ya gharama tuliyolipa ili kununua kweli.—Mt. 6:19.

8. Kutumia wakati kwa njia isiyo ya hekima kunaweza kumfanyaje Mkristo apeperushwe mbali na kweli? Toa mfano.

Wakati. Ili tusipeperushwe pole kwa pole kutoka kwenye kweli, ni lazima tutumie wakati wetu kwa hekima. Tusipokuwa waangalifu, huenda tukaanza kutumia wakati mwingi kujiburudisha, kujishughulisha na mapendezi yetu, kutembelea vituo mbalimbali vya Intaneti, au kutazama televisheni. Ingawa si kosa kufanya mambo hayo, hatua kwa hatua yanaweza kuanza kuchukua wakati ambao hapo awali tuliutumia kujifunza Biblia kibinafsi na kushiriki katika utendaji mwingine wa kiroho. Fikiria kisa cha dada mmoja Mkristo anayeitwa Emma. * Tangu alipokuwa kijana, Emma aliwapenda sana farasi. Kila alipopata nafasi, aliendesha farasi. Baada ya muda, alianza kusumbuka kwa sababu alitumia muda mwingi sana kuendesha farasi. Alifanya mabadiliko na hatimaye akafanikiwa kuacha kutumia muda mwingi kujifurahisha. Alitiwa moyo na simulizi la Cory Wells, ambaye awali alipenda kufanya sarakasi kwa kutumia farasi kwenye maonyesho yanayoitwa rodeo. * Sasa Emma anafurahia kutumia wakati wake mwingi katika utendaji wa kiroho na kushirikiana na familia yake ya Kikristo pamoja na ndugu na dada zake wa kiroho. Anahisi akiwa karibu zaidi na Yehova na ana amani nyingi ya akili, akijua kwamba anatumia wakati wake kwa hekima.

9. Kufuatia faida za kimwili kunaweza kumfanyaje mtu aweke kando mambo ya kiroho?

9 Faida za kimwili. Ili tuendelee kutembea katika kweli, ni lazima tuepuke kutanguliza vitu vya kimwili maishani. Tulipojifunza kweli, tuliacha kutanguliza vitu vya kimwili na kuanza kufuatia mambo ya kiroho. Tulifurahia kudhabihu vitu vya kimwili ili tutembee katika kweli. Hata hivyo, baada ya muda, huenda tukaanza kuona kwamba wengine wanafurahia vifaa vya kisasa vya kielektroni au faida nyingine za kimwili. Huenda tukaanza kuhisi kwamba kuna vitu fulani vizuri tunavyokosa. Kwa kuwa sasa haturidhiki tena na vitu vya lazima, huenda tukaweka kando mambo ya kiroho, na kuanza kujirundikia vitu vya kimwili. Jambo hilo linatukumbusha kuhusu Dema. Upendo wake kuelekea “mfumo wa mambo wa sasa” ulimfanya aache utumishi wake pamoja na mtume Paulo. (2 Tim. 4:10) Kwa nini Dema alimwacha Paulo? Biblia haisemi ikiwa alipenda vitu vya kimwili kuliko mambo ya kiroho au kwamba hakutaka kuendelea kujidhabihu ili kutumikia pamoja na Paulo. Kwa hakika hatungependa kuamsha ndani ya moyo wetu tamaa ya vitu vya kimwili na kuruhusu vitu hivyo vitufanye tupoteze upendo tulio nao kuelekea kweli.

10. Ili tuendelee kutembea katika kweli, ni lazima tukatae kabisa kushinikizwa na nani?

10 Uhusiano wetu na wengine. Ili tuendelee kutembea katika kweli, ni lazima tukatae kabisa kushinikizwa na wengine. Tulipoanza kutembea katika kweli, uhusiano wetu pamoja na marafiki wetu na watu wa familia ambao si Mashahidi ulibadilika. Baadhi yao walielewa; wengine walitupinga moja kwa moja. (1 Pet. 4:4) Ingawa sisi hujitahidi kuwa na uhusiano mzuri pamoja na watu wa familia yetu na kuwatendea kwa fadhili, ni lazima tuwe waangalifu tusilegeze viwango vya kweli ya Biblia ili kuwapendeza. Tutaendelea kujitahidi kuwa na uhusiano mzuri pamoja na watu wa familia yetu. Kwa kuzingatia onyo lililo wazi linalopatikana katika andiko la 1 Wakorintho 15:33, tutasitawisha urafiki wa karibu na wale tu wanaompenda Yehova.

