Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Inunue Kweli Wala Usiiuze Kamwe”

“Inunue Kweli Wala Usiiuze Kamwe”

“Inunue kweli wala usiiuze kamwe, pia hekima na nidhamu na uelewaji.”—MET. 23:23.

NYIMBO: 94, 96

1, 2. (a) Ni kitu gani chenye thamani zaidi tulicho nacho? (b) Ni kweli gani zenye thamani tulizo nazo, na kwa nini tunazithamini? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

NI KITU gani ambacho wewe huona kuwa chenye thamani zaidi kwako? Je, ungekuwa tayari kutoa kitu hicho ili upate kitu kingine chenye thamani ndogo zaidi? Kwa waabudu wa Yehova waliojiweka wakfu, majibu ya maswali hayo ni rahisi. Uhusiano wetu na Yehova ndicho kitu chenye thamani zaidi kwetu, na hatuwezi kubadilishana uhusiano huo na kitu kingine chochote. Pia, tunaiona kweli ya Biblia kuwa yenye thamani sana kwetu kwa sababu imetusaidia kusitawisha uhusiano huo pamoja na Baba yetu wa mbinguni.—Kol. 1:9, 10.

2 Fikiria mambo yote ambayo Mfundishaji wetu Mkuu anatufundisha kupitia Neno lake, Biblia! Anafunua kweli kuhusu jina lake lililo na maana kubwa na sifa zake zenye kuvutia. Anatueleza kuhusu zawadi ya pekee sana ya fidia, ambayo aliandaa kwa upendo kupitia Yesu, Mwana wake. Pia, Yehova anatueleza kuhusu Ufalme wa Kimasihi, na anawapa watiwa-mafuta tumaini la kuishi mbinguni na “kondoo wengine” tumaini la kuishi katika Paradiso duniani. (Yoh. 10:16) Anatufundisha pia mwenendo tunaopaswa kuwa nao. Tunaziona kweli hizo kuwa zenye thamani kwa sababu zinatusaidia kumkaribia Muumba wetu. Kweli hizo hufanya maisha yetu yawe na kusudi.

3. Kununua kweli hakumaanishi nini?

3 Yehova ni Mungu mkarimu. Hawanyimi jambo lolote jema wale wanaotafuta kweli. Yehova hata alitoa uhai wa Mwana wake mpendwa kuwa zawadi ya bure. Ni wazi kwamba Mungu hatarajii kamwe tutoe pesa ili tupate kweli. Na ndio sababu mwanamume aliyeitwa Simoni alipotaka kumpa Petro pesa ili apate mamlaka ya kuwasaidia watu wapate roho takatifu, Petro alimkemea kwa kusema hivi: “Fedha yako na iangamie pamoja nawe, kwa sababu ulidhani utanunua zawadi ya bure ya Mungu kwa kutumia pesa.” (Mdo. 8:18-20) Hivyo basi, maneno “inunue kweli” ambayo yameongozwa na roho yanamaanisha nini?

‘KUNUNUA’ KWELI KUNAMAANISHA NINI?

4. Tutajifunza nini kuhusu kweli katika makala hii?

4 Soma Methali 23:23. Hatuwezi kupata kweli iliyo katika Neno la Mungu bila jitihada yoyote. Ni lazima tuwe tayari kufanya jitihada yoyote inayohitajiwa ili tuipate. Kama mwandikaji mwenye hekima wa kitabu cha Methali alivyoandika, baada ya ‘kununua,’ au kujipatia “kweli,” ni lazima tuwe waangalifu ‘tusiiuze,’ au kuipoteza. Acheni tuzungumzie maana ya ‘kununua’ kweli na gharama ambayo huenda tukalipia ili kuipata. Kufanya hivyo kutatusaidia kuthamini hata zaidi kweli ya Biblia na kuimarisha azimio letu la ‘kutoiuza’ kamwe. Kama tutakavyoona, manufaa tutakayopata hayawezi kulinganishwa kwa vyovyote na gharama yoyote ambayo huenda tukalipia.

5, 6. (a) Tunaweza kununuaje kweli bila kutumia pesa? Toa mfano. (b) Kweli hutunufaishaje?