11. Tunaweza kuepukaje mazoea yasiyo ya Kimaandiko?

11 Mwenendo na njia ya kufikiri isiyompendeza Mungu. Ni lazima wote wanaotembea katika kweli wawe watakatifu. (Isa. 35:8; soma 1 Petro 1:14-16.) Tulipokuwa tukijifunza kweli, sisi sote tulihitaji kufanya mabadiliko ili maisha yetu yapatane na viwango vya Biblia vya uadilifu. Baadhi yetu tulihitaji kufanya mabadiliko makubwa. Iwe tulifanya mabadiliko madogo au makubwa, hatupaswi kamwe kuacha maisha yetu safi na matakatifu na kuanza kuishi maisha machafu kiadili ya ulimwengu huu. Tunaweza kuepukaje kutumbukia katika mwenendo mpotovu kiadili? Tafakari kuhusu bei kubwa ambayo Yehova alilipa kwa ajili yetu ili tuwe watakatifu—damu yenye thamani ya Yesu Kristo, Mwanaye. (1 Pet. 1:18, 19) Ili tuendelee kufurahia msimamo safi mbele za Yehova, jambo tunalopaswa kuendelea kuzingatia akilini na moyoni mwetu nyakati zote ni thamani ya dhabihu ya fidia ya Yesu.

12, 13. (a) Kwa nini ni muhimu kudumisha maoni ya Yehova kuhusu sikukuu? (b) Tutachunguza nini?

12 Mazoea na desturi zisizo za Kimaandiko. Watu wa familia, wafanyakazi, na wanafunzi wenzetu wanaweza kujaribu kutushinikiza tujiunge nao katika sherehe zao. Tunaweza kufanya nini ili tusikubali kushinikizwa nao wanapotaka tushiriki katika desturi na sikukuu zinazomvunjia Yehova heshima? Tunaweza kufanikiwa kupinga hali hiyo ikiwa maoni ya Yehova kuhusu mambo hayo yatakuwa wazi akilini mwetu. Kujikumbusha habari zilizo katika machapisho yetu zinazozungumzia vyanzo vya sikukuu zinazopendwa na watu wengi leo ni jambo litakalokusaidia. Tunapojikumbusha sababu za Kimaandiko zinazotufanya tusishiriki katika sikukuu hizo, tunasadiki kwamba tunatembea katika njia “[inayokubalika] kwa Bwana.” (Efe. 5:10) Kumtumaini Yehova na Neno lake la kweli, kutatulinda dhidi ya mtego wa “kuwaogopa wanadamu.”—Met. 29:25.

13 Kutembea katika kweli si jambo la siku moja, ni njia ya maisha ambayo tungependa kufuata milele na milele. Tunaweza kuimarishaje azimio letu la kuendelea kutembea katika kweli? Acheni tuchunguze njia tatu zitakazotusaidia kufanya hivyo.

IMARISHA AZIMIO LAKO LA KUTEMBEA KATIKA KWELI

14. (a) Kuendelea kununua kweli kutatusaidiaje kuimarisha azimio letu la kutoiuza kamwe? (b) Kwa nini hekima, nidhamu, na uelewaji ni sifa muhimu?

14 Kwanza, endelea kujifunza kuhusu kweli zenye thamani za Neno la Mungu na uzitafakari. Naam, nunua kweli kwa kuwa na kawaida ya kutenga wakati ili ujilishe kweli zenye thamani za Neno la Mungu. Kufanya hivyo kutakusaidia uithamini zaidi kweli na kuimarisha azimio lako la kutoiuza kamwe. Mbali na kununua kweli, andiko la Methali 23:23 linasema kwamba tunapaswa pia kununua “hekima na nidhamu na uelewaji.” Kuwa na ujuzi pekee hakutoshi. Ni lazima tutumie maishani mwetu kweli tunazojifunza. Uelewaji utatusaidia kutambua kwamba maneno yote ya Yehova yana upatano. Hekima itatuchochea tutende kulingana na mambo tunayojifunza. Nyakati nyingine, kweli hututia nidhamu kwa kutusaidia tuone ni mabadiliko gani tunayopaswa kufanya. Acheni sikuzote tuwe tayari kutii mwongozo huo. Thamani yake inazidi kwa mbali thamani ya fedha.—Met. 8:10.