5 Hata kitu ambacho ni cha bure huenda bado kikatugharimu. Neno la Kiebrania linalotafsiriwa ‘nunua’ kwenye Methali 23:23 linaweza pia kumaanisha “jipatie.” Maneno yote mawili yanaonyesha kwamba jitihada inahusika au kitu fulani kinatolewa ili kupata kitu kingine chenye thamani. Fikiria mfano ufuatao unaoweza kutusaidia kuelewa jambo hilo. Tuseme umesikia kwamba kuna ndizi za bure sokoni. Je, ndizi hizo zitafika kimuujiza mezani petu? Hapana. Lazima tufanye jitihada ya kwenda sokoni na kuzichukua. Je, ndizi hizo ni za bure? Bila shaka, lakini ni lazima tufanye jitihada fulani na tutumie wakati wetu kwenda sokoni. Vivyo hivyo, hatuhitaji pesa ili kununua kweli. Hata hivyo, ni lazima tufanye jitihada fulani ili kuipata.

6 Soma Isaya 55:1-3. Maneno hayo ya Yehova yaliyoandikwa na Isaya yanatusaidia kuelewa vizuri zaidi maana ya kununua kweli. Katika mistari hiyo, Yehova analinganisha Neno lake na maji, maziwa, na divai. Kama maji safi na baridi yanavyoburudisha, maneno ya kweli kutoka kwa Mungu huburudisha. Pia, kama maziwa yanavyotuimarisha na kuwasaidia watoto wakue, maneno ya Yehova yenye lishe hutuimarisha na kutusaidia kukua kiroho. Pia, maneno ya Yehova ni kama divai. Jinsi gani? Katika Biblia, divai huhusianishwa na hisia za kushangilia. (Zab. 104:15) Hivyo, kwa kuwaambia watu wake ‘wanunue divai,’ Yehova anatuhakikishia kwamba kuishi kulingana na maneno yake kutatufanya tushangilie. (Zab. 19:8) Huo ni ulinganisho wenye kuvutia sana wa manufaa tunayopata tunapojifunza na kutumia Neno la Mungu la kweli! Tunaweza kulinganisha jitihada hizo na gharama tunayolipia ili kupata kweli. Hivyo basi, acheni tuzungumzie mambo matano yanayohusika katika kununua kweli.

UMETOA NINI ILI UNUNUE KWELI?

7, 8. (a) Kwa nini ni lazima tutumie wakati ili tununue kweli? (b) Mwanafunzi mmoja kijana alikuwa tayari kujidhabihu kadiri gani, na matokeo yalikuwa nini?

Wakati. Hiyo ni gharama ambayo kila mtu anayenunua kweli lazima alipie. Wakati unahusika ili kusikiliza ujumbe wa Ufalme, kusoma Biblia na machapisho yanayotegemea Biblia, kujifunza Biblia kibinafsi, na kujitayarisha na kuhudhuria mikutano ya kutaniko. Ili tufanye mambo hayo, ni lazima ‘tujinunulie’ wakati, yaani, tununue kweli kwa kutumia wakati ambao awali tuliutumia kufanya mambo yasiyo ya maana sana. (Soma Waefeso 5:15, 16 na maelezo ya chini.) Ni kiasi gani cha wakati tutakachotumia kupata ujuzi sahihi wa mafundisho ya msingi ya Biblia? Inategemea na hali zetu. Hakuna mwisho wa kujifunza kuhusu hekima ya Yehova, njia zake, na kazi zake. (Rom. 11:33) Toleo la kwanza la gazeti la Mnara wa Mlinzi lililinganisha kweli na “ua dogo” kisha likasema hivi: “Usiridhike na ua moja la kweli. Kama ua moja la kweli lingetosha kusingekuwa na mengine. Endelea kukusanya, tafuta mengi zaidi.” Tunaweza kujiuliza, ‘Shada langu la maua ya kweli za Biblia ni kubwa kadiri gani?’ Hata tukiishi kwa umilele wote, sikuzote tutakuwa na mambo mengi ya kujifunza kumhusu Yehova. Leo, jambo la muhimu ni kutumia wakati wetu kwa hekima ili tununue kweli nyingi kadiri hali zetu zinavyoturuhusu. Fikiria mfano wa mtu fulani aliyetamani sana kupata kweli.

8 Mariko, * mwanamke kijana kutoka Japani, alienda kusoma huko New York City, Marekani. Wakati huo, alikuwa mfuasi wa kikundi fulani cha kidini kilichoanzishwa nchini Japani mwishoni mwa miaka ya 1950. Dada mmoja painia alipokuwa akihubiri nyumba kwa nyumba alikutana na Mariko. Alipoanza kujifunza kweli za Biblia, alifurahi sana hivi kwamba alimwomba painia huyo ajifunze Biblia pamoja naye mara mbili kwa juma. Licha ya kwamba ratiba yake ya shule ilikuwa na mambo mengi na alifanya kazi ya muda, mara moja Mariko alianza kuhudhuria mikutano ya kutaniko. Pia, aliacha kutumia wakati mwingi pamoja na marafiki ili ajinunulie wakati wa kujifunza kweli. Kujidhabihu kwa njia hiyo kulimsaidia afanye maendeleo ya kiroho haraka. Na katika kipindi cha mwaka mmoja tu, akabatizwa. Miezi sita baadaye, katika mwaka wa 2006, alianza upainia, na anaendelea na utumishi huo mpaka sasa.

9, 10. (a) Ni katika njia gani kununua kweli hubadili maoni yetu kuhusu vitu vya kimwili? (b) Ni fursa gani ambazo mwanamke fulani kijana alitupilia mbali, na anahisije kuhusu uamuzi aliofanya?

9 Faida za kimwili. Ili kununua kweli, huenda tukalazimika kuacha kazi nzuri yenye mshahara mnono. Petro na Andrea walikuwa wavuvi, lakini walipoalikwa na Yesu wawe “wavuvi wa watu,” Biblia inasema “[waliziacha] nyavu zao.” (Mt. 4:18-20) Bila shaka, watu wengi wanaojifunza kweli leo hawawezi tu kuacha kazi zao kwa sababu wana wajibu mbalimbali wa Kimaandiko. (1 Tim. 5:8) Hata hivyo, mara nyingi watu wanaojifunza kweli lazima wabadili mtazamo wao kuelekea vitu vya kimwili na kubadili maoni yao kuhusu mambo wanayotanguliza maishani. Yesu alieleza waziwazi jambo hilo aliposema hivi: “Acheni kujiwekea hazina duniani . . . Badala yake, jiwekeeni hazina mbinguni.” (Mt. 6:19, 20) Fikiria mfano wa mwanamke mmoja kijana.

10 Maria alianza kucheza gofu hata kabla ya kufikia umri wa kuanza kwenda shule. Aliendelea kuboresha ustadi wake wa kucheza gofu alipokuwa katika shule ya sekondari na mwishowe akapata ufadhili wa kwenda chuo kikuu. Mchezo wa gofu ulikuwa ndilo jambo kuu maishani mwake, na lengo lake lilikuwa kupata ufanisi katika mchezo huo akiwa mcheza-gofu wa kulipwa. Kisha Maria akaanza kujifunza Biblia, naye alipenda sana kweli alizokuwa akijifunza. Alifurahishwa na mabadiliko ambayo kweli ilimsaidia kufanya maishani mwake. Alisema hivi: “Kadiri nilivyobadili mtazamo wangu na maisha yangu ili yapatane na viwango vya Biblia, ndivyo furaha yangu ilivyozidi kuongezeka.” Maria alitambua kwamba ingekuwa vigumu kwake kufuatia mambo ya kiroho na wakati uleule kufuatia utajiri. (Mt. 6:24) Alilipia gharama ya kupata kweli kwa kuacha mradi aliokuwa nao tangu utotoni wa kuwa mcheza-gofu wa kulipwa na fursa ya kupata utajiri na umashuhuri. Hivyo, kwa kuwa alinunua kweli, sasa yeye ni painia na anasema kwamba maisha anayoishi sasa ndiyo “maisha yenye furaha zaidi, maisha bora na yenye kuridhisha sana.”