15. Mshipi wa ile kweli hutulindaje?

15 Pili, azimia kwa dhati kuishi kulingana na kweli siku baada ya siku. Jifunge kiunoni mshipi wa ile kweli. (Efe. 6:14) Katika nyakati za Biblia, mshipi wa mwanajeshi ulilinda kiuno chake na viungo vya ndani vya mwili wake. Hata hivyo, ili mshipi huo umlinde, alipaswa kuukaza vizuri kiunoni mwake. Mshipi uliolegea haungemsaidia. Mshipi wetu wa kiroho wa ile kweli hutulindaje? Ikiwa tutajifunga vizuri na kuukaza mshipi huo, kweli itatulinda tusisitawishe maoni au mawazo yenye kasoro na itatusaidia kufikia maamuzi mazuri. Tunaposhawishiwa au kujaribiwa, kweli ya Biblia itaimarisha azimio letu la kutenda yaliyo sawa. Kama tu ambavyo mwanajeshi hawezi kufikiria kamwe kwenda vitani bila kujifunga mshipi kiunoni mwake, ni lazima sisi pia tuazimie kwamba hatutaulegeza kamwe au kuuvua mshipi wetu wa ile kweli. Badala yake, tunafanya yote tuwezayo kuhakikisha kwamba tumeukaza vizuri kwa kuishi kulingana na kweli. Pia, mshipi wa mwanajeshi ulitimiza kazi nyingine muhimu; ulikuwa na mahali pazuri pa kuchomeka upanga wake. Hilo linatuleta kwenye jambo lingine litakalotusaidia tuimarishe azimio letu la kuendelea kutembea katika kweli.

16. Kuwafundisha wengine kweli huimarishaje azimio letu la kuendelea kutembea katika kweli?

16 Tatu, jitahidi kadiri uwezavyo kushiriki kikamili katika kazi ya kuwafundisha wengine kweli ya Biblia. Kufanya hivyo kutakusaidia kuushika kwa nguvu upanga wetu wa kiroho, ambao ni “neno la Mungu.” (Efe. 6:17) Sote tunaweza kujitahidi kuboresha ustadi wetu tukiwa walimu kwa “[kulitumia] sawasawa neno la kweli.” (2 Tim. 2:15) Tunapoendelea kutumia Biblia kuwasaidia wengine kununua kweli na kukataa mafundisho ya uwongo, tunakazia kikiki akilini na moyoni mwetu maneno ya Mungu. Kwa kufanya hivyo, tunaimarisha azimio letu la kuendelea kutembea katika kweli.

17. Kwa nini kweli ni yenye thamani kwako?

17 Kweli ni zawadi yenye thamani kutoka kwa Yehova. Zawadi hiyo imetusaidia kupata kitu kilicho na thamani zaidi kwetu, yaani, uhusiano wa karibu pamoja na Baba yetu wa mbinguni. Mambo ambayo ametufundisha kufikia sasa ni mwanzo tu! Mungu ametuahidi kwamba tutaishi milele ili tuendelee kuongeza kweli nyingine kwenye hazina yetu ya kweli ambazo tayari tumenunua. Hivyo, thamini kweli kama lulu nzuri iliyo na thamani kubwa. Endelea “[kuinunua] kweli wala usiiuze kamwe.” Kisha kama Daudi, utatimiza ahadi hii kwa Yehova: “Nitatembea katika kweli yako.”—Zab. 86:11.

^ fu. 8 Jina limebadilishwa.

^ fu. 8 Tembelea JW Broadcasting, tazama chini ya MAHOJIANO NA MAMBO YALIYOONWA > KWELI HUBADILI MAISHA.