11. Baada ya kununua kweli, huenda uhusiano wetu na wengine ukawaje?

11 Uhusiano wetu na wengine. Tunapochagua kuishi kulingana na kweli ya Biblia, huenda uhusiano wetu pamoja na marafiki au na watu wa ukoo ukabadilika. Kwa nini? Yesu alisali hivi kuhusu wafuasi wake: “Watakase kupitia ile kweli; neno lako ni kweli.” (Yoh. 17:17; maelezo ya chini) Neno “watakase” linaweza pia kumaanisha “uwaweke kando.” Tunapoikubali kweli, tunawekwa kando kutoka kwenye ulimwengu kwa sababu hatuishi tena kama ulimwengu unavyotaka tuishi. Watu hutuona kuwa tofauti kwa sababu viwango vyetu vimebadilika. Tunaishi kulingana na viwango vya kweli ya Biblia. Ingawa hatungependa kusababisha mgawanyiko, huenda baadhi ya marafiki na watu wa karibu wa familia wakajitenga nasi, au hata wakatupinga kwa sababu ya imani yetu mpya. Jambo hilo halitushangazi. Yesu alisema hivi waziwazi: “Kwa kweli, adui za mtu watakuwa watu wa nyumbani mwake.” (Mt. 10:36) Alituhakikishia pia kwamba thawabu tutakazopata kwa kununua kweli zinazidi kwa mbali gharama yoyote ambayo huenda tukalipa.—Soma Marko 10:28-30.

12. Mwanamume mmoja Myahudi alilipa gharama gani ili kupata kweli?

12 Tangu utotoni, Aaron, mwanabiashara Myahudi, alifundishwa kwamba jina la Mungu halikupaswa kutamkwa. Hata hivyo, Aaron alikuwa na kiu ya kupata kweli. Alifurahi sana Shahidi mmoja alipomwonyesha kwamba kwa kuweka irabu katikati ya konsonanti nne za Kiebrania za jina la Mungu, jina hilo linaweza kusomeka kuwa “Yehova.” Akiwa amesisimka sana, alienda kwenye sinagogi na kuwaeleza marabi kuhusu mambo mazuri aliyokuwa amejifunza. Marabi hao waliitikia kwa njia ambayo Aaron hakutazamia hata kidogo. Badala ya kufurahi pamoja naye alipowaeleza kuhusu kweli aliyojifunza kuhusu jina la Mungu, walimtemea mate na kumtendea kama mtu ambaye hakupaswa kushirikiana na wengine. Uhusiano wake pamoja na watu wake wa familia ulidhoofika. Bila kutetereka, aliendelea kununua kweli na alikuwa Shahidi wa Yehova mwenye ujasiri katika kipindi chote cha maisha yake. Kama Aaron, ili tutembee katika kweli, sisi pia tuko tayari kulipa gharama, yaani, kukubali mabadiliko yoyote yanayoweza kutokea iwe ni katika uhusiano wetu na wengine katika jamii au watu wa familia yetu.

13, 14. Tunahitaji kufanya mabadiliko gani katika mwenendo na njia yetu ya kufikiri ili tununue kweli? Toa mfano.

13 Fikira na mwenendo usiopatana na viwango vya Mungu. Ili tukubali kweli na kuishi kulingana na viwango vya Biblia kuhusu maadili, ni lazima tuwe tayari kubadili mwenendo wetu na njia yetu ya kufikiri. Kuhusu mabadiliko hayo, Petro aliandika hivi: “Kama watoto watiifu, acheni kufinyangwa na tamaa mlizokuwa nazo zamani katika hali yenu ya kutojua, lakini iweni watakatifu katika mwenendo wenu wote.” (1 Pet. 1:14, 15) Kwa wakaaji wa jiji la Korintho lililokuwa limejaa upotovu wa maadili, kununua kweli kulimaanisha kwamba walipaswa kufanya mabadiliko makubwa katika njia yao ya maisha. (1 Kor. 6:9-11) Vivyo hivyo leo, ili kununua kweli, watu wengi wameacha kabisa mwenendo usiompendeza Mungu. Pia, Petro aliwakumbusha hivi Wakristo wa siku zake: “Kwa maana wakati uliopita uliwatosha kufanya mapenzi ya mataifa, mlipofanya vitendo vya mwenendo mpotovu, uchu, kunywa kupita kiasi, karamu zenye vurugu, mashindano ya kunywa, na ibada za sanamu zenye kuchukiza.”—1 Pet. 4:3.

14 Devynn na Jasmine walikuwa walevi kwa miaka mingi. Ingawa Devynn alikuwa mhasibu mwenye uzoefu, tatizo lake la ulevi lilimfanya afutwe kazi mara kwa mara. Jasmine alijulikana kuwa mtu mwenye hasira na aliyependa kupigana na watu. Siku moja alipokuwa akitembea barabarani akiwa amelewa, Jasmine alikutana na wamishonari wawili waliokuwa Mashahidi wa Yehova. Wamishonari hao walipanga kujifunza Biblia pamoja naye, lakini walipofika nyumbani kwao juma lililofuata, wote wawili, Jasmine na Devynn walikuwa wamelewa. Hawakutarajia kwamba wamishonari hao wangewajali kiasi cha kuja hadi nyumbani kwao. Lakini hali ilikuwa tofauti walipowatembelea mara ya pili. Jasmine na Devynn walikuwa wanafunzi wa Biblia wenye bidii tangu siku ya kwanza, na walianza kutumia mambo waliyokuwa wakijifunza. Katika kipindi cha miezi mitatu, waliamua kuacha kunywa pombe na baadaye wakafunga ndoa kisheria. Watu wengi walijionea mabadiliko waliyofanya, na jambo hilo liliwachochea wengi katika kijiji chao kujifunza Biblia.

15. Ni jambo gani gumu zaidi ambalo huenda mtu akalazimika kufanya ili kununua kweli, na kwa nini?

15 Desturi na mazoea yasiyo ya Kimaandiko. Kuacha desturi na mazoea yasiyo ya Kimaandiko ni mojawapo ya mambo magumu zaidi unayoweza kufanya ili kununua kweli. Ingawa huenda ikawa rahisi kwa baadhi ya watu kukubali sababu zinazotolewa na Maandiko za kuacha mazoea hayo, huenda wengine wakasita kufanya hivyo kwa sababu ya kushinikizwa na watu wao wa familia, wafanyakazi wenzao, na marafiki wa karibu. Hali inaweza kuwa mbaya hata zaidi, hasa inapohusu desturi zinazohusisha mila za kuwaheshimu watu wa ukoo waliokufa. (Kum. 14:1) Mifano ya watu walioonyesha ujasiri inaweza kutusaidia kufanya mabadiliko yanayohitajika. Fikiria jinsi wakaaji wa jiji la Efeso walivyotenda kwa ujasiri katika karne ya kwanza.

16. Baadhi ya wakaaji wa jiji la Efeso walifanya nini ili kununua kweli?

16 Jiji la Efeso lilijulikana sana kwa mazoea yake ya uchawi. Wakaaji wa jiji hilo waliokuwa wamejiunga na kutaniko la Kikristo hivi karibuni walifanya nini ili kuacha kabisa mazoea hayo yasiyo ya Kimaandiko na hivyo kununua kweli? Biblia inaeleza hivi: “Idadi kubwa ya wale waliozoea kufanya uchawi wakakusanya vitabu vyao pamoja na kuviteketeza mbele ya kila mtu. Nao wakafanya hesabu na kupata vitabu hivyo vilikuwa na thamani ya vipande 50,000 vya fedha. Hivyo kwa njia yenye nguvu, neno la Yehova likazidi kukua na kusitawi.” (Mdo. 19:19, 20) Wakristo hao waaminifu waligharimika kwa njia kubwa sana, nao wakapata baraka ambazo thamani yake haiwezi kulinganishwa na chochote.

17. (a) Gharama tunayopaswa kulipa ili kupata kweli inatia ndani mambo gani? (b) Tutachunguza maswali gani katika makala inayofuata?

17 Wewe binafsi uligharimika kiasi gani ili kupata kweli? Sisi sote hutumia wakati ili kujikusanyia maua ya mfano ya kweli za Biblia. Wengine hununua kweli kwa kuacha fursa za kupata faida za kimwili na pia kwa kuvumilia hali ngumu kwa sababu uhusiano wao pamoja na wengine umebadilika. Na wengi wanahitaji kufanya mabadiliko katika mwenendo wao na njia yao ya kufikiri, na ni lazima waache kabisa desturi na mazoea yasiyo ya Kimaandiko. Lakini hata tugharimike jinsi gani, tunasadiki kabisa kwamba kweli ya Biblia haiwezi kulinganishwa kwa vyovyote na gharama yoyote ambayo huenda tukalipa. Kweli ya Biblia hutusaidia kupata kitu ambacho ni chenye thamani zaidi kwetu, yaani, uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Tunapotafakari baraka tulizo nazo kwa sababu ya kujua kweli, ni jambo lisilowazika kwamba mtu anaweza kufikiria kuiuza. Lakini inawezekanaje mtu akafikia hatua ya kutaka kuiuza kweli, na tunaweza kuepukaje kufanya kosa hilo zito? Tutachunguza maswali hayo katika makala inayofuata.

^ fu. 8 Baadhi ya majina katika makala hii yamebadilishwa.